Hamia kwenye habari

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana kwa Njia Tofauti na Dini Nyingine?

Kwa Nini Mashahidi wa Yehova Wanaadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana kwa Njia Tofauti na Dini Nyingine?

 Tunashikamana kabisa na ufafanuzi wa Biblia kuhusu Mlo wa Jioni wa Bwana unaoitwa pia “chakula cha Bwana,” au Ukumbusho wa Kifo cha Yesu. (1 Wakorintho 11:20; Union Version) Kwa upande mwingine, imani na itikadi za dini nyingine kuhusu mwadhimisho huo hazipatani na Biblia.

Kusudi

 Kusudi la Mlo wa Jioni wa Bwana ni kumkumbuka Yesu, kuonyesha kwamba tunathamini fidia aliyotoa kwa ajili yetu. (Mathayo 20:28; 1 Wakorintho 11:24) Mlo huo si sakramenti, au desturi fulani ya kiibada tunayoweza kufanya ili kupata neema au kusamehewa dhambi. * Biblia inafundisha kwamba tunaweza kusamehewa dhambi zetu kwa kumwamini Yesu, si kwa kuwa wafuasi wa kikundi fulani cha kidini.​—Waroma 3:25; 1 Yohana 2:1, 2.

Uadhimishwe mara ngapi?

 Yesu aliwaamuru wanafunzi wake waadhimishe Mlo wa Jioni wa Bwana, lakini hakusema wafanye hivyo mara nyingi kadiri gani. (Luka 22:19) Watu fulani hufikiri kwamba Mlo huo unapaswa kuadhimishwa kila mwezi, ilhali wengine wanaadhimisha kila juma, kila siku, mara kadhaa kwa siku na wengine mara nyingi kadiri wanavyopenda. Lakini, hebu fikiria mambo yafuatayo.

 Yesu alianzisha Mlo wa Jioni wa Bwana katika siku ya sherehe ya Pasaka ya Wayahudi, naye alikufa baadaye siku hiyohiyo. (Mathayo 26:1, 2) Kwa kuwa Maandiko yanafananisha dhabihu ya fidia ya Yesu na kondoo wa Pasaka, mlo huo haukuanzishwa siku hiyo bila sababu. (1 Wakorintho 5:7, 8) Pasaka iliadhimishwa mara moja kwa mwaka. (Kutoka 12:1-6; Mambo ya Walawi 23:5) Vivyo hivyo, Wakristo wa mapema waliadhimisha Ukumbusho wa kifo cha Yesu mara moja kwa mwaka, * na Mashahidi wa Yehova wanafuata kielelezo hicho kinachotegemea Biblia.

Siku na tarehe

 Mbali tu na kujua Ukumbusho unapaswa kuadhimishwa mara ngapi, kielelezo ambacho Yesu aliweka kinatusaidia kuelewa siku na tarehe ya Ukumbusho huo. Kulingana na kalenda ya Biblia, alianzisha mwadhimisho huo Nisani 14, 33 W.K. baada ya jua kutua. (Mathayo 26:18-20, 26) Tunaendelea kuadhimisha Ukumbusho tarehe hiyohiyo kila mwaka kama tu Wakristo wa karne ya kwanza walivyofanya. *

 Ingawa Nisani 14, 33 W.K. ilikuwa siku ya Ijumaa, inawezekana tarehe hiyo kuwa siku tofauti kila mwaka. Badala ya kufuata kalenda ya sasa ya Kiyahudi, tunatumia kanuni ileile iliyotumiwa wakati wa Yesu ili kujua siku ambayo tarehe ya Nisani 14 itaangukia. *

Mkate na divai

 Yesu alitumia mkate usio na chachu na divai iliyobaki katika sherehe ya Pasaka kwa ajili ya mwadhimisho huo mpya. (Mathayo 26:26-28) Tunaiga mfano aliotuwekea kwa kutumia mkate usio na chachu na ambao haujatiwa kiungo kingine chochote. Pia tunatumia divai nyekundu na hatutumii maji ya matunda au divai iliyoongezwa sukari, vinywaji vikali, au vikolezo.

 Baadhi ya dini hutumia mkate wenye chachu au hamira, lakini chachu imetumiwa na Biblia mara nyingi kurejezea dhambi na kuharibika. (Luka 12:1; 1 Wakorintho 5:​6-8; Wagalatia 5:​7-9) Hivyo, mkate usio na chachu wala viungo vyovyote ndio tu unaostahili kuwakilisha mwili usio na dhambi wa Kristo. (1 Petro 2:22) Zoea lingine ambalo Biblia hupinga ni kutumia maji ya matunda badala ya divai. Baadhi ya dini hufanya hivyo wakidai kukataa kutumia kileo kwa sababu zisizo na msingi wa kimaandiko.​—1 Timotheo 5:23.

Ni mifano, si mwili na damu halisi

 Mkate usio na chachu na divai inayotumiwa wakati wa Ukumbusho si mwili halisi bali unawakilisha damu na mwili wa Kristo. Mifano hiyo haibadiliki kimuujiza kuwa mwili na damu halisi ya Yesu kama wengine wanavyofikiri. Fikiria sababu zifuatazo za Kimaandiko.

  •   Ikiwa Yesu angewaamuru wanafunzi wake wanywe damu yake, angekuwa akivunja amri ya Mungu juu ya matumizi ya damu. (Mwanzo 9:4; Matendo 15:28, 29) Hilo haliwezekani kamwe kwa sababu Yesu hawezi kuwafundisha watu wavunje sheria ya Mungu kuhusu utakatifu wa damu.​—Yohana 8:​28, 29.

  •   Wanafunzi wake hawangeweza kuwa wakinywa damu halisi ya Yesu kwa kuwa bado alikuwa hai. Damu yake haikuwa imemwagwa.​—Mathayo 26:28.

  •   Yesu alitoa dhabihu “mara moja kwa wakati wote.” (Waebrania 9:25, 26) Pia, ikiwa mkate na divai vilibadilika kuwa mwili na damu halisi ya Yesu wakati wa Ukumbusho wa Kifo chake, basi wale waliokula na kunywa wangekuwa wakirudia fidia hiyo.

  •   Yesu alisema: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi,” bali si “kwa kunitoa dhabihu.​—1 Wakorintho 11:24.

 Imani ya watu fulani kwamba mkate na divai hubadilika kimuujiza na kuwa mwili na damu halisi ya Yesu, inategemea tafsiri ya mistari fulani katika Biblia. Kwa mfano, tafsiri nyingi za Biblia zinamwonyesha Yesu akisema hivi kuhusu divai: “Hii ni damu yangu.” (Mathayo 26:28) Hata hivyo, maneno hayo ya Yesu yanaweza pia kutafsiriwa hivi: “Hii inamaanisha damu yangu,” “Hii inawakilisha damu yangu,” au “Hii inaashiria damu yangu.” * Yesu alikuwa akifundisha kwa kutumia mfano kama ilivyokuwa kawaida yake.​—Mathayo 13:34, 35.

Nani wanaokula na kunywa?

 Mashahidi wa Yehova wanapoadhimisha Mlo wa jioni wa Bwana, ni wachache tu wanaoshiriki kula mkate na kunywa divai. Kwa nini?

 Damu ya Yesu iliyomwagwa ilianzisha “agano jipya” ambalo lilichukua nafasi ya agano kati ya Yehova na taifa la Israeli la kale. (Waebrania 8:10-13) Wale walio katika agano hilo hushiriki kula mifano wakati wa Ukumbusho. Si kila Mkristo anayekula, badala yake ni “wale ambao wameitwa” na Mungu kwa njia ya pekee. (Waebrania 9:15; Luka 22:20) Watatawala pamoja na Kristo mbinguni, na Biblia inataja idadi yao kuwa ni 144,000.​—Luka 22:28-30; Ufunuo 5:9, 10; 14:1, 3.

 Tofauti na wale walioitwa kutawala pamoja na Yesu, yaani “kundi dogo,” wengi wetu tuna tumaini la kuwa miongoni mwa “umati mkubwa” utakaoishi milele duniani. (Luka 12:32; Ufunuo 7:9, 10) Ingawa sisi tulio na tumaini la kuishi duniani hatushiriki kula na kunywa mifano wakati wa Ukumbusho, tunajiunga pamoja na “kundi dogo” kuonyesha tunathamini dhabihu ambayo Yesu alitoa kwa ajili yetu.​—1 Yohana 2:2.

^ Kitabu McClintock and Strong’s Cyclopedia, Buku la 9, ukurasa wa 212, kinasema: “Neno sacramenti halipatikani katika A[gano] J[ipya]; wala neno la Kigiriki μυστήριον [my·steʹri·on] halitumiwi kwa njia yoyote kurejezea ubatizo, Mlo wa jioni wa Bwana, au mwadhimisho mwingine wowote.”

^ Ona kitabu The New Schaff-Herzog Encyclopedia of Religious Knowledge, Buku la 4, kurasa 43-​44, na McClintock and Strong’s Cyclopedia, Buku la 8, ukurasa 836.

^ Ona kitabu The New Cambridge History of the Bible, Buku la 1, ukurasa 841.

^ Kalenda ya kisasa ya Kiyahudi inatumia makadirio ya wataalamu wa elimu ya nyota kuamua mwezi wa Nisani unaanza lini, lakini njia hiyo haikutumiwa katika karne ya kwanza. Badala yake, mwezi wa Nisani ulianza wakati ambapo mwezi mpya ulionekana kwa mara ya kwanza Yerusalemu, na hilo linaweza kuwa siku moja au zaidi baada ya makadirio yaliyo kwenye kalenda ya kisasa ya Kiyahudi. Hiyo ni sababu moja inayofanya tarehe ambayo Mashahidi wa Yehova huadhimisha Mlo wa Jioni wa Bwana kuwa tofauti na tarehe ambayo Wayahudi huadhimisha Pasaka leo.

^ Ona A New Translation of the Bible, ya James Moffatt; The New Testament​—A Translation in the Language of the People, ya Charles B. Williams; na The Original New Testament, ya Hugh J. Schonfield.