Hamia kwenye habari

Kwa Nini Yesu Alikufa?

Kwa Nini Yesu Alikufa?

Jibu la Biblia

 Yesu alikufa ili wanadamu wasamehewe dhambi zao na kupokea uzima wa milele. (Waroma 6:23; Waefeso 1:7) Pia kifo cha Yesu kilithibitisha kwamba wanadamu wanaweza kuendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu hata wanapokabili majaribu makali sana.​—Waebrania 4:​15.

 Fikiria jinsi kifo cha mtu mmoja kingeweza kutimiza mambo mengi hivyo.

  1.   Yesu alikufa ili ‘tusamehewe dhambi zetu.’​—Wakolosai 1:​14.

     Mwanadamu wa kwanza, Adamu, aliumbwa akiwa mkamilifu, bila dhambi. Hata hivyo, alichagua kumwasi Mungu. Adamu alipokosa kutii, au alipotenda dhambi, aliwaathiri vibaya wazao wake wote. Biblia inasema: “Kupitia kutotii kwa mtu mmoja wengi walifanywa watenda-dhambi.”​—Waroma 5:19.

     Yesu alikuwa mkamilifu kama Adamu, lakini yeye hakuwahi kutenda dhambi. Hivyo, yeye angeweza kuwa “dhabihu ya upatanisho kwa ajili ya dhambi zetu.” (1 Yohana 2:2) Kama tu kutotii kwa Adamu kulivyoichafua familia ya wanadamu kwa dhambi, ndivyo kifo cha Yesu kilivyofuta doa hilo la dhambi kutoka kwa wote wanaodhihirisha imani kwake.

     Kwa njia fulani, Adamu aliiuza jamii ya wanadamu katika dhambi. Yesu alipokufa kwa hiari kwa ajili yetu, aliwanunua wanadamu wawe wake. Kwa sababu hiyo, “yeyote akitenda dhambi, tuna msaidizi kwa Baba, Yesu Kristo, mtu mwadilifu.”​—1 Yohana 2:1.

  2.   Yesu alikufa “ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”​—Yohana 3:​16.

     Ingawa Adamu aliumbwa aishi milele, dhambi yake ilimletea hukumu ya kifo. Kupitia kwa Adamu, “dhambi iliingia katika ulimwengu na kifo kupitia dhambi, na hivyo kifo kikaenea kwa watu wote kwa sababu wote walikuwa wamefanya dhambi.”​—Waroma 5:12.

     Tofauti na hilo, mbali tu na kuondoa doa la dhambi, kifo cha Yesu kilifuta hukumu ya kifo kwa wote wanaodhihirisha imani kumwelekea. Biblia inakazia jambo hilo kwa njia hii: “Kama vile dhambi ilivyotawala kama mfalme pamoja na kifo, vivyo hivyo pia fadhili zisizostahiliwa zitawale kama mfalme kupitia uadilifu kwa tazamio la uzima wa milele kupitia Yesu Kristo Bwana wetu.”​—Waroma 5:​21.

     Bila shaka, wanadamu leo wanaishi kwa muda mfupi sana. Hata hivyo, Mungu anaahidi kwamba atawapa wanadamu waadilifu uzima wa milele na kufufua wafu ili wao pia wafaidike kutokana na dhabihu ya kifo cha Yesu.​—Zaburi 37:29; 1 Wakorintho 15:22.

  3.   Yesu ‘alikuwa mtiifu mpaka kifo,’ na hivyo kuthibitisha kwamba mwanadamu anaweza kuwa mwaminifu kwa Mungu anapokabili jaribu lolote.​—Wafilipi 2:8.

     Licha ya kuwa na akili na mwili mkamilifu, Adamu alimwasi Mungu kwa sababu kwa ubinafsi alitamani kitu ambacho hakikuwa mali yake. (Mwanzo 2:​16, 17; 3:6) Baadaye, Shetani, adui mkuu wa Mungu, akadai kwamba hakuna mwanadamu anayeweza kumtii Mungu bila ubinafsi, hasa ikiwa uhai wake uko hatarini. (Ayubu 2:4) Hata hivyo, mwanadamu mkamilifu Yesu alimtii Mungu na kudumisha ushikamanifu kwake, hata akakabili kifo kinachofedhehesha na kilicho na maumivu. (Waebrania 7:​26) Suala hilo lilitatuliwa kikamili: Mwanadamu anaweza kudumisha uaminifu wake kwa Mungu anapokabili jaribu lolote lile.

Maswali kuhusu kifo cha Yesu

  •   Kwa nini Yesu alilazimika kuteseka na kufa ili kuwakomboa wanadamu? Kwa nini Mungu hakufuta tu hukumu ya kifo?

     Sheria ya Mungu inasema kwamba “mshahara ambao dhambi hulipa ni kifo.” (Waroma 6:23) Badala ya kumficha Adamu sheria hii, Mungu alimwambia kwamba hukumu ya kutotii ni kifo. (Mwanzo 3:3) Adamu alipofanya dhambi, yule Mungu “asiyeweza kusema uwongo,” alitimiza alichokuwa amesema. (Tito 1:2) Kwa hiyo, Adamu hakuwapitishia wazao wake dhambi tu, bali pia aliwapitishia malipo ya dhambi, yaani, kifo.

     Ingawa wanadamu wenye dhambi wanastahili adhabu ya kifo, Mungu aliwapa “utajiri wa fadhili zake zisizostahiliwa.” (Waefeso 1:7) Uandalizi wake wa kuwakomboa wanadamu, yaani, kumtuma Yesu awe dhabihu kamilifu, ulikuwa uandalizi wa haki na wenye rehema nyingi.

  •   Yesu alikufa lini?

     Yesu alikufa “saa tisa” alasiri siku ya Pasaka ya Wayahudi, yaani, saa ya tisa tangu mapambazuko. (Marko 15:33-37.) Tarehe hiyo inalingana na Ijumaa, Aprili 1, 33 W.K., kulingana na kalenda za kisasa.

  •   Yesu alifia wapi?

     Yesu aliuawa mahali “panapoitwa Mahali pa Fuvu la Kichwa, panapoitwa Golgotha katika Kiebrania.” (Yohana 19:17, 18) Katika siku za Yesu, eneo hilo lilikuwa “nje ya lango” la Yerusalemu. (Waebrania 13:12) Huenda lilikuwa kwenye kilima, kwa kuwa Biblia inasema kwamba wengine walitazama kuuawa kwa Yesu “wakiwa mbali.” (Marko 15:40) Hata hivyo, leo eneo la Golgotha haliwezi kusemwa kihalisi lilikuwa wapi.

  •   Yesu alikufa jinsi gani?

     Ingawa watu wengi wanaamini kwamba Yesu alisulubiwa, yaani, aliuawa kwenye msalaba, Biblia inasema hivi: “Yeye mwenyewe alizichukua dhambi zetu katika mwili wake juu ya mti.” (1 Petro 2:​24, Union Version) Waandikaji wa Biblia walitumia maneno mawili ya Kigiriki kurejelea vifaa vilivyotumika katika kifo cha Yesu​—stau·rosʹ na xyʹlon. Wasomi wengi wamefikia mkataa kwamba maneno hayo yanawakilisha nguzo au mti ulionyooka na kufanyizwa kwa kipande kimoja tu cha mbao.

  •   Kifo cha Yesu kinapaswa kukumbukwa jinsi gani?

     Usiku wa Pasaka ya kila mwaka ya Kiyahudi, Yesu alianzisha mwadhimisho usiohusisha mambo mengi akiwa na wafuasi wake na kuwaamuru hivi: “Endeleeni kufanya hivi kwa kunikumbuka mimi.” (1 Wakorintho 11:24) Saa kadhaa baadaye, Yesu aliuawa.

     Waandikaji wa Biblia walimlinganisha Yesu na mwana-kondoo aliyetolewa dhabihu siku ya Pasaka. (1 Wakorintho 5:7) Kama tu mwadhimisho wa Pasaka ulivyowakumbusha Waisraeli kwamba walikuwa wamekombolewa kutoka utumwani, vivyo hivyo Ukumbusho wa kifo cha Yesu Kristo unawakumbusha Wakristo kwamba wamekombolewa kutoka katika dhambi na kifo. Pasaka ilikuwa sherehe iliyofanywa mara moja kwa mwaka, siku ya Nisani 14 kulingana na kalenda ya Kiyahudi; vivyo hivyo Wakristo wa mapema walifanya Ukumbusho mara moja kila mwaka.

     Kila mwaka, kwenye tarehe inayolingana na Nisani 14, mamilioni ya watu ulimwenguni pote wanaadhimisha kifo cha Yesu.