Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Mungu Humpenda Mtoaji Mchangamfu”

“Mungu Humpenda Mtoaji Mchangamfu”

“Mungu Humpenda Mtoaji Mchangamfu”

TANGU zamani kutoa zawadi kumekuwa sehemu muhimu ya maisha ya kila siku. Mara nyingi watu walitoa zawadi ili wapate kitu walichotaka. Yakobo alimpa Esau mifugo wengi kama zawadi ili apate kibali cha ndugu yake. (Mwanzo 32:13-18; 33:8) Sababu ya Yakobo kusisitiza kwamba Esau akubali zawadi hiyo inaweza kueleweka tunapokumbuka kwamba kulingana na desturi za Mashariki, kukataa kukubali zawadi kulionyesha kwamba mtu hangepata kibali. (Mwanzo 33:10) Pia, ili wapate kibali cha mkuu wa Misri aliyekuwa akitoa chakula (ambaye alikuwa Yosefu ndugu yao), wana wa Yakobo walifuata pendekezo la baba yao la kupeleka zawadi ya mali bora zaidi ya nchi. (Mwanzo 42:30; 43:11, 25, 26) Mfalme Asa alimtumia Ben-hadadi zawadi ya fedha na dhahabu ili amfanye avunje agano lake na Baasha, mfalme wa Israeli.—1 Wafalme 15:18, 19.

Kitabu cha Methali kinasema hivi kuhusu faida ambazo mpaji anapata: “Zawadi ya mwanadamu itamfungulia nafasi kubwa, nayo itamwongoza hata mbele ya watu wakuu.” (Methali 18:16) Zawadi inaweza kupunguza hasira, lakini haiwezi kupunguza hasira ya mtu dhidi ya mtu aliyefanya uzinzi na mke wake, hata mzinzi huyo akimpa zawadi kubwa namna gani.—Methali 21:14; 6:32-35.

Zawadi Zilizotolewa Kwenye Patakatifu

Mungu aliwatoa Walawi kama zawadi kwa ajili ya nyumba ya Haruni, ili waendeleze utumishi wa patakatifu. (Hesabu 18:6, 7) Pia, Wagibeoni na wengi waliofanywa kuwa watumishi wa patakatifu waliitwa Wanethini, jina linalomaanisha “Waliokabidhiwa.” (Yoshua 9:27; 1 Mambo ya Nyakati 9:2; Ezra 8:20) Vivyo hivyo, michango iliyotolewa ili kuendeleza utumishi katika patakatifu na pia dhabihu zilizotolewa ziliitwa zawadi.—Kutoka 28:38; Mambo ya Walawi 23:37, 38; Hesabu 18:29; Mathayo 5:23, 24; Luka 21:1.

Kwa sababu yeye ni Muumba, Yehova ana miliki kila kitu. Kwa hiyo, kwa kutoa vitu vya kimwili kwa ajili ya kuendeleza ibada ya kweli, mtoaji anamrudishia Yehova sehemu ya kile alichopokea kutoka kwa Mungu.—Zaburi 50:10; 1 Mambo ya Nyakati 29:14.

Himizo Kuhusu Zawadi

Kwa kuwa zawadi zinazotolewa ili kuhonga zinaweza kuharibu moyo na kupotosha haki, Maandiko yanatuhimiza tuchukie zawadi kama hizo. Wale wanaofuatilia sana zawadi wanashutumiwa. (Kumbukumbu la Torati 16:19, 20; Mhubiri 7:7; Methali 15:27; Isaya 1:23) Isitoshe, “mtu anayejisifu kwa uwongo juu ya zawadi,” lakini hatendi kulingana na kujisifu kwake, anafananishwa na mawingu ya mvuke na upepo bila mvua. (Methali 25:14) Mtu anayetoa zawadi anaweza kuwa na marafiki wengi, lakini zawadi zake haziwezi kumhakikishia urafiki wa kudumu.—Methali 19:6.

Maandiko ya Kigiriki ya Kikristo yanashutumu kwa uzito mazoea fulani yanayohusiana na kutoa zawadi. Yesu aliwashutumu waandishi na Mafarisayo kwa kupuuza amri ya kumheshimu baba na mama. Kulingana na maoni yao, ikiwa mtu angesema kwamba vitu vyake vya kimwili ni zawadi zilizotolewa kwa Mungu, hakuwa na wajibu wa kuvitumia kuwasaidia wazazi wake, ingawa yeye mwenyewe angeweza kuendelea kuvitumia. (Mathayo 15:1-6) Mtu anapotoa zawadi huku akitazamia kupata faida fulani hastahili sifa yoyote. (Luka 6:30-36; 14:12-14) Ili tumpendeze Yehova, tunapaswa kutoa zawadi bila ubinafsi na bila kujionyesha.—Mathayo 6:2-4; 1 Wakorintho 13:3.

Zawadi Zinazotolewa na Wakristo

Wakristo wa mapema walitoa zawadi, au michango, ili kuwasaidia ndugu zao waliokuwa na uhitaji. (Waroma 15:26; 1 Wakorintho 16:1, 2) Hata hivyo, zawadi hizo zote zilitolewa kwa hiari, kama inavyoonyeshwa na maneno haya ya Paulo: “Kila mmoja na afanye kama alivyoazimia moyoni mwake, si kwa kutopenda wala kwa kulazimishwa, kwa maana Mungu humpenda mtoaji mchangamfu.” (2 Wakorintho 9:7) Kwa kuongezea, waliwasaidia wale waliojitoa kabisa kwa ajili ya huduma ya Kikristo, kama vile mtume Paulo. Hata hivyo, ingawa alithamini sana zawadi alizopewa na ndugu zake, Paulo hakuomba zawadi.—Wafilipi 4:15-17.

Wakristo wanaweza kutoa zawadi zenye thamani zaidi kuliko vitu vya kimwili. Wanaweza kutoa wakati na uwezo wao ili kuwafundisha na kuwajenga wengine kiakili na kiroho, jambo linaloleta furaha nyingi. Zawadi kubwa zaidi ambayo mtu anaweza kumpa mwingine ni kumsaidia aelewe Neno la Mungu, kwa sababu kufanya hivyo kunaweza kumpa mtu uzima wa milele.—Yohana 6:26, 27; 17:3; Matendo 20:35; 2 Wakorintho 12:15; Ufunuo 22:17.