Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Je, Wajua?

Mungu alikuwa na maoni gani kuhusu unajimu katika taifa la Israeli?

Kulingana na kamusi moja, unajimu ni “elimu ya kuchunguza miendo ya sayari, jua, mwezi, na nyota na imani ya kwamba miendo ya vitu hivyo inaweza kuathiri maisha ya wanadamu.” Kila mwaka dunia inapozunguka jua, ni kana kwamba makundi ya nyota yanasonga pia. Tangu zamani, watu wameona mabadiliko hayo na kusema kwamba yana maana kubwa sana kwao.

Huenda unajimu ulianzishwa na Wababiloni wa kale ambao waliabudu nyota na makundi ya nyota. Waisraeli walianza kuabudu nyota walipoiacha ibada ya kweli. Kufikia wakati wa utawala wa Mfalme Yosia wa Yuda, watu wengi sana walikuwa wakifanya unajimu. Maoni ya Mungu kuhusu jambo hilo yalikuwa wazi. Karne nyingi mapema, Sheria ya Musa ilikuwa imekataza ibada ya nyota, na yeyote ambaye aliabudu nyota angeuawa.—Kumbukumbu la Torati 17:2-5.

Kati ya hatua ambazo Mfalme Yosia alichukua ili kubadili mazoea ya kidini ya watu wa Yuda ni kupiga marufuku dhabihu zilizotolewa “kwa jua na kwa mwezi na kwa makundi-nyota ya unajimu na kwa jeshi lote la mbinguni.” Simulizi hilo la Biblia linaonyesha kwamba mfalme huyo alichukua hatua hiyo kwa sababu alitaka “kutembea kwa kumfuata Yehova na kushika amri zake.” (2 Wafalme 23:3-5) Leo, hilo linawawekea kielelezo watu ambao wanataka kumwabudu Mungu “kwa roho na kweli.”—Yohana 4:24.

“Wana wa Zeu” ambao wanatajwa katika Matendo 28:11 walikuwa nani?

Kitabu cha Biblia cha Matendo kinasema kwamba mtume Paulo alipokuwa akielekea Roma, alisafiri kutoka Malta hadi Puteoli kwa mashua iliyokuwa na sanamu ya gubeti ya “Wana wa Zeu.” (Matendo 28:11) Sanamu hizo za “Wana wa Zeu” zilitumiwa sana na mabaharia na wasafiri wa kale.

Kulingana na hadithi za Wagiriki na Waroma, Zeu (anayejulikana pia kama Sumbula) na Leda walikuwa na wana mapacha, walioitwa Castor na Pollux. Hao “Wana wa Zeu” walionwa kuwa mabaharia stadi waliokuwa na uwezo wa kudhibiti upepo na mawimbi. Hivyo, waliabudiwa kama miungu iliyowalinda mabaharia. Mabaharia waliwatolea dhabihu na kuwaomba wawalinde wakati wa dhoruba. Iliaminiwa kwamba miungu hiyo pacha ilionyesha nguvu zao za kulinda kupitia moto wa Mtakatifu Elmo. Nyakati nyingine moto huo ulionekana kwenye milingoti ya meli kulipokuwa na dhoruba.

Ibada ya Castor na Pollux ilikuwa imeenea sana kati ya Wagiriki na Waroma, na kitabu kimoja cha kale kinataja hasa ibada hiyo katika wilaya zilizozunguka Kirene, huko Afrika Kaskazini. Mashua inayotajwa katika kitabu cha Matendo ilikuwa imetoka karibu na eneo hilo, katika jiji la Aleksandria, huko Misri.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Jiwe la maandishi la Wababiloni likionyesha Mfalme Nazimarutashi akiwa na makundi ya nyota

[Picha katika ukurasa wa 9]

Sarufu ya Dinari yenye picha ya “Wana wa Zeu,” 114-113 K.W.K.

[Hisani ya Picha katika ukurasa wa 9]

Stela: Réunion des Musées Nationaux/Art Resource, NY; coin: Courtesy Classical Numismatic Group, Inc./cngcoins.com