Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Endeleeni Kukaza Akili Zenu juu ya Mambo Yaliyo Juu”

“Endeleeni Kukaza Akili Zenu juu ya Mambo Yaliyo Juu”

“Endeleeni kukaza akili zenu juu ya mambo yaliyo juu, si juu ya mambo yaliyo duniani.”—KOL. 3:2.

1, 2. (a) Ni nini kinachoonyesha kwamba kutaniko la Kolosai katika karne ya kwanza lilikuwa hatarini? (b) Ni shauri gani lililotolewa ili kuwasaidia ndugu wa Kolosai kubaki imara?

KUTANIKO la Kikristo la Kolosai katika karne ya kwanza lilikuwa hatarini! Baadhi ya washiriki wa kutaniko hilo walisababisha migawanyiko kwa kusema kwamba watu walipaswa kutii Sheria ya Musa. Wengine walikuwa wakieneza falsafa ya kipagani ya kwamba watu walipaswa kujinyima kabisa raha na anasa. Ili kupinga mafundisho hayo ya uwongo, mtume Paulo aliandika barua yenye kutia moyo, akiwaonya hivi Wakolosai: “Mjihadhari: labda kuna mtu ambaye atawachukua ninyi kama windo lake kupitia falsafa na udanganyifu mtupu kulingana na pokeo la wanadamu, kulingana na mambo ya msingi ya ulimwengu na si kulingana na Kristo.”—Kol. 2:8.

2 Ikiwa Wakristo hao watiwa-mafuta wangekaza akili zao juu ya “mambo ya msingi ya ulimwengu,” basi wangekuwa wakipuuza uandalizi wa Yehova wa wokovu. (Kol. 2:20-23) Ili kuwasaidia walinde uhusiano wao wenye thamani pamoja na Mungu, Paulo aliwahimiza hivi: “Endeleeni kukaza akili zenu juu ya mambo yaliyo juu, si juu ya mambo yaliyo duniani.” (Kol. 3:2) Naam, ndugu za Kristo walipaswa kukaza akili zao juu ya tumaini lao la kupokea  urithi usioharibika ‘lililowekwa akiba kwa ajili yao mbinguni.’—Kol. 1:4, 5.

3. (a) Wakristo watiwa-mafuta hukaza akili zao juu ya tumaini gani? (b) Tutachunguza maswali gani katika makala hii?

3 Leo, Wakristo watiwa-mafuta pia hukaza akili zao juu ya Ufalme wa mbinguni wa Mungu na juu ya tumaini lao la kuwa “warithi pamoja na Kristo.” (Rom. 8:14-17) Lakini namna gani wale walio na tumaini la kuishi duniani? Maneno ya Paulo yanawahusuje? “Kondoo wengine” wanawezaje kukaza akili zao juu ya “mambo yaliyo juu”? (Yoh. 10:16) Na sote tunawezaje kunufaika kwa kuchunguza mifano ya wanaume waaminifu wa kale kama Abrahamu na Musa, ambao licha ya matatizo ya kibinafsi, waliendelea kukaza akili zao juu ya mambo yaliyo juu?

KUKAZA AKILI JUU YA MAMBO YALIYO JUU HUMAANISHA NINI?

4. Kondoo wengine wanawezaje kukaza akili zao juu ya mambo yaliyo juu?

4 Ingawa kondoo wengine hawana tumaini la kuishi mbinguni, wao pia wanaweza kukaza akili zao juu ya mambo yaliyo juu. Jinsi gani? Kwa kumtanguliza Yehova Mungu na masilahi ya Ufalme maishani mwao. (Luka 10:25-27) Tunapofanya hivyo, tunamwiga Kristo, kielelezo chetu. (1 Pet. 2:21) Sawa na ndugu zetu katika karne ya kwanza, tunapambana na mawazo ya uwongo, falsafa za ulimwengu, na mitazamo ya kimwili katika mfumo wa mambo wa Shetani. (Soma 2 Wakorintho 10:5.) Tukiwa waigaji wa Yesu, tunahitaji kuwa macho na kujilinda dhidi ya mambo kama hayo yanayohatarisha hali yetu ya kiroho.

5. Tunawezaje kuchunguza maoni yetu kuhusu kufuatilia vitu vya kimwili?

5 Je, tumeathiriwa na maoni ya ulimwengu kuhusu kufuatilia vitu vya kimwili? Kwa kawaida mawazo na matendo yetu huonyesha mambo tunayopenda. Yesu alisema hivi: “Mahali ilipo hazina yako, ndipo moyo wako utakapokuwa pia.” (Mt. 6:21) Ili kujua moyo wetu unatuongoza wapi, ni vizuri kujichunguza mara kwa mara. Jiulize hivi: ‘Ninatumia muda mwingi kadiri gani kufikiria kuhusu pesa? Je, ninatumia muda mwingi sana kuhangaikia biashara, uwekezaji, au kujitahidi kuwa na maisha yenye starehe zaidi? Au je, ninajitahidi kudumisha jicho linalokazia mambo ya kiroho?’ (Mt. 6:22) Yesu alisema kwamba wale wanaoazimia “kujiwekea hazina duniani” huhatarisha sana hali yao ya kiroho.—Mt. 6:19, 20, 24.

6. Tunawezaje kushinda vita dhidi ya tamaa za mwili?

6 Mwili wetu usio mkamilifu hutuchochea kufuatilia tamaa za mwili. (Soma Waroma 7:21-25.) Tusipoongozwa na roho takatifu ya Mungu maishani mwetu, huenda tukanaswa na “matendo ya giza.” Matendo hayo yanaweza kutia ndani “karamu za kupindukia na vipindi vya kulewa . . . ngono isiyo halali na mwenendo mpotovu.” (Rom. 13:12, 13) Ili kushinda vita dhidi ya “mambo yaliyo duniani,” yaani, mambo yanayovutia mwili, ni lazima tukaze akili zetu juu ya mambo yaliyo juu. Jitihada zinahitajiwa ili kufanya hivyo. Ndiyo sababu mtume Paulo alisema hivi: “Naupigapiga mwili wangu na kuuongoza kama mtumwa.” (1 Kor. 9:27) Bila shaka, ikiwa tunataka kubaki katika shindano la mbio za uzima hatupaswi kujitendea kwa fadhili. Acheni tuchunguze mambo ambayo wanaume wawili waaminifu wa kale walifanya ili ‘kumpendeza Mungu vema.’—Ebr. 11:6.

ABRAHAMU “AKAWA NA IMANI KATIKA YEHOVA”

7, 8. (a) Abrahamu na Sara walikabili matatizo gani? (b) Abrahamu alikaza akili yake juu ya nini?

7 Yehova alipomwagiza Abrahamu aihamishe familia yake hadi nchi ya Kanaani,  alitii kwa hiari. Kwa sababu ya imani na utii wa Abrahamu, Yehova alifanya agano pamoja naye akisema hivi: “Nitafanya taifa kubwa kutokana nawe, nitakubariki.” (Mwa. 12:2) Hata hivyo, miaka mingi baadaye, bado Abrahamu na mke wake, Sara, hawakuwa na mtoto. Je, Yehova alikuwa amesahau ahadi aliyompa Abrahamu? Isitoshe, maisha hayakuwa rahisi huko Kanaani. Abrahamu na familia yake waliacha nyumba yao na watu wao wa ukoo katika jiji lenye ufanisi la Uru, kule Mesopotamia. Walisafiri umbali wa kilomita zaidi ya 1,600 ili kufika Kanaani, ambako waliishi katika mahema, wakavumilia njaa kali, na kukabili waporaji. (Mwa. 12:5, 10; 13:18; 14:10-16) Hata hivyo, hawakutamani kamwe kurudi Uru kuishi maisha ya starehe!—Soma Waebrania 11:8-12, 15.

8 Badala ya kukaza akili juu ya “mambo yaliyo duniani,” Abrahamu “akawa na imani katika Yehova.” (Mwa. 15:6) Naam, alikaza akili zake juu ya mambo yaliyo juu kwa kukazia fikira ahadi za Mungu. Matokeo ni kwamba Abrahamu alithawabishwa kwa sababu ya imani yake. Mungu Aliye Juu Zaidi alimtokea na kumwambia hivi: “‘Tafadhali, tazama juu mbinguni uzihesabu nyota, ikiwa unaweza kuzihesabu.’ Naye akaendelea kumwambia: ‘Ndivyo utakavyokuwa uzao wako.’” (Mwa. 15:5) Bila shaka hilo lilimtia moyo sana! Kila mara Abrahamu alipotazama mbingu zenye nyota, angekumbuka ahadi ya kwamba Yehova angezidisha uzao wake. Na wakati wa Mungu ulipofika, Abrahamu alizaa mrithi, kama alivyoahidiwa.—Mwa. 21:1, 2.

9. Kuiga mfano wa Abrahamu kutatuchocheaje kumtumikia Mungu kwa bidii zaidi?

9 Sawa na Abrahamu, sisi pia tunangojea utimizo wa ahadi za Mungu. (2 Pet. 3:13) Tusipokaza akili zetu juu ya mambo yaliyo juu, tunaweza kuanza kuona kwamba ahadi hizo zinakawia na hivyo kupunguza bidii yetu katika utendaji wa kiroho. Kwa mfano, je, ulijidhabihu zamani ili kufanya upainia au kushiriki katika utumishi mwingine wa pekee? Ikiwa ndivyo, unastahili pongezi. Namna gani sasa? Kumbuka kwamba Abrahamu alikaza akili yake juu ya “jiji lililo na misingi ya kweli.” (Ebr. 11:10) “Alionyesha imani katika Yehova, na hilo likahesabiwa kwake kuwa ni uadilifu.”—Rom. 4:3.

MUSA ALIMWONA “YEYE ASIYEONEKANA”

10. Musa alikuwa na maisha gani akiwa kijana?

10 Musa pia alikaza akili yake juu ya mambo yaliyo juu. Akiwa kijana, ‘alifundishwa hekima yote ya Wamisri.’ Hiyo haikuwa elimu ya kawaida. Musa aliishi na familia ya Farao wakati ambapo Misri ilikuwa serikali kuu zaidi ulimwenguni. Kwa kuwa Musa alipata elimu hiyo ya juu, haishangazi kwamba alikuwa “mwenye nguvu katika maneno na matendo.” (Mdo. 7:22) Hebu wazia fursa nyingi alizokuwa nazo za kuwa mashuhuri! Hata hivyo, Musa alikaza akili yake juu ya mambo ya juu zaidi—kufanya mapenzi ya Mungu.

11, 12. Musa alithamini sana elimu gani, na tunajuaje?

11 Ni wazi kwamba Musa alipokuwa mtoto alifundishwa na Yokebedi, mama yake, kuhusu Mungu wa Waebrania. Musa alithamini sana ujuzi juu ya Yehova na kuuona kuwa wenye thamani zaidi kuliko utajiri wowote ule. Kwa hiyo, aliacha fursa na mapendeleo ambayo inaelekea angepata kwa sababu ya kuishi na familia ya Farao. (Soma Waebrania 11:24-27.) Bila shaka, elimu ya kiroho na imani ya Musa katika Yehova ilimchochea kukaza akili yake juu ya mambo yaliyo juu.

 12 Ingawa Musa alipata elimu bora zaidi ya kilimwengu wakati huo, je, aliitumia kupata kazi bora nchini Misri, kupata umaarufu, au kupata vitu vya kimwili? Hakufanya hivyo. Ikiwa angefanya hivyo, ‘hangekataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, na hangechagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu. Angefurahia dhambi kwa muda.’ Ni wazi kwamba Musa alitumia elimu yake ya kiroho kuendeleza kusudi la Yehova.

13, 14. (a) Ni nini kilichomsaidia Musa kustahili mgawo ambao Yehova angempa? (b) Huenda tukahitaji kufanya nini kama Musa?

13 Musa alimpenda sana Yehova na watu Wake. Alipokuwa na umri wa miaka 40, Musa alifikiri kwamba yuko tayari kuwaweka huru watu wa Mungu kutoka utumwani nchini Misri. (Mdo. 7:23-25) Hata hivyo, kabla Yehova hajampa mgawo huo, Musa alihitaji kufanya jambo lingine. Alihitaji kusitawisha sifa kama vile unyenyekevu, subira, upole, na kujizuia. (Met. 15:33) Musa alihitaji mazoezi ambayo yangemtayarisha kuvumilia majaribu na magumu ambayo angekabili baadaye. Kuwa mchungaji kwa miaka 40 kungempa mazoezi aliyohitaji ili kusitawisha sifa hizo zinazompendeza Mungu.

14 Je, Musa alijifunza kutokana na mazoezi aliyopata akiwa mchungaji? Bila shaka! Neno la Mungu linasema kwamba baadaye Musa alikuwa “mpole zaidi kuliko watu wote waliokuwa juu ya uso wa nchi.” (Hes. 12:3) Alisitawisha unyenyekevu uliomsaidia kushughulika kwa subira na watu mbalimbali na kushughulikia matatizo yao magumu. (Kut. 18:26) Sisi pia huenda tukahitaji kusitawisha sifa za kiroho zitakazotusaidia kuokoka “dhiki kuu” na kuingia katika ulimwengu mpya wa Mungu wenye uadilifu. (Ufu. 7:14) Je, tunaelewana na wengine, kutia ndani wale tunaofikiri wanakasirika au kuudhika upesi sana? Tunahitaji kutii maneno ya mtume Petro, aliyewahimiza hivi waamini wenzake: “Waheshimuni watu wa namna zote, upendeni ushirika mzima wa akina ndugu.”—1 Pet. 2:17.

KUENDELEA KUKAZA AKILI ZETU JUU YA MAMBO YALIYO JUU

15, 16. (a) Kwa nini ni muhimu kuendelea kukaza akili zetu juu ya mambo yanayofaa? (b) Kwa nini ni muhimu kwa Wakristo kudumisha mwenendo mzuri?

15 Tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.” (2 Tim. 3:1) Kwa hiyo, ili tuendelee kuwa macho kiroho, ni lazima tuendelee kukaza akili zetu juu ya mambo yanayofaa. (1 The. 5:6-9) Fikiria jinsi tunavyoweza kufanya hivyo katika sehemu tatu za maisha yetu.

16 Mwenendo wetu: Petro alitambua umuhimu wa kuwa na mwenendo mzuri. Alisema hivi: ‘Dumisheni mwenendo wenu ukiwa mzuri katikati ya mataifa, ili likiwa tokeo la matendo yenu mazuri ambayo wameshuhudia kwa macho, wamtukuze Mungu.’ (1 Pet. 2:12) Tuwe nyumbani, kazini, shuleni, michezoni, au katika huduma, tunajitahidi kabisa kumtukuza Yehova kupitia mwenendo wetu mzuri. Ni kweli kwamba tukiwa wanadamu wasio wakamilifu, sote hukosea. (Rom. 3:23) Hata hivyo, tukiendelea ‘kupigana pigano zuri la imani,’ tunaweza kufanikiwa kushinda vita dhidi ya mwili wetu wenye dhambi.—1 Tim. 6:12.

17. Tunawezaje kuiga mtazamo wa akili ambao Kristo Yesu alikuwa nao? (Tazama picha kwenye ukurasa wa 28.)

17 Mtazamo wetu: Kudumisha mwenendo mzuri kunahusiana sana na kuwa na mtazamo unaofaa. Mtume Paulo alisema hivi: “Iweni na mtazamo huu wa akili ndani yenu ambao ulikuwa pia ndani ya Kristo Yesu.” (Flp. 2:5) Yesu alikuwa na  mtazamo wa aina gani? Alikuwa mnyenyekevu. Unyenyekevu ulimchochea kujidhabihu katika huduma yake. Jambo kuu akilini mwa Yesu lilikuwa kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu. (Marko 1:38; 13:10) Yesu alitegemea kikamili Neno la Mungu kufanya maamuzi. (Yoh. 7:16; 8:28) Alijifunza kwa bidii Maandiko Matakatifu ili aweze kuyanukuu, kuyatetea, na kuyafafanua. Tukiwa wanyenyekevu, tukihubiri na kujifunza Biblia kibinafsi kwa bidii, tutasitawisha zaidi akili kama ya Kristo.

Jambo kuu akilini mwa Yesu lilikuwa kuwahubiria wengine habari njema ya Ufalme wa Mungu (Tazama fungu la 17)

18. Tunaweza kuunga mkono kazi ya Yehova katika njia gani muhimu?

18 Kuunga mkono huduma: Yehova amekusudia kwamba “katika jina la Yesu kila goti lipigwe la wale walio mbinguni na wale walio duniani na wale walio chini ya nchi.” (Flp. 2:9-11) Ingawa Yesu ana cheo kilichokwezwa, anajitiisha kwa unyenyekevu ili kufanya mapenzi ya Baba yake, na tunapaswa kufanya vivyo hivyo. (1 Kor. 15:28) Jinsi gani? Kwa kuunga mkono kwa moyo wote kazi ambayo tumeagizwa tufanye, kazi ya ‘kufanya wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote.’ (Mt. 28:19) Pia, tunapaswa ‘kuwatendea wote mema,’ jirani na ndugu zetu.—Gal. 6:10.

19. Tunapaswa kuazimia kufanya nini?

19 Tunathamini kama nini kwamba Yehova hutukumbusha tuendelee kukaza akili zetu juu ya mambo yaliyo juu! Kwa hiyo, tunahitaji ‘kukimbia kwa uvumilivu shindano la mbio lililowekwa mbele yetu.’ (Ebr. 12:1) Sote na tufanye kazi “kwa nafsi yote kama kwa Yehova,” na Baba yetu wa mbinguni atatuthawabisha kwa sababu ya jitihada zetu za moyo wote.—Kol. 3:23, 24.