Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 SIMULIZI LA MAISHA

Matukio Muhimu Katika Maisha Yangu Nikiwa Mhubiri wa Ufalme

Matukio Muhimu Katika Maisha Yangu Nikiwa Mhubiri wa Ufalme

Mwaka wa 1947, makasisi Wakatoliki huko Santa Ana, El Salvador, walijaribu kuchochea vurugu kuelekea Mashahidi. Ndugu walipokuwa kwenye Funzo la Mnara wa Mlinzi la kila juma, wavulana walirusha mawe makubwa ndani ya nyumba ya wamishonari. Kisha, makasisi wakaongoza maandamano dhidi ya Mashahidi. Baadhi ya waandamanaji walibeba mienge na wengine walibeba sanamu. Kwa muda wa saa mbili, walirusha mawe na kupaaza sauti hivi: “Bikira na aishi milele!” na, “Yehova na afe!” Walifanya hivyo ili kuwatisha wamishonari waondoke mjini. Ninafahamu jambo hilo kwa sababu nilikuwa miongoni mwa wamishonari hao, na nilihudhuria mkutano huo miaka 67 iliyopita. *

MIAKA miwili kabla ya tukio hilo, nilihitimu katika darasa la nne la Shule ya Gileadi iliyofanyiwa karibu na mji wa Ithaca, New York, pamoja na Evelyn Trabert, mmishonari mwenzangu. Tulipewa mgawo wa kutumika huko Santa Ana. Lakini kabla ya kusimulia kuhusu utumishi wangu wa umishonari wa karibu miaka 29, acheni niwaeleze kwa nini niliamua kuingia katika utumishi huo.

URITHI WANGU WA KIROHO

Nilipozaliwa mwaka wa 1923, wazazi wangu, John na Eva Olson, walikuwa wakiishi Spokane, Washington, Marekani. Walikuwa Walutheri lakini hawakukubali fundisho la moto wa mateso kwa kuwa halikupatana na imani yao kwamba Mungu ni upendo. (1 Yoh. 4:8) Baba alifanya kazi ya kuoka mikate, na usiku mmoja mfanyakazi mwenzake alimhakikishia kuwa Biblia haifundishi kuhusu moto wa mateso. Muda mfupi baadaye, wazazi wangu walianza kujifunza na Mashahidi wa Yehova na wakaelewa jambo ambalo Biblia inafundisha hasa kuhusu uhai baada ya kifo.

Nilikuwa na umri wa miaka tisa tu, lakini ninakumbuka nikiwasikia wazazi wangu wakieleza kwa msisimko kuhusu kweli mpya za Biblia walizojifunza. Walisisimka hata zaidi walipojua jina la Mungu wa kweli, Yehova, na kuwekwa huru kutokana na fundisho la Utatu lisiloeleweka. Kama sifongo,  nilianza kufyonza mafundisho hayo mazuri sana ya Kimaandiko nilipokuwa nikijifunza ‘kweli inayomweka mtu huru.’ (Yoh. 8:32) Sikuzote nimefurahia kulichunguza Neno la Mungu na hivyo funzo la Biblia halikunichosha kamwe. Ingawa nilikuwa mwenye haya, niliandamana na wazazi wangu katika kazi ya kuhubiri. Walibatizwa mwaka wa 1934. Nami nikabatizwa mwaka wa 1939 nikiwa na umri wa miaka 16, na kuwa pia mtumishi wa Yehova.

Nikiwa na Mama na Baba kwenye kusanyiko huko St. Louis, Missouri, mwaka wa 1941

Katika kiangazi cha mwaka wa 1940, wazazi wangu waliuza nyumba yao, na sote watatu tukaanza utumishi wa wakati wote tukiwa mapainia huko Coeur d’Alene, Idaho. Tuliishi katika nyumba ya kukodi iliyokuwa juu ya gereji. Nyumba yetu ilitumiwa pia kufanyia mikutano. Wakati huo, makutaniko machache yalikuwa na Majumba ya Ufalme, hivyo yalikutana katika nyumba za watu au vyumba vya kukodi.

Mwaka wa 1941, mimi na wazazi wangu tulihudhuria kusanyiko huko St. Louis, Missouri. Jumapili ilikuwa “Siku ya Watoto,” na watoto wote wenye umri wa kati ya miaka 5 na 18 waliketi mbele ya jukwaa. Alipokuwa akimalizia hotuba yake, Ndugu Joseph F. Rutherford alituambia hivi sisi watoto: “Ninyi nyote . . . watoto . . . ambao mmekubali kumtii Mungu na Mfalme wake, tafadhali simameni!” Sote tukasimama. Kisha, Ndugu Rutherford akasema hivi: “Tazama, mashahidi wapya wa Ufalme zaidi ya 15,000!” Tukio hilo liliimarisha azimio langu la kutumia maisha yangu kufanya upainia.

MIGAWO YA FAMILIA YETU

Miezi michache baada ya kusanyiko la St. Louis, familia yetu ilihamia kusini mwa California. Tulikuwa na mgawo wa kuanzisha kutaniko katika jiji la Oxnard. Tuliishi katika trela ndogo yenye kitanda kimoja tu. Kila usiku, meza ya chakula iligeuzwa kuwa “kitanda” changu na hilo lilikuwa badiliko kubwa kwa kuwa nilizoea kulala katika chumba changu mwenyewe!

Muda mfupi kabla hatujawasili California, Desemba 7, 1941, Japani ilishambulia Pearl Harbor huko Hawaii. Siku iliyofuata, Marekani iliingia katika Vita vya Pili vya Ulimwengu. Wenye mamlaka waliamuru taa zizimwe, na tulikuwa tukizima taa zote usiku. Nyambizi za Japani zilikuwa zikifanya doria kwenye ufuo wa California, na giza lilizuia maadui kushambulia sehemu hususa katika nchi kavu.

Baada ya miezi kadhaa, mnamo Septemba 1942, tulihudhuria Kusanyiko la Kitheokrasi la Ulimwengu Mpya huko Cleveland, Ohio. Katika kusanyiko hilo tulimsikiliza Ndugu Nathan H. Knorr alipokuwa akitoa hotuba yenye kichwa “Amani—Je, Inaweza Kudumu?” Alizungumzia andiko la Ufunuo sura ya 17, linalomtaja “mnyama-mwitu” ambaye “alikuwako, lakini hayuko, na bado yuko karibu kupanda kutoka katika abiso.” (Ufu. 17:8, 11) Ndugu Knorr alieleza kwamba “yule mnyama-mwitu” alikuwa Ushirika wa Mataifa ulioacha kutenda mwaka wa 1939. Biblia ilitabiri kwamba shirika lingine lingechukua mahali pa Ushirika wa Mataifa, na hivyo kungekuwa na kipindi cha amani ya kadiri. Na hivyo ndivyo ilivyokuwa, Vita vya Pili vya Ulimwengu viliisha katika mwaka wa 1945. Baada ya hapo, “mnyama” huyo aliibuka tena akiwa Umoja wa Mataifa. Wakati huo, Mashahidi wa Yehova walipanua kazi yao ya kuhubiri ulimwenguni pote, na tangu wakati huo kumekuwa na ongezeko kubwa kama nini!

Cheti changu cha Gileadi

 Unabii huo ulinisaidia kuelewa matukio ya wakati ujao. Ilipotangazwa kwamba Shule ya Gileadi ingeanza mwaka ufuatao, nilianza kutamani kuwa mmishonari. Mwaka wa 1943, nilipata mgawo wa kuwa painia huko Portland, Oregon. Siku hizo, tulitumia rekodi za gramafoni kuwahubiria wenye nyumba milangoni, na kisha tuliwapa machapisho ya Biblia yaliyozungumzia Ufalme wa Mungu. Mwaka huo wote, niliendelea kufikiria kuhusu utumishi wa umishonari.

Mwaka wa 1944, nilisisimka sana kupokea mwaliko wa kwenda Gileadi pamoja na rafiki yangu mpendwa Evelyn Trabert. Kwa miezi mitano, walimu wetu walitufundisha jinsi ya kupata shangwe tunapojifunza Biblia. Unyenyekevu wao ulituvutia. Nyakati nyingine, ndugu hao walituhudumia tulipokuwa tukila chakula. Tulihitimu Januari 22, 1945.

MGAWO WANGU WA UMISHONARI

Mimi na Evelyn, pamoja na Leo na Esther Mahan, tuliwasili kwenye mgawo wetu nchini El Salvador mnamo Juni 1946. Tulipata shamba hilo likiwa ‘jeupe kwa ajili ya kuvunwa.’ (Yoh. 4:35) Tukio nililotaja mwanzoni mwa simulizi hili linaonyesha jinsi makasisi walivyokasirika. Juma moja tu mapema, tulikuwa tumefanya kusanyiko letu la mzunguko la kwanza huko Santa Ana. Tulitangaza kotekote hotuba ya watu wote na tulifurahi sana watu karibu 500 walipohudhuria. Badala ya kuogopa na kuondoka mjini, tuliazimia hata zaidi kubaki na kuwasaidia watu wenye mioyo minyoofu. Ingawa makasisi walikuwa wamewaonya watu wasisome Biblia na ni wachache walioweza kuinunua, wengi walikuwa na njaa ya kupata kweli. Walithamini jitihada zetu za kujifunza Kihispania ili tuweze kuwafundisha kuhusu Mungu wa kweli, Yehova, na kuhusu ahadi yake nzuri sana ya kurudisha Paradiso duniani.

Wanafunzi watano wa darasa letu la Gileadi waliotumwa nchini El Salvador. Kushoto kwenda kulia: Evelyn Trabert, Millie Brashier, Esther Mahan, mimi, na Leo Mahan

Rosa Ascencio alikuwa kati ya wanafunzi wangu wa kwanza. Alipoanza kujifunza Biblia, alimwacha mwanamume aliyekuwa akiishi naye. Kisha, mwanamume huyo akaanza kujifunza Biblia. Walifunga ndoa, wakabatizwa, na kuwa Mashahidi wa Yehova wenye bidii. Rosa ndiye aliyekuwa painia wa kwanza mwenyeji huko Santa Ana. *

Rosa alikuwa na duka dogo. Alifunga duka lake alipoenda kuhubiri akitumaini kwamba Yehova angemwandalia mahitaji yake. Alipofungua duka lake baada ya saa chache, wateja walikuja kwa wingi. Alijionea ukweli wa andiko la Mathayo 6:33 na alibaki mwaminifu mpaka alipokufa.

Pindi fulani, kasisi mmoja alimtembelea mwanamume aliyemiliki nyumba tuliyokodi tukiwa wamishonari sita, na kumwonya kwamba ikiwa hatatufukuza, yeye na mke wake watafukuzwa kanisani. Mwanamume huyo aliyekuwa pia mfanyabiashara maarufu, alikuwa amechukizwa na tabia ya makasisi na hivyo hakutufukuza. Hata alimwambia kasisi huyo kwamba haogopi kufukuzwa kanisani. Mwanaume huyo alituhakikishia kwamba tungeweza kuendelea kuishi hapo kwa muda tuliotaka.

 RAIA ANAYEHESHIMIKA AWA SHAHIDI

Ofisi ya Tawi iliyojengwa mwaka 1955

Katika mji mkuu, San Salvador, dada mwingine mmishonari alikuwa akijifunza Biblia na mke wa injinia aitwaye Baltasar Perla. Mwanaume huyo mwenye moyo mzuri aliacha kumwamini Mungu kwa sababu ya unafiki wa viongozi wa kidini. Wakati ulipofika wa kujenga ofisi ya tawi, Baltasar hakuwa katika kweli lakini alijitolea kuchora ramani ya ofisi hiyo na kuijenga bila malipo.

Baada ya kushirikiana na watu wa Yehova katika ujenzi huo, Baltasar alisadiki kwamba alikuwa amepata dini ya kweli. Alibatizwa Julai 22, 1955, na muda mfupi baadaye, mkewe, Paulina, akabatizwa. Watoto wao wawili wanamtumikia Yehova kwa uaminifu. Mwanaye, Baltasar, Jr., ametumika katika Betheli ya Brooklyn kwa miaka 49, ambako anategemeza kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote inayoendelea kupanuka, na sasa ni mshiriki wa Halmashauri ya Tawi ya Marekani. *

Tulipoanza kufanya makusanyiko huko San Salvador, Ndugu Perla alitusaidia kupata ukumbi mkubwa wa michezo. Mwanzoni, tulitumia viti vichache tu katika ukumbi huo; lakini kwa baraka za Yehova, tuliendelea kuongezeka kila mwaka na kuujaza ukumbi huo hivi kwamba haukututosha tena! Katika makusanyiko hayo yenye shangwe, nilikutana na wanafunzi wangu wa zamani wa Biblia. Hebu wazia jinsi nilivyohisi wakati wanafunzi hao waliponitambulisha kwa “wajukuu” wangu, yaani, wanafunzi wao waliobatizwa karibuni!

Ndugu F. W. Franz akiwahutubia wamishonari kusanyikoni

Katika kusanyiko moja, ndugu fulani alinifikia na kuniambia kwamba angependa kuungama. Sikumtambua na nilishangaa kwa nini alisema hivyo. Alisema hivi: “Nilikuwa pamoja na wavulana waliowarushia mawe kule Santa Ana.” Sasa alikuwa mtumishi mwenzangu wa Yehova! Moyo wangu ulijaa shangwe. Mazungumzo hayo yalinithibitishia kwamba hakuna kazi yenye kuthawabisha kuliko utumishi wa wakati wote.

Kusanyiko la kwanza la mzunguko tulilohudhuria nchini El Salvador

MAAMUZI YANAYORIDHISHA

Kwa karibu miaka 29, niliendelea na kazi ya umishonari nchini El Salvador, kwanza katika jiji  la Santa Ana, kisha Sonsonate, Santa Tecla, na mwishowe San Salvador. Mwaka wa 1975, baada ya kutafakari na kusali sana, niliamua kuacha mgawo wangu wa umishonari na kurudi Spokane. Wazazi wangu waaminifu waliozeeka walihitaji msaada wangu.

Baada ya Baba kufa mwaka wa 1979, nilimtunza Mama kwa kuwa afya yake iliendelea kuzorota. Aliishi miaka minane zaidi, kisha akafa akiwa na umri wa miaka 94. Katika wakati huo mgumu, nilichoka sana kimwili na kihisia. Mkazo huo wa kihisia ulisababisha malengelenge yenye maumivu makali. Hata hivyo, niliweza kuvumilia jaribu hilo kupitia sala na utegemezo wa upendo kutoka kwa Yehova. Ni kama Yehova alivyosema, ‘hata wakati wa kichwa chenye mvi, mimi mwenyewe nitakuchukua na kukubeba na kukuponyosha.’—Isa. 46:4

Mwaka wa 1990, nilihamia Omak, Washington. Nikiwa huko nilitumikia tena kwenye eneo la lugha ya Kihispania, na wanafunzi wangu kadhaa wa Biblia walibatizwa. Kufikia Novemba 2007, singeweza kuitunza nyumba yangu huko Omak, hivyo nilihamia kwenye nyumba ya kupanga karibu na mji wa Chelan, Washington. Ninathamini sana kwamba kutaniko letu la Kihispania linanitunza vizuri. Kwa kuwa mimi peke yangu ndiye Shahidi aliyezeeka katika kutaniko letu, kwa fadhili ndugu na dada wananiona kuwa kama nyanya yao.

Hata ingawa niliamua kutoolewa na kutokuwa na familia ili niweze kushiriki kikamili zaidi katika huduma “bila kukengeushwa fikira,” nina watoto wengi wa kiroho. (1 Kor. 7:34, 35) Niliona kwamba katika maisha haya, siwezi kupata kila kitu. Kwa hiyo, nimetanguliza mambo yanayopaswa kutangulizwa—wakfu wangu wa kumtumikia Yehova kwa moyo wote. Katika ulimwengu mpya, kutakuwa na wakati mwingi wa kufurahia mambo ya kila aina yanayofaa. Andiko ninalopenda ni Zaburi 145:16, linalotuhakikishia kwamba Yehova ‘atatosheleza tamaa ya kila kitu kilicho hai.’

Utumishi wa upainia hunisaidia kuendelea kuwa kijana moyoni

Nina umri wa miaka 91, na bado nina afya nzuri kiasi, hivyo ninaendelea na upainia. Utumishi wa upainia hunisaidia kuendelea kuwa kijana moyoni na kuwa na kusudi maishani. Nilifika El Salvador kazi ya kuhubiri ilipokuwa ikianza. Licha ya upinzani wa Shetani usiokoma, sasa nchi hiyo ina wahubiri zaidi ya 39,000. Jambo hilo limeimarisha imani yangu kwelikweli. Bila shaka, ni wazi kwamba roho takatifu ya Yehova inategemeza jitihada za watu wake!

^ fu. 4 Tazama Kitabu cha Mwaka cha Mashahidi wa Yehova cha 1981, cha Kiingereza, ukurasa wa 45-46.

^ fu. 19 Kitabu cha Mwaka cha 1981, cha Kiingereza, ukurasa wa 41-42.

^ fu. 24 Kitabu cha Mwaka cha 1981, cha Kiingereza, ukurasa wa 66-67, na 74-75.