Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unamtegemea Mungu Kadiri Gani?

Unamtegemea Mungu Kadiri Gani?

Unamtegemea Mungu Kadiri Gani?

“Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme.”—MATHAYO 6:33.

1, 2. Kijana mmoja alichukua hatua gani kuhusiana na kazi ya kimwili, na kwa nini?

KIJANA mmoja alitaka kutumika zaidi kutanikoni. Tatizo lilikuwa kwamba kazi yake ya kimwili haikumruhusu kuhudhuria mikutano kwa ukawaida. Alishughulikiaje hali hiyo? Alirahisisha maisha yake, akaacha kazi hiyo, na baada ya muda akapata kazi nyingine ambayo haikuhitilafiana na utendaji wake wa Kikristo. Leo, anapata mshahara mdogo kuliko zamani, lakini bado anashughulikia mahitaji ya familia yake na anaweza kusaidia kutaniko.

2 Je, unaelewa ni kwa nini kijana huyo alichukua hatua hiyo? Je, unafikiri ungechukua hatua kama hiyo ikiwa ungekuwa katika hali yake? Inapendeza kwamba Wakristo wengi wamefanya hivyo, na matendo yao yanaonyesha kwamba wana uhakika katika ahadi hii ya Yesu: “Basi, endeleeni kuutafuta kwanza ufalme na uadilifu wake, nanyi mtaongezewa hivi vitu vingine vyote.” (Mathayo 6:33) Wanamtegemea Yehova awape usalama badala ya kuutegemea ulimwengu.—Methali 3:23, 26.

3. Kwa nini huenda watu fulani leo wakajiuliza ikiwa inafaa kuutanguliza Ufalme wa Mungu?

3 Kwa kuwa tunaishi katika wakati mgumu, huenda watu fulani wakashangaa ikiwa mwanamume huyo alifanya uamuzi wenye hekima. Leo, baadhi ya watu ni maskini sana, huku wengine wakifurahia maisha ya hali ya juu sana kupita wakati mwingine wowote katika historia. Watu wengi katika nchi maskini wangefurahia kupata kazi yoyote ili angalau waboreshe maisha yao. Kwa upande mwingine, watu wengi katika nchi zenye utajiri hukabili mikazo ya kudumisha viwango vya juu vya maisha kwa sababu ya uchumi usiotegemeka, mabadiliko kazini, na kwa sababu waajiri wao wanataka wafanye kazi kwa saa nyingi sana. Kwa sababu ya mikazo inayohusiana na kutafuta riziki, huenda wengine wakajiuliza, ‘Je, bado inawezekana kuutafuta kwanza Ufalme?’ Ili kupata jibu la swali hilo, fikiria watu ambao Yesu alikuwa akizungumza nao.

“Acheni Kuhangaika”

4, 5. Yesu alitoa mfano gani kuonyesha kwamba watu wa Mungu hawafai kuhangaika kupita kiasi kuhusu mahitaji ya kila siku?

4 Yesu alikuwa Galilaya, akizungumza na umati mkubwa wa watu kutoka sehemu mbalimbali. (Mathayo 4:25) Huenda ni wachache tu kati ya watu hao waliokuwa matajiri. Yaelekea wengi wao walikuwa maskini. Hata hivyo, Yesu aliwahimiza wasitangulize kutafuta utajiri wa kimwili bali wajiwekee akiba kitu fulani chenye thamani zaidi, yaani, hazina ya kiroho. (Mathayo 6:19-21, 24) Alisema hivi: “Acheni kuhangaika juu ya nafsi zenu kuhusu kile mtakachokula au kile mtakachokunywa, au juu ya miili yenu kuhusu kile mtakachovaa. Je, nafsi haimaanishi zaidi ya chakula na mwili zaidi ya mavazi?”—Mathayo 6:25.

5 Huenda wengi waliomsikiliza Yesu waliona kwamba haiwezekani kufanya yale aliyosema. Watu hao walijua kwamba wasipofanya kazi kwa bidii, familia zao zingeteseka. Lakini, Yesu aliwakumbusha kuhusu ndege. Ndege hutafuta chakula kila siku, hata hivyo Yehova huwajali. Yesu pia aliwakumbusha jinsi ambavyo Yehova huyatunza maua ya mwituni, ambayo yanapendeza hata kuliko jinsi Sulemani alivyokuwa katika utukufu wake wote. Ikiwa Yehova anawajali ndege na kuyatunza maua, je, hatatujali hata zaidi? (Mathayo 6:26-30) Kama vile Yesu alivyosema, uhai (nafsi) wetu na miili yetu ni muhimu zaidi kuliko chakula tunachonunua ili kuendeleza uhai wetu na ni muhimu kuliko mavazi tunayonunua ili kufunika miili yetu. Ikiwa tutajitahidi sana kujilisha na kujivika bila kutenga wakati wa kutosha kumtumikia Yehova, hatutakuwa na kusudi maishani.—Mhubiri 12:13.

Maoni Yenye Usawaziko

6. (a) Wakristo wana jukumu gani? (b) Wakristo humtegemea nani kabisa?

6 Bila shaka, Yesu hakuwatia moyo wasikilizaji wake waache kufanya kazi na kungojea Mungu azipe familia zao mahitaji ya lazima. Hata ndege hutafuta chakula kwa ajili yao na makinda yao. Hivyo, Wakristo walipaswa kufanya kazi ikiwa walitaka kula. Walipaswa kuandalia familia zao. Wakristo walioajiriwa kama watumishi au watumwa walipaswa kuwafanyia mabwana wao kazi kwa bidii. (2 Wathesalonike 3:10-12; 1 Timotheo 5:8; 1 Petro 2:18) Mara nyingi mtume Paulo alifanya kazi ya kutengeneza mahema ili kupata riziki. (Matendo 18:1-4; 1 Wathesalonike 2:9) Hata hivyo, Wakristo hao hawakutegemea kazi ya kimwili ili wawe salama. Walimtegemea Yehova. Hivyo, walifurahia amani ya moyoni ambayo wengi hawakuwa nayo. Mtunga-zaburi alisema hivi: “Wale wanaomtegemea Yehova ni kama Mlima Sayuni, ambao hauwezi kutikiswa, bali hukaa mpaka wakati usio na kipimo.”—Zaburi 125:1.

7. Huenda mtu asiyemtegemea Yehova kabisa akawa na maoni gani?

7 Yeyote asiyemtegemea Yehova kabisa huenda akafikiria kwa njia tofauti. Watu wengi huona utajiri kuwa njia kuu ya kuwa salama. Hivyo, wazazi wamewatia moyo watoto wao kutumia miaka mingi ya ujanani kufuatia elimu ya juu, wakitumaini kwamba itawasaidia kupata kazi zenye mshahara mnono. Kwa kusikitisha, familia kadhaa za Kikristo zimepata hasara kubwa kwa kutumia wakati na jitihada nyingi kwa ajili ya elimu ya juu huku watoto wao wakiacha kuzingatia mambo ya kiroho na kufuatia miradi ya kimwili.

8. Wakristo hudumisha usawaziko gani?

8 Hivyo, Wakristo wenye hekima hutambua kwamba shauri la Yesu ni muhimu leo kama lilivyokuwa katika karne ya kwanza, nao hujitahidi kuwa na usawaziko. Hata wakilazimika kutumia saa nyingi katika kazi ya kimwili ili kutimiza wajibu wao wa Kimaandiko, hawaruhusu kamwe uhitaji wa kupata pesa uwafanye wapuuze mambo muhimu ya kiroho.—Mhubiri 7:12.

“Msihangaike Kamwe”

9. Yesu anawapa uhakikisho gani wale wanaomtegemea Yehova kabisa?

9 Katika Mahubiri yake ya Mlimani, Yesu aliwahimiza wasikilizaji wake hivi: “Msihangaike kamwe na kusema, ‘Tutakula nini?’ au, ‘Tutakunywa nini?’ au, ‘Tutavaa nini?’ Kwa maana vyote hivi ndivyo vitu ambavyo mataifa yanafuatilia kwa tamaa. Kwa maana Baba yenu wa mbinguni anajua mnahitaji vitu hivi vyote.” (Mathayo 6:31, 32) Hayo ni maneno yenye kutia moyo kama nini! Tukimtegemea Yehova kabisa, sikuzote yeye atatutegemeza. Hata hivyo, maneno ya Yesu yanachochea fikira pia. Yanatukumbusha kwamba ikiwa tunafuatilia vitu vya kimwili “kwa tamaa,” basi kufikiri kwetu ni kama kufikiri kwa “mataifa,” yaani, watu wasio Wakristo wa kweli.

10. Kijana fulani alipomwendea Yesu ili kupata shauri, Yesu alionyeshaje kile ambacho kijana huyo alipenda zaidi?

10 Pindi fulani, kijana mmoja tajiri sana alimuuliza Yesu kile alichopaswa kufanya ili apate uzima wa milele. Yesu alimkumbusha matakwa ya Sheria iliyokuwapo wakati huo. Kijana huyo alimhakikishia Yesu hivi: “Nimeyashika yote hayo; ni nini bado ninachokosa?” Huenda wengi waliona kwamba haiwezekani kufanya yale ambayo Yesu alisema katika jibu lake. Alisema hivi: “Ikiwa unataka kuwa mkamilifu, nenda ukauze mali zako na uwape maskini nawe utakuwa na hazina mbinguni, kisha uje uwe mfuasi wangu.” (Mathayo 19:16-21) Kijana huyo alienda zake akiwa amekasirika kwa sababu hakutaka kupoteza mali yake. Haidhuru alimpenda Yehova kadiri gani, alipenda mali zake zaidi.

11, 12. (a) Yesu alisema maneno gani yenye kuchochea fikira kuhusu utajiri? (b) Mali zinaweza kumzuiaje mtu asimtumikie Yehova?

11 Tukio hilo lilimfanya Yesu aseme jambo ambalo wasikilizaji wake hawakutazamia: “Itakuwa vigumu kwa tajiri kuingia katika ufalme wa mbinguni. . . . Ni rahisi zaidi ngamia kupita katika tundu la sindano kuliko tajiri kuingia katika ufalme wa Mungu.” (Mathayo 19:23, 24) Je, Yesu alimaanisha kwamba hakuna tajiri yeyote atakayeurithi Ufalme? La, kwa kuwa aliendelea kusema: “Kwa Mungu mambo yote yanawezekana.” (Mathayo 19:25, 26) Kwa msaada wa Yehova baadhi ya Wakristo waliokuwa matajiri zamani hizo walipata kuwa Wakristo watiwa-mafuta. (1 Timotheo 6:17) Hata hivyo, Yesu alisema maneno hayo yenye kushangaza kwa sababu nzuri. Alikuwa akitoa onyo.

12 Ikiwa mtu anapenda mali zake sana kama yule kijana tajiri, huenda zikamzuia asimtumikie Yehova kwa moyo wote. Inaweza kuwa hivyo kwa mtu ambaye tayari ni tajiri au yule ambaye ‘anaazimia kuwa tajiri.’ (1 Timotheo 6:9, 10) Kutegemea sana vitu vya kimwili kunaweza kumfanya mtu ‘asitambue uhitaji wake wa kiroho.’ (Mathayo 5:3) Hivyo, huenda akaona kwamba hahitaji msaada wa Yehova. (Kumbukumbu la Torati 6:10-12) Huenda akatarajia atendewe kwa njia ya pekee kutanikoni. (Yakobo 2:1-4) Naye anaweza kutumia wakati mwingi kujifurahisha badala ya kumtumikia Yehova.

Sitawisha Maoni Yanayofaa

13. Wakristo wa Laodikia walikuwa na maoni gani yasiyofaa?

13 Kutaniko la karne ya kwanza la Laodikia lilikuwa na maoni yasiyofaa kuhusu mali. Yesu aliliambia hivi: “Unasema: ‘Mimi ni tajiri, nimejipatia utajiri na sihitaji kitu chochote hata kidogo,’ lakini hujui kwamba wewe ni mwenye taabu na wa kusikitikiwa na maskini na kipofu na uchi.” Si mali iliyowafanya watu wa Laodikia kuwa katika hali ya kusikitikiwa kiroho. Walitegemea utajiri kuliko kumtegemea Yehova. Hivyo, wakawa vuguvugu, nao walikuwa karibu ‘kutapikwa kutoka kinywani’ mwa Yesu.—Ufunuo 3:14-17.

14. Kwa nini Wakristo Waebrania walistahili kupongezwa na Paulo?

14 Kwa upande mwingine, Paulo aliwapongeza Wakristo Waebrania kwa sababu ya mtazamo wao wakati wa mateso. Alisema hivi: “Mliwasikitikia wale waliokuwa gerezani na pia kwa shangwe mkavumilia kuporwa mali zenu, mkijua ninyi wenyewe mna miliki bora na yenye kudumu.” (Waebrania 10:34) Wakristo hao hawakuvunjika moyo kwa kupoteza mali zao. Walikuwa na shangwe kwa sababu walitunza miliki yao yenye thamani zaidi, yaani, “miliki [yao] bora na yenye kudumu.” Kama mwanabiashara katika mfano wa Yesu aliyeacha kila kitu ili apate lulu moja yenye thamani, Wakristo hao waliazimia kwamba hawataacha kushikilia tumaini la Ufalme. (Mathayo 13:45, 46) Huo ni mtazamo mzuri kama nini!

15. Dada mmoja huko Liberia alitangulizaje Ufalme?

15 Wengi leo wamesitawisha mtazamo unaofaa kama huo. Kwa mfano, huko Liberia msichana mmoja Mkristo alipewa nafasi ya kusomea katika chuo kikuu. Katika nchi hiyo, wengi huona nafasi hiyo kama njia ya kuwa na maisha mazuri wakati ujao. Hata hivyo, alikuwa painia, yaani, mhubiri wa wakati wote, na alikuwa amepewa mgawo wa kutumika kama painia wa pekee wa muda. Alichagua kutafuta Ufalme kwanza na kubaki katika utumishi wa wakati wote. Alienda kwenye mgawo wake na akaanzisha mafunzo 21 ya Biblia kwa muda wa miezi mitatu. Dada huyo pamoja na maelfu ya wengine kama yeye hutanguliza Ufalme bila kujali kwamba watakosa vitu vya kimwili ambavyo huenda wangepata. Wanadumishaje mtazamo huo katika ulimwengu huu wenye kufuatilia mali? Wamesitawisha sifa nzuri mbalimbali. Acheni tuzungumzie kadhaa.

16, 17. (a) Kwa nini kiasi ni muhimu ikiwa tunataka kumtegemea Yehova? (b) Kwa nini tunapaswa kuwa na uhakika katika ahadi za Mungu?

16 Kiasi: Biblia inasema: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako. Usiwe mwenye hekima machoni pako mwenyewe.” (Methali 3:5-7) Wakati mwingine jambo fulani linaweza kuonekana kuwa sawa kulingana na maoni ya wanadamu. (Yeremia 17:9) Lakini, Mkristo mnyoofu hutafuta mwongozo kwa Yehova. (Zaburi 48:14) ‘Katika njia zake zote’—katika mambo ya kutaniko, elimu au kazi ya kimwili, starehe, au mambo mengine yoyote—yeye hutafuta shauri la Yehova huku akiwa mwenye kiasi.—Zaburi 73:24.

17 Uhakika katika ahadi za Yehova: Paulo alisema: “Yule anayemkaribia Mungu lazima aamini kwamba yeye yuko na kwamba yeye huwa mthawabishaji wa wale wanaomtafuta kwa bidii.” (Waebrania 11:6) Ikiwa tunatilia shaka kwamba Yehova atatimiza ahadi zake, huenda tukaona kuwa ni sawa ‘kuutumia ulimwengu huu kwa ukamili.’ (1 Wakorintho 7:31) Kwa upande mwingine, ikiwa tuna imani thabiti, tutaazimia kuutafuta kwanza Ufalme. Imani thabiti inaweza kusitawishwaje? Kwa kumkaribia Yehova daima, kusali kutoka moyoni, na kujifunza kibinafsi kwa ukawaida. (Zaburi 1:1-3; Wafilipi 4:6, 7; Yakobo 4:8) Kama Mfalme Daudi, tunaweza kusali hivi: “Nimekutegemea wewe, Ee Yehova. Nimesema: ‘Wewe ni Mungu wangu.’ Jinsi ulivyo mwingi wema wako!”—Zaburi 31:14, 19.

18, 19. (a) Bidii huimarishaje tegemeo letu kwa Yehova? (b) Kwa nini Mkristo anapaswa kuwa tayari kujidhabihu?

18 Bidii katika utumishi wa Yehova: Paulo alihusianisha uhakika katika ahadi za Yehova na bidii alipoandika hivi: “Tunatamani kila mmoja wenu aonyeshe bidii ileile ili kuwa na uhakikisho kamili wa tumaini mpaka mwisho.” (Waebrania 6:11) Yehova atatusaidia tukiwa na bidii katika utumishi wake. Kila tunapopata msaada huo, tegemeo letu kwake linakuwa na nguvu zaidi, tunakuwa “imara, thabiti.” (1 Wakorintho 15:58) Imani yetu huimarishwa, na tumaini letu linakuwa hakika zaidi.—Waefeso 3:16-19.

19 Kuwa tayari kujidhabihu: Paulo aliacha kazi ambayo ingempa mapato ili amfuate Yesu. Ni wazi kwamba alichagua jambo bora, licha ya kwamba wakati mwingine alikosa mahitaji ya kimwili. (1 Wakorintho 4:11-13) Yehova hatuahidi kwamba tutaishi maisha ya starehe, na wakati mwingine watumishi wake huvumilia matatizo. Tunapokuwa tayari kurahisisha maisha yetu na kujidhabihu, tunathibitisha kwamba tumeazimia kabisa kumtumikia Yehova.—1 Timotheo 6:6-8.

20. Kwa nini subira ni muhimu kwa mtu anayetanguliza mambo ya Ufalme?

20 Subira: Mwanafunzi Yakobo aliwahimiza Wakristo wenzake hivi: “Onyesheni subira, akina ndugu, mpaka kuwapo kwa Bwana.” (Yakobo 5:7) Ni vigumu kuwa na subira katika ulimwengu huu wenye shughuli nyingi. Tunataka mambo yafanyike haraka. Lakini Paulo anatuhimiza tuwaige wale “ambao kupitia imani na subira huzirithi ahadi.” (Waebrania 6:12) Uwe tayari kumngojea Yehova. Kwa hakika, uzima wa milele katika paradiso duniani ni jambo linalofaa kungojewa!

21. (a) Tunaonyesha nini tunapotanguliza mambo ya Ufalme? (b) Ni nini kitakachozungumziwa katika makala inayofuata?

21 Naam, shauri la Yesu la kuutafuta kwanza Ufalme linafaa. Tunapofanya hivyo, tunaonyesha kwamba kwa kweli tunamtegemea Yehova na tunachagua njia pekee iliyo salama kwa Mkristo. Hata hivyo, Yesu alitushauri pia tuendelee “kuutafuta kwanza . . . uadilifu [wa Mungu].” Katika makala inayofuata tutaona ni kwa nini himizo hilo linahitajiwa hasa leo.

Je, Unaweza Kueleza?

• Yesu alitutia moyo tuwe na usawaziko gani kuhusiana na vitu vya kimwili?

• Tunajifunza nini kutokana na mfano wa Yesu wa ngamia na tundu la sindano?

• Ni sifa gani za Kikristo zinazotusaidia kuutafuta kwanza Ufalme wa Mungu?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 21]

Wengi waliomsikiliza Yesu walikuwa maskini

[Picha katika ukurasa wa 23]

Yule kijana tajiri alipenda mali zake kuliko Mungu

[Picha katika ukurasa wa 23]

Mwanabiashara katika mfano wa Yesu alidhabihu kila kitu ili apate lulu moja yenye thamani

[Picha katika ukurasa wa 24]

Yehova atatusaidia tukiwa na bidii katika utumishi wake