Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Maswali Kutoka kwa Wasomaji

Zaburi 102:26 inasema kwamba dunia na mbingu “zitaangamia.” Je, hilo linamaanisha kwamba Dunia itaharibiwa?

Mtunga-zaburi alisema hivi aliposali kwa Yehova: “Wewe uliiweka misingi ya dunia zamani za kale, nazo mbingu ni kazi ya mikono yako. Hizo zitaangamia, lakini wewe mwenyewe utaendelea kusimama; nazo zote zitachakaa kama vazi. Utazibadili kama mavazi, nazo zitamaliza zamu yake.” (Zaburi 102:25, 26) Muktadha unaonyesha kwamba mistari hiyo inazungumzia hali ya Mungu ya kuwapo milele, bali si uharibifu wa dunia. Pia, muktadha unaonyesha jinsi ukweli huo muhimu unavyowafariji watumishi wa Mungu.

Mtunga-zaburi anaanza kwa kueleza mateso yake, labda akiwa uhamishoni huko Babiloni. Anaomboleza kwamba maisha yake ni mafupi “kama moshi.” Mahangaiko mengi yanadhoofisha mwili wake, na kufanya mifupa yake iwe na “moto mkali kama jiko.” Amechoka, ‘amekauka kama majani tu,’ naye anahisi upweke “kama ndege aliye peke yake juu ya dari.” Majaribu yaliyompata yamemfanya akose hamu ya kula na anaomboleza kila siku. (Zaburi 102:3-11) Hata hivyo, mtunga-zaburi hajakata tamaa. Kwa nini? Kwa sababu ya mambo ambayo Yehova ameahidi kulifanyia Sayuni, au Yerusalemu.

Ingawa Sayuni limeharibiwa, Yehova ameahidi kwamba litarudishwa katika hali yake ya awali. (Isaya 66:8) Hivyo, mtunga-zaburi anamwambia Yehova hivi kwa uhakika: “Utakuwa na rehema juu ya Sayuni, kwa maana ni majira ya kumwonyesha kibali, kwa maana wakati uliowekwa umefika. Kwa maana hakika Yehova atajenga Sayuni.” (Zaburi 102:13, 16) Kisha mtunga-zaburi anazungumzia tena mateso yanayompata. Anakata kauli kwamba ikiwa Yerusalemu ambalo liko katika hali ya ukiwa linaweza kurudishwa katika hali yake ya awali kwa nguvu za Mungu, basi ni hakika kwamba Yehova anaweza kumwokoa kutokana na hali yake ya taabu. (Zaburi 102:17, 20, 23) Kuna jambo lingine linalomchochea mtunga-zaburi amtegemee Yehova kabisa. Jambo gani? Kwamba Mungu ni wa milele.

Hali ya Yehova ya kuwapo milele inatofautiana sana na maisha mafupi ya mtunga-zaburi. Mtunga-zaburi anamwambia Yehova: “Miaka yako ni ya vizazi vyote.” (Zaburi 102:24) Kisha anasema: “Wewe uliiweka misingi ya dunia zamani za kale, nazo mbingu ni kazi ya mikono yako.”—Zaburi 102:25.

Lakini, hata miaka mingi ambayo dunia na mbingu zimekuwapo haiwezi kulinganishwa na hali ya Yehova ya kuwapo milele. Mtunga-zaburi anaendelea kusema hivi: “Hizo [dunia na mbingu] zitaangamia, lakini wewe mwenyewe utaendelea kusimama.” (Zaburi 102:26) Dunia na mbingu zinazoonekana zinaweza kuangamia. Naam, katika maandiko mengine Yehova alisema kwamba zitadumu milele. (Zaburi 119:90; Mhubiri 1:4) Lakini zingeweza kuharibiwa ikiwa hilo lingekuwa kusudi la Mungu. Hata hivyo, Mungu hawezi kufa. Uumbaji unaoonekana unaendelea ‘kusimama milele’ kwa sababu Mungu anautunza. (Zaburi 148:6) Ikiwa Yehova angeacha kurudisha upya uumbaji unaoonekana, basi uumbaji ‘wote ungechakaa kama vazi.’ (Zaburi 102:26) Kama vile mwanadamu anavyoishi kwa muda mrefu kuliko muda ambao mavazi yake yanadumu, ndivyo Yehova angeishi kwa muda mrefu kuliko muda ambao uumbaji wake utadumu—ikiwa angechagua kufanya hivyo. Hata hivyo, maandiko mengine yanatuonyesha kwamba hayo si mapenzi yake. Neno la Mungu linatuhakikishia kwamba Yehova ameamua dunia na mbingu halisi zidumu milele.—Zaburi 104:5.

Inafariji kujua kwamba Yehova atakuwapo sikuzote ili kutimiza ahadi zake zote. Hata tukipatwa na majaribu gani, tunapomlilia, tunaweza kuwa na uhakika kwamba “hakika ataielekea sala ya wale waliovuliwa kila kitu, naye hataidharau sala yao.” (Zaburi 102:17) Naam, uhakikisho ambao Yehova anatoa kwenye Zaburi ya 102 kwamba atawategemeza watu wake ni thabiti hata kuliko dunia yetu.