Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Waamuzi

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Waamuzi

Neno la Yehova Liko Hai

Mambo Makuu Katika Kitabu cha Waamuzi

YEHOVA huitikiaje watu wake wanapomwonyesha kisogo na kuanza kuabudu miungu ya uwongo? Namna gani ikiwa wanakataa kumtii tena na tena na kumwomba msaada wakati tu wanapojikuta katika taabu? Hata wakati huo, je, Yehova hutoa njia ili waponyoke? Kitabu cha Waamuzi kinajibu maswali hayo na mengine yaliyo muhimu. Kitabu hicho kilichoandikwa na nabii Samweli yapata mwaka wa 1100 K.W.K., kinatia ndani matukio ya kipindi cha miaka 330 hivi, yaani, tangu kifo cha Yoshua hadi kutawazwa kwa mfalme wa kwanza wa Israeli.

Kitabu cha Waamuzi ni chenye thamani kubwa kwetu kwa kuwa ni sehemu ya neno au ujumbe wa Mungu wenye nguvu. (Waebrania 4:12) Masimulizi yenye kusisimua yaliyomo hutupa ufahamu wa ndani kuhusu utu wa Mungu. Yale tunayojifunza kutokana na masimulizi hayo huimarisha imani yetu na kutusaidia kushikilia imara “uzima ulio wa kweli,” uzima wa milele katika ulimwengu mpya wa Mungu ulioahidiwa. (1 Timotheo 6:12, 19; 2 Petro 3:13) Matendo ya wokovu ambayo Yehova anatimiza kwa ajili ya watu wake yanaonyesha kimbele ukombozi mkubwa zaidi ambao ataleta wakati ujao kupitia Mwana wake, Yesu Kristo.

KWA NINI WAAMUZI WALIHITAJIWA?

(Waamuzi 1:1–3:6)

Baada ya wafalme wa nchi ya Kanaani kushindwa chini ya uongozi wa Yoshua, makabila mojamoja ya Israeli yanaenda kwenye urithi wao na kuimiliki nchi. Hata hivyo, Waisraeli wanashindwa kuwafukuza wakaaji wa nchi. Kushindwa huko kunatokeza mtego kwa Waisraeli.

Kizazi kinachotokea baada ya siku za Yoshua ‘hakimjui Yehova wala ile kazi ambayo amefanyia Israeli.’ (Waamuzi 2:10) Isitoshe, watu wanaanza kufanya mapatano ya ndoa pamoja na Wakanaani na kutumikia miungu yao. Hivyo, Yehova anaacha Waisraeli washindwe na maadui wao. Hata hivyo, ukandamizaji unapokuwa mkali, wana wa Israeli wanamlilia Mungu wa kweli awasaidie. Chini ya hali hizo za kidini, kijamii, na kisiasa, Yehova anatokeza waamuzi ili kuwaokoa watu wake kutoka kwa maadui wao.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

1:2, 4—Kwa nini kabila la Yuda linatajwa kuwa la kwanza kumiliki nchi ambayo linapewa? Kwa kawaida, pendeleo hilo lingekuwa la kabila la Rubeni, mzaliwa wa kwanza wa Yakobo. Lakini katika unabii wake kabla ya kufa, Yakobo alitabiri kwamba Rubeni hangepata ukuu kwa kuwa alipoteza haki ya kuwa mzaliwa wa kwanza. Simeoni na Lawi, ambao walitenda kwa ukatili, wangetawanywa katika Israeli. (Mwanzo 49:3-5, 7) Hivyo, aliyefuata katika ukuu ili kupokea pendeleo hilo alikuwa Yuda, mwana wa nne wa Yakobo. Simeoni, aliyeandamana na Yuda, alipokea eneo dogo la nchi lililotawanyika kotekote katika eneo kubwa la Yuda. *Yoshua 19:9.

1:6, 7—Kwa nini vidole gumba vya mikono na vya miguu vya wafalme walioshindwa vilikatwa? Yaelekea mtu aliyepoteza vidole gumba vyake vya mikono na vya miguu hangeweza kufanya lolote jeshini. Bila vidole gumba vya mikono, askari-jeshi angewezaje kutumia upanga au mkuki? Na kupoteza vidole gumba vya miguu kungemfanya mtu asiweze kusimama vizuri.

Mambo Tunayojifunza:

2:10-12. Tunapaswa kuwa na programu ya kawaida ya funzo la Biblia ili ‘tusisahau matendo ya Yehova.’ (Zaburi 103:2) Wazazi wanahitaji kukazia kweli ya Neno la Mungu katika mioyo ya watoto wao.—Kumbukumbu la Torati 6:6-9.

2:14, 21, 22. Yehova anaruhusu mambo mabaya yawapate watu wake wasiotii kwa kusudi fulani, yaani, ili kuwapa nidhamu, kuwasafisha, na kuwachochea wamrudie.

YEHOVA ANASIMAMISHA WAAMUZI

(Waamuzi 3:7–16:31)

Masimulizi yenye kusisimua ya matendo ya waamuzi yanaanza na Othnieli kukomesha kukandamizwa kwa Waisraeli kwa muda wa miaka minane na mfalme fulani wa Mesopotamia. Akitumia mbinu fulani ya ujasiri, Mwamuzi Ehudi anamuua Egloni, mfalme mnene wa Wamoabu. Akiwa peke yake, Shamgari mwenye ujasiri aua Wafilisti 600 akitumia mchokoo wa ng’ombe. Akitiwa moyo na Debora, anayetumikia kama nabii wa kike, na kutegemezwa na Yehova, Baraka na jeshi lake lenye wanaume elfu kumi tu wanashinda jeshi lenye nguvu la Sisera. Yehova anasimamisha Gideoni naye anampa yeye na wanaume wake 300 ushindi juu ya Wamidiani.

Kupitia Yeftha, Yehova anakomboa Israeli kutoka mikononi mwa Waamoni. Tola, Yairi, Ibzani, Eloni, na Abdoni ni kati ya wanaume 12 ambao wanahukumu Israeli. Kipindi cha Waamuzi kinamalizika na Samsoni, ambaye anapigana na Wafilisti.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

4:8—Kwa nini Baraka alisisitiza kwamba nabii wa kike Debora aende pamoja naye kwenye uwanja wa vita? Yaonekana Baraka alihisi kuwa hafai kwenda peke yake kupigana na jeshi la Sisera. Kuwa pamoja na nabii huyo kulimhakikishia yeye na wanaume wake kwamba waliongozwa na Mungu na kuliwapa uhakika. Hivyo, kusisitiza kwa Baraka kwamba Debora aandamane naye, hakukuwa ishara ya udhaifu, bali ishara ya imani yenye nguvu.

5:20—Nyota zilipiganaje zikiwa mbinguni kwa niaba ya Baraka? Biblia haisemi kama jambo hilo lilihusisha msaada wa malaika, vipande vingi vya mawe kutoka kwenye nyota ambavyo vilionwa kuwa ishara mbaya na wanaume wenye hekima wa Sisera, au labda ubashiri wa Sisera ambao haukutimia. Lakini bila shaka Mungu aliingilia kati kwa njia fulani.

7:1-3; 8:10—Kwa nini Yehova alisema kwamba wanaume wa Gideoni 32,000 walikuwa wengi sana kupigana na jeshi la adui 135,000? Ni kwa sababu Yehova alikusudia kumpa Gideoni na wanaume wake ushindi. Mungu hakutaka wafikiri kwamba waliwashinda Wamidiani kwa sababu ya nguvu zao wenyewe.

11:30, 31—Je, Yeftha alikuwa akifikiria dhabihu ya kibinadamu alipoweka nadhiri yake? Yeftha hangeweza kufikiria jambo kama hilo kwa kuwa Sheria ilisema: “Asipatikane ndani yako yeyote anayempitisha mwana wake au binti yake katikati ya moto.” (Kumbukumbu la Torati 18:10) Hata hivyo, Yeftha alikuwa akifikiria mtu wala si mnyama. Yaelekea wanyama waliofaa kwa ajili ya dhabihu hawakuwekwa katika nyumba za Waisraeli. Nalo toleo la mnyama halingekuwa jambo la pekee. Yaelekea Yeftha alijua kwamba mtu kutoka nyumbani mwake ambaye angekuja kumlaki angekuwa binti yake. Mtu huyo angepaswa kutolewa “kuwa toleo la kuteketezwa” katika maana ya kwamba angejitolea kikamili kumtumikia Yehova mahali patakatifu.

Mambo Tunayojifunza:

3:10. Kufanikiwa katika mambo ya kiroho hakutegemei hekima ya kibinadamu, bali roho ya Yehova.—Zaburi 127:1.

3:21. Ehudi alitumia upanga wake kwa ustadi na ujasiri. Tunapaswa kujifunza ustadi wa kutumia “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” Hii inamaanisha lazima tutumie Maandiko kwa ujasiri katika huduma yetu.—Waefeso 6:17; 2 Timotheo 2:15.

6:11-15; 8:1-3, 22, 23. Tunajifunza mambo matatu muhimu kutokana na sifa ya kiasi ya Gideoni: (1) Tunapopewa pendeleo fulani la utumishi, tunapaswa kufikiria kazi inayohusiana na daraka hilo badala ya kufikiria umashuhuri au sifa inayotokana na pendeleo hilo. (2) Kuonyesha kiasi ni njia ya hekima tunaposhughulika na watu ambao wana mwelekeo wa ugomvi. (3) Kuwa na kiasi hutulinda tusihangaikie sana cheo.

6:17-22, 36-40. Sisi pia tunapaswa kuwa waangalifu na ‘kutoamini kila neno lililoongozwa na roho.’ Badala yake, tunahitaji ‘kuyajaribu maneno yaliyoongozwa na roho ili kuona kama yanatokana na Mungu.’ (1 Yohana 4:1) Ili kuhakikisha kwamba shauri analotarajia kutoa lina msingi imara juu Neno la Mungu, ni jambo la hekima kwa mzee Mkristo mpya atafute shauri kutoka kwa mzee mwenye uzoefu zaidi.

6:25-27. Gideoni alitumia busara ili kutowakasirisha wapinzani wake bila sababu. Tunapohubiri habari njema, tunapaswa kuwa waangalifu tusiwakasirishe wengine bila sababu kwa namna tunavyozungumza.

7:6. Kuhusu kumtumikia Yehova, tunapaswa kuwa macho na makini kama wale wanaume 300 wa Gideoni.

9:8-15. Ni jambo la kipumbavu kama nini kuwa na kiburi na kujitakia cheo au mamlaka!

11:35-37. Bila shaka, kielelezo kizuri cha Yeftha kilichangia sana kumsaidia binti yake kukuza imani yenye nguvu na roho ya kujidhabihu. Leo, wazazi wanaweza pia kuwawekea watoto wao kielelezo kama hicho.

11:40. Kumpongeza mtu anayeonyesha roho ya kujitoa katika utumishi wa Yehova ni jambo lenye kumtia moyo.

13:8. Katika kuwafundisha watoto wao, wazazi wanapaswa kuomba mwongozo wa Yehova na kuufuata.—2 Timotheo 3:16.

14:16, 17; 16:16. Kumsumbua mtu mwingine kwa kulia na kumkasirisha kunaweza kuharibu uhusiano.—Methali 19:13; 21:19.

MAKOSA MENGINE KATIKA ISRAELI

(Waamuzi 17:1–21:25)

Sehemu ya mwisho ya kitabu cha Waamuzi ina masimulizi mawili makuu. Simulizi la kwanza linahusu mwanamume anayeitwa Mika ambaye anatengeneza sanamu nyumbani mwake na kumkodi Mlawi ili awe kuhani wake. Baada ya kuharibu jiji la Laishi au Leshemu, wana wa Dani wanajenga jiji lao wenyewe na wanalipa jina la Dani. Wakitumia sanamu ya Mika na kuhani wake, wanaanzisha aina nyingine ya ibada huko Dani. Yaelekea, Laishi linatekwa kabla ya kifo cha Yoshua.—Yoshua 19:47.

Tukio la pili linatukia muda mfupi baada ya kifo cha Yoshua. Uhalifu mkubwa wa kingono unaofanywa na wanaume fulani wa jiji la Benyamini la Gibea unafanya karibu kabila lote la Benyamini liangamizwe, na ni wanaume 600 tu wanaookolewa. Hata hivyo, mpango maalumu unafanywa ili wapate wake, na hesabu yao inaongezeka hadi wanaume wa vita karibu 60,000 wakati wa utawala wa Daudi.—1 Mambo ya Nyakati 7:6-11.

Maswali ya Kimaandiko Yajibiwa:

17:6; 21:25—Ikiwa “kila mmoja alikuwa na mazoea ya kufanya yaliyokuwa mema machoni pake mwenyewe,” je, hilo lilichochea machafuko? Sivyo hasa, kwa kuwa Yehova alifanya maandalizi ya kutosha ili kuongoza watu wake. Aliwapa Sheria na makuhani ili kuwaelimisha katika njia zake. Kupitia Urimu na Thumimu, kuhani mkuu angeweza kutafuta mwongozo wa Mungu kuhusu masuala muhimu. (Kutoka 28:30) Pia, kila jiji lilikuwa na wanaume wazee wenye uwezo wa kutoa mashauri yanayofaa. Mwisraeli aliyekubali maandalizi hayo, alipata mwongozo unaofaa kwa ajili ya dhamiri yake. Katika njia hiyo, kufanya ‘yale yaliyokuwa mema machoni pake mwenyewe’ kulikuwa na matokeo mazuri. Kwa upande mwingine, ikiwa mtu angepuuza Sheria na kufanya maamuzi yake mwenyewe kuhusu mwenendo na ibada, matokeo yangekuwa mabaya.

20:17-48—Kwa nini Yehova aliruhusu Wabenyamini washinde makabila mengine mara mbili, ingawa wao ndio waliostahili kuadhibiwa? Kwa kuruhusu makabila yenye uaminifu yashindwe kwanza, Yehova alijaribu azimio lao la kuondoa uovu katika Israeli.

Mambo Tunayojifunza:

19:14, 15. Kwa kukataa kuonyesha ukaribishaji, watu wa Gibea walidhihirisha kwamba walikuwa wamepungukiwa kiadili. Wakristo wanashauriwa ‘wafuate mwendo wa ukaribishaji-wageni.’—Waroma 12:13.

Ukombozi Ulio Mbele Yetu

Hivi karibuni, Ufalme wa Mungu mikononi mwa Kristo Yesu utaharibu ulimwengu huu mwovu na kuleta ukombozi mkubwa kwa ajili ya wanyoofu na wasio na lawama. (Methali 2:21, 22; Danieli 2:44) ‘Maadui wote wa Yehova wataangamia, na wanaompenda watakuwa kama jua linaposonga katika nguvu zake.’ (Waamuzi 5:31) Acheni basi tuwe kati ya wale wanaompenda Yehova kwa kutumia yale tunayojifunza katika kitabu cha Waamuzi.

Kweli muhimu inayoonyeshwa tena na tena katika masimulizi ya Waamuzi ni hii: Utii kwa Yehova huongoza kwenye baraka nyingi, kutotii huongoza kwenye msiba. (Kumbukumbu la Torati 11:26-28) Ni muhimu kama nini kwamba ‘tutii kutoka moyoni’ mapenzi ya Mungu ambayo ametufunulia!—Waroma 6:17; 1 Yohana 2:17.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Walawi hawakupewa urithi katika Nchi ya Ahadi ila tu majiji 48 yaliyotawanyika katika Israeli.

[Ramani katika ukurasa wa 25]

(Ona mpangilio kamili katika nakala iliyochapishwa)

“Yehova alikuwa akisimamisha waamuzi, nao walikuwa wakiwaokoa kutoka mkononi mwa waporaji wao.”—Waamuzi 2:16

WAAMUZI

1. Othnieli

2. Ehudi

3. Shamgari

4. Baraka

5. Gideoni

6. Tola

7. Yairi

8. Yeftha

9. Ibzani

10. Eloni

11. Abdoni

12. Samsoni

DANI

MANASE

NAFTALI

ASHERI

ZEBULONI

ISAKARI

MANASE

GADI

EFRAIMU

DANI

BENYAMINI

RUBENI

YUDA

[Picha katika ukurasa wa 26]

Umejifunza nini kutokana na kusisitiza kwa Baraka kwamba Debora aende kwenye uwanja wa vita?