Waamuzi 2:1-23
2 Kisha malaika wa Yehova+ akatoka Gilgali+ na kwenda Bokimu na kusema: “Niliwatoa Misri na kuwaleta katika nchi ambayo niliapa kwamba ningewapa mababu zenu.+ Pia nikasema, ‘Sitavunja kamwe agano langu pamoja nanyi.+
2 Nanyi msifanye agano na wakaaji wa nchi hii,+ bomoeni madhabahu zao.’+ Lakini hamkutii sauti yangu.+ Kwa nini hamkutii?
3 Ndiyo maana nilisema, ‘Sitawafukuza kutoka mbele yenu,+ nao watakuwa mtego kwenu,+ nanyi mtashawishiwa kuifuata miungu yao.’”+
4 Malaika wa Yehova alipowaambia Waisraeli wote maneno hayo, watu wakaanza kulia kwa sauti kubwa.
5 Kwa hiyo wakapaita mahali hapo Bokimu,* nao wakamtolea Yehova dhabihu hapo.
6 Yoshua alipowaruhusu watu waende zao, kila Mwisraeli alienda kwenye eneo lake la urithi ili kuimiliki nchi.+
7 Na watu wakaendelea kumtumikia Yehova sikuzote za Yoshua na sikuzote za wazee walioendelea kuishi baada ya Yoshua kufa ambao walikuwa wameona mambo yote makuu ambayo Yehova aliwatendea Waisraeli.+
8 Kisha Yoshua mwana wa Nuni, mtumishi wa Yehova, akafa akiwa na umri wa miaka 110.+
9 Basi wakamzika kwenye eneo lake la urithi kule Timnath-heresi+ katika eneo lenye milima la Efraimu, upande wa kaskazini wa Mlima Gaashi.+
10 Na watu wote wa kizazi hicho wakafa na kuzikwa kama walivyozikwa mababu zao,* na kizazi kingine kikatokea ambacho hakikumjua Yehova wala mambo aliyowafanyia Waisraeli.
11 Na Waisraeli wakatenda maovu machoni pa Yehova, wakaabudu* Mabaali.+
12 Basi wakamwacha Yehova, Mungu wa baba zao, aliyewatoa katika nchi ya Misri.+ Nao wakafuata miungu mingine, miungu ya watu waliowazunguka,+ wakaiinamia, na hivyo wakamkasirisha Yehova.+
13 Wakamwacha Yehova na kuabudu Baali na sanamu za Ashtorethi.+
14 Ndipo hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli, akawatia mikononi mwa waporaji, nao wakapora mali zao.+ Akawatia* mikononi mwa maadui waliowazunguka+ wala hawakuweza tena kuwashinda maadui wao.+
15 Popote walipoenda, mkono wa Yehova uliwapinga na kuwaletea msiba,+ kama Yehova alivyokuwa amesema na kama Yehova alivyokuwa amewaapia,+ nao wakateseka sana.+
16 Basi Yehova alikuwa akiwapa waamuzi ambao waliwaokoa kutoka mikononi mwa waporaji.+
17 Lakini walikataa kuwasikiliza hata waamuzi hao, nao walifanya ukahaba na miungu mingine na kuiinamia. Waliacha haraka njia ambayo mababu zao walifuata, ambao walitii amri za Yehova.+ Walikataa kutii.
18 Wakati wowote Yehova alipowapa waamuzi,+ Yehova alikuwa pamoja na mwamuzi huyo, akawaokoa kutoka mikononi mwa maadui wao sikuzote za mwamuzi huyo; kwa maana Yehova aliwahurumia*+ kwa sababu ya kilio chao cha uchungu kilichosababishwa na wale waliowakandamiza+ na wale waliowatesa.
19 Hata hivyo mwamuzi huyo alipokufa, walitenda tena mambo maovu zaidi kuliko baba zao kwa kuifuata miungu mingine, kuiabudu na kuiinamia.+ Hawakuacha mazoea yao na tabia yao ya ukaidi.
20 Mwishowe hasira ya Yehova ikawaka dhidi ya Waisraeli,+ akasema, “Kwa sababu taifa hili limevunja agano langu+ nililofanya na mababu zao, na halijanitii,+
21 basi mimi sitafukuza kutoka mbele yao taifa hata moja ambalo Yoshua aliacha alipokufa.+
22 Nitafanya hivyo ili kuwajaribu Waisraeli nione kama wataishika njia yangu mimi, Yehova,+ na kutembea katika njia hiyo kama baba zao walivyofanya.”
23 Kwa hiyo Yehova akaruhusu mataifa hayo yabaki. Hakuyafukuza haraka, wala hakuyatia mikononi mwa Yoshua.
Maelezo ya Chini
^ Maana yake “Wanaolia.”
^ Tnn., “wakakusanywa kwa mababu zao.” Huu ni msemo wa kishairi unaorejelea kifo.
^ Au “wakatumikia.”
^ Tnn., “Akawauza.”
^ Au “alighairi.”