Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Pigana Pigano Zuri la Imani”

“Pigana Pigano Zuri la Imani”

“Pigana Pigano Zuri la Imani”

JE, UNAWEZA kuwazia askari yeyote wakati wa vita ambaye hangefurahi kuagizwa hivi: “Rudi nyumbani ukakae na mke na familia yako kwa muda fulani”?

Katika siku za Mfalme Daudi wa Israeli, askari mmoja alipata agizo kama hilo. Uria Mhiti aliitwa na mfalme mwenyewe na kuambiwa arudi nyumbani kwake, lakini akakataa. Alipoulizwa kuhusu tabia hiyo isiyo ya kawaida, Uria alijibu kwamba sanduku la agano, lililowakilisha kuwapo kwa Mungu, na jeshi la Israeli, lilikuwa vitani. “Nami,” akauliza, “niende nyumbani kwangu kula na kunywa na kulala na mke wangu?” Uria aliona jambo hilo kuwa lisilowazika wakati huo wa hatari.—2 Samweli 11:8-11.

Jinsi Uria alivyotenda hutokeza maswali muhimu, kwa kuwa sisi pia tunaishi wakati wa vita. Leo vita fulani vinaendelea ambavyo ni tofauti na vita vyovyote ambavyo vimepiganwa na mataifa ya ulimwengu. Vita hivyo hufanya vile vita viwili vya ulimwengu vionekane kuwa si kitu, nawe unahusika katika vita hivyo. Vita hivyo ni hatari sana, naye adui ni mwenye kutisha. Katika vita hivyo, hakuna risasi zinazofyatuliwa, wala mabomu kuangushwa, lakini hiyo haimaanishi kwamba vita hivyo si vikali.

Kabla ya kuchukua silaha, unapaswa kujua kusudi la vita hivyo na kama inafaa kupigana. Je, kuna faida za kupigana vita hivyo? Kusudi la vita hivyo linaonyeshwa wazi na mtume Paulo katika barua yake kwa Timotheo: “Pigana pigano zuri la imani.” Naam, katika vita hivi hupaswi kupigania ngome fulani, bali “imani,” ambayo ni kweli zote za Kikristo kama zinavyoonyeshwa katika Biblia. Bila shaka, unapaswa kukubali kabisa “imani” hiyo ili uweze kuipigania na kushinda.—1 Timotheo 6:12.

Askari mwenye hekima hujitahidi kujua adui wake. Katika pigano hili, adui ana uzoefu wa miaka mingi kuhusu mbinu za vita, naye ana silaha nyingi anazoweza kutumia. Pia ana uwezo unaozidi wa kibinadamu. Ni mkatili, mwenye jeuri na mjanja; yeye ni Shetani. (1 Petro 5:8) Ni kazi bure kutumia silaha halisi, ujanja, au hila za kibinadamu kupigana na adui huyo. (2 Wakorintho 10:4) Unaweza kutumia nini ili kupigana vita hivyo?

Silaha kuu ni “upanga wa roho, yaani, neno la Mungu.” (Waefeso 6:17) Mtume Paulo anaonyesha jinsi silaha hiyo ilivyo na matokeo: “Neno la Mungu liko hai nalo lina nguvu na ni lenye makali zaidi kuliko upanga wowote wenye makali kuwili nalo huchoma hata kufikia kugawanya nafsi na roho, na viungo na urojorojo wake, nalo linaweza kutambua fikira na makusudio ya moyo.” (Waebrania 4:11, 12) Bila shaka, silaha hiyo inapaswa kutumiwa kwa ustadi na kwa uangalifu kwa kuwa ni kali sana nayo inalenga shabaha vizuri sana hivi kwamba inaweza kupenya mawazo na makusudi ya ndani ya mtu.

Yaelekea unajua kwamba jeshi linaweza kuwa na silaha za hali ya juu sana, lakini silaha hizo ni bure ikiwa askari hawajui kuzitumia kwa ustadi. Vivyo hivyo, unahitaji kuzoezwa ili kutumia upanga wako vizuri. Inafurahisha kwamba unaweza kupata mazoezi kutoka kwa askari wenye uzoefu mwingi. Yesu aliwaita askari hao wanaowazoeza wengine “mtumwa mwaminifu na mwenye busara,” ambaye amepewa daraka la kuandaa chakula cha kiroho, yaani, maagizo ya wakati unaofaa, kwa ajili ya wafuasi wake. (Mathayo 24:45) Unaweza kutambua jamii hiyo ya mtumwa kwa kuchunguza jinsi inavyofundisha kwa bidii na kutoa maonyo ya wakati unaofaa kuhusu mbinu za adui. Mambo ya hakika yanaonyesha kwamba jamii hiyo ni washiriki waliotiwa mafuta wa kutaniko la Kikristo la Mashahidi wa Yehova.—Ufunuo 14:1.

Jamii hiyo ya mtumwa imefanya mengi zaidi ya kutoa maagizo tu. Imeonyesha roho kama ya mtume Paulo, aliyeliandikia kutaniko la Thesalonike hivi: “Tulikuwa wapole katikati yenu, kama mama mwenye kunyonyesha anavyowatunza kwa upendo watoto wake mwenyewe. Kwa hiyo, tukiwa na upendo mwororo kwa ajili yenu, tulipendezwa vema kuwapa ninyi, si habari njema ya Mungu tu, bali pia nafsi zetu wenyewe, kwa sababu ninyi mlikuwa wapendwa kwetu.” (1 Wathesalonike 2:7, 8) Kila askari Mkristo ana daraka la kutumia mazoezi yanayotolewa kwa upendo.

Suti Kamili ya Silaha

Umepewa suti kamili ya silaha ya mfano ili kujilinda. Unaweza kupata orodha ya silaha zinazofanyiza suti hiyo katika Waefeso 6:13-18. Askari mwenye tahadhari hatatoka nje ikiwa hana sehemu fulani ya suti yake ya kiroho au ikiwa inahitaji kurekebishwa.

Mkristo anahitaji kuvaa suti kamili ya silaha, lakini ngao kubwa ya imani ni muhimu sana. Ndiyo sababu Paulo aliandika hivi: “Zaidi ya mambo yote, ichukueni ngao kubwa ya imani, ambayo kwa kuitumia mtaweza kuizima mishale yote inayowaka moto ya yule mwovu.”—Waefeso 6:16.

Ngao kubwa inayoweza kukinga mwili mzima, inafananisha ubora wa imani. Ni lazima uwe na imani yenye nguvu katika mwongozo wa Yehova, ukikubali bila shaka yoyote kwamba ahadi zake zote zitatimia. Unapaswa kuhisi kana kwamba ahadi hizo zimekwisha timizwa. Usitilie shaka hata kidogo kwamba mfumo wote wa ulimwengu wa Shetani utaharibiwa hivi karibuni, kwamba dunia itageuzwa kuwa paradiso, na kwamba watu walio washikamanifu kwa Mungu watakuwa wakamilifu.—Isaya 33:24; 35:1, 2; Ufunuo 19:17-21.

Hata hivyo, katika vita visivyo vya kawaida vinavyoendelea sasa, unahitaji kuwa na rafiki. Wakati wa vita, askari hufanya urafiki wa karibu wanapotiana moyo na kulindana, na hata nyakati nyingine kuokoana katika kifo. Ingawa marafiki ni muhimu, unahitaji kuwa rafiki ya Yehova mwenyewe ili kuokoka vita hivyo. Ndiyo sababu Paulo anamalizia orodha yake ya silaha zinazofanyiza suti hiyo kwa maneno haya: “Huku kwa kila namna ya sala na dua mkiendeleza sala kila wakati katika roho.”—Waefeso 6:18.

Tunapenda kuwa pamoja na rafiki wa karibu. Tunatafuta wakati wa kuwa naye. Kwa kuzungumza na Yehova kwa ukawaida katika sala, anakuwa halisi kwetu, kama rafiki mwenye kutumainika. Mwanafunzi Yakobo anatutia moyo hivi: “Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi.”—Yakobo 4:8.

Mbinu za Adui

Nyakati nyingine kushindana na ulimwengu huu ni kama kutembea katika eneo lenye mabomu ya ardhini. Unaweza kushambuliwa kutoka upande wowote, na adui hujaribu kukushambulia kwa ghafula. Hata hivyo, uwe na hakika kwamba Yehova ameandaa ulinzi wote unaohitaji.—1 Wakorintho 10:13.

Huenda adui akaamua kushambulia kweli za Biblia ambazo ni muhimu kwa imani yako. Waasi-imani wanaweza kutumia maneno yenye kuvutia, wakakusifu-sifu, au kutoa hoja zilizopotoka ili wajaribu kukushinda. Lakini mwasi-imani hakutakii mema. Andiko la Methali 11:9 linasema: “Mwasi-imani humletea mwenzake uharibifu kwa kinywa chake, lakini waadilifu huokolewa kwa ujuzi.”

Lingekuwa kosa kufikiri kwamba unahitaji kusikiliza au kusoma vitabu vya waasi-imani ili uweze kupinga hoja zao. Hoja zao mbaya na zilizopotoka zinaweza kusababisha madhara ya kiroho na kuchafua imani yako kama kidonda chenye kuoza kinachoenea haraka. (2 Timotheo 2:16, 17) Badala yake, iga mtazamo wa Mungu kuelekea waasi-imani. Ayubu alisema hivi kumhusu Yehova: “Hakuna mwasi-imani yeyote atakayekuja mbele zake.”—Ayubu 13:16.

Huenda adui akatumia mbinu nyingine ambayo imekuwa na matokeo ya kadiri fulani. Ikiwa jeshi linalosafiri kwenda vitani litashawishiwa kuacha safari yao na kujiingiza katika mambo yasiyo ya adili, hiyo inaweza kuleta mvurugo.

Vitumbuizo vya ulimwengu, kama vile sinema na vipindi vya televisheni visivyo vya adili na muziki uliopotoka, ni mtego wenye kunasa. Wengine hudai kwamba wanaweza kutazama vipindi au kusoma vichapo visivyo vya adili bila kuathiriwa. Lakini mtu mmoja aliyekuwa na zoea la kutazama sinema zilizoonyesha mambo ya kingono waziwazi alikiri: “Huwezi kusahau picha hizo kamwe, kadiri unavyofikiri juu ya picha hizo ndivyo unavyotamani kufanya mambo uliyoona . . . Picha hizo hukufanya ufikiri kwamba unakosa jambo fulani.” Je, inafaa kujiweka katika hali ambayo unaweza kuathiriwa na shambulizi hili lisilo la moja kwa moja?

Njia nyingine ambayo adui huyo hutumia kutushambulia ni kutushawishi kwa vitu vya kimwili. Inaweza kuwa vigumu kutambua hatari hiyo kwa sababu sote tuna mahitaji ya kimwili. Tunahitaji makao, chakula, na nguo na si vibaya kuwa na vitu vizuri. Hatari inaweza kutokana na mtazamo wa mtu kuelekea vitu vya kimwili. Huenda pesa zikawa muhimu zaidi ya mambo ya kiroho. Tunaweza kuwa wenye kupenda pesa. Ni vizuri kukumbuka kwamba mali haiwezi kutimiza mambo yote. Ni ya muda tu, lakini utajiri wa kiroho hudumu milele.—Mathayo 6:19, 20.

Ikiwa jeshi halina moyo wa kupigana, ni vigumu kushinda. “Je, umejionyesha kuwa umevunjika moyo siku ya taabu? Nguvu zako zitakuwa chache.” (Methali 24:10) Shetani ametumia kivunja-moyo kwa matokeo sana. Kuvaa “tumaini la wokovu kama kofia ya chuma” kunaweza kukusaidia kukabiliana na kivunja-moyo. (1 Wathesalonike 5:8) Jaribu kuwa na tumaini lenye nguvu kama la Abrahamu. Alipoambiwa amtoe mwana wake wa pekee Isaka awe dhabihu, Abrahamu hakusitasita. Aliamini kwamba Mungu angetimiza ahadi Yake ya kubariki mataifa yote kupitia uzao wake na kwamba iwapo ingekuwa lazima, Mungu angemfufua Isaka ili kutimiza ahadi hiyo.—Waebrania 11:17-19.

Usiache Pigano

Huenda wengine ambao wamepigana kwa ujasiri kwa muda mrefu wameanza kuchoka na hivyo hawapigani wakiwa waangalifu kama zamani. Kielelezo cha Uria, kilichotajwa mwanzoni mwa makala hii kinaweza kuwasaidia wote wanaopigana wadumishe mtazamo unaofaa. Wengi wa Wakristo wenzetu ambao ni wapiganaji wanalazimika kuvumilia magumu, kukabili hatari, au kuteseka kutokana na baridi na njaa. Kama Uria, hatutaki kufikiria starehe ambazo tunaweza kufurahia sasa au kushindwa na tamaa ya kuishi maisha rahisi. Tunataka kudumu katika jeshi la Yehova la ulimwenguni pote la wapiganaji waaminifu na kuendelea kupigana hadi tuweze kufurahia baraka nyingi tulizoahidiwa.—Waebrania 10:32-34.

Ingekuwa hatari kuacha kuwa macho, labda tukifikiri kwamba shambulio la mwisho liko mbali sana. Mfano wa Mfalme Daudi hukazia hatari hiyo. Kwa sababu fulani hakuwa pamoja na majeshi yake vitani. Kwa hiyo, Daudi alitenda dhambi nzito ambayo ilimletea mateso na maumivu makali katika maisha yake yote.—2 Samweli 12:10-14.

Je, inafaa kushiriki katika vita hivyo, kukabili magumu ya vita, kuvumilia dhihaka, na kuacha anasa za ulimwengu zenye kutilika shaka? Wale wanaoendelea na pigano hilo kwa mafanikio wanakubali kwamba ulimwengu unaweza kuwa na vitu vyenye kuvutia, kama nyuzi za dhahabu zenye kumetameta, lakini vinapochunguzwa kwa ukaribu havina thamani kubwa. (Wafilipi 3:8) Isitoshe, mara nyingi anasa hizo huleta maumivu na kukata tamaa.

Mkristo anayepigana vita hivyo vya kiroho hufurahia ushirika wa karibu pamoja na marafiki wa kweli, dhamiri safi, na tumaini zuri. Wakristo waliotiwa mafuta kwa roho wanatazamia kupewa uhai usioweza kufa huko mbinguni na kuishi pamoja na Kristo Yesu. (1 Wakorintho 15:54) Wengi wa wapiganaji Wakristo wanatumaini kupewa uhai mkamilifu wa kibinadamu katika paradiso ya kidunia. Bila shaka, tunapaswa kufanya yote tuwezayo kupata tuzo hizo. Na tofauti na vita vya ulimwengu, tuna hakika kwamba tutashinda vita hivyo maadamu tu tunaendelea kuwa waaminifu. (Waebrania 11:1) Lakini mfumo huu ulio chini ya udhibiti wa Shetani utaharibiwa kabisa.—2 Petro 3:10.

Unapoendelea na vita hivyo, kumbuka maneno haya ya Yesu: “Jipeni moyo! Mimi nimeushinda ulimwengu.” (Yohana 16:33) Alishinda kwa kuendelea kuwa mwangalifu na kudumisha utimilifu chini ya jaribu. Sisi pia tunaweza kufanya hivyo.

[Blabu katika ukurasa wa 27]

Hakuna risasi zinazofyatuliwa, wala mabomu kuangushwa, lakini hiyo haimaanishi kwamba vita hivyo si vikali

[Blabu katika ukurasa wa 30]

Tuna hakika kwamba tutashinda vita hivyo maadamu tu tunaendelea kuwa waaminifu

[Picha katika ukurasa wa 26]

Kofia ya wokovu itatusaidia kukabiliana na kivunja-moyo

Tumia ngao kubwa ya imani kujikinga na “mishale inayowaka moto” ya Shetani

[Picha katika ukurasa wa 28]

“Mkaribieni Mungu, naye atawakaribia ninyi”

[Picha katika ukurasa wa 29]

Tunapaswa kuwa na imani kwamba Mungu atatimiza ahadi zake