Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova ‘Husamehe Kabisa’

Yehova ‘Husamehe Kabisa’

Yehova ‘Husamehe Kabisa’

KUSAMEHE mkosaji humaanisha kuacha kinyongo kwa sababu ya kosa alilokufanyia na kutolipiza kisasi.

Kulingana na sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli, ili mtu ambaye amemkosea Mungu au mwanadamu mwenzake asamehewe dhambi zake, kwanza ilimbidi kurekebisha kosa lake kama Sheria ilivyoagiza, na mara nyingi alihitaji kutoa toleo la damu kwa Yehova. (Mambo ya Walawi 5:5–6:7) Ndiyo sababu Paulo alitaja kanuni hii: “Karibu vitu vyote husafishwa kwa damu kulingana na Sheria, na isipokuwa damu yamwagwa hakuna msamaha utukiao.” (Waebrania 9:22) Hata hivyo, damu ya dhabihu za wanyama haikuweza kuondoa dhambi na kumfanya mtu awe na dhamiri safi kabisa. (Waebrania 10:1-4; 9:9, 13, 14) Badala yake, agano jipya lililotabiriwa liliwawezesha watu kupata msamaha wa kweli kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Yesu Kristo. (Yeremia 31:33, 34; Mathayo 26:28; 1 Wakorintho 11:25; Waefeso 1:7) Hata alipokuwa duniani, Yesu alionyesha kwamba ana uwezo wa kusamehe dhambi alipomponya mtu aliyepooza.—Mathayo 9:2-7.

Yehova ‘husamehe kabisa,’ kama inavyoonyeshwa na mifano ya Yesu ya mwana mpotevu na mfalme aliyemsamehe mtumwa wake deni la talanta 10,000 (dinari 60,000,000, au dola za Marekani 40,000,000 hivi). Lakini mtumwa huyo alikataa kumsamehe mtumwa mwenzake deni la dinari 100 tu (dola 70 hivi). (Isaya 55:7; Luka 15:11-32; Mathayo 18:23-35) Hata hivyo, Yehova haongozwi na hisia tu anaposamehe, yeye huadhibu makosa mabaya. (Zaburi 99:8) Yoshua aliwaonya Waisraeli kwamba Yehova hangewasamehe kama wangeasi.—Yoshua 24:19, 20; linganisha na Isaya 2:6-9.

Kuna njia maalumu ambayo Mungu ameweka ya kuomba na kupata msamaha. Ni lazima mtu akiri dhambi zake, atambue kwamba amemkosea Mungu, aungame kabisa, ahisi majuto ya moyoni kwa sababu ya kosa lake, na aazimie kuacha kabisa mwenendo wake mbaya. (Zaburi 32:5; 51:4; 1 Yohana 1:8, 9; 2 Wakorintho 7:8-11) Ni lazima ajitahidi kadiri awezavyo kurekebisha kosa alilofanya au madhara aliyosababisha. (Mathayo 5:23, 24) Kisha ni lazima amwombe Mungu msamaha kwa msingi wa dhabihu ya fidia ya Kristo.—Waefeso 1:7.

Inafaa kuomba msamaha wa Mungu kwa niaba ya wengine, hata kwa niaba ya kutaniko lote. Musa aliomba msamaha kwa niaba ya taifa la Israeli, akiungama dhambi za taifa zima, Yehova akamsikiliza. (Hesabu 14:19, 20) Wakati wa kuweka hekalu wakfu, Sulemani pia alimwomba Yehova awasamehe watu wake wakitenda dhambi na kuacha mwenendo mbaya. (1 Wafalme 8:30, 33-40, 46-52) Ezra aliungama mbele za watu wote dhambi za Wayahudi waliorudi kutoka utekwani. Kwa sababu ya himizo na sala yake ya kutoka moyoni, watu walirekebisha makosa yao ili kupata msamaha wa Yehova. (Ezra 9:13–10:4, 10-19, 44) Yakobo alimhimiza mtu aliye mgonjwa kiroho awaite wanaume wazee wa kutaniko ili wamwombee, na “ikiwa amefanya dhambi, atasamehewa.” (Yakobo 5:14-16) Hata hivyo, “kuna dhambi ambayo yapasisha kifo.” Hiyo ni dhambi dhidi ya roho takatifu, yaani, kuzoea kufanya dhambi kimakusudi. Dhambi hiyo haisameheki. Mkristo hapaswi kuwaombea wale wanaofanya dhambi hiyo.—1 Yohana 5:16; Mathayo 12:31; Waebrania 10:26, 27.

Isitoshe, ni takwa la Kikristo kuwasamehe wengine makosa waliyotufanyia haidhuru wametukosea mara ngapi. (Luka 17:3, 4; Waefeso 4:32; Wakolosai 3:13) Mungu hatawasamehe wale wanaokataa kuwasamehe wengine. (Mathayo 6:14, 15) Hata “mtu mwovu” anapotengwa na kutaniko la Kikristo kwa sababu ya kosa zito, baada ya muda anaweza kusamehewa, akithibitisha kwamba ametubu kikweli. Anaporudishwa, wote kutanikoni wanaweza kumwonyesha upendo. (1 Wakorintho 5:13; 2 Wakorintho 2:6-11) Hata hivyo, si lazima Wakristo wawasemehe wale wanaozoea kufanya dhambi kimakusudi bila kutubu. Watu hao wanakuwa adui za Mungu.—Waebrania 10:26-31; Zaburi 139:21, 22.