Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Unachopaswa Kujua Kuhusu Uchawi

Unachopaswa Kujua Kuhusu Uchawi

Unachopaswa Kujua Kuhusu Uchawi

SI RAHISI kufafanua uchawi wa siku hizi. Hiyo ni kwa sababu wachawi hutofautiana sana. Hawatambui mamlaka kuu wala fundisho wala kitabu chochote kitakatifu cha kuungamanisha itikadi. Wanatofautiana pia katika mapokeo, taratibu, matambiko, na maoni kuhusu miungu wapaswayo kuiheshimu. Mwandishi mmoja asema: “Ulimwengu wa mafumbo humwandalia mtu ‘soko huria’ la maoni.” Mwingine asema: “Wapagani wengi wa siku zetu hutofautiana katika karibu kila jambo.”

Kwa wengi tofauti hizo si tatizo. Kitabu kimoja kinachotoa mwongozo kwa wale wanaotaka kuwa wachawi chasema: “Ukitatizwa na habari inayoonekana kuwa yatofautiana, ichunguze habari hiyo kisha uamue mambo utakayofuata. Ongozwa na hisia zako. Yaani, uwe huru kuchagua habari katika matambiko yaliyochapishwa na katika vitabu vya kujifunzia matambiko ili kuamua kinachoonekana kuwa sawa.”

Kwa wale wanaoitambua kweli, tofauti hizo ni tatizo. Kweli ni mambo ya hakika, yaliyo halisi. Mambo hayawezi kuwa kweli kwa sababu tu mtu ahisi au atumaini au aamini kwamba ni ya kweli. Kwa mfano, wakati mmoja madaktari waliamini kwamba wanaweza kuponya nimonia kwa kumpasua kuku aliye hai vipande viwili na kuviweka juu ya kifua cha mgonjwa. Bila shaka, wagonjwa wengi waliamini kwa moyo mweupe kwamba matibabu hayo yangewaponya. Hata hivyo, itikadi zao na matumaini yao hayakupatana na mambo ya hakika—matibabu hayo hayaponyi nimonia. Watu hawaibuni kweli; wao hujitahidi kuifahamu.

Biblia hudai ina kweli juu ya mambo ya kiroho. Alipokuwa duniani, Yesu Kristo alisali hivi kwa Baba yake: “Neno lako ni kweli.” (Yohana 17:17) Mtume Paulo aliandika: “Andiko lote limepuliziwa na Mungu.” (2 Timotheo 3:16) Wachawi wengi hawakubaliani na jambo hilo. Badala yake, hutafuta upulizio na mwongozo katika ngano, dini za kale, na hata riwaya za kisayansi. Lakini je, si jambo la busara angalau kuchunguza maoni ya Biblia? Kwani Biblia inatambuliwa kuwa kitabu kitakatifu karibu ulimwenguni pote. Pia ni mojawapo ya maandishi ya zamani sana ya kidini ambayo yamedumu. Biblia iliandikwa kwa muda wa miaka zaidi ya 1,600, hata hivyo mafundisho yake yanapatana. Ebu tulinganishe mafundisho ya Biblia na baadhi ya itikadi za kawaida zinazoshikiliwa sasa na wale wanaoendeleza uchawi.

Ni Nani Wanaokaa Katika Makao ya Roho?

Swali la msingi katika kutafuta uelewevu wa kiroho ni hili, Ni nani wanaokaa katika makao ya roho? Ingawa wachawi wengi wa kisasa wana imani katika mambo ya asili na huabudu miungu mingi, baadhi yao huabudu mungu-mama mkuu, ambaye ana madaraka matatu ya kuwa mwanamwali, mama, na bikizee, akiwakilisha vipindi muhimu maishani. Mpenzi wake ni mungu mwenye pembe. Wachawi wengine huabudu mungu wa kiume na mungu wa kike pamoja. Mwandishi mmoja asema: “Mungu wa kike na Mungu wa kiume huonekana kuwa udhihirisho wa nguvu za asili za kike na za kiume. Kila mmoja [akiwa na] tabia za pekee ambazo zikiunganishwa hutokeza uhai kwa upatano.” Mwandishi mwingine asema: “Mojawapo ya mambo muhimu zaidi katika Uchawi ni uchaguzi wako wa miungu (Miungu ya Kiume/Miungu ya Kike) utakayoshirikiana nayo. . . . Uchawi hukupa uhuru wa kuchagua na hivyo kuheshimu aina zako mwenyewe za Miungu.”

Biblia haiungi mkono yoyote ya maoni hayo. Yesu Kristo alitumia huduma yake yote kuwafundisha wengine juu ya Yehova, “Mungu pekee wa kweli.” (Yohana 17:3) Biblia yasema: “BWANA ni mkuu mwenye kusifiwa sana; na wa kuhofiwa kuliko miungu yote. Maana miungu yote ya watu si kitu.”—1 Mambo ya Nyakati 16:25, 26.

Namna gani Ibilisi? Kamusi ya Webster’s Ninth New Collegiate Dictionary yafafanua uchawi kuwa “mawasiliano na ibilisi.” Ni vigumu sana leo upate mchawi anayekubaliana na ufafanuzi huo, kwa kuwa wengi hawakubali hata kuweko kwa Shetani Ibilisi. Mwanamke mmoja kijana, ambaye gazeti la The Irish Times lilimwita “mchawi mashuhuri na kiongozi wa kimojawapo cha vikundi maarufu zaidi cha wachawi nchini Ireland,” asababu hivi: “Kuamini katika Ibilisi kwamaanisha kukubali Ukristo . . . [Ibilisi] hawezi kuwepo katika ulimwengu ambapo hakuna Mungu.”

Biblia huthibitisha kuwepo kwa Ibilisi na humlaumu kwa mateseko na misukosuko iliyopo duniani. (Ufunuo 12:12) Yesu alifundisha kwamba Ibilisi yupo na pia akaonyesha kwamba inawezekana kufanya mapenzi ya Ibilisi bila kujua. Kwa mfano, viongozi wa kidini wa karne ya kwanza waliojiona kuwa waadilifu walisisitiza kwamba walikuwa, kwa njia fulani, wana wa Mungu na waliamini kwamba wanafanya mapenzi ya Mungu. Yesu ambaye angeweza kufahamu yaliyokuwa mioyoni mwao, alijua hivyo sivyo ilivyo. Aliwaambia waziwazi hivi: “Nyinyi mwatoka kwa baba yenu Ibilisi, nanyi mwataka kufanya tamaa za baba yenu.” (Yohana 8:44) Isitoshe, kitabu cha Biblia cha Ufunuo chasema kwamba Ibilisi ‘anaiongoza vibaya dunia nzima inayokaliwa.’—Ufunuo 12:9.

Je, Mizungu Kidogo Inafaa?

Sikuzote mizungu imehusianishwa na mafumbo. * Watu wengi wa kale na wa siku hizi huamini kwamba mizungu inayofanywa na wachawi hufanywa ili kuwadhuru wengine. Wachawi wanaaminiwa kuwa na uwezo wa kuletea mtu maumivu makali na hata kifo kupitia mizungu. Tangu zamani, wachawi wamelaumiwa kwa kusababisha misiba mingi sana, kutia ndani ugonjwa, kifo, na kutofaulu kwa mazao.

Wachawi leo hukataa katakata lawama hizo. Ingawa wanakiri kuwepo mara kwa mara kwa mchawi mlaghai anayefanya maovu, wengi husema kwamba uwezo wao wa kufanya mizungu hutumiwa kunufaisha wala si kudhuru. Wachawi wanaofuata Wicca hufundisha kwamba madhara ya mizungu yatamrudia mtu anayeifanya mara tatu na husema kwamba jambo hilo huzuia wachawi wasitoe laana. Mifano ya ile iitwayo eti mizungu yenye manufaa hutia ndani maneno ya kiuchawi ya kujikinga, kutakasa nyumba yako kutokana na nguvu zenye kudhuru zilizoachwa na wapangaji wa awali, kufanya mtu akupende, kukuza uponyaji na afya, kuzuia usipoteze kazi, na kupata fedha. Kwa kuwa inaaminiwa kwamba uchawi una nguvu nyingi hivyo, si ajabu kwamba umepata kupendwa sana.

Hata hivyo, Biblia haitofautishi mizungu mizuri na mizungu mibaya. Katika Sheria iliyopewa Musa, Mungu alijulisha msimamo wake waziwazi kabisa. Alisema: “Usifanye mizungu.” (Mambo ya Walawi 19:26, NW) Pia tunasoma: “Asionekane kwako mtu . . . atazamaye nyakati mbaya [“afanyaye mizungu,” NW], wala mwenye kubashiri, wala msihiri, wala mtu alogaye kwa kupiga mafundo, wala mtu apandishaye pepo.”—Kumbukumbu la Torati 18:10, 11.

Kwa nini Mungu alisema hivyo? Si kwa sababu anakusudia kutunyima mambo yenye manufaa. Yehova aliwapa watu wake sheria hizo kwa sababu aliwapenda na hakutaka hofu na ushirikina ziwafanye watumwa. Badala yake yeye anawaalika watumishi wake wamwombe vitu wanavyohitaji. Yeye ndiye Mpaji wa “kila zawadi njema na kila upaji mkamilifu.” (Yakobo 1:17) Mtume Yohana aliwahakikishia waamini wenzake hivi: “Chochote kile tuombacho twapokea kutoka [kwa Mungu], kwa sababu tunashika amri zake na kufanya mambo yanayopendeza machoni pake.”—1 Yohana 3:22.

Namna Gani Roho Waovu?

Wachawi wengi hukubaliana na Biblia juu ya jambo hili: Roho waovu wako. Katika taarifa moja mwendelezaji mmoja wa uchawi aonya: “Mazimwi yako: Yako, katika ulimwengu usioonekana ulio kama wetu, ambao umejaa viumbe hai. . . . Maneno ‘Jini,’ ‘Pepo Mbaya’ na ‘Roho Mwovu’ ni sahihi. Roho ni wenye nguvu sana. . . . Wale wenye akili nyingi zaidi . . . wanaweza (ikiwa mtu anaweza kuwasaidia kwa kuwafungulia mlango) kuingia katika ulimwengu wetu. . . . Wanaweza kuingia mwilini mwako . . . hata kukudhibiti kwa kadiri fulani. Naam, maelezo hayo yanafanana kabisa na hadithi za zamani za kupagawa na Roho Waovu.”

Katika nyakati za Biblia, kupagawa na roho waovu kuliathiri watu kwa njia tofauti-tofauti. Baadhi ya wale waliopagawa walishindwa kuongea, wengine wakawa vipofu, wengine wakashikwa na wazimu, na wengine wakawa na nguvu zinazozidi zile za binadamu. (Mathayo 9:32; 12:22; 17:15, 18; Marko 5:2-5; Luka 8:29; 9:42; 11:14; Matendo 19:16) Nyakati nyingine mateso yaliongezeka pale roho waovu wengi walipompagaa mtu wakati uleule. (Luka 8:2, 30) Basi, Yehova ana sababu nzuri kwelikweli ya kuonya watu wake wajiepushe na uchawi na mazoea mengine ya kimafumbo.

Dini Inayotegemea Kweli

Wengi wanavutiwa na uchawi leo kwa sababu huo waonekana kuwa dini inayoabudu nguvu za asili, isiyo hatari, na isiyodhuru. Uchawi umekubaliwa katika jumuiya fulani. Watu hawauogopi. Badala yake, mara nyingi umepuuzwa. Katika hali ambapo kuvumiliwa kwa maoni mbalimbali ya kidini hufanya watu wakubali hata mambo ya ajabu, uchawi umeheshimiwa sana.

Kwa kweli, ulimwengu wa dini umekuwa soko ambapo watu wako huru kuchagua dini ambayo inatosheleza mahitaji yao, kama vile tu mtu awezavyo kununua viatu. Tofauti na hilo, Yesu alisema kuna uchaguzi mara mbili tu. Alisema: “Ingieni kupitia lango jembamba; kwa sababu ni pana na yenye nafasi barabara inayoongoza kuingia katika uharibifu, na wengi ndio wanaoingia kupitia hiyo; lakini lango ni jembamba na barabara ni yenye kufinyana inayoongoza kuingia katika uhai, na wachache ndio wanaoipata.” (Mathayo 7:13, 14) Bila shaka, tuko huru kuchagua njia tutakayofuata. Lakini kwa kuwa hali yetu njema ya milele yahusika, uchaguzi wetu ni muhimu sana. Ili kupata nuru ya kiroho, ni lazima tufuate njia ya ile kweli—njia ambayo yapatikana katika Neno la Mungu, Biblia peke yake.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Katika Kiingereza, wengine hutumia neno “magick” ili kuonyesha tofauti kati ya mafumbo na mizungu ya kuigiza. Ona Amkeni! la Septemba 8, 1993, ukurasa wa 26, “Je! Kuna Hatari Katika Kufanya Mizungu?”

[Picha katika ukurasa wa 5 6, 7]

Wengi leo huuona uchawi kuwa dini isiyodhuru ya kuabudu nguvu za asili

[Picha katika ukurasa wa 6]

Sikuzote mizungu imehusianishwa na mafumbo

[Picha katika ukurasa wa 6]

Je, wachawi wanafanya mapenzi ya Ibilisi bila kujua?

[Picha katika ukurasa wa 7]

Biblia hufunua njia ya kweli