Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Wanaopigana na Mungu Hawatashinda!

Wanaopigana na Mungu Hawatashinda!

Wanaopigana na Mungu Hawatashinda!

“Watapigana nawe; lakini hawatakushinda.”—YEREMIA 1:19.

1. Yeremia alipokea utume gani, na kazi yake iliendelea kwa muda gani?

YEHOVA alimpa kijana Yeremia utume wa kuwa nabii kwa mataifa. (Yeremia 1:5) Hilo lilitukia wakati wa utawala wa Mfalme Yosia wa Yuda aliyekuwa mwema. Huduma ya kiunabii ya Yeremia iliendelea hata katika kile kipindi chenye msukosuko kilichotangulia ushindi wa Babiloni dhidi ya Yerusalemu na kupelekwa kwa watu wa Mungu uhamishoni.—Yeremia 1:1-3.

2. Yehova alimtiaje Yeremia nguvu, na kupigana na nabii huyo kulimaanisha nini?

2 Ujumbe wa hukumu ambao Yeremia alipaswa kutangaza bila shaka ungetokeza upinzani. Basi, Mungu alimtia nguvu Yeremia kwa ajili ya mambo ambayo yangetokea. (Yeremia 1:8-10) Kwa mfano, roho ya nabii huyo ilitiwa nguvu kwa maneno haya: “Watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.” (Yeremia 1:19) Kupigana na Yeremia kungekuwa kupigana na Mungu. Leo, Yehova ana kikundi cha watumishi walio kama manabii wanaofanya kazi kama ile ya Yeremia. Kama nabii huyo, wanatangaza kwa ujasiri neno la Mungu la kiunabii. Na ujumbe huo unaathiri watu wote na mataifa yote, vizuri au vibaya, ikitegemea jinsi wanavyouitikia. Kama ilivyokuwa wakati wa Yeremia, kuna wale wanaopigana na Mungu kwa kuwapinga watumishi wake na kazi yao waliyopewa na Mungu.

Watumishi wa Yehova Washambuliwa

3. Kwa nini watumishi wa Yehova wamekuwa wakishambuliwa?

3 Watu wa Yehova wamekuwa wakishambuliwa tangu mwanzoni-mwanzoni mwa karne ya 20. Katika nchi nyingi, watu wenye nia mbaya wamejaribu kuzuia—naam, kunyamazisha—kutangazwa kwa habari njema za Ufalme wa Mungu. Wamechochewa na Mpinzani wetu mkuu, Ibilisi, ambaye “hutembea huku na huku kama simba anayenguruma, akitafuta sana kunyafua mtu fulani.” (1 Petro 5:8) “Nyakati zilizowekwa rasmi za mataifa” zilipoisha mwaka wa 1914, Mungu alimtawaza Mwana wake awe Mfalme mpya wa dunia, akampa amri hii: “Uwe na enzi kati ya adui zako.” (Luka 21:24; Zaburi 110:2) Akitumia mamlaka yake, Kristo alimfukuza Shetani kutoka mbinguni na kumtupa duniani. Akijua kwamba wakati wake ni mfupi, Ibilisi anawaghadhibikia Wakristo watiwa-mafuta na waandamani wao. (Ufunuo 12:9, 17) Kushambuliwa tena na tena na wale wapiganao na Mungu kumetokeza nini?

4. Watu wa Yehova walipata majaribu gani wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, lakini ni nini kilichotokea mwaka wa 1919 na 1922?

4 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Kwanza, watumishi watiwa-mafuta wa Yehova walikabili majaribu mengi ya imani. Walidhihakiwa na kuchongewa, wakakimbizwa na vikundi vya wafanya-ghasia, na kupigwa. Kama vile Yesu alivyotabiri, walikuwa “vitu vya kuchukiwa na mataifa yote.” (Mathayo 24:9) Taharuki ya vita ilipokuwa ikiendelea, adui za Ufalme wa Mungu walitumia mbinu iliyokuwa imetumiwa dhidi ya Yesu Kristo. Waliwasingizia watu wa Yehova kuwa wachochezi isivyo kweli, nao walishambulia sehemu ya maana sana ya tengenezo la Mungu lionekanalo. Mwezi wa Mei 1918, serikali ilitoa idhini za kumkamata msimamizi wa Watch Tower Society, J. F. Rutherford, na washirika wake saba wa karibu zaidi. Wanaume hao wanane walihukumiwa vifungo virefu gerezani na kupelekwa kwenye jela ya kitaifa huko Atlanta, Georgia, Marekani. Waliachiliwa miezi tisa baadaye. Mei 1919 mahakama ya rufani yenye kuzunguka ikaamua kuwa washtakiwa hao hawakuhukumiwa kwa haki, kwa hiyo hukumu hiyo ikafutwa. Kesi hiyo ilipangiwa kufanywa upya, lakini baadaye serikali ikayafuta mashtaka, na Ndugu Rutherford na wenzake wakaondolewa mashtaka kabisa. Walirudia utendaji wao, na mikusanyiko iliyofanywa huko Cedar Point, Ohio, mwaka wa 1919 na mwaka wa 1922 ikachochea upya kazi ya kuhubiri Ufalme.

5. Mashahidi wa Yehova walipatwa na nini katika Ujerumani ya Nazi?

5 Serikali za kidikteta zilitokea katika miaka ya 1930, na Ujerumani, Italia, na Japani zikaungana kuunda mamlaka Zilizofungamana. Mapema katika mwongo huo, watu wa Mungu walianza kunyanyaswa kikatili, hasa katika Ujerumani ya Nazi. Walipigwa marufuku. Nyumba zikasakwa, na wenye nyumba kukamatwa. Maelfu ya watu wakafungwa katika kambi za mateso kwa sababu walikataa kukana imani yao. Vita dhidi ya Mungu na watu wake ilikusudiwa kuwafagilia mbali Mashahidi wa Yehova katika milki hiyo ya kidikteta. * Mashahidi walipoenda katika mahakama za Ujerumani ili kupigania haki zao, Wizara ya Sheria ya Serikali hiyo ilitayarisha maelezo marefu ili kuhakikisha kuwa Mashahidi hawafaulu. Ilisema hivi: “Mahakama hazipaswi kushindwa kwa sababu tu ya zile zionekanazo kuwa hatua rasmi za kisheria; lakini zapaswa kutafuta na kupata njia licha ya magumu ya hizo hatua rasmi, ili kutimiza majukumu yake muhimu.” Hiyo ilimaanisha kuwa haki haingepatikana. Wanazi walisisitiza kwamba utendaji wa Mashahidi wa Yehova ulikuwa hatari, au wenye chuki, nao ‘ulivuruga muungano wa Kitaifa wa Kisoshalisti.’

6. Ni jitihada zipi zilizofanywa za kukomesha kazi yetu wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili na baadaye?

6 Wakati wa Vita ya Ulimwengu ya Pili, watu wa Mungu walipigwa marufuku na kuwekewa vizuizi katika Australia, Kanada, na nchi nyinginezo za Jumuiya ya Madola ya Uingereza—barani Afrika, Asia, na visiwa vya Karibea na vya Pasifiki. Nchini Marekani, maadui wenye uvutano na watu waliopashwa habari zisizo za kweli ‘walitunga madhara kwa njia ya sheria.’ (Zaburi 94:20) Lakini masuala ya kusalimu bendera na sheria za jumuiya zenye kupinga kuhubiri nyumba hadi nyumba yalipiganiwa mahakamani, na maamuzi mazuri nchini Marekani yalitokeza msingi wa kutegemeza uhuru wa ibada. Kwa msaada wa Yehova, jitihada za adui ziliambulia patupu. Vita ilipokoma barani Ulaya, marufuku ziliondolewa. Maelfu ya Mashahidi waliokuwa mateka katika kambi za mateso wakaachiliwa huru, lakini huo haukuwa mwisho wa kupigana. Mara baada ya Vita ya Ulimwengu ya Pili, ile Vita Baridi ikazuka. Mataifa ya Ulaya Mashariki yalizidi kuwakandamiza watu wa Yehova. Hatua rasmi zilichukuliwa ili kuingilia na kusimamisha utendaji wetu wa kutoa ushahidi, kuzuia kuenezwa kwa vichapo vya Biblia, na kukomesha makusanyiko ya hadharani. Wengi walitiwa gerezani au kupelekwa katika kambi za kazi ngumu.

Waendelea na Kazi ya Kuhubiri!

7. Mashahidi wa Yehova wamepatwa na hali gani nchini Poland, Urusi, na nchi nyinginezo katika miaka ya karibuni?

7 Kadiri miongo ilivyopita, kazi ya kuhubiri Ufalme ilianza kutokea wazi. Mwaka wa 1982, Poland, ingawa bado ilikuwa chini ya utawala wa Kikomunisti, iliruhusu mikusanyiko ya siku moja ifanywe. Mikusanyiko ya kimataifa ikafanywa huko mwaka wa 1985. Mikusanyiko mikubwa sana ya kimataifa ikafuata mwaka wa 1989, maelfu ya wahudhuriaji wakatoka Urusi na Ukrainia. Mwaka huo Hungaria na Poland zikawaandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova. Ukuta wa Berlin ulibomolewa katika vuli ya mwaka wa 1989. Miezi michache baadaye, tukaandikishwa kisheria nchini Ujerumani Mashariki, na muda mfupi baadaye, mkusanyiko wa kimataifa ukafanywa jijini Berlin. Na mwanzoni mwa mwongo wa mwisho wa karne ya 20, jitihada zilikuwa zinafanywa za kukutana kibinafsi na akina ndugu nchini Urusi. Baadhi ya maofisa jijini Moscow walifikiwa, na mwaka wa 1991, Mashahidi wa Yehova wakaandikishwa kisheria. Tangu wakati huo kazi imesitawi sana nchini Urusi na katika jamhuri ambazo zilikuwa sehemu ya Muungano wa Sovieti.

8. Ni nini kilichowapata watu wa Yehova katika ile miaka 45 baada ya kumalizika kwa Vita ya Ulimwengu ya Pili?

8 Ingawa mnyanyaso ulipungua katika maeneo fulani, uliongezeka kwingineko. Katika ile miaka 45 baada ya mwisho wa vita ya ulimwengu ya pili, nchi nyingi zilikataa kuwaandikisha kisheria Mashahidi wa Yehova. Isitoshe, sisi wenyewe au utendaji wetu ulipigwa marufuku katika nchi 23 barani Afrika, 9 barani Asia, 8 barani Ulaya, 3 katika Amerika ya Latini, na 4 katika mataifa fulani ya visiwa.

9. Mashahidi wa Yehova wamepatwa na mambo gani nchini Malawi?

9 Mashahidi wa Yehova nchini Malawi walipatwa na minyanyaso mikali kuanzia mwaka wa 1967. Kwa sababu ya msimamo wao wa kutokuwamo wakiwa Wakristo wa kweli, waamini wenzetu waliokuwa huko walikataa kununua kadi za chama cha kisiasa. (Yohana 17:16) Baada ya mkutano wa chama cha Malawi Congress Party mwaka wa 1972, ukatili ulianzishwa tena. Akina ndugu waliondoshwa nyumbani kwao na kunyimwa kazi ya kuajiriwa. Maelfu waliitoroka nchi hiyo ili kuepuka kuuawa. Lakini, je, hao wapiganao na Mungu na watu wake walishinda? La hasha! Hali zilipobadilika, kilele cha wahubiri wa Ufalme wapatao 43,767 waliripoti nchini Malawi mwaka wa 1999, na zaidi ya 120,000 wakahudhuria mikusanyiko ya wilaya huko. Ofisi mpya ya tawi imejengwa katika jiji kuu.

Wanatafuta Kisingizio

10. Kama ilivyo na kisa cha Danieli, wapinzani wa siku hizi wa watu wa Mungu wamefanya nini?

10 Waasi-imani, makasisi, na watu wengine hawawezi kuvumilia ujumbe wetu wa Neno la Mungu. Wakiwa chini ya mkazo wa vikundi vya dini za Jumuiya ya Wakristo, wapinzani hutafuta njia iitwayo eti ya kisheria ili kuhalalisha vita yao dhidi yetu. Ni mbinu gani ambazo hutumiwa nyakati nyingine? Wenye kula njama walifanya nini ili kumshambulia Danieli? Katika Danieli 6:4, 5, twasoma hivi: “Mawaziri na maamiri wakatafuta sana kupata sababu za kumshitaki Danieli kwa habari za mambo ya ufalme; lakini hawakuweza kuona sababu wala kosa; kwa maana alikuwa mwaminifu, wala halikuonekana kosa wala hatia ndani yake. Ndipo wale watu wakasema, Hatutapata sababu ya kumshitaki Danieli huyo, tusipoipata katika mambo ya sheria ya Mungu wake.” Hali kadhalika, leo wapinzani hutafuta kisingizio. Wao hupiga makelele wakisema juu ya “madhehebu hatari,” na kujaribu kuwataja Mashahidi wa Yehova. Kwa kutoa habari zisizo za kweli, visingizio, na uwongo, wao hushambulia ibada yetu na kushikamana kwetu na kanuni za Mungu.

11. Wapinzani fulani wa Mashahidi wa Yehova wametoa madai gani yasiyo ya kweli?

11 Katika nchi fulani, dini na mashirika ya kisiasa hukataa kutambua kwamba tuna “namna ya ibada iliyo safi na isiyo na unajisi kwa maoni ya Mungu wetu.” (Yakobo 1:27) Ingawa utendaji wetu wa Kikristo waendelezwa katika nchi 234, wapinzani wanadai kwamba sisi si “dini ijulikanayo.” Kabla tu ya mkusanyiko wa kimataifa mwaka wa 1998, gazeti moja la Athens liliwanukuu makasisi wa Othodoksi ya Kigiriki wakidai kwamba “[Mashahidi wa Yehova] si ‘dini ijulikanayo,’” licha ya uamuzi wa Mahakama ya Ulaya ya Haki za Kibinadamu uliokuwa tofauti na maneno yao. Siku chache baadaye, gazeti jingine katika jiji hilohilo lilimnukuu msemaji mmoja wa kanisa akisema: “[Mashahidi wa Yehova] si ‘Wakristo,’ kwa kuwa hawana imani ya Kikristo inayoonyeshwa na Yesu Kristo.” Hilo ni jambo lenye kushangaza, kwa kuwa hakuna kikundi kingine chochote cha kidini ambacho hukazia zaidi kumwiga Yesu kuliko wafanyavyo Mashahidi wa Yehova!

12. Tunapopigana vita ya kiroho, ni lazima tufanye nini?

12 Sisi hujitahidi kutetea na kuthibitisha habari njema kwa njia halali. (Wafilipi 1:7) Na hatuwezi kuridhiana au kughushi kushikamana kwetu kwa uthabiti na viwango vya Mungu vya uadilifu. (Tito 2:10, 12) Kama Yeremia, ‘twajifunga viuno na kusema maneno yote ambayo Yehova hutuamuru,’ bila kuwaruhusu wapiganao na Mungu watufadhaishe kwa njia yoyote. (Yeremia 1:17, 18) Neno Takatifu la Yehova limetuonyesha waziwazi njia tunayopaswa kufuata. Hatutaki kamwe kutegemea “mkono [dhaifu] wa mwili” au kutafuta “usalama nchini Misri,” yaani, ulimwengu huu. (2 Mambo ya Nyakati 32:8; Isaya 30:3, Biblia Habari Njema; 31:1-3) Tunapopigana vita ya kiroho, lazima tuendelee kumtumaini Yehova kwa moyo wetu wote, tuache aelekeze hatua zetu, na kutotegemea akili zetu wenyewe. (Mithali 3:5-7) Tusipomtegemea Yehova, naye asipotulinda, kazi yetu yote itakuwa “bure.”—Zaburi 127:1.

Wanyanyaswa Lakini Hawaridhiani

13. Kwa nini inaweza kusemwa kwamba mashambulizi ya kishetani dhidi ya Yesu hayakufaulu?

13 Yesu, aliyeshtakiwa isivyo kweli kuwa mchochezi na mwenye kuvuruga utaratibu uliokuwako, ndiye kielelezo bora kabisa cha ujitoaji kwa Yehova bila kuridhiana. Baada ya kuchunguza kisa cha Yesu, Pilato alitaka kumwachilia. Lakini umati, ukichochewa na viongozi wa kidini, ukapiga makelele Yesu atundikwe, ingawa hakuwa na hatia. Badala yake, waliomba Baraba aachiliwe—mtu aliyefungwa gerezani kwa sababu ya uchochezi na uuaji-kimakusudi! Pilato akajaribu tena kubadili maoni ya wapinzani hao wasiotumia akili, lakini hatimaye alishindwa na makelele ya watu. (Luka 23:2, 5, 14, 18-25) Ijapokuwa Yesu alikufa kwenye mti, shambulio hilo katili la kishetani dhidi ya Mwana wa Mungu asiye na hatia lilishindwa kabisa, kwa kuwa Yehova alimfufua Yesu na kumkweza hadi mkono Wake mwenyewe wa kuume. Na kupitia Yesu aliyetukuzwa, roho takatifu ilimwagwa siku ya Pentekoste ya mwaka wa 33 W.K., ikianzisha kutaniko la Kikristo—‘uumbaji mpya.’—2 Wakorintho 5:17; Matendo 2:1-4.

14. Ni nini kilichotokea wakati viongozi wa kidini wa Kiyahudi walipowapinga wafuasi wa Yesu?

14 Punde baadaye, watu wa kidini waliwatisha mitume, lakini wafuasi wa Kristo hawakuacha kusema juu ya mambo waliyokuwa wameona na kusikia. Wanafunzi wa Yesu walisali: “Yehova, yaangalie matisho yao, na kuwaruhusu watumwa wako kufuliza kusema neno lako kwa ujasiri wote.” (Matendo 4:29) Yehova alijibu dua yao kwa kuwajaza roho takatifu na kuwatia nguvu waendelee na kazi yao ya kutangaza bila woga. Muda si muda mitume wakaagizwa tena waache kuhubiri, lakini Petro na wale mitume wengine wakajibu hivi: “Lazima sisi tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.” (Matendo 5:29) Kutishwa, kukamatwa, wala kupigwa viboko hakukuwazuia wasipanue utendaji wao wa Ufalme.

15. Gamalieli alikuwa nani, naye aliwashaurije wapinzani wa kidini wa wafuasi wa Yesu?

15 Watawala wa kidini waliitikiaje? “Wakahisi wamechomwa sana nao wakawa wakitaka kuwamaliza [mitume].” Hata hivyo, mwalimu wa Sheria aitwaye Gamalieli, Farisayo, alikuwapo, naye alistahiwa sana na watu wote. Baada ya kuwatoa mitume nje ya jumba la Sanhedrini kwa muda mfupi, aliwashauri wapinzani hao wa kidini hivi: “Wanaume wa Israeli, jiangalieni nyinyi wenyewe kuhusu lile mkusudialo kufanya kwa habari ya watu hawa. . . . Nawaambia nyinyi, Msijiingize katika mambo ya watu hawa, bali waacheni; (kwa sababu, ikiwa mpango huu au kazi hii ni kutoka kwa wanadamu, itapinduliwa; lakini ikiwa ni kutoka kwa Mungu, hamtaweza kuwapindua;) ama sivyo, huenda mkaonwa kuwa wapiganaji dhidi ya Mungu kwa kweli.”—Matendo 5:33-39.

Hakuna Silaha Inayofanyika Juu Yetu Itakayofanikiwa

16. Kwa maneno yako mwenyewe, unaweza kufafanuaje uhakikishio ambao Yehova huwapa watu wake?

16 Gamalieli alitoa shauri zuri, na tunathamini wakati mtu anapotutetea. Pia twakubali kwamba uhuru wa ibada umetegemezwa na maamuzi ya mahakama yaliyofanywa na mahakimu wasio na ubaguzi. Bila shaka kushikamana kwetu na Neno la Mungu hakupendezi makasisi wa Jumuiya ya Wakristo na viongozi wengine wa Babiloni Mkubwa, milki ya ulimwengu ya dini isiyo ya kweli. (Ufunuo 18:1-3) Ingawa wao, pamoja na watu ambao wamechochea hupigana nasi, tuna uhakikishio huu: “Kila silaha itakayofanyika juu yako haitafanikiwa na kila ulimi utakaoinuka juu yako katika hukumu utauhukumu kuwa mkosa. Huu ndio urithi wa watumishi wa BWANA, na haki yao inayotoka kwangu mimi, asema BWANA.”—Isaya 54:17.

17. Japo wapinzani hupigana na sisi, kwa nini tuna ujasiri?

17 Adui zetu hupigana na sisi bila sababu, lakini hatupotezi ujasiri. (Zaburi 109:1-3) Hatutaruhusu kamwe watu wanaochukia ujumbe wetu wa Biblia watuogofye turidhiane imani yetu. Ijapokuwa twatarajia vita yetu ya kiroho izidi kuongezeka, twajua matokeo. Kama Yeremia, tutaona utimizo wa maneno haya ya kiunabii: “Nao watapigana nawe; lakini hawatakushinda; maana mimi nipo pamoja nawe, asema BWANA, ili nikuokoe.” (Yeremia 1:19) Naam, tunajua kwamba wapiganao na Mungu hawatashinda!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Ona makala yenye kichwa “Waaminifu na Wenye Ujasiri Japo Mnyanyaso wa Nazi,” ukurasa wa 24-28.

Ungejibuje?

• Kwa nini watumishi wa Yehova wameshambuliwa?

• Wapinzani wamepigana na watu wa Yehova katika njia zipi?

• Kwa nini tunaweza kuwa na hakika ya kwamba wale wapiganao na Mungu hawatashinda?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 17]

Yeremia alihakikishiwa kwamba Yehova angekuwa pamoja naye

[Picha katika ukurasa wa 18]

Waokokaji wa kambi za mateso

[Picha katika ukurasa wa 18]

Umati wenye ghasia ukiwashambulia Mashahidi wa Yehova

[Picha katika ukurasa wa 18]

J. F. Rutherford na wenzake

[Picha katika ukurasa wa 21]

Kuhusu Yesu, wale wapiganao na Mungu hawakushinda