Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Bado Biblia Inabadili Maisha Yako?

Je, Bado Biblia Inabadili Maisha Yako?

“Mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu.”—ROM. 12:2.

NYIMBO: 61, 52

1-3. (a) Inaweza kuwa vigumu kwetu kufanya mabadiliko gani baada ya kubatizwa? (b) Tunapoona kwamba kufanya mabadiliko fulani ni vigumu kuliko tulivyotarajia, tunaweza kujiuliza maswali gani? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

KEVIN [1] alipojifunza kweli, jambo kuu kwake lilikuwa kusitawisha urafiki wa karibu na Yehova. Hata hivyo, kwa miaka mingi alikuwa amejihusisha na kucheza kamari, kuvuta sigara, ulevi, na madawa ya kulevya. Ili apate kibali cha Mungu, Kevin alihitaji kuacha mazoea hayo yasiyopatana na Maandiko. Alifanikiwa kufanya hivyo kwa kumtegemea Yehova na nguvu za Neno Lake lililoandikwa.—Ebr. 4:12.

2 Je, baada ya kubatizwa Kevin aliacha kufanya mabadiliko maishani mwake? Hapana. Bado alihitaji kuendelea kusitawisha na kuboresha sifa zake za Kikristo. (Efe. 4:31, 32) Kwa mfano, alishangaa kujua kwamba ilikuwa vigumu sana kwake kudhibiti hasira. Kevin anakiri hivi: “Ilikuwa vigumu kudhibiti hasira yangu kuliko kuacha mwenendo wangu wa zamani!” Kusali kwa bidii na kujifunza Biblia kwa kina kulimsaidia Kevin afanye mabadiliko yaliyohitajika.

3 Kama Kevin, wengi wetu tulifanya mabadiliko makubwa kabla ya kubatizwa ili tuishi kulingana na matakwa ya msingi ya Biblia. Baada ya kubatizwa, tulitambua kwamba tunahitaji kuendelea kufanya mabadiliko, yasiyoonekana wazi, ili tumwige zaidi Mungu na Kristo. (Efe. 5:1, 2; 1 Pet. 2:21) Kwa mfano, huenda tumetambua kwamba tuna mtazamo wa kuwachambua chambua wengine, tunawaogopa wanadamu, tuna mwelekeo wa kupiga porojo zenye kuumiza, au udhaifu mwingine. Je, imekuwa vigumu kwako kufanya mabadiliko hayo kuliko ulivyotarajia? Ikiwa ndivyo, basi huenda ukajiuliza, ‘Kwa kuwa tayari nimefanya mabadiliko makubwa, kwa nini imekuwa vigumu kwangu kufanya mabadiliko madogo madogo? Ninaweza kufanya nini ili Biblia iendelee kubadili maisha yangu?’

UWE NA MATARAJIO HALISI

4. Kwa nini hatuwezi kumpendeza Yehova nyakati zote?

4 Sisi ambao tunamjua na tunampenda Yehova tunatamani kutoka moyoni kufanya mambo yanayomfurahisha. Hata hivyo, sisi si wakamilifu. Hata tuwe na tamaa kubwa kadiri gani, hatuwezi kumpendeza Mungu nyakati zote. Hali yetu ni kama ya mtume Paulo, aliyesema hivi: “Nina uwezo wa kutaka, bali uwezo wa kufanya yaliyo mazuri haupo.”—Rom. 7:18; Yak. 3:2.

5. Tulifanya mabadiliko gani kabla ya kubatizwa, lakini huenda tunaendelea kupambana na udhaifu gani?

5 Tumeondolea mbali dhambi ambazo zingefanya tusistahili kuwa katika kutaniko la Kikristo. (1 Kor. 6:9, 10) Hata hivyo, bado sisi si wakamilifu. (Kol. 3:9, 10) Kwa hiyo, kubatizwa au kukaa katika kweli kwa muda mrefu hakumaanishi kwamba hatutafanya makosa, kurudia mazoea fulani ya zamani, au kupambana na mtazamo na mwelekeo usiofaa. Huenda tukahitaji kupambana na udhaifu fulani kwa miaka mingi.

6, 7. (a) Ni nini kinachotuwezesha kuwa rafiki za Yehova ingawa sisi si wakamilifu? (b) Kwa nini hatupaswi kusita kumwomba Yehova msamaha?

6 Ingawa sisi si wakamilifu, bado tunaweza kufurahia kumtumikia Yehova au kuwa rafiki zake. Fikiria hili: Yehova alipotuvuta kwake, alijua kwamba wakati mwingine tutakosea. (Yoh. 6:44) Kwa kuwa Mungu anajua utu wetu na kilicho moyoni mwetu, bila shaka alijua ni udhaifu gani hasa ambao ungetusumbua. Na alijua kwamba mara kwa mara tutakosea. Hata hivyo, bado Yehova alitaka tuwe rafiki zake.

7 Upendo ulimchochea Yehova atupatie zawadi yenye thamani sana, yaani, dhabihu ya fidia ya Mwana wake mpendwa. (Yoh. 3:16) Tukitubu na kumwomba Yehova msamaha kwa msingi wa dhabihu hiyo yenye thamani tunapokosea, tunaweza kuwa na uhakika kwamba uhusiano wetu pamoja naye haujavunjika. (Rom. 7:24, 25; 1 Yoh. 2:1, 2) Je, tuhisi kwamba fidia haiwezi kutusaidia kwa sababu sisi si safi au tuna dhambi? La hasha! Hilo ni kama kukataa kunawa mikono wakati ni michafu. Kwa kweli, fidia imeandaliwa kwa ajili ya watenda dhambi wanaotubu. Nayo inatuwezesha kuwa rafiki za Yehova hata ingawa sisi si wakamilifu.—Soma 1 Timotheo 1:15.

8. Kwa nini hatupaswi kupuuza udhaifu wetu?

8 Bila shaka, hatupuuzi udhaifu wetu. Kuwa rafiki za Yehova kunahusisha kujitahidi kumwiga kwa ukaribu Mungu na Kristo na kusitawisha sifa zinazowapendeza. (Zab. 15:1-5) Isitoshe, kunahusisha kujitahidi kudhibiti mwelekeo wetu wenye dhambi, na ikiwezekana kuuondoa kabisa. Iwe tumebatizwa karibuni au tumekuwa katika kweli kwa miaka mingi, tunapaswa ‘kuendelea kurekebishwa upya.’—2 Kor. 13:11.

9. Tunajuaje kwamba tunaweza kuendelea kuvaa utu mpya?

9 Jitihada zinahitajika ili tuendelee ‘kurekebishwa upya’ na kuvaa “utu mpya.” Paulo aliwakumbusha waabudu wenzake hivi: “Mnapaswa kuuondolea mbali utu wa zamani unaolingana na mwenendo wenu wa kwanza na ambao unaharibiwa kulingana na tamaa zake za udanganyifu; bali kwamba mnapaswa kufanywa upya katika nguvu zinazoendesha akili yenu, na mnapaswa kuvaa utu mpya ulioumbwa kulingana na mapenzi ya Mungu katika uadilifu wa kweli na ushikamanifu.” (Efe. 4:22-24) Maneno ya lugha ya awali yanayotafsiriwa “mnapaswa kufanywa upya” yanaonyesha kwamba kuvaa utu mpya ni jambo linaloendelea. Jambo hilo linatia moyo kwa sababu linatuhakikishia kwamba hata iwe tumemtumikia Yehova kwa muda gani, tunaweza kufanya maendeleo katika kusitawisha na kuboresha sifa za Kikristo ambazo ni sehemu ya utu mpya. Naam, Biblia inaweza kuendelea kubadili maisha yetu.

KWA NINI NI VIGUMU SANA?

10. Tunapaswa kufanya nini ili Biblia iendelee kutusaidia kufanya mabadiliko, na huenda tukajiuliza maswali gani?

10 Ikiwa tunataka Neno la Mungu liendelee kufanya mabadiliko ndani yetu, ni lazima tujitahidi. Lakini kwa nini jitihada nyingi zinahitajika? Ikiwa Yehova anabariki jitihada zetu, je, haipaswi kuwa rahisi zaidi kufanya maendeleo ya kiroho? Kwa nini Yehova haingilii kati na kudhibiti mwelekeo wetu usiofaa ili iwe rahisi kwetu kuonyesha sifa za kiroho?

11-13. Kwa nini Mungu anatazamia tujitahidi kushinda udhaifu wetu?

11 Tunapotafakari kuhusu uumbaji, tunatambua kwamba Yehova ana nguvu sana. Kwa mfano, kila sekunde, jua hubadili tani milioni tano za vitu vyake vya asili kuwa nishati au nguvu. Ni kiasi kidogo tu cha nishati hiyo kinachofika duniani, hata hivyo, kinatosha kutupatia joto na mwanga unaohitajika ili kuendeleza uhai. (Zab. 74:16; Isa. 40:26) Yehova yuko tayari kuwapatia wanadamu kiasi fulani cha nguvu inapohitajika. (Isa. 40:29) Naam, Mungu angeweza kutupatia nguvu ili tushinde udhaifu wowote bila kufanya jitihada nyingi au kulazimika kujifunza kutokana na makosa yetu. Basi kwa nini hafanyi hivyo?

12 Yehova ametupatia zawadi isiyo na kifani, yaani, uhuru wa kuchagua. Tunapochagua kufanya mapenzi ya Mungu na kujitahidi kadiri tuwezavyo, tunaonyesha kina cha upendo wetu kwa Yehova na tamaa yetu ya kumfurahisha. Pia, tunathibitisha kwamba tunaunga mkono enzi yake kuu. Shetani anatilia shaka haki ya Yehova ya kutawala, hivyo tunapojitahidi kwa hiari kutetea enzi yake kuu, bila shaka Baba yetu mwema na mwenye shukrani anathamini sana. (Ayu. 2:3-5; Met. 27:11) Lakini, ikiwa Yehova angeingilia kati na kudhibiti mwelekeo wetu wenye dhambi ili tushinde udhaifu wetu bila kujitahidi, madai yetu ya kuwa washikamanifu na kuunga mkono enzi yake kuu yangekuwa maneno matupu tu.

13 Kwa hiyo, Yehova anatuambia tufanye “jitihada . . . yenye bidii” kusitawisha sifa za kiroho. (Soma 2 Petro 1:5-7; Kol. 3:12) Anatazamia tujitahidi sana kudhibiti mawazo na hisia zetu. (Rom. 8:5; 12:9) Tunapojitahidi kutoka moyoni kufanya hivyo, tunaridhika sana kwa kutambua kwamba bado Biblia inabadili maisha yetu.

RUHUSU NENO LA MUNGU LIENDELEE KUKUBADILISHA

14, 15. Tunaweza kufanya nini ili tusitawishe sifa ambazo Yehova anakubali? (Tazama sanduku “ Biblia na Sala Ilibadili Maisha Yao.”)

14 Tunapaswa kufanya nini ili tusitawishe sifa za kiroho na kumpendeza Yehova? Tunapaswa kufanya mengi zaidi ya kujiamulia wenyewe sifa tunazotaka kuboresha katika utu wetu. Tunahitaji kutia bidii na kufuata maagizo ya Mungu, kwa kuwa andiko la Waroma 12:2 linasema hivi: “Acheni kufanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo, bali mgeuzwe kwa kufanya upya akili yenu, ili mjihakikishie wenyewe mapenzi ya Mungu yaliyo mema na yenye kukubalika na makamilifu.” Kupitia Neno lake na roho takatifu, Yehova anatusaidia tutambue mapenzi yake na kuyafanya. Pia, anatusaidia tubadili maisha yetu ili tuishi kulingana na matakwa yake. Tunapaswa kujitahidi kusoma Biblia kila siku, kutafakari, na kusali ili tupate roho takatifu. (Luka 11:13; Gal. 5:22, 23) Tukikubali mwongozo wa roho takatifu ya Mungu na kuiga maoni ya Yehova kama yanavyofunuliwa katika Neno lake, basi mawazo, maneno, na matendo yetu yatazidi kufanana na ya Mungu. Hata hivyo, bado tutahitaji kuendelea kupambana na udhaifu wetu.—Met. 4:23.

Unaweza kunufaika ukikusanya na kupitia maandiko na makala zinazozungumzia udhaifu wako (Tazama fungu la 15)

15 Zaidi ya kusoma Biblia kila siku, tunahitaji kujifunza Neno la Mungu na machapisho ya Kikristo tukiwa na nia ya kuiga sifa nzuri za Yehova. Wengine wamenufaika kwa kukusanya na kusoma mara kwa mara maandiko na makala za Mnara wa Mlinzi au Amkeni! ambazo zinazungumzia jinsi ya kusitawisha sifa za Kikristo au jinsi ya kushinda udhaifu fulani.

16. Kwa nini hatupaswi kuvunjika moyo ikiwa hatufanyi mabadiliko haraka?

16 Ikiwa unafanya maendeleo ya kiroho polepole, ni vizuri ukumbuke kwamba kukua kunahitaji wakati. Kusitawisha sifa za kiroho ni jambo linaloendelea. Tunapaswa kuwa na subira tunapoendelea kuiruhusu Biblia ibadili maisha yetu. Huenda mwanzoni tukahitaji kujitia nidhamu ili tutende kulingana na Maandiko. Hata hivyo, baada ya muda, inaelekea itakuwa rahisi zaidi kufikiri na kutenda kama Mungu, na litakuwa jambo la kawaida kwetu kuwa na mawazo na matendo kama ya Mungu.—Zab. 37:31; Met. 23:12; Gal. 5:16, 17.

TAFAKARI BARAKA ZA WAKATI UJAO

17. Tukiwa washikamanifu kwa Yehova, tunaweza kutazamia nini wakati ujao?

17 Hatimaye, waabudu washikamanifu wa Yehova watapata fursa ya kumtumikia milele wakiwa wakamilifu. Wakati huo, hatutahitaji jitihada nyingi ili kuonyesha sifa za kiroho, bali sikuzote tutafurahia kufanya hivyo. Kwa sasa, fidia imetufungulia njia ya kumwabudu Mungu wetu mwenye upendo. Ingawa sisi si wakamilifu, tunaweza kufanya hivyo ikiwa tutaendelea kuruhusu nguvu za Neno lake zitugeuze.

18, 19. Kwa nini tuna uhakika kwamba Biblia inaweza kuendelea kubadili maisha yetu?

18 Kevin, aliyetajwa mwanzoni, alijitahidi sana kudhibiti hasira. Alitafakari na kutumia kanuni za Biblia, na alikubali msaada na ushauri kutoka kwa Wakristo wenzake. Kwa miaka michache, Kevin alifanya maendeleo makubwa. Hatimaye, akastahili kuwa mtumishi wa huduma, na kwa miaka 20 iliyopita, ametumikia akiwa mzee wa kutaniko. Hata hivyo, anatambua kwamba bado anahitaji kuendelea kupambana ili asirudie udhaifu wake.

19 Kisa cha Kevin kinaonyesha kwamba Biblia inawasaidia watu wa Mungu waendelee kufanya mabadiliko maishani. Kwa hiyo, tusikate tamaa tunapoendelea kuruhusu Neno la Mungu litugeuze na kutusaidia kuwa na uhusiano wa karibu na Yehova. (Zab. 25:14) Tunapoona Yehova akibariki jitihada zetu, tutakuwa na uhakika zaidi kwamba Biblia inaweza kuendelea kubadili maisha yetu.—Zab. 34:8.

^ [1] (fungu la 1) Jina limebadilishwa.