Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Na Alitimize Kusudi Lako Lote”

“Na Alitimize Kusudi Lako Lote”

“[Pata] furaha tele katika Yehova, naye atakupa maombi ya moyo wako.”​​—ZAB. 37:4.

NYIMBO: 135, 81

1. Kijana anahitaji kufanya uamuzi gani kuhusu wakati ujao, lakini kwa nini hakuna haja ya kuwa na wasiwasi kupita kiasi? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

IKIWA wewe ni kijana huenda ukakubali kwamba kabla ya kuanza safari, ni jambo la hekima kujua unapotaka kwenda. Maisha ni kama safari, na wakati unaofaa wa kupanga unapotaka kwenda ni unapokuwa kijana. Ni kweli kwamba si rahisi kufanya mipango. Msichana anayeitwa Heather anasema hivi: “Inaogopesha sana. Unahitaji kuamua jinsi utakavyotumia maisha yako.” Lakini jipe moyo. Yehova anawaambia hivi watu wake: “Usitazame huku na huku, kwa maana mimi ni Mungu wako. Nitakutia nguvu. Nitakusaidia kwelikweli.”​​—Isa. 41:10.

2. Unajuaje kwamba Yehova anataka upangie wakati ujao wenye furaha?

2 Yehova anakuhimiza upangie wakati wako ujao kwa hekima. (Mhu. 12:1; Mt. 6:​20) Anataka uwe na furaha. Tunajua hilo tunapochunguza mambo yenye kupendeza katika uumbaji wake kama vile mandhari nzuri, sauti tamu, na ladha mbalimbali ya vyakula. Fikiria pia jinsi anavyotutunza na kutufundisha kuishi maisha bora zaidi. Yehova anawaambia hivi wale wanaokataa ushauri wake: “Mlichagua jambo ambalo halikunipendeza. . . . Tazama! Watumishi wangu watashangilia, lakini ninyi mtaona aibu. Tazama! Watumishi wangu watapiga vigelegele kwa shangwe kwa sababu ya hali nzuri ya moyo.” (Isa. 65:​12-​14) Yehova hutukuzwa watu wake wanapofanya maamuzi ya hekima maishani.​​—Met. 27:11.

MIPANGO ITAKAYOKUFANYA UWE NA FURAHA

3. Yehova anapendekeza ufanye nini?

3 Yehova anakupendekezea mipango gani? Aliwaumba wanadamu wapate furaha kwa kumjua na kumtumikia kwa uaminifu. (Zab. 128:1; Mt. 5:3) Hilo ni tofauti kabisa na wanyama alioumba, ambao wanaridhika tu kula, kunywa, na kupata watoto. Mungu anataka upate furaha kwa kupangia mambo mengine, tofauti na yale yanayowaridhisha wanyama. Muumba wako ni “Mungu wa upendo,” “Mungu mwenye furaha,” aliyewaumba wanadamu “kwa mfano wake.” (2 Kor. 13:11; 1 Tim. 1:​11; Mwa. 1:​27) Utakuwa mwenye furaha ukimwiga Mungu wetu mwenye upendo. Je, umewahi kujionea ukweli wa andiko hili: “Kuna furaha zaidi katika kutoa kuliko ilivyo katika kupokea”? (Mdo. 20:35) Huo ni ukweli wa msingi kuhusu maisha ya mwanadamu. Kwa hiyo, Yehova anataka ufanye mipango ambayo itaonyesha kwamba unampenda Mungu na wanadamu wenzako.​​—Soma Mathayo 22:​36-​39.

4, 5. Ni nini kilichomfanya Yesu awe na furaha?

4 Yesu Kristo aliwawekea ninyi vijana mfano bora kabisa. Bila shaka, alipokuwa mtoto alicheza na kufurahia maisha. Neno la Mungu linasema kwamba kuna “wakati wa kucheka . . . na wakati wa kurukaruka.” (Mhu. 3:4) Yesu pia alimkaribia Yehova kwa kujifunza Maandiko. Alipokuwa na umri wa miaka 12, walimu waliokuwa hekaluni walishangazwa na “uelewaji wake na majibu yake” kuhusu mambo ya kiroho.​​—Luka 2:​42, 46, 47.

5 Yesu aliendelea kuwa mwenye furaha hata alipokuwa mtu mzima. Ni nini kilichomfanya awe na furaha? Kati ya mambo mengi aliyofahamu, Yesu alijua pia kwamba Mungu alitaka ‘awatangazie maskini habari njema na kupata kuona tena kwa vipofu.’ (Luka 4:​18) Kufanya mapenzi ya Mungu kulimfanya Yesu awe na furaha. Andiko la Zaburi 40:8 linaonyesha hisia zake, linasema hivi: “Ee Mungu wangu, nimependezwa na kufanya mapenzi yako.” Yesu alifurahia kuwafundisha watu kuhusu Baba yake wa mbinguni. (Soma Luka 10:21.) Pindi moja baada ya kumfundisha mwanamke fulani kuhusu ibada ya kweli, Yesu aliwaambia hivi wanafunzi wake: “Chakula changu ni mimi kufanya mapenzi yake aliyenituma na kuimaliza kazi yake.” (Yoh. 4:​31-​34) Kumpenda Mungu na wanadamu kulimfanya Yesu awe na furaha. Ukifanya hivyo, utakuwa mwenye furaha pia.

6. Kwa nini ni jambo la hekima kuzungumzia mipango yako ya wakati ujao pamoja na Wakristo wakomavu?

6 Wakristo wengi walipata furaha kwa kutumikia wakiwa mapainia walipokuwa vijana. Kwa nini usizungumzie mipango yako pamoja na baadhi yao? “Mipango huvunjika mahali ambapo hapana mazungumzo ya siri, lakini katika wingi wa washauri mambo hutimizwa.” (Met. 15:22) Watu waliokomaa kiroho kama hao watakueleza kwamba utumishi wa wakati wote huandaa elimu itakayokunufaisha katika maisha yako yote. Yesu alifundishwa na Baba yake alipokuwa mbinguni na aliendelea kujifunza hata alipokuwa katika huduma yake hapa duniani. Kwa mfano, alipata shangwe alipoona jinsi habari njema ilivyogusa mioyo ya watu na alipata shangwe pia kwa kudumisha utimilifu alipojaribiwa. (Soma Isaya 50:4; Ebr. 5:8; 12:2) Acheni tuchunguze baadhi ya mambo katika utumishi wa wakati wote yanayoweza kukufanya uwe mwenye furaha kwelikweli.

KUFANYA WANAFUNZI NDIYO KAZI BORA ZAIDI

7. Kwa nini vijana wengi wanafurahia kufanya wanafunzi?

7 Yesu alisema: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu . . . na kuwafundisha.” (Mt. 28:​19, 20) Ikiwa umepanga kuingia katika utumishi wa wakati wote ukiwa painia, umechagua kazi inayoridhisha sana na inayomtukuza Mungu. Kama ilivyo na kazi nyingine yoyote, unahitaji muda ili upate ustadi. Ndugu anayeitwa Timothy aliyeanza upainia akiwa tineja, alisema hivi: “Ninafurahia kumtumikia Yehova wakati wote kwa sababu ninapofanya hivyo ninaonyesha kwamba ninampenda. Mwanzoni, nisingeweza kuanzisha mafunzo ya Biblia, lakini baadaye nilipohamia eneo lingine, nilianzisha mafunzo kadhaa ndani ya mwezi mmoja. Mwanafunzi mmoja alianza kuhudhuria mikutano. Baada ya kuhudhuria Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja * ambayo hufanywa kwa miezi miwili, nilipokea mgawo mpya na nikaanzisha mafunzo manne. Ninapenda kuwafundisha watu kwa kuwa ninashuhudia roho takatifu ikibadili maisha yao.”​​—1 The. 2:​19.

8. Vijana fulani Wakristo wameongezaje utendaji wao katika kazi ya kufanya wanafunzi?

8 Baadhi ya vijana Wakristo wamejifunza lugha nyingine. Kwa mfano, Jacob, anayeishi Amerika Kaskazini, aliandika hivi: “Nilipokuwa na umri wa miaka saba, wanafunzi wengi niliosoma nao walikuwa wametoka Vietnam. Nilitaka kuwafundisha kumhusu Yehova, kwa hiyo baada ya muda nilifanya mipango ya kujifunza lugha yao. Nilijifunza hasa kwa kulinganisha gazeti la Mnara wa Mlinzi la Kiingereza na la Kivietnam. Pia, nilitafuta marafiki katika kutaniko la Kivietnam lililokuwa karibu. Nilipokuwa na umri wa miaka 18, nilianza upainia. Baadaye, nilihudhuria Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja. Shule hiyo inanisaidia katika mgawo wangu wa sasa nikiwa painia katika kikundi cha Kivietnam, ambapo mimi pekee ndiye mzee. Wavietnam wengi wanashangaa kwamba nimejifunza lugha yao. Wao hunikaribisha nyumbani, na mara nyingi mimi huanzisha funzo la Biblia pamoja nao. Baadhi yao wamefikia hatua ya kubatizwa.”​​—Linganisha Matendo 2:​7, 8.

9. Kazi ya kufanya wanafunzi inatuelimishaje?

9 Kazi ya kufanya wanafunzi hukuelimisha kwa kuwa unajifunza kuwa na mazoea mazuri ya kufanya kazi, unaboresha ustadi wako wa kuwasiliana, na unakuwa na uhakika na busara. (Met. 21:5; 2 Tim. 2:​24) Vilevile, unapofanya wanafunzi utapata shangwe kubwa kwa sababu utaelewa msingi wa Kimaandiko wa imani yako. Pia, utajifunza kufanya kazi kwa ukaribu na Yehova.​​—1 Kor. 3:9.

10. Unawezaje kushiriki katika shangwe ya kufanya wanafunzi hata katika eneo lisilo na matokeo?

10 Unaweza kufurahia kazi ya kufanya wanafunzi hata ikiwa watu wachache tu katika eneo lenu ndio wanaokubali habari njema. Kazi ya kufanya wanafunzi inahusisha watu wengi wanaofanya kazi kwa umoja. Kutaniko zima hutafuta watu wanyoofu. Huenda ndugu au dada mmoja tu ndiye aliyempata mtu ambaye mwishowe atakuwa mwanafunzi, lakini kutaniko zima lilishiriki katika kazi ya kuwatafuta watu wanyoofu na wote wanashangilia kumpata mwanafunzi huyo. Kwa mfano, Brandon alitumikia akiwa painia kwa miaka tisa katika eneo ambalo halikuwa na matokeo. Anasema hivi: “Ninapenda kuhubiri habari njema kwa sababu Yehova ametuagiza tufanye hivyo. Nilianza upainia muda mfupi baada ya kumaliza shule. Ninafurahia kuwatia moyo ndugu vijana katika kutaniko letu na kuona wakifanya maendeleo ya kiroho. Baada ya kuhudhuria Shule ya Biblia ya Ndugu Waseja, nilipata mgawo mpya. Ni kweli kwamba sijapata mtu ambaye amefanya maendeleo hadi kufikia ubatizo katika eneo hilo, lakini wengine wamefaulu. Ninafurahi kwamba nilipanga kushiriki kikamili katika kazi ya kufanya wanafunzi.”​​—Mhu. 11:6.

MIPANGO YAKO INAWEZA KUKUELEKEZA WAPI?

11. Vijana wengi wamefurahia aina gani ya utumishi mtakatifu?

11 Kuna fursa nyingi za kumtumikia Yehova. Kwa mfano, vijana wengi wanajitolea katika kazi ya ujenzi. Majumba mengi ya Ufalme yanahitajiwa. Kujenga majumba hayo ni kazi takatifu inayomtukuza Mungu na inayoweza kukufanya uwe na furaha. Kama ilivyo na utumishi mwingine wa wakati wote, kushirikiana na wafanyakazi wenzako huleta shangwe. Kujenga majengo ya ibada pia hukuelimisha kwa kuwa unajifunza kujali usalama, kufanya kazi kwa bidii, na kushirikiana na wanaoongoza.

Wale wanaoingia katika utumishi wa wakati wote watapata baraka nyingi (Tazama fungu la 11 hadi 13)

12. Utumishi wa upainia unaweza kutupatia fursa zipi nyingine?

12 Ndugu anayeitwa Kevin anasema hivi: “Tangu nilipokuwa mvulana mdogo, nilikuwa na lengo la kumtumikia Yehova wakati wote. Mwishowe, nilianza upainia nilipokuwa na umri wa miaka 19. Ili nijitegemeze, niliajiriwa kufanya kazi ya muda na ndugu aliyekuwa mjenzi. Nilijifunza kuweka paa, madirisha, na milango. Kisha, baada ya kimbunga kutokea, nilitumika kwa miaka miwili kujenga Majumba ya Ufalme na nyumba za akina ndugu nikiwa katika kikosi cha kutoa msaada. Niliposikia kwamba kuna uhitaji wa wajenzi nchini Afrika Kusini, nilijaza fomu na nikapokea mwaliko. Hapa Afrika, ninashiriki kujenga Majumba ya Ufalme, na ninafurahia kukamilisha mradi mmoja baada ya mwingine kila baada ya majuma kadhaa. Kikundi chetu cha ujenzi ni kama familia. Tunaishi pamoja, tunajifunza Biblia pamoja, na kufanya kazi pamoja. Pia, ninafurahia kuhubiri na ndugu kutanikoni kila juma. Mipango niliyofanya nikiwa mvulana imenifanya niwe mwenye furaha kuliko nilivyotarajia.”

13. Utumishi wa Betheli unawasaidiaje vijana wawe wenye furaha?

13 Baadhi ya vijana waliofikia malengo yao ya kumtumikia Yehova wakati wote sasa wanatumikia Betheli. Utumishi wa Betheli unaleta furaha kwa sababu mambo yote unayofanya hapo unamfanyia Yehova. Familia ya Betheli inasaidia kuandaa chakula cha kiroho. Mwanabetheli anayeitwa Dustin anasema hivi: “Nilijiwekea lengo la kuwa mtumishi wa wakati wote nilipokuwa na umri wa miaka tisa, na nilianza upainia nilipomaliza shule. Baada ya mwaka mmoja na nusu, nilialikwa Betheli, ambapo nilijifunza kutumia mashine ya kuchapisha na baadaye nilijifunza kutayarisha programu za kompyuta. Nikiwa Betheli, ninafurahia kupata habari moja kwa moja kutoka shambani kuhusu maendeleo ya ulimwenguni pote ya kazi ya kufanya wanafunzi. Ninapenda kutumikia hapa kwa sababu kazi tunazofanya zinawasaidia watu wamkaribie Yehova.”

UNAPANGA KUFANYA NINI WAKATI UJAO?

14. Unaweza kufanya mipango ya kuingia katika utumishi wa wakati wote jinsi gani?

14 Unaweza kufanya mipango gani ili uwe mhudumu Mkristo wa wakati wote? Zaidi ya yote, sifa za kiroho zitakusaidia ufanikiwe kumtumikia Yehova kikamili. Kwa hiyo, uwe na bidii katika kujifunza Neno la Mungu, tafakari kwa kina maana ya mambo unayojifunza, na utafute njia za kuonyesha imani yako katika mikutano ya kutaniko. Unapokuwa shuleni, unaweza kupata uzoefu na ustadi wa kuhubiri habari njema. Jifunze kupendezwa na watu kwa kuwauliza kwa busara maoni yao na kusikiliza majibu yao. Pia, unaweza kujitolea kufanya kazi kutanikoni kama vile kusaidia kufanya usafi na kudumisha Jumba la Ufalme. Yehova anafurahia kuwatumia watu wanyenyekevu na walio tayari kutumika. (Soma Zaburi 110:3; Mdo. 6:​1-3) Mtume Paulo alimwalika Timotheo ajiunge naye katika utumishi wa umishonari kwa sababu “alishuhudiwa vema na akina ndugu.”​​—Mdo. 16:​1-5.

15. Unaweza kufanya mipango gani ili ujiruzuku?

15 Kwa kawaida watumishi wa wakati wote wanahitaji kujiruzuku. (Mdo. 18:​2, 3) Labda miaka michache ya kujifunza ufundi fulani itakuwezesha kupata kazi ya muda inayopatikana kwa urahisi katika eneo lenu. Unapofanya mipango, zungumza na mwangalizi wenu wa mzunguko na mapainia katika mzunguko wenu. Waulize kazi zinazowafaa mapainia. Na kama Biblia inavyosema, “mkabidhi Yehova mwenyewe kazi zako nayo mipango yako itafanywa imara.”​​—Met. 16:3; 20:18.

16. Kumtumikia Yehova kikamili ukiwa kijana kutakutayarishaje kwa ajili ya majukumu mengine wakati ujao?

16 Unaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova anataka ‘ushike imara’ wakati ujao wenye furaha. (Soma 1 Timotheo 6:​18, 19.) Utumishi wa wakati wote unakusaidia kukomaa ukiwa Mkristo kwa sababu unafanya kazi na watumishi wengine wa wakati wote. Wengi wametambua kwamba kumtumikia Yehova kikamili walipokuwa vijana kunawasaidia pia kuwa na ndoa nzuri zaidi. Mara nyingi, wale waliokuwa mapainia kabla ya kufunga ndoa wameendelea katika utumishi huo wakiwa wenzi wa ndoa.​​—Rom. 16:​3, 4.

17, 18. Kufanya mipango kunahusisha moyo wako katika njia gani?

17 Kufanya mipango kunahusisha moyo wako. Zaburi 20:4 inasema hivi kumhusu Yehova: “Na akupe kulingana na moyo wako, naye na alitimize kusudi lako lote.” Hivyo, fikiria jinsi unavyotaka kutumia maisha yako. Fikiria kile ambacho Yehova anafanya katika siku zetu na jinsi unavyoweza kushiriki katika utumishi wake. Kisha upange kufanya kile kitakachomfurahisha.

18 Kumtumikia Yehova kikamili kutafanya uridhike sana kwa sababu hayo ndiyo maisha yanayomtukuza Mungu. Naam, “[pata] furaha tele katika Yehova, naye atakupa maombi ya moyo wako.”​​—Zab. 37:4.

^ fu. 7 Sasa ni Shule ya Waeneza-Injili wa Ufalme.