Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

“Ufalme Wako na Uje”—Biblia Kitabu cha Unabii Sahihi, Sehemu ya 8

“Ufalme Wako na Uje”

“Ufalme Wako na Uje”—Biblia Kitabu cha Unabii Sahihi, Sehemu ya 8

Hii ndiyo makala ya mwisho katika mfululizo wa makala nane katika gazeti la “Amkeni!” zinazozungumzia jambo la pekee kuhusu Biblia—unabii wake, au utabiri. Makala hizi zinajibu maswali haya: Je, unabii wa Biblia ulibuniwa na wanadamu werevu? Au kuna mambo yanayoonyesha kwamba uliongozwa na roho ya Mungu? Tunakukaribisha uchunguze uthibitisho.

KWA miaka elfu mbili hivi, watu wanaodai kuwa Wakristo wamekuwa wakisali kwamba Ufalme wa Mungu uje. Sala hiyo inategemea maneno ya Yesu mwenyewe. Aliwafundisha wanafunzi wake wasali hivi: “Ufalme wako na uje. Mapenzi yako na yatendeke duniani kama ilivyo mbinguni.”​—Mathayo 6:10.

Ufalme huo ambao watu wengi sana husali kuuhusu ni nini? Ni serikali ya Mungu ya kimbingu, na itachukua mahali pa serikali nyingine zote. Akiwa Mfalme aliyewekwa rasmi wa Ufalme huo, Yesu Kristo hutimiza mapenzi ya Mungu mbinguni na duniani. (Danieli 2:44; 7:13, 14) Kwa wakati wake, Mungu atajibu sala hiyo ya kielelezo kwa kumaliza uovu na kuteseka na kuuokoa “umati mkubwa” usioweza kuhesabika wa waabudu washikamanifu. (Ufunuo 7:9, 10, 13-17) Kisha, “waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”​—Zaburi 37:29.

Je, kuna njia yoyote ya kujua ni hali gani hususa tunazoweza kutarajia chini ya utawala wa Kristo? Ndiyo! Yesu alipokuwa hapa duniani alionyesha tamaa na uwezo wake wa kutatua matatizo ya wanadamu. Acheni tuchunguze unabii wa Biblia na kuona jinsi Yesu alivyotangulia kuonyesha kile ambacho atafanya duniani pote akiwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu.

Unabii wa 1:

“Yehova . . . anakomesha vita mpaka kwenye mwisho wa dunia. Upinde anauvunja na kuukata mkuki vipande-vipande; magari ya kukokotwa anayateketeza motoni.”—Zaburi 46:8, 9.

Utimizo: Yesu Kristo, yule “Mkuu wa Amani,” ataleta amani ya kudumu duniani. Kupitia programu yenye amani ya kuelimisha watu na kuondoa silaha duniani, Ufalme wa Mungu utawaunganisha wanadamu wote katika undugu mmoja wa kweli wa kimataifa.​—Isaya 2:2-4; 9:6, 7; 11:9.

Historia inafunua nini?

Yesu aliwafundisha wafuasi wake wasitumie silaha, lakini waishi kwa amani kati yao wenyewe. Mmoja wa wanafunzi wake alipotumia silaha kumlinda, Yesu alimwambia: “Rudisha upanga wako mahali pake, kwa maana wale wote wanaouchukua upanga wataangamia kwa upanga.” (Mathayo 26:51, 52) Yesu alisema kwamba Wakristo wa kweli wangetambuliwa kwa upendo wanaoonyeshana.—Yohana 13:34, 35.

Unabii wa 2:

“Kutakuwa na wingi wa nafaka duniani; juu ya milima kutakuwa na mafuriko.”​—Zaburi 72:16.

Utimizo: Ufalme wa Mungu utaondoa utapiamlo, upungufu wa chakula, na njaa. Kila mtu atakuwa na chakula kingi kizuri.

Historia inafunua nini?

Huruma ya Yesu kuelekea watu wenye njaa ilionekana wazi, na uwezo wake wa kimuujiza wa kulisha umati mkubwa ulikuwa wenye kustaajabisha. Mtu mmoja aliyejionea muujiza huo aliripoti hivi: “[Yesu] akauamuru umati uketi kwenye majani naye akachukua ile mikate mitano na wale samaki wawili, akatazama juu mbinguni, akatoa baraka na, baada ya kuimega ile mikate, akawagawia wanafunzi, nao wanafunzi wakaugawia ule umati. Kwa hiyo wote wakala wakashiba, nao wakaokota vipande vilivyobaki, vikapu kumi na viwili vilivyojaa. Na bado wale waliokula walikuwa wanaume karibu elfu tano, bila kuhesabu wanawake na watoto wachanga.”​—Mathayo 14:14, 19-21.

Unabii wa 3:

“Hakuna mkaaji atakayesema: ‘Mimi ni mgonjwa.’” (Isaya 33:24) “Macho ya vipofu yatafunguliwa, na masikio ya viziwi yatazibuliwa. Wakati huo kilema atapanda juu kama vile paa anavyofanya, na ulimi wa bubu utapaaza sauti kwa furaha.”​—Isaya 35:5, 6.

Utimizo: Ufalme wa Mungu utaondoa magonjwa na udhaifu wa aina zote. Vipofu wataona, na viziwi watasikia na kusema. Hakuna mtu atakayehitaji tena dawa, hospitali, au madaktari.

Historia inafunua nini?

Yesu alipowafundisha watu kuhusu Ufalme wa Mungu, aliwaponya wote waliokuwa wagonjwa na wenye udhaifu. Kwa hiyo, kwa kiwango kidogo, Yesu alionyesha kile ambacho atafanya duniani pote akiwa Mfalme wa Ufalme wa kimbingu wa Mungu.​—Luka 7:22; 9:11.

Unabii wa 4:

Mungu “kwa kweli atameza kifo milele.”—Isaya 25:8.

Utimizo: Wakati Yesu atakapotawala akiwa Mfalme wa Ufalme wa Mungu, wale “waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho” watafufuliwa waishi katika dunia iliyo paradiso. (Yohana 5:28, 29) Yesu atashinda kifo, adui yetu mkatili zaidi, na hivyo kutuwezesha kufurahia uzima wa milele.​—Zaburi 37:29.

Historia inafunua nini?

Katika pindi tatu hivi, Yesu alionyesha nguvu zake kwa kumfufua mtu aliyekuwa amekufa. (Luka 7:11-15; 8:41-55; Yohana 11:38-44) Baada ya Yesu mwenyewe kufa, watu 500 hivi walishuhudia kwamba alikuwa amefufuliwa.​—1 Wakorintho 15:3-8.

Mfululizo huu wa makala nane umezungumzia unabii mwingi wa Biblia ambao umetimia. Unabii huo wote, pamoja na mwingine mwingi, unaonyesha kwamba Biblia si kitabu kilichobuniwa na wanadamu werevu tu. Badala yake, kuna uthibitisho wa wazi kwamba kiliongozwa na roho ya Mungu. Hakuna shaka kwamba “Maandiko yote Matakatifu yameandikwa kwa uongozi wa Mungu.”​—2 Timotheo 3:16, Biblia Habari Njema.

Kwa kuwa Biblia ni kitabu cha unabii wa kweli, una kila sababu ya kuamini kwamba “bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena; nawe hakika utapaangalia mahali pake, naye hatakuwapo. Bali wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”​—Zaburi 37:10, 11.