Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Husamehe Dhambi Nzito?

Je, Mungu Husamehe Dhambi Nzito?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Husamehe Dhambi Nzito?

REHEMA ni mojawapo ya sifa kuu za Mungu. (Zaburi 86:15) Mungu huonyesha rehema kwa kadiri gani? Mtunga-zaburi aliandika hivi: “Kama ungekuwa unaangalia makosa, Ee Yah, Ee Yehova, ni nani angesimama? Kwa maana kwako wewe kuna msamaha wa kweli, ili upate kuogopwa.” (Zaburi 130:3, 4) Andiko lingine linasema hivi: “Kama vile mashariki ilivyo mbali sana na magharibi, ndivyo ameweka makosa yetu mbali sana na sisi. Kama vile baba anavyowaonyesha wanawe rehema, ndivyo ambavyo Yehova amewaonyesha rehema wale wanaomwogopa. Kwa maana yeye mwenyewe analijua vema umbo letu, akikumbuka kwamba sisi ni mavumbi.”—Zaburi 103:12-14.

Ni wazi kwamba rehema ya Yehova ni kamili na inatolewa kwa ukarimu, nayo hutilia maanani udhaifu na kutokamilika kwetu—kwamba sisi ni “mavumbi.” Fikiria mifano ya Biblia inayoonyesha kiwango cha rehema ya Mungu.

Mtume Petro alimkana Kristo mara tatu. (Marko 14:66-72) Kabla ya kuwa mwamini, mtume Paulo aliwatesa wafuasi wa Kristo. Ulipofika wakati wa baadhi yao kuuawa, Paulo alipiga kura dhidi yao. Hata alikubaliana na kuuawa kwa mmoja wao. (Matendo 8:1, 3; 9:1, 2, 11; 26:10, 11; Wagalatia 1:13) Kabla ya kuwa Wakristo, washiriki fulani wa kutaniko la Korintho walikuwa walevi, wanyang’anyi, na wezi. (1 Wakorintho 6:9-11) Hata hivyo, wote hao walipata kibali cha Mungu. Kwa nini Mungu aliwasamehe?

Hatua Tatu za Kupata Rehema ya Mungu

“Nilionyeshwa rehema, kwa sababu nilikosa ujuzi nami nilitenda kwa ukosefu wa imani,” aliandika Paulo. (1 Timotheo 1:13) Maneno yake ya wazi yanaonyesha kwamba hatua ya kwanza tunayopaswa kuchukua ili tupate msamaha wa Mungu ni kupata ujuzi sahihi wa Yehova na viwango vyake vinavyoonyeshwa katika Biblia. (2 Timotheo 3:16, 17) Kwa hakika hatuwezi kumpendeza Muumba wetu ikiwa hatumjui vema. “Uzima wa milele ndio huu,” Yesu alisema aliposali kwa Baba yake, “waendelee kupata ujuzi juu yako wewe, Mungu wa pekee wa kweli, na juu ya yule uliyemtuma, Yesu Kristo.”—Yohana 17:3.

Watu wenye mioyo minyoofu wanapopata ujuzi huo, wanajutia sana makosa waliyofanya wakati uliopita na wanachochewa kutubu kutoka moyoni. Hiyo ndiyo hatua ya pili ili tupate msamaha wa Mungu. Andiko la Matendo 3:19 linasema hivi: “Kwa hiyo, tubuni na mgeuke ili dhambi zenu zipate kufutwa.”

Andiko hilo pia linataja hatua ya tatu—kugeuka. Kugeuka kunamaanisha kuacha mwenendo na mtazamo wa zamani na kufuata viwango vya Mungu na maoni yake. (Matendo 26:20) Kwa maneno mengine, mtu anapobadili tabia yake anaonyesha kwamba anasema kweli anapomwambia Mungu, “Ninaomba msamaha.”

Msamaha wa Mungu Una Mipaka

Kuna watu ambao dhambi zao hazisamehewi na Mungu. Paulo aliandika: “Tukizoea kutenda dhambi kimakusudi baada ya kupokea ujuzi sahihi juu ya kweli, hakuna tena dhabihu yoyote iliyobaki kwa ajili ya dhambi, lakini kuna tarajio hakika lenye kuogopesha la hukumu.” (Waebrania 10:26, 27) Maneno ‘kuzoea kutenda dhambi kimakusudi’ yanarejelea ubaya uliokolea ndani ya mtu, moyo ambao ni mwovu kwelikweli.

Yuda Iskariote alisitawisha moyo kama huo. “Ingalikuwa afadhali kwake kama mtu huyo asingalizaliwa,” akasema Yesu. (Mathayo 26:24, 25) Kuhusu viongozi fulani wa kidini wa wakati huo, Yesu alisema hivi: “Ninyi mmetoka kwa baba yenu Ibilisi . . . Anaposema uwongo, yeye husema kulingana na mwelekeo wake mwenyewe, kwa sababu yeye ni mwongo na ndiye baba ya uwongo.” (Yohana 8:44) Kama Shetani, watu hao walikuwa wabaya kabisa. Hawakujutia kile walichofanya bali walikuwa sugu zaidi katika njia zao za uovu. * Ni kweli kwamba kwa sababu ya kutokamilika na udhaifu, Wakristo wa kweli pia wanafanya dhambi, mara nyingine hata wanafanya dhambi nzito. Lakini dhambi zao hazionyeshi kwamba wao ni waovu.—Wagalatia 6:1.

Alionyesha Rehema Mpaka Mwisho

Yehova haangalii tu dhambi iliyofanywa bali yeye huangalia pia mtazamo wa mtenda-dhambi. (Isaya 1:16-19) Hebu fikiria kwa muda kuhusu watenda-maovu wawili waliotundikwa kando ya Yesu. Ni wazi kwamba wote wawili walikuwa wamefanya makosa mazito, kwa kuwa mmoja wao alisema: “Sisi tunapokea kwa ukamili kile tunachostahili kwa mambo tuliyofanya; lakini mtu huyu [Yesu] hakufanya jambo lolote lisilofaa.” Maneno ya huyo mtenda-maovu yanaonyesha kwamba alijua jambo fulani kumhusu Yesu. Inaelekea ujuzi huo ulibadili mtazamo wake. Jambo hilo linaonyeshwa na maneno yake yaliyofuata, alipomsihi Yesu hivi: “Unikumbuke utakapoingia katika ufalme wako.” Yesu aliitikiaje ombi hilo lililotoka moyoni? “Kwa kweli mimi nakuambia leo,” Yesu alimwambia, “Utakuwa pamoja nami katika Paradiso.”—Luka 23:41-43.

Hebu fikiria jambo hilo: Maneno ya mwisho ya Yesu yalitia ndani kumwonyesha rehema mtu aliyekiri kwamba amefanya jambo linalostahili kifo. Hilo linatia moyo kama nini! Kwa hiyo, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yesu Kristo na Baba yake, Yehova, watawaonyesha rehema wote wanaoonyesha toba ya kweli haidhuru wamefanya nini wakati uliopita.—Waroma 4:7.

JE, UMEJIULIZA HIVI?

▪ Unaweza kufafanuaje rehema ya Mungu?—Zaburi 103:12-14; 130:3, 4.

▪ Mtu anapaswa kuchukua hatua gani ili apate kibali cha Mungu?—Yohana 17:3; Matendo 3:19.

▪ Yesu alimwahidi nini mtenda-maovu aliyetundikwa?Luka 23:43.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 12 Ona makala yenye kichwa “Je, Umeitendea Dhambi Roho Takatifu?” kwenye ukurasa wa 16-20 katika Mnara wa Mlinzi la Julai 15, 2007.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Yesu alionyesha kwamba dhambi nzito zinaweza kusamehewa