Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Hivi Karibuni Uhalifu ‘Hautakuwapo Tena’

Hivi Karibuni Uhalifu ‘Hautakuwapo Tena’

Hivi Karibuni Uhalifu ‘Hautakuwapo Tena’

“Bado muda kidogo tu, na mtu mwovu hatakuwako tena.”—ZABURI 37:10.

MUUMBA wetu Yehova Mungu anapendezwa sana na wanadamu, naye si Mungu asiyejali kama watu wengine wanavyoamini. (Zaburi 11:4, 5) Isitoshe, yeye huona kila uhalifu, kila ukosefu wa haki, kutia ndani ule ambao hauonwi na wanadamu. “Macho ya Yehova yako kila mahali, yakiwaangalia wabaya na wema.” (Methali 15:3) Kwa hiyo uwe na hakika kwamba waovu kwa kweli wako “kwenye udongo unaoteleza.”—Zaburi 73:12, 18.

Hata hivyo, ingawa huenda watu wasio na lawama na wanyoofu wakawa maskini kimwili na hata kudharauliwa, wao wana taraja zuri. Mtunga-zaburi Daudi, aliandika hivi: “Mwangalie mtu asiye na lawama na uendelee kumwangalia mnyoofu, kwa maana wakati ujao wa mtu huyo utakuwa wenye amani.” (Zaburi 37:37) Maneno hayo yanaweza kutufariji leo kwa njia ya pekee, kwa kuwa hivi karibuni tuna tumaini la kuyaona yakitimizwa ulimwenguni pote.

Tunaishi Katika Siku za Mwisho

Miaka 2,000 iliyopita, wanafunzi wa Yesu Kristo walimuuliza swali ambalo jibu lake lilihusisha wakati ujao. “Tuambie,” wakamuuliza, “ni nini itakayokuwa ishara ya . . . umalizio wa mfumo wa mambo?” (Mathayo 24:3) Jibu la Yesu linaelezwa kwa urefu katika Biblia kwenye sura ya 24 ya Mathayo, sura ya 13 ya Marko, na sura ya 21 ya Luka. Masimulizi hayo yanafafanua kwamba siku za mwisho za ulimwengu huu zingekuwa na vita, njaa, magonjwa, matetemeko makubwa ya nchi, na kuongezeka sana kwa uasi-sheria.

Hali zenye hatari ambazo Yesu alitabiri zilianza mnamo 1914. Kama vile mwanahistoria Eric Hobsbawm anavyosema katika kitabu chake Age of Extremes, karne ya 20 “ilikuwa bila shaka ndiyo karne yenye mauaji mengi zaidi kuwahi kurekodiwa.”

Kuhusu kuongezeka kwa uovu leo, Biblia inasema: “Wakati waovu wanapochipuka kama majani na wote wanaotenda mambo yenye kuumiza wanapochanuka, ni ili wao wapate kuangamizwa milele.” (Zaburi 92:7) Naam, uthibitisho ni wazi: Kuongezeka sana kwa uasi-sheria tunakoona leo, ambako kunafananishwa na kuchipuka kwa majani katika majira yake, ni ishara ya kwamba kuharibiwa kwa waovu kumekaribia! Je, hiyo si habari njema?—2 Petro 3:7.

“Waadilifu . . . Wataimiliki Dunia”

“Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake,” inasema Zaburi 37:29. Uhalifu na ukosefu wote wa haki utakwisha. Kwa hiyo, kila kitu kinachohusiana na uhalifu hakitakuwapo: ving’ora, kufuli, mahakama, wanasheria, polisi, na magereza. Biblia inaahidi hivi: “Mambo ya zamani hayatakumbukwa akilini, wala hayataingia moyoni.”—Isaya 65:17.

Ndiyo, dunia na wanadamu wataona mabadiliko ambayo hayajawahi kutukia tena. (Isaya 11:9; 2 Petro 3:13) Hilo ndilo tumaini hakika ambalo Mashahidi wa Yehova wanalo, nao wanakualika ujionee mwenyewe kutimizwa kwa tumaini hilo. Kumbuka, Yule ambaye aliongoza Maandiko Matakatifu akitumia roho yake ‘hawezi kusema uwongo.’—Tito 1:2.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

MSAADA WA KIROHO KWA WAFUNGWA

Kwa miaka mingi, Mashahidi wa Yehova nchini Marekani wamepokea barua kutoka kwa wafungwa katika vituo 4,169. Vituo hivyo vinatia ndani magereza, hospitali, na vituo vya kuwatibu waraibu wa dawa za kulevya. Wafungwa fulani wanaomba vichapo vya Biblia; wengine wanaomba funzo la Biblia bila malipo. Mashahidi wanaostahili huwasiliana na wafungwa hao. Kwa kweli, ulimwenguni pote, Mashahidi hutembelea magereza ili kujifunza Biblia na wafungwa wanaume na wanawake ambao wameomba msaada wa kiroho. Wengi wa wafungwa hao wamefanya mabadiliko makubwa katika utu wao, wamebatizwa na kuwa Wakristo wanaotii sheria.