Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Vijana Huuliza

Ninaweza Kukabilianaje na Ugonjwa au Ulemavu?

Ninaweza Kukabilianaje na Ugonjwa au Ulemavu?

“UZURI wa vijana ni nguvu zao,” inasema Methali 20:29. Ikiwa wewe ni mgonjwa au mlemavu, huenda ukahisi kwamba andiko hilo haliwezi kukuhusu kamwe. Lakini linaweza kukuhusu! Ukweli wa mambo ni kwamba vijana wengi walemavu na wenye magonjwa ya kudumu wameshinda vizuizi vikubwa. Mwandishi wa Amkeni! aliwahoji vijana wanne walio na hali hizo.

Hiroki kutoka Japani ameugua ugonjwa wa kupooza ubongo tangu utotoni. Anasema hivi: “Misuli ya shingo yangu haiwezi kushikilia kichwa changu, na mikono yangu hufanya kinyume cha ninachotaka ifanye. Mimi huwategemea wengine wanisaidie.”

Natalie na ndugu yake, James, kutoka Afrika Kusini, ni mbilikimo. Natalie pia ana uti wa mgongo uliopinda. “Nimefanyiwa upasuaji wa uti wa mgongo mara nne,” anasema, “na kwa sababu ya kupinda kwa uti wangu wa mgongo, mapafu yangu ni dhaifu.”

Timothy, kutoka Uingereza, aligunduliwa kuwa ana tatizo la kuchoka daima (chronic fatigue syndrome) alipokuwa na umri na miaka 17. “Katika muda usiozidi miezi miwili,” anasema, “nilibadilika kutoka mtu mwenye afya nzuri anayeweza kufanya mambo mengi na kuwa mnyonge sana hivi kwamba nisingeweza kusimama kwa miguu yangu.”

Danielle, kutoka Australia, aligunduliwa kuwa ana ugonjwa wa kisukari alipokuwa na umri wa miaka 19. “Kwa kuwa dalili za kisukari hazionekani waziwazi,” anasema, “watu fulani hawatambui kwamba huo ni ugonjwa hatari. Lakini ukweli ni kwamba kisukari ni ugonjwa unaoweza kuniua.”

Ikiwa una ugonjwa au ulemavu fulani, bila shaka utatiwa moyo na maneno ya Hiroki, Natalie, Timothy, na Danielle. Ikiwa una afya nzuri, maelezo yao yanaweza kukusaidia uwaelewe wale wanaopambana na ulemavu au ugonjwa.

Amkeni!: Ni nini hasa kinachofanya hali yako iwe ngumu?

Natalie: Ni jinsi watu wanavyonitazama. Sijihisi huru. Nahisi ni kana kwamba watu hunitazama daima.

Danielle: Ukiwa na kisukari, tatizo kuu ni kujua vyakula unavyopaswa kula, kiasi unachopaswa kula, na vyakula unavyopaswa kuepuka. Nisipokuwa mwangalifu kuhusiana na vyakula, hilo linaweza kusababisha kiwango cha sukari katika damu kupungua na kufanya nipoteze fahamu kwa muda mrefu.

Hiroki: Nina kiti maalumu cha magurudumu ambacho kinafaa hali yangu, na mwili wangu huwa katika mkao wa aina moja kwa saa 15 hivi kwa siku. Pia silali vizuri. Mimi huamshwa na kelele ndogo.

Timothy: Mwanzoni, tatizo langu kuu lilikuwa kukubali kwamba mimi ni mgonjwa. Niliaibikia hali yangu.

Amkeni!: Ni matatizo gani mengine unayokabili?

Danielle: Kisukari hunifanya nihisi mchovu sana. Ninahitaji kulala zaidi kuliko vijana wa umri wangu. Pia kisukari ni ugonjwa wa kudumu ambao hauna tiba.

Natalie: Bila shaka, kuwa mbilikimo huathiri maisha yangu. Inakuwa vigumu kufanya mambo ya kawaida kama vile kufikia vitu vilivyowekwa kwenye rafu dukani. Mimi hutatizika zaidi ninapoenda kununua vitu nikiwa peke yangu.

Timothy: Mimi hupatwa na maumivu yanayoendelea kwa muda mrefu na pia kushuka moyo. Kabla ya kupata ugonjwa huo, ningeweza kufanya mambo mengi. Nilikuwa nimeajiriwa na pia ningeweza kuendesha gari. Nilicheza michezo mbalimbali kama vile kandanda na skwoshi. Sasa ninalazimika kutumia kiti cha magurudumu maisha yangu yote.

Hiroki: Ulemavu hufanya iwe vigumu kwangu kuzungumza. Jambo hilo hunifanya niogope kuzungumza. Nyakati nyingine, mikono yangu hujitupa-tupa na kumgonga mtu. Hilo linapotukia, siwezi hata kuomba msamaha kwa sababu ya tatizo langu la kuzungumza.

Amkeni!: Ni nini kimekusaidia kukabiliana na hali yako?

Danielle: Mimi hujaribu kukaza fikira zangu kwenye mambo yenye kutia moyo. Nina familia inayonijali, marafiki wenye upendo kutanikoni, na zaidi ya yote, nina Yehova Mungu, ambaye hunitegemeza. Pia mimi hujitahidi kupata habari za karibuni zaidi kuhusu kisukari. Mimi hujitahidi kutunza afya yangu.

Natalie: Sala ni chanzo cha nguvu. Mimi hujaribu kushughulikia tatizo moja kwa wakati mmoja. Kuwa na shughuli nyingi hunisaidia nisiwe na mawazo yenye kuvunja moyo. Na nina wazazi wawili wanaonijali ambao ninaweza kuwaambia yaliyo moyoni.

Timothy: Mimi hufanya jambo fulani la kiroho kila siku, hata ikiwa ni kwa muda mfupi tu. Kwa mfano, mimi huanza siku kwa kusoma andiko la siku. Kusoma Biblia na sala ni muhimu sana hasa ninaposhuka moyo.

Hiroki: Mimi hujaribu nisihangaikie mambo ambayo siwezi kubadili. Kuhangaikia mambo hayo ni kupoteza wakati. Badala yake, mimi hujitahidi sana kuimarisha uhusiano wangu na Mungu, na situmii hali yangu kuwa udhuru wa kutojifunza Biblia. Ninapokosa usingizi, mimi hutumia fursa hiyo kusali.—Ona Waroma 12:12.

Amkeni!: Wengine wamekutiaje moyo?

Hiroki: Wazee hunipongeza kwa mambo machache ninayoweza kufanya. Ndugu na dada kutanikoni hunipeleka kwenye ziara zao za kurudia na mafunzo ya Biblia.—Ona Waroma 12:10.

Danielle: Huenda jambo ambalo hunigusa moyo sana ni wakati ndugu na dada kutanikoni wananipongeza. Hilo hufanya nihisi kwamba ninathaminiwa, na hunitia moyo kuendelea.

Timothy: Kuna dada mmoja mzee ambaye hujitahidi kuzungumza nami kwenye mikutano. Wazee na wake zao pia wamenitia moyo na kunipatia mapendekezo mazuri. Mzee mmoja wa kutaniko ambaye ana umri wa miaka 84, amenisaidia kuweka miradi ninayoweza kutimiza. Mtumishi mmoja wa huduma alinialika niambatane naye kwenye huduma, na akapanga tuhubiri eneo ambalo kiti changu cha magurudumu kinaweza kupita kwa urahisi.—Ona Zaburi 55:22.

Natalie: Mara tu ninapoingia kwenye Jumba la Ufalme, ndugu na dada zangu wa kiroho hunisalimu kwa shauku. Kila mara, wale wazee kwa umri huniambia jambo la kunitia moyo licha ya hali ngumu ambayo wao wenyewe wanakabili.—Ona 2 Wakorintho 4:16, 17.

Amkeni!: Ni nini hukusaidia kuwa na mtazamo unaofaa?

Hiroki: Nikiwa Shahidi wa Yehova, mimi hushirikiana na tengenezo lenye watu ambao wana tumaini zuri ajabu. Kutambua kwamba mimi ni sehemu ya tengenezo hilo hunisaidia kuwa na mtazamo unaofaa.—Ona 2 Mambo ya Nyakati 15:7.

Danielle: Mimi hufikiria pendeleo ambalo nimepata la kuelewa kusudi la Mungu. Kuna watu ambao wana afya nzuri lakini hawana furaha kama mimi.—Ona Methali 15:15.

Natalie: Nimeona kwamba ni muhimu kushirikiana na watu wenye mtazamo unaofaa. Pia inatia moyo kusoma masimulizi ya watu ambao wanamtumikia Yehova licha ya majaribu. Ninapoenda kwenye Jumba la Ufalme, mimi hujua kwamba nitaimarishwa na kukumbushwa kwamba ni pendeleo kubwa kuwa Shahidi wa Yehova.—Ona Waebrania 10:24, 25.

Timothy: Andiko la 1 Wakorintho 10:13 linasema kwamba Yehova hatatuacha tujaribiwe kupita tunavyoweza kuhimili. Hivyo mimi hujiambia kwamba ikiwa Muumba wangu ana uhakika kwamba ninaweza kukabiliana na jaribu, kwa nini niwe na shaka?

 

MAMBO YA KUFIKIRIA

  • Hiroki na Timothy wanalazimika kutumia kiti cha magurudumu. Ikiwa wewe pia unatumia kiti cha magurudumu, maneno yao yanaweza kukusaidiaje kudumisha mtazamo unaofaa?

  • Danielle anasema kwamba “kwa kuwa dalili za kisukari hazionekani waziwazi, watu fulani hawatambui kwamba huo ni ugonjwa hatari.” Je, wewe una ugonjwa ambao ‘dalili zake hazionekani waziwazi?’ Ikiwa unao, unajifunza nini kutoka na maneno ya Danielle?

  • Natalie anasema kwamba tatizo lake kuu ni kukabiliana na jinsi ambavyo watu humtazama. Unaweza kumsaidiaje mtu kama Natalie ajihisi huru? Ikiwa una ugonjwa au ulemavu ambao unakufanya ujihisi kama Natalie, unaweza kuigaje mtazamo wake mzuri?

  • Andika hapa chini majina ya watu unaowajua ambao ni walemavu au wana ugonjwa wa kudumu.

  • Unaweza kufanya nini kuwatia moyo watu hao?