Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Ni Vibaya Kuomboleza?

Je, Ni Vibaya Kuomboleza?

Maoni ya Biblia

Je, Ni Vibaya Kuomboleza?

“ZAIDI YA HAYO, AKINA NDUGU, HATUTAKI NYINYI MWE WASIO NA UJUZI KUHUSU WALE AMBAO WAMELALA KATIKA KIFO; ILI MSIPATE KUWA NA MAJONZI KAMA VILE WALE WENGINE WASIO NA TUMAINI.”—1 WATHESALONIKE 4:13.

BIBLIA huonyesha kuwa kuna tumaini kwa wafu. Ufufuo uliofanywa na Yesu, pamoja na mafundisho yake, yalielekeza kwenye wakati ambapo wafu watafufuliwa. (Mathayo 22:23-33; Marko 5:35, 36, 41, 42; Luka 7:12-16) Tumaini hilo lituathirije? Maneno ya mtume Paulo yaliyonukuliwa juu yaonyesha kwamba tumaini hilo laweza kutufariji mpendwa anapokufa.

Ikiwa umewahi kufiwa na mpendwa wako, bila shaka uliumia kihisia-moyo. Theresa, aliyefiwa na mumewe mwenye umri wa miaka 42 muda mfupi baada ya kufanyiwa upasuaji wa moyo, asema hivi: “Nilishtuka sana! Mwanzoni, niliogopa sana. Kisha nilihisi uchungu mwingi ulioongezeka siku baada ya siku. Nililia sana.” Je, kuhisi hivyo kunaonyesha ukosefu wa imani katika ahadi ya Yehova ya kuwafufua wafu? Je, maneno ya Paulo yanaonyesha kwamba ni vibaya kuomboleza?

Mifano ya Biblia ya Watu Walioomboleza

Twapata majibu ya maswali hayo kwa kuchunguza mifano ya Biblia ya watu walioomboleza. Katika visa vingi, kulikuwa na kipindi cha kuomboleza baada ya kifo cha mshiriki wa familia. (Mwanzo 27:41; 50:7-10; Zaburi 35:14) Watu waliomboleza kwa sababu ya huzuni nyingi.

Fikiria jinsi wanaume wenye imani walivyoomboleza wakati wapendwa wao walipokufa. Kwa mfano, Abrahamu alikuwa na imani yenye nguvu kwamba Mungu anaweza kuwafufua wafu. (Waebrania 11:19) Hata akiwa na uhakika huo, mke wake alipokufa, ‘alimlilia Sara na kumwombolezea.’ (Mwanzo 23:1, 2) Wana wa Yakobo walipomdanganya kuwa mwanawe mpendwa Yosefu alikuwa amekufa, Yakobo ‘alirarua mavazi yake . . . akamlilia.’ (Mwanzo 37:34, 35) Hata baada ya miaka mingi, Yakobo bado alihuzunika sana alipofikiria kifo cha mwanawe mpendwa! (Mwanzo 42:36-38) Mfalme Daudi aliomboleza sana na waziwazi, wanawe wawili, Amnoni na Absalomu, walipokufa. Japo wote wawili waliitaabisha familia ya Daudi, bado walikuwa wanawe, na vifo vyao vilimhuzunisha sana.—2 Samweli 13:28-39; 18:33.

Nyakati nyingine, taifa zima la Israeli liliomboleza. Kwa mfano, liliomboleza baada ya Musa kufa. Andiko la Kumbukumbu la Torati 34:8 latueleza kwamba Waisraeli waliomboleza kwa siku 30.

Hatimaye, kuna mfano wa Yesu Kristo. Lazaro, rafikiye wa karibu, alikufa. Yesu alipoona jinsi dada za Lazaro, Martha na Maria, na rafiki zao walivyotoa machozi, “akapiga kite katika roho na kuwa mwenye kutaabika.” Japo alijua kwamba muda si muda angemfufua rafikiye, bado ‘alitokwa na machozi.’ Yesu aliwapenda Martha na Maria, rafikize wapendwa. Basi, alihuzunika sana alipoona huzuni yao kwa sababu ya kifo cha ndugu yao.—Yohana 11:33-36.

Abrahamu, Yakobo, Daudi, na Yesu walidhihirisha imani kubwa katika Yehova na ahadi zake, lakini bado walihuzunika. Je, kuomboleza kulionyesha kwamba walikuwa dhaifu kiroho? Je, huzuni yao ilionyesha kwamba hawakuamini ufufuo? La hasha! Kuomboleza ni itikio la kawaida mpendwa anapokufa.

Kwa Nini Sisi Huomboleza

Mungu hakukusudia kamwe wanadamu wafe. Kusudi la Mungu tangu awali, alilowaeleza Adamu na Hawa, lilikuwa kwamba dunia igeuzwe kuwa paradiso yenye kupendeza iliyojaa familia yenye upendo na furaha. Kifo kingetokea endapo tu wenzi hao wa kwanza wangekosa kumtii Yehova. (Mwanzo 1:28; 2:17) Kwa kusikitisha, Adamu na Hawa hawakutii, na kwa sababu ya kutotii, “kifo kikasambaa kwa watu wote.” (Waroma 5:12; 6:23) Hivyo, kifo ni adui mkatili ambaye hakukusudiwa awepo.—1 Wakorintho 15:26.

Basi, si ajabu kwamba, kifo cha mpendwa husababisha maumivu makali ya kihisia-moyo kwa wale waliofiwa. Hutokeza pengo kubwa maishani mwao. Theresa, mjane aliyetajwa hapo awali, alisema hivi kuhusu mumewe: “Nina hakika nitamwona tena wakati wa ufufuo, lakini kwa sasa ninamkosa sana. Hilo ndilo linaloniumiza.” Kifo cha mzazi chaweza kutukumbusha kwamba hata sisi twaweza kufa. Kifo cha kijana hutuhuzunisha hasa kwa sababu hakuishi kwa muda mrefu.—Isaya 38:10.

Naam, kifo si jambo la asili. Maumivu yanayoletwa na kifo yanatarajiwa, na Yehova haoni kuomboleza kuwa ni kukosa imani katika ufufuo. Kama tulivyoona kupitia mifano ya Abrahamu, Yakobo, Daudi, taifa la Israeli, na Yesu, kuonyesha huzuni yetu waziwazi hakumaanishi kwamba tumepungukiwa kiroho. *

Hata hivyo, ijapokuwa sisi Wakristo huhuzunika kwa sababu ya kifo, hatupati majonzi “kama vile wale wengine wasio na tumaini.” (1 Wathesalonike 4:13) Hatuhuzuniki kupita kiasi kwa kuwa twaelewa vema hali ya wafu. Twajua kwamba hawana maumivu wala hawataabiki, bali ni kana kwamba wamelala usingizi mzito kwa amani. (Mhubiri 9:5; Marko 5:39; Yohana 11:11-14) Tuna hakika kabisa kwamba Yesu, aliye “ufufuo na uhai,” atatimiza ahadi yake ya kuwafufua “wote wale waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho.”—Yohana 5:28, 29; 11:24, 25.

Hivyo basi, ikiwa kwa sasa unaomboleza, jipe moyo kwa kujua kwamba Yehova huelewa maumivu yako. Acha ujuzi huo na tumaini lako katika ufufuo upunguze huzuni yako na ukusaidie kukabiliana na hasara uliyopata.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Ili kupata msaada wa kukabiliana na huzuni, ona ukurasa wa 14-19 wa broshua Mtu Fulani Umpendaye Anapokufa, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.