Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA TANO

Aliwatetea Watu wa Mungu

Aliwatetea Watu wa Mungu

1-3. (a) Kwa nini huenda Esta aliogopa kwenda mbele ya mume wake? (b) Tutachunguza maswali gani kumhusu Esta?

ESTA alijaribu kutuliza moyo wake alipokaribia ua wa jumba la mfalme huko Shushani. Haikuwa rahisi. Jumba hilo lilikuwa la kustaajabisha, lilikuwa na michongo yenye rangi mbalimbali ya ng’ombe dume wenye mabawa, wapiga-mishale, nguzo ndefu zilizorembeshwa, sanamu kubwa sana, na michongo ya simba ambayo ilikuwa kwenye kuta za matofali yenye kung’aa. Pia, lilikuwa limejengwa karibu na Milima ya Zagros iliyofunikwa kwa theluji kwenye eneo lililoinuka karibu na maji safi ya mto Choaspes. Mambo hayo yote yalikusudiwa kumkumbusha kila mgeni mamlaka kuu ya mtu ambaye Esta alikuwa anaenda kumwona, na ambaye alijiita “mfalme mkuu.” Pia, mfalme huyo alikuwa mume wake.

2 Mume mwenye mamlaka kwelikweli! Bila shaka, Ahasuero alikuwa tofauti kabisa na mume ambaye msichana mwaminifu Myahudi angetazamia kupata! * Hakuwa kama Abrahamu, mwanamume ambaye kwa unyenyekevu alikubali mwongozo wa Mungu na kumsikiliza Sara, mke wake. (Mwa. 21:12) Mfalme huyo hakujua mengi au jambo lolote kumhusu Yehova, Mungu wa Esta, wala Sheria Yake. Hata hivyo, Ahasuero alijua sheria za Waajemi kutia ndani sheria iliyokataza jambo ambalo Esta alikuwa karibu kufanya. Jambo gani? Sheria hiyo ilisema mtu yeyote ambaye angeenda mbele ya mfalme wa Waajemi bila kuitwa na mfalme, angeuawa. Esta hakuwa ameitwa, lakini alikuwa anaenda mbele ya mfalme. Alipokaribia ua wa ndani mahali ambapo mfalme angemwona akiwa kwenye kiti chake, huenda Esta alihisi kwamba anakaribia kuuawa.​—Soma Esta 4:11; 5:1.

3 Kwa nini Esta alihatarisha uhai wake? Na tunajifunza nini kutokana na imani ya mwanamke huyo wa pekee? Kwanza, acheni tuchunguze jinsi Esta alivyokuja kuwa malkia huko Uajemi.

Malezi ya Esta

4. Malezi ya Esta yalikuwaje, na alikuja kuishije na binamu yake Mordekai?

4 Esta alikuwa yatima. Hatujui mengi kuhusu wazazi wake waliompa jina Hadasa, neno la Kiebrania linalomaanisha “mhadasi,” mmea wenye kupendeza unaochanua maua meupe. Wazazi wa Esta walipokufa, mmoja wa watu wake wa ukoo, mwanamume mwenye huruma anayeitwa Mordekai, alimsikitikia mtoto huyo. Alikuwa binamu ya Esta, lakini alimzidi kwa umri. Alimchukua Esta na kumlea kama binti yake.​—Esta 2:5-7, 15.

Mordekai alikuwa na sababu nzuri ya kujivunia kuwa baba mlezi wa Esta

5, 6. (a) Mordekai alimleaje Esta? (b) Esta na Mordekai waliishi maisha ya aina gani huko Shushani?

5 Mordekai na Esta walikuwa Wayahudi waliohamishwa na waliishi katika mji mkuu wa Waajemi, ambako huenda walidhihakiwa kwa sababu ya dini yao na Sheria waliyofuata. Lakini Esta alisitawisha uhusiano wa karibu na binamu yake aliyemfundisha kumhusu Yehova, Mungu mwenye rehema ambaye aliwaokoa watu wake kutoka katika matatizo mengi zamani—na ambaye angewaokoa tena. (Law. 26:44, 45) Ni wazi kwamba uhusiano wa karibu na wenye upendo ulisitawi kati ya Esta na Mordekai.

6 Inaonekana Mordekai alikuwa ofisa katika makao ya mfalme huko Shushani na kwa kawaida aliketi kwenye lango pamoja na watumishi wengine wa mfalme. (Esta 2:19, 21; 3:3) Hatujui mambo ambayo Esta alifanya alipokuwa kijana, lakini inaonekana alimsaidia binamu yake mkubwa na akasaidia kutunza nyumba yake, ambayo huenda ilikuwa katika sehemu ya mji iliyotengewa watu maskini ng’ambo ya mto kutoka kwenye jumba la mfalme. Labda alifurahia kwenda sokoni huko Shushani, ambako mafundi wa dhahabu na wa fedha, na wafanyabiashara wengine waliuza bidhaa zao. Esta hakuwazia kwamba baadaye angepata kwa wingi vitu hivyo vyenye thamani; hakujua mambo ambayo yangetukia baadaye.

“Alikuwa Mrembo”

7. Kwa nini Vashti aliondolewa kuwa malkia, na matokeo yalikuwa nini?

7 Siku moja, kulikuwa na porojo katika jiji la Shushani kuhusu matatizo yaliyokuwa katika nyumba ya mfalme. Katika sherehe fulani kubwa, ambapo Ahasuero alikuwa akiwatumbuiza wakuu wake kwa mlo mkubwa na divai, aliamua kumwita malkia wake mrembo, Vashti, aliyekuwa akisherehekea kando pamoja na wanawake. Lakini Vashti akakataa kuja. Akiwa ameaibika na kukasirika, mfalme aliwauliza washauri wake jinsi ya kumwadhibu Vashti. Matokeo yalikuwa nini? Aliondolewa kuwa malkia. Watumishi wa mfalme wakaanza kutafuta kotekote nchini mabikira warembo ambao mfalme angechagua mmoja kati yao awe malkia.​—Esta 1:1–2:4.

8. (a) Kwa nini huenda Mordekai alikuwa na wasiwasi Esta alipozidi kukua? (b) Unafikiri tunawezaje kufuata mashauri yenye usawaziko kuhusu urembo? (Ona pia Methali 31:30.)

8 Tunaweza kuwazia Mordekai akimtazama Esta mara kwa mara kwa wasiwasi na wakati huohuo akijivunia kwamba binamu yake mdogo alikuwa amekomaa na kuwa msichana mrembo sana. Tunasoma hivi: “Mwanamke [huyo] kijana alikuwa mrembo na mwenye umbo linalopendeza.” (Esta 2:7) Biblia inatoa maoni yanayofaa kuhusu urembo, lakini mwanamke mrembo anahitaji pia kuwa mnyenyekevu na mwenye hekima. La sivyo, anaweza kuwa na majivuno, kiburi, na kusitawisha moyoni tabia nyingine zisizofaa. (Soma Methali 11:22.) Je, umewahi kujionea jambo hilo? Katika kisa cha Esta, je, urembo wake ungemsaidia au ungemfanya awe na kiburi? Baada ya muda, ingejulikana.

9. (a) Nini kilichotukia watumishi wa mfalme walipomwona Esta, na kwa nini ilikuwa vigumu kwa Esta kuachana na Mordekai? (b) Kwa nini Mordekai alimruhusu Esta aolewe na mpagani asiye mwamini? (Tia ndani sanduku.)

9 Watumishi wa mfalme walimwona Esta. Wakamchukua kutoka kwa Mordekai, na kumpeleka kwenye jumba la mfalme lililokuwa ng’ambo ya mto. (Esta 2:8) Haikuwa rahisi kuachana, kwa sababu Esta alikuwa kama binti ya Mordekai. Mordekai hakutaka Esta aolewe na mpagani asiye mwamini, hata awe mfalme, lakini hangeweza kuzuia jambo hilo. * Kabla hajachukuliwa, lazima Esta alisikiliza kwa makini mashauri ya Mordekai. Alipokuwa akipelekwa kwenye jumba la mfalme huko Shushani, alikuwa na maswali mengi akilini. Angeishi maisha ya aina gani?

Alipata Kibali “Machoni pa Kila Mtu Aliyemwona”

10, 11. (a) Kwa nini ilikuwa rahisi kwa Esta kuathiriwa na maisha yake mapya? (b) Mordekai alionyeshaje kwamba alimhangaikia Esta?

10 Maisha ya Esta yalibadilika na kuwa tofauti kabisa. Alikuwa kati ya “wanawake wengi vijana” waliokusanywa kutoka maeneo mbalimbali ya Milki ya Uajemi. Lazima tamaduni, lugha, na mitazamo yao ilitofautiana kabisa. Chini ya usimamizi wa ofisa aliyeitwa Hegai, wanawake hao vijana wangerembeshwa sana, wangekandwa kwa mafuta yenye marashi kwa mwaka mmoja. (Esta 2: 8, 12) Huenda maisha hayo yaliwafanya wafikirie sana urembo wao, wawe na kiburi, na mashindano. Esta aliathiriwaje?

11 Bila shaka, Mordekai alijali sana hali ya Esta. Tunasoma kwamba kila siku, alienda karibu na nyumba ya wanawake ili apate kujua hali ya Esta. (Esta 2:11) Lazima alifurahi sana alipopata habari, labda kutoka kwa wafanyakazi wa jumba la mfalme. Kwa nini?

12, 13. (a) Watu walikuwa na maoni gani kumhusu Esta? (b) Kwa nini Mordekai alifurahi alipotambua kwamba Esta hakuwa amefunua alikuwa Myahudi?

12 Hegai alivutiwa sana na tabia ya Esta hivi kwamba akamtendea kwa fadhili na kumpa vijakazi saba na mahali bora katika nyumba ya wanawake. Simulizi hilo linasema: “Wakati huo wote Esta alikuwa akizidi kupata kibali machoni pa kila mtu aliyemwona.” (Esta 2:9, 15) Je, ni urembo tu uliofanya kila mtu avutiwe naye? Hapana, Esta alikuwa na sifa nyingine nzuri.

Esta alijua kwamba sifa ya unyenyekevu na hekima ni muhimu kuliko urembo

13 Kwa mfano, tunasoma: “Esta hakuwa amesema kuhusu watu wake wala kuhusu jamaa zake, kwa maana Mordekai alikuwa amemwamuru kwamba asiseme.” (Esta 2:10) Mordekai alikuwa amemwagiza Esta asifunue kwamba alikuwa Myahudi; bila shaka alijua watawala Waajemi waliwabagua watu wake. Mordekai alifurahi kama nini alipojua ingawa hakuwa karibu naye, bado Esta aliendelea kuwa mwenye hekima na mtiifu!

14. Leo, vijana wanawezaje kumwiga Esta?

14 Leo pia, vijana wanaweza kuwaletea furaha wazazi na walezi wao. Wanapokuwa peke yao—au wakiwa na watu wasio na busara, waliopotoka kiadili, au wajeuri—wanaweza kushinda vishawishi, na kufanya mambo yanayofaa. Kama Esta, wao pia wanaweza kumfanya Baba yao wa mbinguni afurahi.​—Soma Methali 27:11.

15, 16. (a) Esta alifanikiwaje kupendwa na mfalme? (b) Kwa nini huenda ilikuwa vigumu kwa Esta kubadili maisha yake?

15 Wakati ulipofika wa Esta kwenda mbele ya mfalme, aliruhusiwa kuchagua vitu ambavyo alifikiri angehitaji, labda ili kujirembesha zaidi. Hata hivyo, kwa busara Esta aliomba tu vitu ambavyo Hegai alimwambia. (Esta 2:15) Inaelekea alijua kwamba urembo peke yake haungefurahisha moyo wa mfalme; angemvutia zaidi kwa kuwa mnyenyekevu na mwenye kiasi. Je, ni kweli?

16 Simulizi linajibu hivi: “Mfalme akampenda Esta kuliko wale wanawake wengine wote, hata akapata kibali na fadhili zenye upendo kuliko wale mabikira wengine wote. Ndipo mfalme akamvika taji la kifalme juu ya kichwa chake na kumfanya kuwa malkia badala ya Vashti.” (Esta 2:17) Haikuwa rahisi kwa msichana huyo mnyenyekevu Myahudi kubadili maisha yake—sasa alikuwa malkia mpya, mke wa mtawala mwenye nguvu zaidi duniani wakati huo! Je, cheo hicho kipya kingemfanya awe na kiburi? La, hasha!

17. (a) Esta aliendeleaje kumtii baba yake mlezi? (b) Kwa nini leo tunahitaji kumwiga Esta?

17 Esta aliendelea kumheshimu Mordekai, baba yake mlezi. Hakufunua kwamba yeye ni Myahudi. Zaidi ya hayo, Mordekai alipomfunulia kuhusu njama ya kumuua Ahasuero, kwa utii Esta alimweleza mfalme, na watu waliopanga njama hiyo wakauawa. (Esta 2:20-23) Bado alionyesha imani yake kwa Mungu kwa kuwa mnyenyekevu na mtiifu. Leo tunahitaji kumwiga Esta, kwa sababu watu wengi hawapendi kuwa watiifu, na badala yake wanapendelea kuwa waasi na wasiotii! Lakini watu walio na imani ya kweli ni watiifu kama vile Esta.

Imani ya Esta Yajaribiwa

18. (a) Kwa nini Mordekai alikataa kumwinamia Hamani? (Ona pia maelezo ya chini.) (b) Leo, wanaume na wanawake wenye imani wanaigaje mfano wa Mordekai?

18 Mwanamume anayeitwa Hamani alipandishwa cheo katika makao ya Ahasuero. Mfalme alimchagua Hamani kuwa waziri mkuu, na akawa mshauri wake mkuu na mtu wa pili kwa cheo katika milki yake. Hata mfalme aliagiza kwamba kila mtu amwinamie anapomwona. (Esta 3:1-4) Sheria hiyo ilimsababishia Mordekai matatizo. Alipaswa kumtii mfalme, lakini hangefanya hivyo ikiwa jambo hilo lingemvunjia Mungu heshima. Hamani alikuwa Mwagagi. Hilo linamaanisha kwamba alikuwa mzao wa Agagi, mfalme wa Waamaleki ambaye aliuawa na Samweli, nabii wa Mungu. (1 Sam. 15:33) Waamaleki walikuwa waovu sana na hivyo wakawa maadui wa Yehova na Waisraeli. Waamaleki walikuwa na hatia mbele za Mungu. * (Kum. 25:19) Myahudi mwaminifu angewezaje kumwinamia Mwamaleki? Mordekai hakufanya hivyo. Alisimama imara. Leo pia, wanaume na wanawake wenye imani wamehatarisha uhai wao kwa kutii kanuni hii: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Mdo. 5:29.

19. Hamani alitaka kufanya nini, na alifanikiwaje kumshawishi mfalme?

19 Hamani alikasirika. Lakini hakutaka kumwangamiza Mordekai peke yake. Alitaka kuwaangamiza watu wote wa Mordekai! Hamani alimshawishi mfalme aamini kwamba Wayahudi ni watu wabaya. Bila kuwataja, alisema wao si watu muhimu na kwamba “wa[me]tawanyika na kujitenga kati ya vikundi vya watu.” Hata alisema hawakutii sheria za mfalme; na hivyo, walikuwa waasi hatari. Kisha, akajitolea kutoa mchango mkubwa kwa hazina ya mfalme ili kusaidia kazi ya kuwaua Wayahudi wote katika milki hiyo. * Ahasuero akampa Hamani pete yake ya kifalme ya mhuri ili atie mhuri amri yoyote aliyotaka itekelezwe.—Esta 3:5-10.

20, 21. (a) Agizo la Hamani liliwaathirije Wayahudi kotekote katika Milki ya Uajemi, kutia ndani Mordekai? (b) Mordekai alimhimiza Esta afanye nini?

20 Muda mfupi baadaye, wajumbe walizunguka kwa farasi kila mahali katika milki hiyo kubwa wakipeleka ujumbe wa kuangamizwa kwa Wayahudi. Wazia jinsi tangazo hilo lilivyowaathiri mabaki ya Wayahudi jijini Yerusalemu, waliokuwa wamerudi kutoka uhamishoni Babiloni, na ambao walikuwa wakijitahidi kujenga upya kuta za jiji hilo. Huenda Mordekai aliposikia habari hizo mbaya aliwafikiria Wayahudi hao, marafiki na watu wake wa ukoo huko Shushani. Akiwa amefadhaika alirarua mavazi yake, akavaa magunia, akajipaka majivu kichwani, na kulia kwa sauti katikati ya jiji. Hata hivyo, Hamani aliendelea kunywa pamoja na mfalme, bila kujali huzuni ambayo alikuwa amewasababishia Wayahudi na rafiki zao jijini Shushani.​Soma Esta 3:12–4:1.

21 Mordekai alijua kwamba alipaswa kuchukua hatua. Angefanya nini? Esta alisikia kuhusu mfadhaiko wake na akaagiza apelekewe mavazi, lakini Mordekai alikataa kufarijiwa. Labda alikuwa akijiuliza kwa nini Yehova, Mungu wake, aliruhusu Esta achukuliwe kutoka kwake na kuwa malkia wa mtawala mpagani. Sasa inaonekana alielewa sababu. Hivyo, Mordekai akamtumia malkia ujumbe, akimwomba Esta azungumze na mfalme ili kuwatetea “watu wake mwenyewe.”​—Esta 4:4-8.

22. Kwa nini Esta aliogopa kwenda mbele ya mume wake aliyekuwa mfalme? (Ona pia maelezo ya chini.)

22 Bila shaka, Esta alihangaishwa na ujumbe huo. Lilikuwa jaribu kali sana la imani yake. Aliogopa na jambo hilo lilionekana wazi katika jibu lake kwa Mordekai. Alimkumbusha kuhusu sheria ya mfalme. Ikiwa angeenda mbele ya mfalme bila kuitwa, angeuawa. Lakini hangeuawa kama mfalme angemnyooshea fimbo yake ya dhahabu. Je, Esta alikuwa na sababu yoyote ya kutazamia kwamba hangeuawa, hasa akikumbuka kilichompata Vashti alipokataa kwenda mbele ya mfalme alipoagizwa kufanya hivyo? Alimwambia Mordekai kwamba mfalme hakuwa amemwita kwa siku 30! Hivyo, Esta hakujua ikiwa alikuwa amepoteza kibali cha mfalme ambaye hisia zake zilibadilika-badilika. *​—Esta 4:9-11.

23. (a) Mordekai alisema nini ili kuimarisha imani ya Esta? (b) Kwa nini tunapaswa kumwiga Mordekai?

23 Mordekai alimjibu Esta kwa uhakika ili kuimarisha imani yake. Alimhakikishia kwamba ikiwa hangechukua hatua, wokovu wa Wayahudi ungetoka katika chanzo kingine. Na wakati ambapo Wayahudi wangeanza kuuawa, Esta pia angeuawa. Mordekai alionyesha imani yake yenye nguvu kwa Yehova, ambaye hangeacha kamwe watu wake waangamizwe na ahadi zake zikose kutimizwa. (Yos. 23:14) Kisha, Mordekai akamuuliza Esta: “Ni nani anayejua ikiwa si kwa ajili ya wakati kama huu kwamba umefikia heshima ya kifalme?” (Esta 4:12-14) Je, hatupaswi kumwiga Mordekai? Alimtegemea kabisa Yehova Mungu wake. Je, tunafanya hivyo pia?​—Met. 3:5, 6.

Imani Yenye Nguvu Yashinda Woga wa Kifo

24. Esta alionyeshaje imani na ujasiri?

24 Sasa Esta alipaswa kufanya uamuzi. Alimwomba Mordekai awaambie Wayahudi wenzake wajiunge naye kufunga kwa siku tatu, na akamalizia ujumbe wake kwa maneno haya yanayoonyesha imani na ujasiri ambayo bado yanakumbukwa leo: “Nikiangamia, na niangamie.” (Esta 4:15-17) Alisali kwa bidii sana katika siku hizo tatu kuliko wakati mwingine wowote maishani mwake. Mwishowe, wakati ukafika. Akavalia mavazi bora ya malkia ili avutie mbele ya mfalme. Kisha, akaenda kwa mfalme.

Esta alihatarisha uhai wake ili awalinde watu wa Mungu

25. Eleza jinsi mambo yalivyokuwa Esta alipoenda mbele ya mume wake.

25 Kama ilivyoelezwa mwanzoni mwa sura hii, Esta aliingia katika ua wa mfalme. Tunaweza tu kuwazia jinsi alivyohangaika akilini na moyoni na jinsi alivyosali kwa bidii. Akaingia ndani ya ua, mahali ambapo angeweza kumwona Ahasuero akiwa ameketi kwenye kiti chake. Labda aliutazama uso wa mfalme ili ajaribu kutambua hisia zake. Ikiwa Esta alihitaji kungoja, ulionekana kuwa muda mrefu sana. Lakini baada ya muda mume wake akamwona. Kwa kweli, alishangaa lakini akatulia. Akamnyooshea fimbo yake ya dhahabu!​—Esta 5:1, 2.

26. Kwa nini Wakristo wa kweli wanahitaji ujasiri kama wa Esta, na kwa nini huo ulikuwa tu mwanzo wa kazi yake?

26 Esta alikuwa amepata nafasi ya kuzungumza na mfalme. Alikuwa ameamua kumtetea Mungu wake na watu wake, akiwawekea mfano mzuri watumishi wote waaminifu wa Mungu. Leo, Wakristo wa kweli wanajitahidi kuiga mfano wa Esta. Yesu alisema kwamba wafuasi wake wa kweli wangeonyesha upendo wa kujidhabihu. (Soma Yohana 13:34, 35.) Mara nyingi, ili tuonyeshe upendo huo tunahitaji ujasiri kama wa Esta. Lakini huo ulikuwa tu mwanzo wa kazi yake. Angewezaje kumsadikisha mfalme kwamba Hamani, mshauri wake aliyempenda, alikuwa amepanga njama? Angefanya nini ili kuwaokoa watu wake? Tutachunguza maswali hayo katika sura inayofuata.

^ fu. 2 Watu wengi wanadhani kwamba Ahasuero alikuwa Shasta wa Kwanza, ambaye alitawala Milki ya Uajemi mwanzoni mwa karne ya tano K.W.K.

^ fu. 9 Ona sanduku “Maswali Kumhusu Esta,” kwenye Sura ya 16.

^ fu. 18 Huenda Hamani alikuwa mmoja wa wazao wa mwisho-mwisho wa Waamaleki, kwa sababu wale ‘waliobaki’ walikuwa wameangamizwa katika siku za Mfalme Hezekia.​—1 Nya. 4:43.

^ fu. 19 Hamani alitoa mchango wa talanta 10,000 za fedha, kiasi ambacho leo ni sawa na mamilioni ya dola. Ikiwa Ahasuero alikuwa Shasta wa Kwanza, basi huenda pesa hizo zilimchochea akubali pendekezo la Hamani. Shasta alihitaji pesa nyingi ili apigane na Wagiriki katika vita vilivyosababisha uharibifu mkubwa.

^ fu. 22 Shasta wa Kwanza alikuwa mkatili na mwenye hisia zilizobadilika-badilika. Mwanahistoria Mgiriki, Herodoto, aliandika mambo fulani kuhusu vita kati ya Shasta na Wagiriki. Mfalme aliagiza daraja la meli lijengwe kwenye mlango wa bahari wa Hellespont. Dhoruba ilipofagilia mbali daraja hilo, Shasta aliagiza mafundi wake wakatwe vichwa na watu wake “waadhibu” Hellespont kwa kupiga maji huku ujumbe wa matusi ukisomwa kwa sauti kubwa. Wakati wa vita hivyo, tajiri fulani alipoomba mwanawe asijiunge na jeshi, Shasta aliagiza kijana huyo akatwe vipande viwili na mwili wake uwekwe mahali palipo wazi ili kuwa onyo kwa wengine.