Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA KUMI NA NANE

Alikata “Kauli Moyoni Mwake”

Alikata “Kauli Moyoni Mwake”

1, 2. Fafanua safari ya Maria na ueleze kwa nini ilikuwa vigumu kwake kusafiri.

MARIA hakustarehe alipokuwa ameketi juu ya punda. Alikuwa amesafiri kwa saa nyingi. Mbele yake, Yosefu alikuwa akitembea akimwongoza mnyama huyo kuelekea Bethlehemu. Kwa mara nyingine, Maria alihisi kitoto kikicheza tumboni.

2 Biblia inasema kwamba wakati huo Maria alikuwa “karibu kuzaa.” (Luka 2:5) Wenzi hao walipopita shamba moja baada ya lingine, huenda wakulima fulani waliwatazama na kujiuliza kwa nini mwanamke mwenye mimba aliamua kusafiri. Ni nini kilichomfanya Maria asafiri mbali hivyo kutoka nyumbani kwao Nazareti?

3. Ni mgawo gani ambao Maria alipewa, na tutajifunza nini kumhusu?

3 Mambo yalianza miezi kadhaa mapema mwanamke huyo Myahudi alipopata mgawo wa pekee zaidi katika historia ya wanadamu. Angezaa mtoto ambaye angekuwa Masihi, Mwana wa Mungu! (Luka 1:35) Alipokaribia kuzaa, walihitaji kusafiri. Wakati wa safari hiyo, Maria alikumbwa na mambo yaliyojaribu imani yake. Acheni tuone ni nini kilichomsaidia kubaki imara kiroho.

Safari ya Kuelekea Bethlehemu

4, 5. (a) Kwa nini Yosefu na Maria walikuwa wakielekea Bethlehemu? (b) Agizo la Kaisari lilitimiza unabii gani?

4 Si Yosefu na Maria tu waliokuwa wakisafiri. Kaisari Augusto alikuwa ameagiza kwamba watu wote katika nchi waandikishwe na watu walihitaji kwenda walikozaliwa ili waandikishwe. Yosefu alifanya nini? Simulizi hilo linasema: “Yosefu pia akapanda kutoka Galilaya, kutoka jiji la Nazareti, akaingia Yudea, kwenye jiji la Daudi, linaloitwa Bethlehemu, kwa sababu alikuwa mshiriki wa nyumba na familia ya Daudi.”​—Luka 2:1-4.

5 Agizo la Kaisari halikuwa jambo la kawaida tu. Unabii ulioandikwa karne saba hivi mapema ulitabiri kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu. Kulikuwa na mji ulioitwa Bethlehemu kilomita 11 tu kutoka Nazareti. Hata hivyo, unabii ulitaja kihususa “Bethlehemu Efratha.” (Soma Mika 5:2.) Ili kufika kwenye kijiji hicho kutoka Nazareti, wasafiri walitembea kilomita 150 hivi kwenye barabara yenye milima-milima wakipitia Samaria. Yosefu alipaswa kwenda kwenye mji huo wa Bethlehemu uliokuwa chimbuko la ukoo wa Mfalme Daudi, na Yosefu na mke wake walikuwa wa ukoo huo.

6, 7. (a) Kwa nini huenda ilikuwa vigumu kwa Maria kusafiri kwenda Bethlehemu? (b) Kwa kuwa Maria alikuwa mke wa Yosefu, maamuzi yake yalitegemea nini? (Ona pia maelezo ya chini.)

6 Je, Maria angeunga mkono uamuzi wa Yosefu wa kutii agizo hilo? Ingekuwa safari ngumu kwake. Inaelekea yalikuwa majira ya vuli, na huenda msimu wa mvua ulikuwa umeanza huku majira ya kiangazi yakiisha. Isitoshe, maneno “akapanda kutoka Galilaya” yanafaa, kwa kuwa mji wa Bethlehemu ulikuwa zaidi ya mita 760 juu ya usawa wa bahari na huo ungekuwa mwinuko mrefu sana wenye kuchosha baada ya kutembea siku kadhaa. Labda safari hiyo ilichukua muda mrefu zaidi kwa kuwa Maria angehitaji kupumzika mara kwa mara kutokana na hali yake. Wakati kama huo, huenda mwanamke angetamani kukaa karibu na watu wake wa ukoo na rafiki ambao wangemsaidia wakati uchungu wa kuzaa ungeanza. Bila shaka, alihitaji ujasiri ili asafiri.

Safari ya kwenda Bethlehemu haikuwa rahisi

7 Hata hivyo, Luka anaandika kwamba Yosefu alienda “kuandikishwa pamoja na Maria.” Pia, anasema kwamba Yosefu ‘alikuwa amemwoa Maria kama ilivyoahidiwa.’ (Luka 2:4, 5) Sasa Maria alikuwa ameolewa na hivyo maamuzi yake yalimtegemea sana Yosefu. Maria alimwona mumewe kuwa kichwa cha familia, na akakubali jukumu alilopewa na Mungu la kuwa msaidizi kwa kuunga mkono maamuzi yake. * Hivyo, alimtii mumewe na kuthibitisha kwamba alikuwa na imani.

8. (a) Ni nini kingine ambacho huenda kilimchochea Maria kwenda Bethlehemu pamoja na Yosefu? (b) Kwa nini mfano wa Maria ni kielelezo bora kwa watu waaminifu?

8 Ni nini kingine kilichomchochea Maria kutii? Je, alijua unabii uliosema kwamba Masihi angezaliwa Bethlehemu? Biblia haisemi. Hatuwezi kupuuza uwezekano huo, kwa kuwa viongozi wa kidini na watu kwa ujumla walijua unabii huo. (Mt. 2:1-7; Yoh. 7:40-42) Maria pia aliyajua Maandiko vizuri. (Luka 1:46-55) Vyovyote vile, iwe Maria alisafiri ili kumtii mumewe, ili kutii agizo la Kaisari, au kwa sababu ya unabii wa Yehova, au kwa kuchochewa na mambo hayo yote, aliweka mfano bora. Yehova anawathamini sana wanaume na wanawake wanaoonyesha unyenyekevu na utii. Mfano wa Maria wa utii ni kielelezo bora kwetu kwa sababu siku hizi watu wengi hawapendi kujitiisha.

Kuzaliwa kwa Kristo

9, 10. (a) Huenda Maria na Yosefu walifikiria nini walipokuwa wakikaribia Bethlehemu? (b) Kwa nini Yosefu na Maria walilala zizini?

9 Lazima Maria alifurahi sana walipokaribia Bethlehemu. Walipopanda milima na kupita mashamba ya mizeituni, mojawapo ya mimea ya mwisho-mwisho kuvunwa, huenda Maria na Yosefu walifikiria historia ya kijiji hicho kidogo. Kilikuwa kidogo sana kuhesabiwa kati ya majiji ya Yuda kama nabii Mika alivyosema; lakini huko ndiko walikozaliwa Boazi, Naomi, na baadaye Daudi, zaidi ya miaka elfu moja mapema.

10 Maria na Yosefu walipata kijiji hicho kikiwa kimejaa watu. Wengi walikuwa wamefika kabla yao ili kuandikishwa, hivyo, hawakupata nafasi katika chumba cha wageni. * Walilazimika kulala zizini. Tunaweza kuwazia jinsi Yosefu alivyohangaika alipomwona mkewe akiwa na maumivu makali yaliyozidi kuongezeka. Hapo ndipo uchungu wake wa kuzaa ulianzia.

11. (a) Kwa nini wanawake wanaelewa vizuri hali iliyomkabili Maria? (b) Yesu alikuwa “mzaliwa wa kwanza” katika njia gani?

11 Wanawake wanaelewa vizuri jinsi Maria alivyohisi. Miaka 4,000 hivi mapema, Yehova alikuwa ametabiri kwamba wanawake wangezaa kwa uchungu kwa sababu walirithi dhambi. (Mwa. 3:16) Inaelekea Maria pia alizaa kwa uchungu. Simulizi la Luka halitaji uchungu ambao Maria alipata, linasema tu: “Akamzaa mwana wake, mzaliwa wa kwanza.” (Luka 2:7) Ndiyo, alikuwa “mzaliwa wa kwanza” wa watoto saba hivi wa Maria. (Marko 6:3) Hata hivyo, mwana huyo angekuwa wa pekee. Mbali na kuwa mwana wake mzaliwa wa kwanza, pia alikuwa “mzaliwa wa kwanza wa viumbe vyote” vya Yehova, Mwana mzaliwa-pekee wa Mungu!​—Kol. 1:15.

12. Maria alimlaza mtoto wapi, na kwa nini hali ilikuwa tofauti na jinsi inavyoonyeshwa kwenye michoro na michezo ya kuigiza?

12 Sasa simulizi hilo linataja jambo linalojulikana sana: “Akamfunga vitambaa na kumlaza katika hori.” (Luka 2:7) Ulimwenguni pote michoro, na michezo ya kuigiza kuhusu kuzaliwa kwa Yesu inarembesha sana tukio hilo. Hata hivyo, fikiria mambo haya hakika. Hori ni chombo cha kulishia wanyama wa kufugwa. Kumbuka, familia hiyo ilikuwa katika zizi ambalo kwa kawaida halikuwa na hewa wala mazingira safi. Ni wazazi gani ambao wangechagua mtoto wao azaliwe mahali kama hapo ikiwa wangepata mahali bora? Wazazi wengi hutaka kuwapa watoto wao vitu bora. Basi lazima Maria na Yosefu walitaka kumpa Mwana wa Mungu kilicho bora zaidi!

13. (a) Maria na Yosefu walifanyaje yote waliyoweza kulingana na hali yao? (b) Leo, wazazi wenye hekima wanawezaje kutanguliza mambo ya kiroho kama Yosefu na Maria?

13 Hata hivyo, hawakuruhusu hali yao iwakatishe tamaa; walijitahidi wawezavyo. Kwa mfano, ona kwamba Maria alimtunza mtoto huyo kwa kumfunga kwa vitambaa, kisha akamlaza kwa uangalifu ndani ya hori ili alale, na kuhakikisha kwamba alikuwa salama. Hata katika hali hiyo ngumu, Maria alijitahidi kumwandalia mtoto wake kilicho bora. Pia, yeye na Yosefu walijua kwamba jambo muhimu zaidi ambalo wangemfanyia mtoto huyo ni kumtunza kiroho. (Soma Kumbukumbu la Torati 6:6-8.) Leo, wazazi wenye hekima wanatanguliza mambo ya kiroho wanapowalea watoto wao katika ulimwengu huu uliopotoka.

Watiwa Moyo na Wachungaji

14, 15. (a) Kwa nini wachungaji walitamani kumwona yule mtoto? (b) Wachungaji walifanya nini baada ya kumwona Yesu kwenye hori?

14 Kwa ghafula kukawa na kelele. Wachungaji wakaingia zizini wakiwa na hamu ya kuona ile familia na hasa yule mtoto. Wanaume hao walikuwa wamesisimuka sana, nyuso zao ziking’aa kwa shangwe. Walikuja haraka kutoka milimani walikokuwa wakiishi na mifugo yao. * Waliwaambia wazazi hao waliokuwa wameshangaa kuhusu jambo la ajabu lililokuwa limewapata. Walipokuwa wakichunga kondoo usiku, malaika aliwatokea ghafula. Utukufu wa Yehova ulikuwa umemulika pande zote na malaika akawaambia Kristo au Masihi alikuwa amezaliwa Bethlehemu. Wangempata mtoto huyo akiwa amelala kwenye hori, akiwa amefungwa vitambaa. Kisha, jambo lenye kupendeza zaidi likatokea, wakaona umati mkubwa wa malaika, uliokuwa ukimtukuza Mungu!​—Luka 2:8-14.

15 Si ajabu kwamba wanaume hao wanyenyekevu walikimbia na kuingia Bethlehemu! Lazima walisisimuka kumwona mtoto huyo mchanga akiwa amelala kwenye hori kama tu malaika alivyosema. Walieneza habari hizo njema. “Wakasema mambo yaliyokuwa yamesemwa . . . Na wote waliosikia wakastaajabu juu ya mambo waliyoambiwa na wachungaji.” (Luka 2:17, 18) Inaelekea viongozi wa kidini wa siku hizo waliwadharau wachungaji. Lakini kwa kweli Yehova aliwathamini wanaume hao wanyenyekevu na waaminifu. Hata hivyo, Maria alikuwa na maoni gani?

Yehova aliwathamini wale wachungaji wanyenyekevu na waaminifu

16. Ni nini kinachoonyesha kwamba Maria alichukua mambo kwa uzito, na hilo linafunua nini kuhusu chanzo cha imani yake?

16 Bila shaka, Maria alikuwa amechoka sana baada ya kuzaa, hata hivyo, alisikiliza kila neno kwa makini. Zaidi ya hayo: “Maria akaanza kuyahifadhi maneno hayo yote, akikata kauli moyoni mwake.” (Luka 2:19) Kwa kweli, mwanamke huyu alichukua mambo kwa uzito. Alijua kwamba ujumbe huo wa malaika ulikuwa muhimu. Mungu wake, Yehova, alitaka amjue mwana aliyezaliwa na umuhimu wake. Lakini hakusikiliza tu. Alihifadhi maneno hayo moyoni ili ayatafakari tena na tena katika miezi na miaka ambayo ingefuata. Hiyo ni sababu moja iliyofanya Maria awe na imani yenye nguvu ambayo ilionekana katika maisha yake yote.​—Soma Waebrania 11:1.

Maria aliwasikiliza wachungaji kwa makini na akahifadhi maneno yao moyoni

17. Tunawezaje kuiga mtazamo wa Maria kuelekea kweli za kiroho?

17 Je, utaiga mfano wa Maria? Yehova amejaza kweli muhimu za kiroho kwenye Neno lake. Hata hivyo, ili tufaidike na kweli hizo tunapaswa kuzichunguza. Tunafanya hivyo kwa kusoma Biblia kwa ukawaida, si kama hadithi tu bali kama Neno la Mungu lililoongozwa na roho. (2 Tim. 3:16) Kisha, kama Maria, tunahitaji kuyahifadhi mambo ya kiroho moyoni na kuyatafakari. Tukitafakari mambo tunayosoma katika Biblia, na kufikiria jinsi tunavyoweza kutumia mashauri ya Yehova kikamili, tutaimarisha imani yetu.

Maneno Zaidi ya Kuhifadhi

18. (a) Maria na Yosefu walifuataje Sheria ya Musa Yesu alipokuwa mtoto mchanga? (b) Matoleo ambayo Yosefu na Maria walitoa hekaluni yalifunua nini kuhusu hali yao ya kiuchumi?

18 Yule mtoto alipokuwa na siku nane, Maria na Yosefu walimtahiri kulingana na Sheria ya Musa, na wakamwita Yesu kama walivyoagizwa. (Luka 1:31) Kisha, siku ya 40 wakatoka Bethlehemu na kumpeleka hekaluni huko Yerusalemu, umbali wa kilomita kumi hivi, wakatoa matoleo ya kujitakasa ambayo Sheria iliwaruhusu maskini, yaani, njiwa-tetere wawili au hua wawili. Hawakuaibika kwa sababu walishindwa kutoa kondoo-dume na njiwa-tetere kama wazazi wenye uwezo walivyotoa. Vyovyote vile, walitiwa moyo sana walipokuwa huko.​—Luka 2:21-24.

19. (a) Simeoni alimwambia Maria maneno gani ambayo alipaswa kuhifadhi moyoni? (b) Ana alitendaje alipomwona Yesu?

19 Mwanamume mzee anayeitwa Simeoni aliwakaribia na kumwambia Maria mambo zaidi aliyopaswa kuhifadhi moyoni. Alikuwa ameahidiwa kwamba angemwona Masihi kabla ya kufa, na roho takatifu ya Yehova ikamwonyesha kwamba Yesu ndiye Mwokozi aliyeahidiwa. Pia, Simeoni alimtahadharisha Maria kuhusu uchungu ambao siku moja angehisi. Alisema angehisi kana kwamba amechomwa na upanga mrefu. (Luka 2:25-35) Huenda maneno hayo yenye kuvunja moyo yalimsaidia Maria kuvumilia wakati mgumu aliokabili miaka 33 baadaye. Baada ya Simeoni, nabii wa kike anayeitwa Ana alimwona Yesu na akaanza kumwambia kila mtu aliyetumaini kukombolewa kwa Yerusalemu.​—Soma Luka 2:36-38.

Maria na Yosefu walitiwa moyo sana walipoenda kwenye hekalu la Yehova huko Yerusalemu

20. Kwa nini Maria na Yosefu walifanya uamuzi mzuri kwa kumpeleka Yesu hekaluni?

20 Yosefu na Maria walikuwa wamefanya uamuzi mzuri sana wa kumleta mtoto wao kwenye hekalu la Yehova lililokuwa Yerusalemu! Huo ulikuwa mwanzo wa mwana wao kwenda kwenye hekalu la Yehova. Wakiwa huko walimtolea Yehova matoleo bora na wakapata maagizo na kutiwa moyo. Bila shaka, siku hiyo Maria alitoka hekaluni akiwa ameimarishwa imani zaidi na moyo wake ukiwa umejaa mambo ya kiroho ambayo angetafakari na kuwaambia wengine.

21. Tunawezaje kuhakikisha kwamba kama Maria imani yetu itaendelea kuimarika?

21 Ni jambo linalopendeza kuona wazazi leo wakiiga mfano huo. Wazazi ambao ni Mashahidi wa Yehova huwapeleka watoto wao kwenye mikutano ya Kikristo kwa uaminifu. Wazazi hao hufanya yote wanayoweza, na kuwatia moyo waamini wenzao. Nao hutoka katika mikutano hiyo wakiwa na nguvu na furaha zaidi, na wakiwa na mambo mengi mazuri ya kuwaambia wengine. Inafurahisha kama nini kukutana nao! Tukifanya hivyo, kama Maria imani yetu itaimarika zaidi.

^ fu. 7 Ona tofauti kati ya safari hii na simulizi la safari ya mapema zaidi: “Maria akaondoka. . . akaenda” kumtembelea Elisabeti. (Luka 1:39) Wakati huo, kabla hajaolewa, Maria angesafiri bila kumjulisha Yosefu. Lakini baada ya kuolewa, Yosefu ndiye aliyefanya uamuzi wa kusafiri, si Maria.

^ fu. 10 Ilikuwa kawaida kwa miji kuwa na chumba cha kulala kwa ajili ya wasafiri.

^ fu. 14 Kwa kuwa wachungaji hao walikuwa wakiishi nje na mifugo yao, hilo linathibitisha kile ambacho kinaonyeshwa na matukio ya Biblia: Kristo hakuzaliwa Desemba wakati ambapo mifugo ingekuwa zizini, bali alizaliwa mwanzoni mwa Oktoba.