Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake

Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake

Igeni Imani Yao

Alijifunza Kusamehe Kutoka kwa Bwana Wake

PETRO hangeweza kusahau pindi yenye kuhuzunisha ambapo macho yake na ya Yesu yalikutana. Je, aliona katika macho ya Yesu ishara ya kutoridhika au ya kumshtumu? Hatuwezi kusema kwa uhakika aliona nini; Maandiko yanasema tu hivi: ‘Bwana aligeuka na kumtazama Petro.’ (Luka 22:61) Lakini kwa kumtazama tu, Petro alitambua uzito wa kosa lake. Alitambua kwamba alikuwa amefanya jambo lilelile ambalo Yesu alikuwa ametabiri, ingawa Petro alikuwa amesisitiza kwamba hangeweza kamwe kulifanya—yaani, kumkana Bwana wake mpendwa. Petro alishuka moyo na labda, hiyo ndiyo iliyokuwa pindi mbaya zaidi katika maisha yake yote.

Lakini hali ya Petro haikuwa bila matumaini. Kwa kuwa Petro alikuwa mtu mwenye imani kubwa, bado alikuwa na nafasi ya kuacha mwenendo wake wenye makosa na kujifunza mojawapo ya mambo makuu zaidi ambayo Yesu alifundisha. Alijifunza kuhusu msamaha. Kwa kuwa kila mmoja wetu anahitaji kujifunza jambo hilohilo, acheni tuone jinsi Petro alivyojifunza somo hilo gumu.

Petro Alihitaji Kujifunza Mambo Mengi

Miezi sita hivi mapema Petro alimuuliza Yesu swali fulani akiwa kwenye jiji la kwao la Kapernaumu. Aliuliza hivi: “Bwana, ndugu yangu atanitendea dhambi mara ngapi nami nimsamehe? Mpaka mara 7?” Yaelekea Petro alifikiri kwamba kusamehe mara saba ni tendo la ukarimu, kwa kuwa viongozi wa kidini wa siku hizo walifundisha kwamba mtu anapaswa kusamehe mara tatu tu! Yesu alimjibu: “Ninakuambia, si, Mpaka mara 7, bali, Mpaka mara 77.”—Mathayo 18:21, 22.

Je, Yesu alimaanisha kwamba Petro alipaswa kuweka rekodi ya makosa ambayo ametendewa? Hapana; kwa kumwambia asamehe mara 77 badala ya 7, Yesu alikuwa akimaanisha kwamba hakuna mwisho wa kusamehe. Yesu alionyesha kwamba Petro alikuwa ameathiriwa na roho ngumu ya kutosamehe na ya kuweka hesabu ya makosa iliyokuwa imeenea sana siku hizo. Lakini kama Mungu, msamaha wetu haupaswi kuwa na mipaka.

Petro hakubishana na Yesu. Lakini, je, Petro aliguswa moyo na somo alilojifunza kutoka kwa Yesu? Nyakati nyingine tunajifunza kwa kadiri kubwa zaidi kuhusu msamaha tunapotambua jinsi sisi wenyewe tunavyohitaji kusamehewa. Kwa hiyo, na tuzingatie mambo yaliyotukia kabla ya kifo cha Yesu. Wakati huo mgumu, Yesu alihitaji kumsamehe Petro makosa mengi ambayo alifanya.

Uhitaji Unaoongezeka wa Kusamehe

Usiku wa mwisho wa maisha ya Yesu duniani ulikuwa muhimu. Yesu alikuwa na mambo mengi ya kuwafundisha mitume wake—kwa mfano, aliwafundisha kuhusu unyenyekevu. Yesu aliwawekea mfano wa unyenyekevu kwa kuosha miguu yao, kazi iliyofanywa na wafanyakazi wa hali ya chini kabisa. Mwanzoni, Petro alimuuliza Yesu sababu ya kufanya hivyo. Kisha akakataa kuoshwa miguu. Halafu akasisitiza kwamba Yesu amwoshe sio miguu tu bali pia mikono na kichwa! Yesu aliendelea kuwa mwenye subira na kumweleza Petro kwa utulivu umuhimu na maana ya jambo alilokuwa akifanya.—Yohana 13:1-17.

Hata hivyo, muda mfupi baadaye, mitume walianza kubishana kuhusu ni nani kati yao aliyekuwa mkuu zaidi ya wote. Bila shaka, Petro alishiriki katika mabishano hayo yenye aibu yaliyoonyesha kiburi cha kibinadamu. Lakini, Yesu akawarekebisha kwa fadhili na hata akawapongeza kwa jambo moja zuri walilofanya, yaani, kushikamana kwa uaminifu na Bwana wao. Kisha, akatabiri kwamba wote wangemwacha. Hata hivyo, Petro alisema kwamba angeshikamana na Yesu hadi kifo. Kinyume cha maneno ya Petro, Yesu alisema kwamba Petro angemkana Bwana wake mara tatu usiku huohuo kabla ya jogoo kuwika mara mbili. Petro alipinga maneno ya Yesu na kujivuna kwamba angekuwa mwaminifu zaidi ya mitume wengine wote!—Mathayo 26:31-35; Marko 14:27-31; Luka 22:24-28.

Je, Yesu alikuwa karibu kukosa subira kumwelekea Petro? Kwa kweli, katika wakati huo wote mgumu, Yesu hakuacha kutafuta sifa nzuri za wanafunzi wake wasio wakamilifu. Ingawa alijua kuwa Petro angemkana, Yesu alisema: “Nimeomba dua kwa ajili yako ili imani yako isififie; na wewe, mara tu utakapokuwa umerudi, watie nguvu ndugu zako.” (Luka 22:32) Kwa hiyo, alionyesha alikuwa na uhakika kwamba Petro angerudia hali yake nzuri ya kiroho, na kuendelea na utumishi wake kwa uaminifu. Hiyo ni roho ya kusamehe na yenye fadhili kama nini!

Baadaye, katika bustani ya Gethsemane, Petro alihitaji kurekebishwa zaidi ya mara moja. Yesu aliwaambia Petro, Yakobo, na Yohana, waendelee kukesha alipokuwa akisali. Yesu alikuwa na maumivu makali ya kihisia na alihitaji msaada, lakini Petro na mitume hao wengine walilala tena na tena. Yesu alisema maneno haya yaliyoonyesha huruma na msamaha: “Bila shaka, roho inataka, lakini mwili ni dhaifu.”—Marko 14:32-38.

Punde si punde, umati ulifika, huku umebeba mienge, mapanga, na marungu. Huu ulikuwa wakati wa kutenda kwa tahadhari na busara. Lakini, kwa ghafula Petro akachomoa upanga wake na kumshambulia Malko, mtumwa wa kuhani mkuu, na kulikata sikio lake. Kwa utulivu Yesu alimkosoa Petro, akamponya Malko, kisha akaeleza kanuni ya kutotenda kwa jeuri ambayo wafuasi wake wameifuata hadi leo. (Mathayo 26:47-55; Luka 22:47-51; Yohana 18:10, 11) Petro alikuwa amefanya makosa mengi ambayo Bwana wake alihitaji kumsamehe. Kisa chake kinaweza kutukumbusha kwamba “sisi sote hujikwaa mara nyingi.” (Yakobo 3:2) Sote tunahitaji msamaha wa Mungu nyakati zote. Lakini kuna mambo mengi yaliyomsubiri Petro usiku huo. Alifanya kosa kubwa hata zaidi.

Petro Afanya Kosa Kubwa

Yesu aliuambia umati uliokuja kumshika kwamba, ikiwa walikuwa wanamtafuta yeye, wanapaswa kuwaacha mitume wake waende. Petro alitazama asijue la kufanya wakati umati huo ulipomkamata na kumfunga Yesu. Kisha, Petro pamoja na mitume wenzake wakakimbia.

Labda Petro na Yohana waliacha kukimbia walipokaribia nyumba ya Anasi ambaye hapo awali alikuwa Kuhani Mkuu. Hapa ndipo Yesu alipopelekwa mara ya kwanza ili kuhojiwa. Baadaye alipokuwa akipelekwa kwa Kayafa, Petro na Yohana walimfuata lakini ‘wakiwa mbali kiasi.’ (Mathayo 26:58; Yohana 18:12, 13) Petro hakuwa mwoga, kwa kuwa hangeweza kufanya hivyo bila kuwa na ujasiri wa kadiri fulani. Umati huo ulikuwa na silaha, na Petro alikuwa tayari amemjeruhi moja wao. Hata hivyo, katika tukio hili Petro haonyeshi upendo mshikamanifu ambao alidai alikuwa nao—yaani, kuwa tayari kufa pamoja na Bwana wake ikihitajika.—Marko 14:31.

Kama Petro, wengi leo wangependa kumfuata Kristo ‘wakiwa mbali kiasi’—kwa njia ambayo watu wengine hawatatambua kwamba wanamfuata. Lakini kama vile Petro mwenyewe alivyoandika baadaye, njia pekee ya kumfuata Kristo inavyofaa ni kuwa na ukaribu na yeye kadiri iwezekanavyo, kuiga kielelezo chake katika mambo yote, bila kujali matokeo.—1 Petro 2:21.

Petro aliufuata kwa tahadhari umati uliokuwa umemkamata Yesu hadi kwenye lango la mojawapo ya nyumba za kifahari jijini Yerusalemu. Hiyo ilikuwa nyumba ya Kayafa, kuhani mkuu tajiri na mwenye mamlaka. Kwa kawaida nyumba hizo zilijengwa kuzunguka ua na zilikuwa na lango upande wa mbele. Alipofika langoni, Petro alikatazwa kuingia ndani. Yohana aliyekuwa tayari ameingia ndani, alikuja na kuzungumza na mlinda lango ambaye alimruhusu Petro aingie. Inaonekana Petro hakukaa karibu na Yohana; wala hakujaribu kuingia ndani ya nyumba ili awe karibu na Bwana wake. Alikaa uani ambako baadhi ya watumwa na watumishi walikuwa wakiota moto ili kupisha usiku wenye baridi, huku wakiwatazama mashahidi wa uwongo walipokuwa wakiingia na kutoka kwenye chumba ambamo kesi dhidi ya Yesu ilikuwa ikiendelea.—Marko 14:54-57; Yohana 18:15, 16, 18.

Katika mwangaza wa moto, msichana aliyemruhusu Petro aingie aliweza kumwona vizuri na akamtambua. Alisema hivi kwa kumshutumu: “Wewe, pia, ulikuwa pamoja na Yesu Mgalilaya!” Petro hakutarajia hayo, kwa hiyo akakana kumjua Yesu na kusema kuwa haelewi yale ambayo msichana huyo alisema. Alienda kusimama karibu na lango ili asionekane, lakini msichana mwingine akamtambua na kusema jambo lilelile: “Mtu huyu alikuwa pamoja na Yesu Mnazareti.” Lakini Petro akaapa: “Simjui mtu huyo!” (Mathayo 26:69-72) Labda baada ya kumkana Yesu mara ya pili, ndipo Petro aliposikia jogoo akiwika, lakini alikuwa amevurugika kiasi cha kwamba hangeweza kukumbuka unabii ambao Yesu alikuwa ametoa saa chache mapema.

Muda mfupi baadaye, Petro alikuwa bado anajaribu sana kuepuka asitambuliwe. Lakini watu fulani waliokuwa wamesimama uani wakamkaribia. Mmoja wao alikuwa mtu wa ukoo wa Malko, yule mtumwa ambaye Petro alimkata sikio. Alimwambia Petro hivi: “Mimi nilikuona katika bustani pamoja naye, sivyo?” Petro alihisi kwamba alipaswa kuwathibitishia kuwa walikosea. Aliapa kuhusu jambo hilo, yaelekea akisema kwamba angepaswa kulaaniwa kama alikuwa akisema uwongo. Punde tu aliposema maneno hayo, jogoo aliwika. Hiyo ndiyo iliyokuwa mara ya pili kwa Petro kusikia jogoo akiwika usiku huo.—Yohana 18:26, 27; Marko 14:71, 72.

Yesu alikuwa ametoka nje na kusimama katika roshani. Wakati huo, kama ilivyotajwa mwanzoni, macho ya Yesu na ya Petro yalikutana. Ndipo Petro akatambua jinsi alivyokuwa amemkosea Bwana wake. Petro aliondoka uani huku akihisi mwenye hatia sana. Alienda kwenye barabara za jiji zilizoangazwa na mwezi uliokuwa unatua. Petro hakuwa anaona vizuri. Machozi yalimlengalenga, kisha akaanza kulia kwa uchungu.—Marko 14:72; Luka 22:61, 62.

Baada ya kutambua uzito wa kosa kama hilo, ni rahisi sana mtu afikiri kwamba dhambi yake ni kubwa mno isiweze kusamehewa. Huenda hata Petro alifikiri hivyo. Je, Petro angeweza kusamehewa?

Je, Petro Alisamehewa?

Baada ya kumkana Yesu, Petro alikuwa na uchungu mwingi sana kufikia mapambazuko, na matukio ya siku hiyo yalizidisha tu uchungu wake. Lazima alijilaumu sana Yesu alipokufa alasiri baada ya kuteswa kwa saa nyingi! Haikosi Petro aliumia sana kila alipofikiria jinsi alivyochangia uchungu wa Bwana wake katika siku Yake ya mwisho duniani akiwa mwanadamu. Ingawa alikuwa na huzuni nyingi sana, Petro hakuacha avunjike moyo kabisa. Tunajua hivyo kwa sababu muda mfupi baadaye Petro alianza kushirikiana na ndugu zake tena. (Luka 24:33) Bila shaka, mitume wote walihuzunika kwa sababu ya jinsi walivyotenda usiku huo wenye huzuni, na walitiana moyo kwa kadiri fulani walipokusanyika pamoja.

Sasa tunaona Petro akifanya uamuzi bora sana. Mtumishi wa Mungu anapofanya kosa, lililo muhimu si uzito wa kosa lake, bali ni jitihada anazofanya ili kuinuka tena na kurekebisha mambo. (Methali 24:16) Petro alionyesha imani ya kweli kwa kukusanyika na ndugu zake licha ya kushuka moyo. Mtu anapolemewa na huzuni au majuto, anaweza kushawishiwa kujitenga na wengine, lakini hilo ni jambo hatari. (Methali 18:1) Jambo la busara ni kukaa karibu na waamini wenzake ili apate nguvu za kuendelea kumtumikia Mungu.—Waebrania 10:24, 25.

Kwa kuwa alikuwa pamoja na ndugu zake, Petro alisikia habari zenye kushtua kwamba mwili wa Yesu haukuwa kaburini. Petro na Yohana walikimbia kwenda kaburini ambapo Yesu alikuwa amezikwa na kiingilio kuzibwa kabisa. Yohana, ambaye yaelekea alikuwa mdogo kwa umri kuliko Petro, alifika kwanza. Lakini akasita alipokuta kaburi likiwa wazi. Petro hakusita hata kidogo. Ingawa alikuwa anahema kwa sababu ya kukimbia, aliingia ndani ya kaburi moja kwa moja. Na lo! Kaburi lilikuwa tupu!—Yohana 20:3-9.

Je, Petro aliamini kwamba Yesu alikuwa amefufuliwa? Mwanzoni hakuamini, ingawa wanawake waaminifu walisema kwamba malaika walikuwa wamewatokea na kuwaambia kuwa Yesu amefufuliwa kutoka kwa wafu. (Luka 23:55–24:11) Kufikia jioni, shaka na huzuni ya Petro ilikuwa imetoweka. Yesu alikuwa hai akiwa kiumbe wa roho mwenye nguvu! Aliwatokea mitume wake wote. Lakini kwanza alifanya jambo fulani la faragha. Mitume walisema hivi siku hiyo: “Kwa kweli Bwana alifufuliwa naye alimtokea Simoni!” (Luka 24:34) Pia, baadaye mtume Paulo aliandika kuhusu siku hiyo ya pekee ambapo Yesu “alimtokea Kefa, kisha wale kumi na wawili.” (1 Wakorintho 15:5) Kefa na Simoni ni majina mengine ya Petro. Yesu alimtokea Petro siku hiyo—yaelekea akiwa peke yake.

Biblia haisemi ni nini kilichotendeka wakati Yesu na Petro walipokutana. Tunaweza tu kuwazia jinsi Petro alivyofurahi kumwona Bwana wake mpendwa akiwa hai tena, na kupata nafasi ya kuonyesha huzuni na toba yake. Zaidi ya yote, Petro alitaka kusamehewa. Hapana shaka kwamba Yesu alimsamehe kabisa. Leo, Wakristo wanaoanguka katika dhambi wanahitaji kukumbuka kisa cha Petro. Hatupaswi kamwe kufikiri kwamba Mungu hawezi kutusamehe. Yesu alimwiga kabisa Baba yake ambaye ‘anasamehe kwa njia kubwa.’—Isaya 55:7.

Uthibitisho Zaidi wa Msamaha

Yesu aliwaambia mitume wake waende Galilaya, ili wakutane naye tena. Walipofika huko, Petro aliamua kwenda kuvua samaki katika Bahari ya Galilaya. Mitume kadhaa waliandamana naye. Kwa mara nyingine tena, Petro alijikuta amerudia maisha yake ya awali ya kuvua samaki. Petro aliposikia mlio wa mbao za mashua, sauti ya mawimbi yakipigapiga mashua, na alipogusa nyavu ngumu kwa mikono yake, alikumbuka maisha yake ya awali. Je, usiku huo aliwaza jinsi anavyopaswa kuendesha maisha yake wakati huo ambapo huduma ya Yesu duniani ilikuwa imeisha? Je, alikuwa ameanza kuvutiwa tena na maisha ya kawaida ya uvuvi? Vyovyote vile, hawakuvua samaki hata mmoja usiku wote.—Mathayo 26:32; Yohana 21:1-3.

Lakini, kulipopambazuka, mtu fulani aliwaita akiwa ufuoni na kuwahimiza watupe nyavu zao upande ule mwingine wa mashua. Walitii na kuvua samaki 153! Petro alimtambua mtu huyo. Akaruka kutoka kwenye mashua na kuogolea mpaka ufuoni. Huko ufuoni, Yesu aliwapa chakula cha samaki aliyepikwa kwenye moto wa makaa. Kisha, Yesu alimkazia fikira Petro.

Alimuuliza Petro kama alimpenda Bwana wake “kuliko hawa”—yaonekana akielekeza kidole kwenye samaki wengi waliokuwa wamevuliwa. Je, Petro alipenda biashara ya uvuvi kuliko alivyompenda Yesu moyoni mwake? Kama vile Petro alivyomkana Bwana wake mara tatu, Yesu alimpa nafasi ya kukiri upendo wake mara tatu mbele ya mitume wenzake. Alipokuwa akifanya hivyo, Yesu alimweleza jinsi ya kuonyesha upendo huo: kwa kutanguliza utumishi mtakatifu, kulisha, na kuchunga kondoo wa Kristo, ambao ni wafuasi wake waaminifu.—Yohana 21:4-17.

Hivyo, Yesu alithibitisha kwamba bado yeye na Baba yake wangeendelea kumtumia Petro. Mtume huyo angetimiza daraka muhimu katika kutaniko chini ya mwongozo wa Kristo. Huo ni uthibitisho ulioje kwamba Yesu alikuwa amemsamehe Petro kabisa! Kwa kweli, rehema ya Yesu ilimgusa Petro moyo sana.

Petro aliendelea kutimiza daraka lake kwa miaka mingi. Aliwatia nguvu ndugu zake, kama vile Yesu alivyomwamuru usiku uliotangulia kifo Chake. Kwa subira na fadhili, Petro alifanya kazi ya uchungaji na kulisha wafuasi wa Kristo. Mwanamume huyo aliyeitwa pia Simoni aliishi kupatana na jina alilopewa na Yesu—Petro, au Mwamba—kwa kuwa imara, mwenye nguvu, mwenye uvutano mzuri na mwenye kutegemeka kutanikoni. Sifa hizo zinaonekana katika barua zake mbili zenye upendo ambazo zilikuja kuwa vitabu muhimu vya Biblia. Barua hizo pia zinaonyesha kwamba Petro hakusahau jambo alilojifunza kutoka kwa Yesu kuhusu msamaha.—1 Petro 3:8, 9; 4:8.

Ni vizuri pia tujifunze jambo hilo. Je, sikuzote sisi humwomba Mungu msamaha kwa makosa yetu mengi? Je, tunakubali msamaha wa Mungu na kuamini kwamba msamaha huo unatufanya kuwa safi? Na je, tunawasamehe wengine pia? Tukifanya hivyo, tunaiga imani ya Petro—na rehema ya Bwana wake.

[Blabu katika ukurasa wa 22]

Yesu alihitaji kumsamehe Petro makosa mengi aliyofanya, lakini ni nani kati yetu asiyehitaji kusamehewa kila siku?

[Picha katika ukurasa wa 23]

‘Bwana aligeuka na kumtazama Petro’

[Picha katika ukurasa wa 24]

“Bwana . . . alimtokea Simoni!”