Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kuhusu Tumaini la Wafu

Kuhusu Tumaini la Wafu

Tunayojifunza Kutoka kwa Yesu

Kuhusu Tumaini la Wafu

Yesu aliwafufua angalau watu watatu na hivyo kuonyesha kuna tumaini kwa ajili ya wafu. (Luka 7:11-17; 8:49-56; Yohana 11:1-45) Ili kuelewa tumaini la wafu ni lazima kwanza tuelewe kisababishi na chanzo cha kifo.

Kwa Nini Tunakuwa Wagonjwa na Kufa?

Yesu alipowasamehe watu dhambi zao, waliponywa. Kwa mfano, Yesu alimwambia hivi mtu aliyepooza: “‘Ni jambo gani lililo rahisi zaidi, kusema, Dhambi zako zimesamehewa, au kusema, Simama, utembee? Hata hivyo, ili mjue kwamba Mwana wa binadamu ana mamlaka duniani ya kusamehe dhambi—’ ndipo akamwambia yule mwenye kupooza: ‘Simama, chukua kitanda chako, uende nyumbani kwako.’” (Mathayo 9:2-6) Kwa hiyo, dhambi ndiyo inayosababisha magonjwa na kifo. Tulirithi dhambi kutoka kwa mtu wa kwanza, Adamu.—Luka 3:38; Waroma 5:12.

Kwa Nini Yesu Alikufa?

Yesu hakuwahi kutenda dhambi. Kwa hiyo, hakustahili kufa. Kwa kufa kwa ajili yetu, Yesu alilipia dhambi zetu. Alisema kwamba damu yake ‘ingemwagwa kwa ajili ya wengi kwa msamaha wa dhambi.’—Mathayo 26:28.

Yesu pia alisema: ‘Mwana wa binadamu alikuja, si kuhudumiwa, bali kuhudumu na kutoa nafsi yake kuwa fidia badala ya wengi.’ (Mathayo 20:28) Yesu alisema kuwa bei aliyolipa ilikuwa “fidia” kwa sababu iliwakomboa wengine kutoka kwa kifo. Yesu pia alisema: “Mimi nimekuja ili wapate kuwa na uzima na wapate kuwa nao kwa wingi.” (Yohana 10:10) Ili tuelewe kabisa tumaini la wafu, tunapaswa pia kujua wafu wako katika hali gani sasa.

Ni Nini Kinachotukia Mtu Anapokufa?

Lazaro, rafiki ya Yesu alipokufa, Yesu alifafanua ni nini kinachotukia mtu anapokufa. Aliwaambia wanafunzi wake hivi: “‘Lazaro rafiki yetu anapumzika, lakini ninafunga safari kwenda [Bethania] ili kumwamsha kutoka usingizini.’ . . . Walifikiri alikuwa akisema juu ya kupumzika katika usingizi. Kwa hiyo, wakati huo, Yesu akawaambia waziwazi: ‘Lazaro amekufa.’” Hivyo Yesu alionyesha wazi kwamba wafu wamelala, hawana fahamu.—Yohana 11:1-14.

Yesu alipomfufua, rafiki yake Lazaro alikuwa amekufa kwa siku nne. Hata hivyo, Biblia haitaji Lazaro akisimulia mambo aliyofanya wakati huo. Alipokuwa amekufa, Lazaro alikuwa amepoteza fahamu na hakujua lolote.—Mhubiri 9:5, 10; Yohana 11:17-44.

Kuna Tumaini Gani kwa Wafu?

Wafu watafufuliwa wakiwa na taraja la kuishi milele. Yesu alisema: “Saa inakuja ambayo wale wote waliomo ndani ya makaburi ya ukumbusho wataisikia sauti yake [Yesu] na kutoka.”—Yohana 5:28, 29.

Tumaini hilo ni wonyesho wa upendo wa Mungu. Yesu alisema: “Mungu aliupenda ulimwengu sana hivi kwamba akamtoa Mwana wake mzaliwa-pekee, ili kila mtu anayemwamini asiangamizwe bali awe na uzima wa milele.”—Yohana 3:16; Ufunuo 21:4, 5.

Kwa habari zaidi, ona sura ya 6 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? *

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 15 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.