Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Faida za Kujifunza Ukweli Kuhusu Moto wa Mateso

Faida za Kujifunza Ukweli Kuhusu Moto wa Mateso

Faida za Kujifunza Ukweli Kuhusu Moto wa Mateso

WALE ambao wanawafundisha watu kwamba moto wa mateso ni mahali ambapo watu wanateswa, wanaendeleza fundisho ambalo linamharibia Yehova Mungu sifa. Biblia inaonyesha wazi kwamba Mungu atawaharibu waovu wote. (2 Wathesalonike 1:6-9) Lakini hasira yenye uadilifu si sifa kuu ya Mungu.

Mungu si mkatili au asiye na fadhili. Hata anauliza: “Je! Mimi ninafurahia kufa kwake mtu mwovu?” (Ezekieli 18:23, Union Version) Ikiwa Mungu hafurahii kufa kwa mtu mwovu, anaweza namna gani kufurahia kuwaona waovu wakiteseka?

Sifa kuu ya Mungu ni upendo. (1 Yohana 4:8) Kwa kweli, “Mwenyezi-Mungu ni mwema kwa wote, ni mwenye huruma kwa viumbe vyake vyote.” (Zaburi 145:9, Biblia Habari Njema) Mungu anataka tumpende kutoka moyoni.—Mathayo 22:35-38.

Unachochewa na Nini—Kuogopa Moto wa Mateso au Kumpenda Mungu?

Fundisho la kwamba nafsi zinateseka katika moto wa mateso linawachochea watu wamwogope Mungu isivyofaa. Kwa kutofautisha, mtu anayejifunza ukweli kumhusu Mungu na kumpenda anamwogopa kwa njia inayofaa. “Woga wa BWANA ni mwanzo wa akili: na wote wanaofanya hivi wana akili njema,” inasema Zaburi 111:10. (Zaire Swahili Bible) Hiyo si hofu ya kupita kiasi, bali ni kumcha na kumheshimu sana Muumba. Inatufanya tuwe na woga unaofaa wa kutompendeza.

Fikiria jinsi kujifunza ukweli kuhusu moto wa mateso kulivyomsaidia Kathleen, mwenye umri wa miaka 32 ambaye hapo awali alikuwa akitumia dawa za kulevya. Maisha yake yalihusisha jeuri, kujichukia, ukosefu wa maadili, na kuhudhuria karamu. Anasema: “Ningemtazama binti yangu mwenye umri wa mwaka mmoja na kufikiri hivi, ‘Ona ninavyomtendea. Nitateketezwa kwa sababu ya kumtendea hivi.’” Kathleen alijaribu kuachana na dawa za kulevya, lakini hakufaulu. “Nilitaka kuwa mtu mzuri,” alisema, “lakini kila kitu maishani mwangu na ulimwenguni kilikuwa kibaya sana. Sikuona sababu ya kuwa mzuri.”

Kathleen alikutana na Mashahidi wa Yehova. “Nilijifunza kwamba hakukuwa na moto wa mateso. Uthibitisho wa Maandiko ulipatana na akili,” akasema Kathleen. “Nilitulizwa sana kujua kwamba singeteketezwa katika moto wa mateso.” Alijifunza pia ahadi ya Mungu kwamba wanadamu wataishi milele katika dunia iliyosafishwa uovu. (Zaburi 37:10, 11, 29; Luka 23:43) “Sasa nina tumaini halisi, tumaini la kuishi milele katika Paradiso!” akasema.

Je, Kathleen angeweza kuacha kutumia dawa za kulevya bila kuogopa moto wa mateso? Anaeleza hivi: “Nilipokuwa na hamu ya kutumia dawa za kulevya, nilisali, nikimwomba Yehova Mungu anisaidie. Nilifikiria maoni yake kuhusu mazoea kama hayo yenye kuchafua nami sikutaka kumhuzunisha. Alijibu sala zangu.” (2 Wakorintho 7:1) Kuogopa kutompendeza Mungu kulimsaidia Kathleen ashinde uraibu wake.

Naam, kumpenda na kumwogopa Mungu kwa njia inayofaa kunaweza kutuchochea kufanya mapenzi ya Mungu ili tuwe na furaha ya kudumu, bali si kuogopa moto wa mateso. Mtunga-zaburi alisema: “Heri ni kila mutu anayeogopa BWANA, anayetembea katika njia zake.”—Zaburi 128:1, ZSB.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 9]

NI NANI WATAKAOACHILIWA KUTOKA HADESI?

Tafsiri fulani za Biblia zinawachanganya watu kwa kutumia maneno mawili tofauti ya Kigiriki, yaani, Geʹen·na na Haiʹdes, kuwakilisha “moto wa mateso.” Katika Biblia, neno Geʹen·na linamaanisha kuharibiwa kabisa, bila tumaini la kufufuliwa. Tofauti na hilo, wale walio katika Haiʹdes, au Hadesi, wana tumaini la kufufuliwa.

Hivyo, baada ya Yesu kufa na kufufuliwa, mtume Petro aliwahakikishia wasikilizaji wake kwamba Yesu ‘hakuachwa Hadeze.’ (Matendo 2:27, 31, 32; Zaburi 16:10; Zaire Swahili Bible) Neno lililotafsiriwa “Hadeze” (hadesi) katika mstari huo ni neno la Kigiriki Haiʹdes. Yesu hakutupwa katika moto wa mateso. “Hadeze” lilikuwa kaburi. Lakini si Yesu tu anayeachiliwa na Mungu kutoka Hadesi.

Biblia inasema hivi kuhusiana na ufufuo: “Mauti na Hadeze zikatoa wafu waliokuwa ndani yao.” (Ufunuo 20:13, 14, ZSB) Kutoa watu katika “Hadeze” kutamaanisha kwamba Mungu atawarudisha hai wale anaoamua kuwa wanastahili kufufuliwa. (Yohana 5:28, 29; Matendo 24:15) Hilo ni tumaini zuri kama nini la wakati ujao, kuwaona wapendwa wetu waliokufa wakitoka kaburini! Yehova, Mungu wa upendo usio na kifani, atafanya hivyo.