Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mashahidi wa Yehova Wanavunja Ndoa za Watu?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanavunja Ndoa za Watu?

Je, Mashahidi wa Yehova Wanavunja Ndoa za Watu?

“MWENZI mmoja anapobadili dini yake, ndoa yao itavunjika.” Hivyo ndivyo watu wengi wanavyodai. Nyakati nyingine onyo hilo linatolewa kwa mwenzi wa ndoa anayeamua kuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova. Lakini je, madai hayo yanakuwa kweli sikuzote?

Inaeleweka kwamba mwenzi wa ndoa anapoanza kupendezwa na dini au kubadili imani ambayo amekuwa nayo kwa muda mrefu, yule mwenzi mwingine anaweza kushtuka. Huenda akawa na wasiwasi, akakata tamaa, na hata kukasirika.

Mara nyingi, mke ndiye huwa wa kwanza kutaka kubadili dini yake. Ikiwa mke wako anajifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova, hilo linaweza kuwa na matokeo gani kwa ndoa yako? Ikiwa wewe ni mke anayeshirikiana na Mashahidi wa Yehova, unaweza kufanya nini ili kupunguza wasiwasi wa mume wako?

Maoni ya Mume

Mke wa Mark, anayeishi nchini Australia, alianza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova baada ya wao kuwa wameoana kwa miaka 12. “Nilikuwa na ndoa yenye furaha na kazi yenye kuridhisha sana,” anasema Mark. “Mambo yalikuwa shwari. Kisha mke wangu akaamua kuanza kujifunza Biblia pamoja na Mashahidi wa Yehova. Nilihisi kwamba maisha yangu yangebadilika. Mwanzoni nilikuwa na wasiwasi alipoanza kujifunza Biblia, lakini aliponiambia kwamba alikuwa ameamua kubatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova, nilihangaika sana.”

Mark alianza kujiuliza ikiwa ndoa yake ingevunjika kwa sababu ya dini mpya ya mke wake. Alifikiria kumwambia aache kujifunza Biblia na kumkataza kabisa asishirikiane na Mashahidi. Hata hivyo, badala ya kumkataza, Mark aliacha wakati upite. Ndoa yake ilipatwa na nini?

Mark anasema hivi: “Inafurahisha kwamba ndoa yetu ni imara zaidi sasa kuliko ilivyokuwa mwanzoni. Imeendelea kuwa bora tangu mke wangu abatizwe na kuwa Shahidi wa Yehova miaka 15 iliyopita.” Ni nini ambacho kimesaidia ndoa hiyo ifanikiwe? Mark anasema hivi: “Ninaona ni kwa sababu mke wangu alifuata mashauri mazuri ya Biblia. Sikuzote amejaribu kunitendea kwa heshima.”

Mashauri Kutoka kwa Wake Waliofanikiwa

Ikiwa wewe ni mke anayeshirikiana na Mashahidi wa Yehova unaweza kusema na kufanya nini ili kupunguza wasiwasi ambao huenda mwenzi wako akawa nao? Fikiria maelezo haya ya wanawake kutoka sehemu mbalimbali ulimwenguni.

Sakiko anayeishi Japani: “Nimeolewa kwa miaka 31 na nina watoto watatu. Nimekuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova kwa miaka 22 sasa. Nyakati nyingine ni vigumu kuishi na mume ambaye hana imani kama yako. Lakini mimi ninajitahidi kufuata shauri la Biblia la kuwa ‘mwepesi kuhusu kusikia, si mwepesi wa kusema, si mwepesi wa ghadhabu.’ (Yakobo 1:19) Mimi ninajaribu kuwa mwenye fadhili kwa mume wangu na kukubali mapendezi yake ikiwa hayapingani na kanuni za Biblia. Hilo limesaidia ndoa yetu ifanikiwe.”

Nadezhda anayeishi Urusi: “Nimeolewa kwa miaka 28 na nilibatizwa na kuwa Shahidi miaka 16 iliyopita. Kabla ya kujifunza Biblia, sikufikiri kwamba mume wangu anapaswa kuwa kichwa cha familia. Nilipenda kujifanyia maamuzi yangu mwenyewe katika mambo mengi. Hata hivyo, hatua kwa hatua niligundua kwamba kufuata kanuni za Biblia kulichangia amani na furaha ya familia yetu. (1 Wakorintho 11:3) Polepole niliweza kujitiisha, na mume wangu ametambua mabadiliko niliyofanya.”

Marli anayeishi Brazili: “Nina watoto wawili na nimeolewa kwa miaka 21. Nilibatizwa na kuwa Shahidi miaka 16 iliyopita. Nilijifunza kwamba Yehova Mungu anawataka wenzi wa ndoa waishi pamoja na hataki watengane. Kwa hiyo, mimi ninajaribu kuwa mke mwema, kuzungumza, na kutenda kwa njia inayomfurahisha Yehova na mume wangu.”

Larisa anayeishi Urusi: “Nilipokuwa mmoja wa Mashahidi wa Yehova miaka 19 hivi iliyopita, nilitambua kwamba jambo muhimu zaidi ni kubadili maisha yangu. Mume wangu anaweza kuona jinsi ambavyo Biblia imenichochea kutenda mema, kwamba imenisaidia kumthamini zaidi. Mwanzoni, tungebishana kuhusu kuwalea watoto wetu, lakini tumesuluhisha tofauti hizo. Mume wangu anawaruhusu watoto wahudhurie mikutano ya kidini pamoja nami kwa sababu anaona kwamba wanafundishwa mambo yanayowafaidi.”

Valquíria anayeishi Brazili: “Nina mtoto mmoja na nimeolewa kwa miaka 19. Miaka 13 iliyopita, nilibatizwa na kuwa Shahidi wa Yehova. Mwanzoni, mume wangu hakutaka nishiriki katika kazi ya kuhubiri. Lakini nilijifunza kumjibu kwa upole na kumsaidia kuona kwamba Biblia ilikuwa ikinifanya niwe na utu mzuri. Hatua kwa hatua mume wangu alielewa jinsi ilivyo muhimu kwangu kushiriki katika kazi ya kuhubiri. Siku hizi, yeye ananitegemeza kabisa katika utendaji wangu wa kiroho. Ninapoenda kujifunza Biblia na watu katika maeneo ya vijijini, yeye ananipeleka kwa gari na kusubiri nje hadi nimalize.”

Inaboresha Ndoa

Ikiwa mwenzi wako anashirikiana na Mashahidi wa Yehova, usiwe na wasiwasi kwamba ndoa yako itavunjika. Kama wenzi wengi wa ndoa ulimwenguni pote wamejionea, Biblia inaboresha ndoa.

Mume mmoja ambaye si Shahidi wa Yehova anakiri hivi waziwazi: “Mwanzoni nilikuwa na wasiwasi mke wangu alipokuwa Shahidi wa Yehova, lakini sasa ninahisi kwamba nimepata faida nyingi sana.” Mume mwingine alisema hivi kuhusu mke wake: “Uaminifu, bidii, na utimilifu wa mke wangu umenifanya nivutiwe sana na Mashahidi wa Yehova. Ndoa yetu imeboreshwa sana kwa sababu ya imani yake. Kila mmoja wetu amejifunza kukubali maoni ya mwenzake na tunaona ndoa yetu kuwa kifungo cha maisha.”

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 13]

Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Ndoa?

Mashahidi wa Yehova wanaiona Biblia kuwa Neno la Mungu lililoongozwa na roho. Kwa hiyo, wao wanachukua kwa uzito kile inachosema kuhusu ndoa. Ona jinsi Biblia inavyojibu maswali yafuatayo:

Je, Mashahidi wa Yehova wanawatia moyo washiriki wao watengane na wenzi wao wasio Mashahidi? Hapana. Mtume Paulo aliandika hivi: “Ikiwa ndugu yeyote ana mke asiyeamini, na bado mke huyo anakubali kukaa pamoja naye, basi asimwache; na mwanamke aliye na mume asiyeamini, na bado mume huyo anakubali kukaa pamoja naye, basi asimwache mume wake.” (1 Wakorintho 7:12, 13) Mashahidi wa Yehova wanaishi kupatana na amri hiyo.

Je, mke ambaye ni mmoja wa Mashahidi wa Yehova anatiwa moyo kupuuza maoni ya mume wake ikiwa hana imani kama yake? Hapana. Mtume Petro anaandika: “Ninyi wake, jitiisheni kwa waume zenu wenyewe, ili, ikiwa wowote si watiifu kwa lile neno, wavutwe bila neno kupitia mwenendo wa wake zao, kwa sababu wamekwisha kushuhudia kwa macho mwenendo wenu ulio safi kiadili pamoja na heshima kubwa.”—1 Petro 3:1, 2.

Je, Mashahidi wa Yehova wanafundisha kwamba mume ana mamlaka isiyo na mipaka? Hapana. Mtume Paulo alisema: “Nataka mjue kwamba kichwa cha kila mwanamume ni Kristo; nacho kichwa cha mwanamke ni mwanamume; nacho kichwa cha Kristo ni Mungu.” (1 Wakorintho 11:3) Mke Mkristo atamheshimu mume wake akiwa kichwa cha familia. Hata hivyo, mamlaka ya mume ina mipaka. Anawajibika mbele za Mungu na Kristo. Hivyo, mume anapomwamuru mke wake atende kwa njia inayovunja sheria ya Mungu, mke Mkristo ‘atamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.’—Matendo 5:29.

Je, Mashahidi wa Yehova wanafundisha kwamba haifai kutalikiana? Hapana. Yesu Kristo alisema: “Ninawaambia kwamba mtu yeyote anayemtaliki mke wake na kumwoa mwingine, ila kwa sababu ya uasherati [ukosefu wa maadili katika ngono], anafanya uzinzi.” (Mathayo 19:9) Hivyo, Mashahidi wa Yehova wanakubali na kuamini maoni ya Yesu kwamba uzinzi ni msingi wa kutalikiana. Lakini pia wanaamini kwamba ndoa haipaswi kuvunjwa kwa sababu ndogondogo. Wanawatia moyo washiriki wao wafuate maneno haya ya Yesu: “Mwanamume atamwacha baba yake na mama yake naye atashikamana na mke wake, na hao wawili watakuwa mwili mmoja. . . . Kwa hiyo, kile ambacho Mungu ameunganisha mtu yeyote asikitenganishe.”—Mathayo 19:5, 6.