Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kubali Mamlaka ya Yehova

Kubali Mamlaka ya Yehova

Kubali Mamlaka ya Yehova

“Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake; na bado amri zake si mzigo mzito.”—1 YOH. 5:3.

1, 2. (a) Kwa nini watu wengi leo wanachukia wazo la kunyenyekea chini ya mamlaka? (b) Je, kweli watu wasiopenda kujitiisha chini ya mamlaka ya wengine wako huru? Eleza.

“MAMLAKA.” Watu wengi leo wanachukia neno hilo. Wengi wanachukia wazo la kunyenyekea chini ya mtu mwingine. Watu wasiopenda kujitiisha chini ya mamlaka ya wengine wana mtazamo huu, “Hakuna mtu anayepaswa kuniambia jambo la kufanya.” Hata hivyo, je, kweli watu hao wako huru? Hapana! Wengi wao wanafuata viwango vya watu wengine wengi ambao ‘wanafanyizwa kulingana na mfumo huu wa mambo.’ (Rom. 12:2) Badala ya kuwa huru, wao ni “watumwa wa uharibifu,” kama mtume Petro Mkristo alivyosema. (2 Pet. 2:19) Wanatembea “kulingana na mfumo wa mambo wa ulimwengu huu, kulingana na mtawala wa mamlaka ya hewa,” Shetani Ibilisi.—Efe. 2:2.

2 Mwandishi mmoja alisema hivi kwa majivuno: “Siwapi wazazi wangu au kasisi au mhudumu wa kanisa au mwalimu wa dini ya Kihindu au Biblia mamlaka ya kuniamulia yaliyo mema.” Ni kweli kwamba watu fulani wanaweza kutumia mamlaka yao vibaya na huenda wasistahili kuonyeshwa utii. Lakini je, suluhisho ni kukataa kabisa mwongozo wowote ule? Ukitupia jicho vichwa vikuu vya magazeti utapata jibu lenye kusikitisha. Inahuzunisha sana kwamba wakati huu ambapo wanadamu wanahitaji sana mwongozo, wengi wao hawautaki hata kidogo.

Maoni Yetu Kuhusu Mamlaka

3. Wakristo wa karne ya kwanza walionyesha kwa njia gani kwamba hawakufanya chochote kile walichoambiwa wafanye na wanadamu wenye mamlaka?

3 Tukiwa Wakristo, msimamo wetu ni tofauti na wa ulimwengu. Hilo halimaanishi kwamba tunafanya chochote kile tunachoambiwa tufanye. Badala yake, nyakati nyingine ni lazima tukatae kufanya mambo fulani ambayo wengine wanatuagiza, hata ikiwa wana mamlaka. Hata Wakristo wa karne ya kwanza walifanya hivyo. Kwa mfano, mitume walipoagizwa waache kuhubiri, hawakusikiliza vitisho vya kuhani mkuu na washiriki wengine wa Sanhedrini wenye mamlaka. Hawakuacha kutenda mambo yanayofaa ili kuwatii wanadamu wenye mamlaka.—Soma Matendo 5:27-29.

4. Ni mifano gani katika Maandiko ya Kiebrania inayoonyesha kwamba watu wengi wa Mungu walikataa mambo yasiyofaa yaliyopendwa na wengi?

4 Watumishi wengi wa Mungu walioishi kabla ya Ukristo walitenda kwa njia hiyohiyo. Kwa mfano, Musa “alikataa kuitwa mwana wa binti ya Farao, akachagua kutendewa vibaya pamoja na watu wa Mungu,” hata ingawa kufanya hivyo kulichochea “hasira ya mfalme.” (Ebr. 11:24, 25, 27) Yosefu alikataa aliposhawishiwa na mke wa Potifa aliyekuwa na uwezo wa kulipiza kisasi na kumdhuru. (Mwa. 39:7-9) Danieli “aliazimia moyoni mwake kwamba hatajitia unajisi kwa vyakula vitamu vya mfalme,” hata ingawa haikuwa rahisi kwa ofisa mkuu wa makao ya mfalme wa Babiloni kukubali msimamo wa Danieli. (Dan. 1:8-14) Mifano hiyo inaonyesha kwamba, tangu zamani, watu wa Mungu wamechukua msimamo imara wa kutenda yaliyo mema, bila kujali matokeo. Hawakukubaliana na wanadamu ili tu kuwapendeza; sisi pia hatupaswi kufanya hivyo.

5. Maoni yetu kuhusu mamlaka yanatofautiana kwa njia gani na yale ya ulimwengu?

5 Msimamo wetu hodari haupaswi kuonwa kuwa ukaidi; na sisi si kama waasi wanaopinga mfumo fulani wa kisiasa. Badala yake, tumeazimia kukubali mamlaka ya Yehova kuliko ya mwanadamu yeyote. Sheria ya mwanadamu inapopingana na sheria ya Mungu, hatuhitaji kufikiria sana kile tutakachofanya. Kama mitume wa karne ya kwanza, tunamtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.

6. Kwa nini kutii amri za Yehova ni jambo lenye faida sikuzote?

6 Ni nini ambacho kimetusaidia kukubali mamlaka ya Mungu? Tunakubaliana na maneno ya Methali 3:5, 6: “Mtegemee Yehova kwa moyo wako wote wala usitegemee uelewaji wako mwenyewe. Mtambue yeye katika njia zako zote, naye atanyoosha mapito yako.” Tunaamini kwamba jambo lolote ambalo Mungu anataka tufanye litatuletea faida mwishowe. (Soma Kumbukumbu la Torati 10:12, 13.) Ndiyo, Yehova aliwaambia Waisraeli kwamba yeye ndiye “anayekufundisha ili ujifaidi mwenyewe, Yeye anayekufanya uende katika njia unayopaswa kutembea ndani yake.” Kisha akaongeza hivi: “Laiti ungesikiliza amri zangu! Ndipo amani yako ingekuwa kama mto, na uadilifu wako kama mawimbi ya bahari.” (Isa. 48:17, 18) Tunaamini maneno hayo. Tunasadiki kwamba sikuzote tunafaidika tunapotii amri za Mungu.

7. Tunapaswa kufanya nini tusipoelewa kikamili amri fulani iliyo katika Neno la Mungu?

7 Tunakubali mamlaka ya Yehova na kumtii hata tusipoelewa kikamili kwa nini takwa fulani liko katika Neno lake. Huo si ujinga; ni imani. Tunapofanya hivyo tunaonyesha kwamba tunasadiki kutoka moyoni kuwa Yehova anajua mambo yanayoweza kutuletea faida. Pia, tunapotii tunaonyesha kwamba tunampenda, kwa kuwa mtume Yohana aliandika hivi: “Kumpenda Mungu humaanisha hivi, kwamba tuzishike amri zake.” (1 Yoh. 5:3) Lakini kuna jambo lingine kuhusu utii wetu ambalo hatupaswi kupuuza.

Kuzoeza Nguvu Zetu za Ufahamu

8. Kuna uhusiano gani kati ya ‘kuzoeza nguvu zetu za ufahamu’ na kukubali mamlaka ya Yehova?

8 Biblia inatuambia kwamba ‘nguvu zetu za ufahamu zinapaswa kuzoezwa kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia.’ (Ebr. 5:14) Hivyo, lengo letu si kutii amri za Mungu kidesturi tu. Badala yake, tunataka kuwa na uwezo wa “kutofautisha yaliyo sawa na yaliyo makosa pia” kwa kutegemea kanuni za Yehova. Tunataka kuona hekima ya njia za Yehova ili tuweze kusema hivi kama mtunga-zaburi: “Sheria yako imo ndani yangu.”—Zab. 40:8.

9. Tunaweza kufanya nini ili kupatanisha dhamiri yetu na kanuni za Yehova, na kwa nini ni jambo la maana kufanya hivyo?

9 Ili kuthamini sheria za Mungu kama mtunga-zaburi alivyofanya, tunahitaji kutafakari mambo tunayosoma katika Biblia. Kwa mfano, tunapojifunza kuhusu takwa fulani la Yehova, tunaweza kujiuliza hivi: ‘Kwa nini amri hii au kanuni hii ni ya hekima? Kwa nini nitafaidika nikitii? Ni matokeo gani mabaya ambayo yamewapata wale ambao wamepuuza shauri la Mungu kuhusu jambo hili?’ Tukipatanisha dhamiri yetu na kanuni za Yehova kwa njia hiyo, itakuwa rahisi zaidi kufanya maamuzi yanayopatana na mapenzi yake. Hilo litatuwezesha ‘kuendelea kufahamu yale yaliyo mapenzi ya Yehova’ na kutii. (Efe. 5:17) Si rahisi kufanya hivyo nyakati zote.

Shetani Anawachochea Watu Kudharau Mamlaka ya Mungu

10. Shetani ametumia njia gani moja kuwachochea watu wadharau mamlaka ya Mungu?

10 Kwa muda mrefu, Shetani amewachochea watu wadharau mamlaka ya Mungu. Roho yake ya kujitegemea inaonekana kwa njia nyingi. Kwa mfano, fikiria jinsi ambavyo watu hawaheshimu mpango wa ndoa ulioanzishwa na Mungu. Wengine wanaamua kuishi pamoja bila kuoana, na wengine wanapanga njama za kuwaacha wenzi wao wa ndoa. Huenda watu hao wakakubaliana na maneno ya mwanamke mmoja mwigizaji aliyesema hivi: “Mtu hawezi kuwa na mwenzi mmoja tu wa ndoa.” Aliongeza: “Simjui mtu yeyote aliye mwaminifu au anayetaka kuwa mwaminifu kwa mwenzi wake.” Vivyo hivyo, mwigizaji mwingine maarufu alisema hivi kuhusu mahusiano yake yaliyovunjika: “Sidhani kwamba tumeumbwa ili tuwe na mwenzi mmoja tu muda wote wa maisha yetu.” Tunapaswa kujiuliza hivi: ‘Je, ninakubali mamlaka ya Yehova katika ndoa, au maoni yangu yamepotoshwa na mtazamo wa ulimwengu wa kutojali?’

11, 12. (a) Kwa nini inaweza kuwa vigumu kwa vijana kukubali mamlaka ya Yehova? (b) Simulia kisa kinachoonyesha kwamba ni upumbavu kupuuza sheria na kanuni za Yehova.

11 Je, wewe ni kijana aliye katika tengenezo la Yehova? Ikiwa ndivyo, huenda Shetani anakulenga katika jitihada zake za kukuchochea udharau mamlaka ya Yehova. “Tamaa zinazotukia ujanani” na mkazo kutoka kwa vijana wenzako unaweza kukufanya ufikiri kwamba sheria za Mungu ni mzigo mzito. (2 Tim. 2:22) Usiruhusu hilo litukie. Jitahidi kuona hekima ya kanuni za Mungu. Kwa mfano, Biblia inakuambia ‘ukimbie uasherati.’ (1 Kor. 6:18) Kuhusiana na hilo, jiulize hivi: ‘Kwa nini amri hiyo ni ya hekima? Ninaweza kupata faida gani ninapoitii?’ Huenda unawajua watu fulani waliopuuza shauri la Mungu na kupatwa na matokeo mabaya sana. Je, kweli wana furaha sasa? Je, wana maisha bora kuliko yale waliyofurahia katika tengenezo la Yehova? Je, kweli wamepata siri fulani ya furaha ambayo watumishi wengine wa Mungu bado hawajapata?—Soma Isaya 65:14.

12 Fikiria maelezo yaliyotolewa muda fulani uliopita na Mkristo anayeitwa Sharon: “Kwa sababu ya kupuuza sheria ya Yehova, nimeambukizwa ugonjwa hatari wa UKIMWI. Mara nyingi, ninakumbuka jinsi nilivyokuwa mwenye furaha kwa miaka mingi nikimtumikia Yehova.” Alitambua kwamba ni upumbavu kuvunja sheria za Yehova na kwamba alipaswa kuziheshimu sana. Sheria za Yehova zinakusudiwa kutulinda. Sharon alikufa majuma saba tu baada ya kuandika maneno hayo. Kama kisa hicho chenye kusikitisha kinavyoonyesha, Shetani hana kitu chochote kizuri cha kuwapa wale wanaokuwa sehemu ya ulimwengu huu mwovu. Akiwa “baba ya uwongo,” anatoa ahadi nyingi, lakini hazitimii kamwe, kama ahadi aliyompa Hawa. (Yoh. 8:44) Ndiyo, sikuzote ni jambo bora kukubali mamlaka ya Yehova.

Jihadhari na Roho ya Kujitegemea

13. Tunapaswa kujihadhari na roho ya kujitegemea katika jambo gani?

13 Ili kukubali mamlaka ya Yehova, tunapaswa kujihadhari na roho ya kujitegemea. Mtazamo wa kiburi unaweza kutufanya tuhisi kwamba hatuhitaji mwongozo wa mtu yeyote. Kwa mfano, tunaweza kukataa mashauri yanayotolewa na wale wanaoongoza kati ya watu wa Mungu. Mungu amefanya mpango ili jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara iandae chakula cha kiroho kwa wakati unaofaa. (Mt. 24:45-47) Tunapaswa kutambua kwa unyenyekevu kwamba hiyo ndiyo njia ambayo Yehova anatumia kuwatunza watu wake leo. Uwe kama wale mitume waaminifu. Wanafunzi fulani walipokwazwa, Yesu aliwauliza mitume: “Je, ninyi pia mnataka kwenda?” Petro akajibu: “Bwana, tutaenda kwa nani? Wewe una maneno ya uzima wa milele.”—Yoh. 6:66-68.

14, 15. Kwa nini tunapaswa kutii mashauri ya Biblia kwa unyenyekevu?

14 Kukubali mamlaka ya Yehova kunatia ndani kutii mashauri yanayotegemea Neno lake. Kwa mfano, jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara imekuwa ikituhimiza “tukae macho na kutunza akili zetu.” (1 The. 5:6) Shauri hilo linafaa sana katika hizi siku za mwisho ambapo watu wengi ‘wanajipenda wenyewe, na wanapenda pesa.’ (2 Tim. 3:1, 2) Je, mitazamo hiyo inaweza kuwa na uvutano juu yetu? Ndiyo. Miradi isiyo ya kiroho inaweza kutufanya tusinzie kiroho au kuwa na mtazamo wa kupenda mali. (Luka 12:16-21) Hivyo, ni jambo la hekima kukubali mashauri ya Biblia na kuepuka maisha ya ubinafsi yanayopendwa na wengi katika ulimwengu wa Shetani!—1 Yoh. 2:16.

15 Wazee waliowekwa rasmi wanawagawia washiriki wa kutaniko chakula cha kiroho kinachotoka kwa jamii ya mtumwa mwaminifu na mwenye busara. Biblia inatuhimiza hivi: “Watiini wale wanaoongoza katikati yenu na mnyenyekee, kwa maana wanaendelea kuzilinda nafsi zenu kama wale watakaotoa hesabu; ili wafanye hivyo kwa shangwe na si kwa kuugua, kwa maana kufanya hivyo kungewadhuru ninyi.” (Ebr. 13:17) Je, hilo linamaanisha kwamba wazee wa kutaniko hawawezi kukosea? Hapana! Mungu anaona kasoro zao waziwazi kuliko mwanadamu yeyote. Lakini bado anataka tujinyenyekeze. Kushirikiana na wazee, hata ingawa si wakamilifu, kunaonyesha kwamba tunakubali mamlaka ya Yehova.

Umuhimu wa Unyenyekevu

16. Tunaweza kuonyesha jinsi gani kwamba tunamheshimu Yesu ambaye ndiye Kichwa cha kutaniko la Kikristo?

16 Sikuzote tunapaswa kukumbuka kwamba kwa kweli Yesu ndiye Kichwa cha kutaniko. (Kol. 1:18) Hilo ni jambo moja linalotufanya tujinyenyekeze chini ya mwelekezo wa wazee waliowekwa rasmi na “kuwafikiria kwa njia inayozidi ile ya kawaida.” (1 The. 5:12, 13) Bila shaka, wazee wa kutaniko wanaweza kuonyesha kwamba hata wao wanajinyenyekeza kwa kuwa waangalifu kufundisha ujumbe wa Mungu katika kutaniko, bali si maoni yao wenyewe. ‘Hawapiti mambo yaliyoandikwa’ ili kuendeleza maoni fulani ya kibinafsi.—1 Kor. 4:6.

17. Kwa nini roho ya kujitakia makuu ni hatari?

17 Wote katika kutaniko wanapaswa kuwa waangalifu wasijitafutie utukufu. (Met. 25:27) Inaonekana kwamba mwanafunzi mmoja ambaye mtume Yohana alikutana naye alinaswa na mtego huo. Yohana aliandika hivi: “Diotrefe, anayependa kuwa na mahali pa kwanza katikati yao, hapokei kwa heshima jambo lolote kutoka kwetu. Hiyo ndiyo sababu, nikija, nitakumbusha matendo yake ambayo anaendelea kufanya, akipiga porojo juu yetu kwa maneno maovu.” (3 Yoh. 9, 10) Sisi pia tunaweza kujifunza somo fulani leo kutokana na jambo hilo. Tuna sababu nzuri ya kung’oa mzizi wowote wa kujitakia makuu ambao huenda ukawa ndani yetu. Biblia inasema hivi: “Kiburi hutangulia kuanguka, na roho ya majivuno hutangulia kujikwaa.” Ni lazima wale wanaokubali mamlaka ya Mungu waepuke mtego wa kuwa na kimbelembele, kwa maana wasipoepuka mtego huo watapata aibu.—Met. 11:2; 16:18.

18. Ni nini kitakachotusaidia kukubali mamlaka ya Yehova?

18 Ndiyo, azimia kuipinga roho ya ulimwengu ya kujitegemea na ukubali mamlaka ya Yehova. Mara kwa mara, tafakari na kuthamini pendeleo kubwa ulilo nalo la kumtumikia Yehova. Kwa kuwa wewe ni mmoja wa watu wa Mungu, hilo linaonyesha kwamba amekuvuta kupitia roho yake takatifu. (Yoh. 6:44) Usichezee kamwe uhusiano wako pamoja na Mungu. Katika sehemu zote za maisha yako, jitahidi kuonyesha kwamba unakataa roho ya kujitegemea na kwamba unakubali mamlaka ya Yehova.

Je, Unakumbuka?

• Kukubali mamlaka ya Yehova kunatia ndani nini?

• Kuna uhusiano gani kati ya kuzoeza nguvu zetu za ufahamu na kukubali mamlaka ya Yehova?

• Ni njia gani ambazo Shetani anatumia kujaribu kuwachochea watu wadharau mamlaka ya Mungu?

• Kwa nini unyenyekevu ni muhimu ili kukubali mamlaka ya Yehova?

[Maswali ya Funzo]

[Picha katika ukurasa wa 18]

“Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu”

[Picha katika ukurasa wa 20]

Sikuzote ni jambo la hekima kufuata kanuni za Mungu