Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Tazama! Nuru Ni ya Ajabu!

Tazama! Nuru Ni ya Ajabu!

Tazama! Nuru Ni ya Ajabu!

IKIWA umewahi kupapasa-papasa gizani ukitafuta njia, unajua jinsi kufanya hivyo kunavyokatisha tamaa. Nuru inasaidia sana! Huenda pia umewahi kuwa katika hali inayoweza kulinganishwa na giza. Huenda hilo lilitukia uliposhindwa kutatua tatizo fulani. Kisha, pole kwa pole ukaanza kuona nuru—ukaanza kutambua kwamba kuna suluhisho. Kutoka kwenye giza la aina hiyo na kuingia kwenye nuru ni jambo zuri ajabu.

Kwa ujumla, watu katika karne ya kwanza walikuwa katika giza la kiroho. Akiwaandikia watu waliokuwa wameacha imani yao ya zamani na kukubali Ukristo, mtume Petro aliandika hivi: ‘Mungu aliwaita ninyi kutoka katika giza kuingia katika nuru yake ya ajabu.’ (1 Petro 2:9) Ni kana kwamba walitoka katika giza zito sana na kuingia katika nuru inayong’aa. Hali hiyo inaweza kulinganishwa na kuwa peke yako bila tumaini kisha unakuwa mshiriki wa familia iliyo na tumaini la wakati ujao ulio salama.—Waefeso 2:1, 12.

“Umeacha Upendo Uliokuwa Nao Mwanzoni”

Wakristo wa mapema walipata “ile kweli”—imani ya kweli ya Kikristo. (Yohana 18:37) Waliona nuru ya ajabu ya kweli na wakatoka katika giza la kiroho na kuingia katika nuru inayoangaza. Hata hivyo, baada ya muda, bidii ya kwanza ya Wakristo fulani ilipoa. Kwa mfano, kufikia mwishoni mwa karne ya kwanza, tatizo zito lilikuwa limesitawi katika kutaniko huko Efeso. Yesu Kristo aliyefufuliwa alifunua tatizo hilo aliposema: “Nina jambo hili dhidi yako, kwamba umeacha upendo uliokuwa nao mwanzoni. Kwa hiyo kumbuka umeanguka kutoka wapi, nawe utubu na kufanya yale matendo ya mwanzoni.” (Ufunuo 2:4, 5) Wakristo huko Efeso walipaswa kuamsha tena upendo wao kumwelekea Mungu na pia kuelekea kweli.

Namna gani sisi? Sisi pia tumepata shangwe ya kuona nuru, yaani, kujua kweli ya ajabu ya Neno la Mungu. Tumepata kuipenda kweli. Lakini matatizo yanayowapata watu kwa kawaida yanaweza kupunguza upendo wetu kuelekea kweli. Matatizo hususa ya hizi “siku za mwisho” yanaweza pia kupunguza upendo huo. Tunaishi katika “nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo”—ulimwengu uliojaa watu “wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, wenye kujidai, wenye majivuno, wakufuru, wasiotii wazazi, wasio na shukrani, wasio washikamanifu.” (2 Timotheo 3:1, 2) Uvutano wa watu hao unaweza kupunguza bidii yetu na kufanya upendo wetu kwa Yehova upoe.

Ikiwa tumepoteza upendo tuliokuwa nao mwanzoni, tunapaswa ‘kukumbuka tumeanguka kutoka wapi, na tutubu.’ Tunapaswa kurudia hali ya kiroho tuliyokuwa nayo mwanzoni. Zaidi ya hilo, tunapaswa kuwa waangalifu tusiache kamwe kuithamini kweli. Ni muhimu kama nini kwamba sisi sote tuendelee kuwa na mtazamo mzuri wenye furaha na kumpenda Yehova na kweli yake!

‘Kweli Inayotuweka Sisi Huru’

Nuru ya kweli ya Kimaandiko ni ya ajabu kwa sababu Biblia inajibu maswali muhimu ambayo yamewahangaisha wanadamu kwa maelfu ya miaka. Maswali hayo ni kama vile: Kwa nini tupo hapa? Ni nini kusudi la maisha? Kwa nini kuna uovu? Je, kuna uhai baada ya kifo? Yehova ametupa nuru ya kweli za ajabu za mafundisho ya Biblia. Je, hatupaswi kuwa wenye shukrani sana? Tusipuuze kamwe mambo ambayo tumejifunza!

Yesu aliwaambia wanafunzi wake: “Mtaijua kweli, nayo kweli itawaweka ninyi huru.” (Yohana 8:32) Dhabihu ya fidia ya Yesu imetufungulia njia ya kuwekwa huru kutoka katika dhambi na kifo. Lakini kweli hizo zenye thamani zimetuweka huru kutoka katika hali ya kutokuwa na ujuzi na uhakika katika ulimwengu huu uliojaa giza. Kutafakari na kuthamini mambo ambayo tumejifunza, kutatusaidia kuimarisha upendo wetu kwa Yehova na kwa Neno lake.

Mtume Paulo aliwaandikia hivi Wakristo huko Thesalonike: “Mlipolipokea neno la Mungu, ambalo mlilisikia kutoka kwetu, mlilikubali, si kama neno la wanadamu, bali, kama vile lilivyo kwa kweli, kama neno la Mungu, ambalo pia linafanya kazi ndani yenu waamini.” (1 Wathesalonike 2:13) Wathesalonike walisikia na ‘kulipokea neno la Mungu kwa shangwe.’ Hawakuwa tena “gizani.” Badala yake, wakawa “wana wa nuru.” (1 Wathesalonike 1:4-7; 5:4, 5) Wakristo hao walijifunza kwamba Yehova ndiye Muumba na kwamba yeye ni mweza-yote, ana hekima, upendo, na rehema. Kama wafuasi wengine wa Kristo, walijifunza pia kwamba Yehova amefanya mpango wa kufuta dhambi zao kupitia dhabihu ya fidia ya Mwana wake, Yesu Kristo.—Matendo 3:19-21.

Ingawa Wathesalonike hawakujua kweli yote, walijua mahali ambapo wangeweza kupata ujuzi. Maandiko yaliyoongozwa na roho yanaweza kumfanya mtu wa Mungu awe na “uwezo kamili, akiwa na vifaa kamili kwa ajili ya kila kazi njema.” (2 Timotheo 3:16, 17) Wakristo huko Thesalonike wangeendelea kujifunza, na kujionea tena na tena kwamba nuru inayotoka kwa Mungu ni ya ajabu kwelikweli. Walikuwa na sababu ya kushangilia nyakati zote. (1 Wathesalonike 5:16) Sisi pia tuna sababu ya kufanya hivyo.

Nuru kwa Barabara Yetu

Akieleza kwa nini nuru ni ya ajabu, mtunga-zaburi aliimba hivi: “Neno lako ni taa ya mguu wangu, na nuru kwa barabara yangu.” (Zaburi 119:105) Mwongozo tunaopata kutoka katika Neno la Mungu unaweza kutusaidia kuchagua njia ya maisha inayofaa zaidi na hivyo kuwa na kusudi maishani. Si lazima tuwe kama meli isiyo na mwelekeo. Kujua na kuifuata kweli kunatuzuia ‘tusirushwe huku na huku kama kwa mawimbi na kuchukuliwa huku na huku na kila upepo wa fundisho.’—Waefeso 4:14.

Biblia inasema: “Msiweke tegemeo lenu katika watu wenye vyeo, wala katika mtu wa udongo, ambaye hana wokovu wowote.” Pia inasema: “Mwenye furaha ni yule ambaye Mungu wa Yakobo ni msaada wake, ambaye tumaini lake liko katika Yehova Mungu wake.” (Zaburi 146:3, 5) Zaidi ya hilo, kumtumaini Yehova kunatusaidia kushinda woga na wasiwasi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Msihangaike juu ya kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na kutoa shukrani maombi yenu na yajulishwe Mungu; na amani ya Mungu yenye ubora unaozidi fikira zote itailinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.” (Wafilipi 4:6, 7) Kwa kweli tunapata faida tunapoongozwa na nuru ya Neno la Mungu.

Kuangaza Kama Mianga Katika Ulimwengu

Nuru ya Neno la Mungu ni ya ajabu pia kwa sababu inawawezesha wanadamu kupata pendeleo kubwa kuliko yote. Yesu aliwaagiza hivi wafuasi wake: “Nendeni mkafanye wanafunzi kutoka kwa watu wa mataifa yote, mkiwabatiza katika jina la Baba na la Mwana na la roho takatifu, na kuwafundisha kushika mambo yote ambayo nimewaamuru ninyi. Na, tazama! mimi nipo pamoja nanyi siku zote mpaka umalizio wa mfumo wa mambo.” Kabla ya kutoa amri hiyo Yesu alisema: “Nimepewa mamlaka yote mbinguni na duniani.”—Mathayo 28:18-20.

Wazia ni nani anayewasaidia Wakristo wa kweli kuhubiri habari njema na kuwafundisha watu wa mataifa yote kweli za Biblia. Yesu aliwaahidi wafuasi wake kwamba angekuwa pamoja nao. Kwa kweli amekuwa akiwasaidia na kuwategemeza katika huduma yao wanapoendelea ‘kuacha nuru yao iangaze,’ kupitia huduma yao na ‘matendo mengine mazuri.’ (Mathayo 5:14-16) Malaika pia wanahusika katika kazi hii ya kueneza Injili. (Ufunuo 14:6) Na namna gani Yehova Mungu? Mtume Paulo aliandika hivi: “Mimi nilipanda, Apolo akatia maji, lakini Mungu akaendelea kuikuza.” Ni pendeleo zuri kama nini kuwa “wafanyakazi wenzi wa Mungu”!—1 Wakorintho 3:6, 9.

Pia, wazia jinsi jitihada zetu katika kazi hii tuliyopewa na Mungu zinavyobarikiwa. Pendeleo letu tulilopewa na Mungu la ‘kuangaza kama mianga katika ulimwengu’ halina kifani. Kwa kurudisha nuru ya Neno la Mungu kupitia maneno na matendo yetu, tutaweza kuwasaidia sana watu wenye mioyo minyoofu. (Wafilipi 2:15) Na tunaweza kushangilia tunapohubiri na kufundisha kwa bidii, ‘kwa maana Mungu hakosi kuwa mwadilifu hivi kwamba asahau kazi yetu na upendo tulioonyesha kwa ajili ya jina lake.’—Waebrania 6:10.

‘Nunua Dawa ya Macho ya Kupaka Katika Macho’

Yesu alisema hivi katika ujumbe wake kwa kutaniko la Laodikia la karne ya kwanza: “Nunua kutoka kwangu . . . dawa ya macho ya kupaka katika macho yako ili upate kuona. Wale wote ninaowapenda, mimi huwakaripia na kuwatia nidhamu.” (Ufunuo 3:18, 19) Suluhisho la pekee la upofu wa kiroho ni “dawa ya macho,” yaani, mafundisho na nidhamu ya Yesu. Ikiwa tunataka kuendelea kuwa na mtazamo mzuri wa kiroho, tunapaswa kukubali na kutii mashauri yake na mwongozo unaopatikana katika Biblia nzima. Pia, tunapaswa kuwa na mtazamo wa akilini kama wa Kristo na kuiga mfano wake. (Wafilipi 2:5; 1 Petro 2:21) Dawa hiyo ya macho haitolewi bila malipo. Yesu alisema: ‘Inunue kutoka kwangu.’ Tunanunua dawa hiyo kwa kujitahidi na kwa kutumia wakati wetu.

Tukiondoka mahali palipo na giza na kuingia katika chumba kilicho na nuru, huenda macho yetu yakachukua muda kuzoea hali. Vivyo hivyo, inachukua muda kujifunza Neno la Mungu na kuona nuru ya kweli. Inachukua muda kutafakari yale tunayojifunza na kufikiria jinsi kweli ilivyo yenye thamani. Hata hivyo, gharama hiyo si kubwa sana. Kwa nini? Kwa sababu nuru ni ya ajabu!

[Picha katika ukurasa wa 14]

“Nunua kutoka kwangu . . . dawa ya macho ya kupaka katika macho yako ili upate kuona”