Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Yehova Huwajali Watu wa Kawaida

Yehova Huwajali Watu wa Kawaida

Yehova Huwajali Watu wa Kawaida

JE, NI lazima tuwe watu mashuhuri au wa pekee kwa njia fulani ili Mungu atutambue? Rais wa 16 wa Marekani, Abraham Lincoln, alisema hivi: “Bwana huwapenda watu wa kawaida. Ndiyo sababu anawaumba kwa wingi.” Wengi hujihisi kuwa watu wa kawaida wasio na kipawa chochote. Kuwa mtu wa kawaida kunaweza kumaanisha kuwa duni, wa hali ya chini. Vilevile, neno “kawaida” linaweza kumaanisha kutokuwa na uwezo, au cheo cha pekee, kutofikia viwango vya kawaida. Je, unapenda kushirikiana na watu wa aina gani? Watu wenye majivuno, wenye kujiamini, na wenye kiburi? Au je, unapenda kushirikiana na watu wenye urafiki, wanyenyekevu, wasiojivuna, ambao wanapendezwa na wengine kikweli?

Kwa kuwa watu wengi hudhulumiwa na kudharauliwa ulimwenguni leo, baadhi yao hawaamini kwamba Mungu anapendezwa nao. Msomaji mmoja wa gazeti hili aliandika hivi: “Nililelewa katika familia ambayo haikuwa na upendo. Nilidharauliwa, nilichokozwa, na kuchekelewa. Nilipokuwa mdogo nilihisi sifai kitu. Hisia hizo za utotoni bado hunilemea ninapokabili magumu maishani.” Hata hivyo, kuna sababu zinazofanya tuamini kwamba Mungu anapendezwa na watu wa kawaida.

Mungu Anapendezwa na Watu wa Kawaida

Mfalme Daudi aliandika hivi: “BWANA ndiye mkuu mwenye kusifiwa sana, wala ukuu wake hautambulikani.” (Zaburi 145:3) Hata hivyo, ukuu wake haumzuii asitujali kwa upendo na huruma. (1 Petro 5:7) Kwa mfano, mtunga-zaburi alisema hivi: “BWANA yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.”—Zaburi 34:18.

Mambo yanayovutia watu ulimwenguni kama vile urembo, umashuhuri, au utajiri, si muhimu machoni pa Mungu. Sheria ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ilionyesha kwamba aliwajali maskini, mayatima, wajane, na wageni. Mungu aliwaambia hivi Waisraeli ambao walitendwa kikatili huko Misri: “Usimwonee mgeni, wala kumtendea jeuri; . . . usimtese mjane yeyote aliyefiwa na mumewe, wala mtoto yatima. Ukiwatesa watu hao katika neno lo lote, nao wakanililia mimi, hakika yangu nitasikia kilio chao.” (Kutoka 22:21-24) Isitoshe, nabii Isaya alionyesha kwamba alikuwa na hakika kuwa Mungu anawajali watu wa hali ya chini: “Maana umekuwa ngome ya maskini, ngome ya mhitaji katika dhiki yake, mahali pa kukimbilia wakati wa tufani, kivuli wakati wa hari; wakati uvumapo upepo wa watu watishao, kama dhoruba ipigayo ukuta.”—Isaya 25:4.

Yesu Kristo, ambaye ni “mwakilisho sawasawa” wa Mungu, alipendezwa kikweli na watu wa kawaida katika huduma yake, na hivyo aliwaachia wanafunzi wake mfano wa kuiga. (Waebrania 1:3) Yesu “alihisi sikitiko,” alipoona umati uliokuwa “umechunwa ngozi na kutupwa huku na huku kama kondoo wasio na mchungaji.”—Mathayo 9:36.

Ona pia kwamba Yesu aliwachagua watu “wasio na elimu na wa kawaida” kuwa mitume wake. (Matendo 4:13) Baada ya kifo cha Yesu, wanafunzi wake walianza kuwaalika watu wa kila aina wasikie Neno la Mungu. Mtume Paulo aliandika kwamba “mtu yeyote asiye mwamini au mtu wa kawaida” angeweza kujiunga na kutaniko la Kikristo na kuwa mwamini. (1 Wakorintho 14:24, 25) Badala ya kuwachagua watu walio mashuhuri ulimwenguni, Mungu aliwachagua watu wa hali ya chini na wa kawaida wamtumikie. Mtume Paulo alisema hivi: “Mwatazama wito wake kwenu, akina ndugu, kwamba si wengi wenye hekima katika njia ya kimwili walioitwa, si wengi wenye nguvu, si wengi wa uzawa wa kikabaila; bali Mungu alivichagua vitu vipumbavu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha watu wenye hekima; na Mungu alivichagua vitu dhaifu vya ulimwengu, ili apate kuaibisha vitu vyenye nguvu; na Mungu alivichagua vitu vinyonge vya ulimwengu na vitu vyenye kudharauliwa, vitu ambavyo havipo, ili apate kuvifanya viwe si kitu vitu ambavyo vipo, ili mwili wowote usipate kujisifu machoni pa Mungu.”—1 Wakorintho 1:26-29.

Vilevile Mungu anapendezwa kikweli nasi leo. Mapenzi ya Mungu ni kwamba “watu wa namna zote waokolewe na kuja kwenye ujuzi sahihi wa kweli.” (1 Timotheo 2:4) Kwa kuwa Mungu aliwapenda wanadamu hivi kwamba alimtuma Mwanawe duniani afe kwa ajili yetu, hatupaswi kuhisi kwamba hatupendwi ama hatufai. (Yohana 3:16) Yesu Kristo aliwaonyesha wafuasi wake umuhimu wa kumtendea hata yule wa hali ya chini zaidi miongoni mwa ndugu zake kana kwamba wanamtendea Yesu mwenyewe. Alisema hivi: “Kwa kadiri ambayo mlimfanyia hilo mmoja wa wadogo zaidi sana wa ndugu zangu hawa, mlinifanyia mimi hilo.” (Mathayo 25:40) Hata ulimwengu uwe na maoni gani juu yetu, sisi ni wa pekee machoni pa Mungu maadamu tunaipenda kweli.

Hivyo ndivyo Francisco, * mvulana yatima wa Brazili, alivyohisi baada ya kukuza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Anasema hivi: “Kumjua Yehova na tengenezo lake kumenisaidia kushinda hisia zangu za kutojiamini na haya. Nilipata kujua kwamba Yehova anapendezwa na kila mmoja wetu.” Yehova akawa Baba halisi kwa Francisco.

Yehova Anawajali Vijana

Yehova anapendezwa kikweli na kijana mmojammoja. Tuwe vijana au wazee, hatungependa kamwe kujitukuza. Hata hivyo, huenda tukawa na vipawa na sifa ambazo Mungu anaweza kutumia wakati ujao. Yehova anajua marekebisho tunayopaswa kufanya na mazoezi tunayohitaji ili tutumie sifa na vipawa tulivyo navyo kikamili. Kwa mfano, ona simulizi katika 1 Samweli sura ya 16. Kwa kuwa wengine walionekana kuwa wanastahili zaidi kuwa wafalme wa Israeli machoni pa nabii Samweli, Yehova alieleza sababu za kumchagua Daudi, mwana mdogo wa Yese, kuwa mfalme wa baadaye wa Israeli: “Usimtazame uso wake, wala urefu wa kimo chake; kwa maana mimi nimemkataa [kaka ya Daudi]. BWANA haangalii kama binadamu aangaliavyo; maana wanadamu huitazama sura ya nje, bali BWANA huutazama moyo.”—1 Samweli 16:7.

Je, vijana leo wanaweza kuwa na hakika kwamba Yehova anapendezwa nao kikweli? Mfikirie Ana, mwanamke kijana anayeishi Brazili. Kama vile vijana wengi, Ana aliudhika kuona ufisadi na ukosefu wa haki. Kisha baba yake alianza kumpeleka yeye na dada zake kwenye mikutano ya Kikristo. Baada ya muda alianza kufurahia yale aliyojifunza katika Neno la Mungu. Ana alianza kusoma Biblia pamoja na vichapo vya Kikristo na kusali kwa Yehova Mungu. Hatua kwa hatua alikuza uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Anasema hivi: “Nilifurahia kuendesha baiskeli hadi mlima ulio karibu na nyumba yetu ambapo niliweza kutazama machweo ya jua yenye kuvutia. Nilisali kwa Yehova na kumshukuru kwa fadhili na ukarimu wake, nikijitahidi kumweleza kadiri nilivyompenda. Nilipata utulivu na amani ya akili kwa kumjua Yehova Mungu na makusudi yake.” Je, wewe pia unajitahidi kutafuta wakati wa kutafakari jinsi Yehova anavyokupenda na kukujali?

Ni kweli kwamba malezi yetu yanaweza kutuzuia tusiwe na uhusiano wa karibu na Yehova. Kwa mfano, mfikirie Lidia. Alipomweleza baba yake jambo fulani lililomhangaisha sana, baba yake alimjibu vikali na kusema: “Huo ni upuuzi.” Ijapokuwa alielewa kwamba baba yake alitaka asahau tatizo hilo, Lidia anasema: “Kujifunza Biblia kulinisaidia kupata yote niliyotamani na hata zaidi. Nilipenda sana sifa zenye kuvutia za Yehova, akawa rafiki yangu wa karibu zaidi. Sasa nina Baba anayenipenda na anayeelewa hali yangu, ambaye ninaweza kumweleza hisia zangu na mambo yanayonihangaisha sana moyoni. Ninaweza kutumia muda mrefu kuongea na Aliye mkuu ulimwenguni, nikiwa na hakika kwamba atanisikiliza.” Maandiko kama vile Wafilipi 4:6, 7 yalimsaidia kujua kwamba Yehova anampenda na kumjali. Andiko hilo linasema hivi: “Msihangaikie kitu chochote, bali katika kila jambo kwa sala na dua pamoja na utoaji-shukrani acheni maombi yenu ya bidii yajulishwe kwa Mungu; na amani ya Mungu izidiyo fikira yote kwa ubora italinda mioyo yenu na nguvu zenu za akili kwa njia ya Kristo Yesu.”

Msaada wa Kutimiza Mahitaji Yako

Yehova anamhangaikia mtumishi wake mmojammoja na pia kutaniko lake la ulimwenguni pote. Tunaweza kuonyesha kwamba tunampenda Baba yetu wa mbinguni kwa kutenga wakati kuongea naye. Hatupaswi kamwe kupuuza uhusiano wetu pamoja naye. Daudi alikumbuka sikuzote uhusiano wake pamoja na Yehova. Alisema hivi: “Ee BWANA, unijulishe njia zako, unifundishe mapito yako, uniongoze katika kweli yako, na kunifundisha. Maana Wewe ndiwe Mungu wa wokovu wangu, nakungoja Wewe mchana kutwa.”—Zaburi 25:4, 5.

Huenda hujawahi kusikia kwamba unaweza kuwa na uhusiano wa karibu pamoja na Mungu. Hata uwe na matatizo gani, unaweza kuwa na hakika kwamba Aliye Juu atakusaidia kupatana na mapenzi yake. (1 Yohana 5:14, 15) Kwa hiyo, jifunze kutoa sala hususa, ukifikiria hali yako na mahitaji yako.

Umuhimu wa kutambua mahitaji yetu unakaziwa katika sala ambayo Mfalme Sulemani alitoa wakati hekalu lilipozinduliwa: “Ikiwa nchi imeingia njaa, au tauni, au ukosefu wa mvua, au ukungu, au nzige, au panzi; ikiwa adui wamewahusuru katika nchi ya miji yao, au ukiwapo msiba wo wote au uele wo wote; yo yote atakayoyaomba na kusihi mtu awaye yote, au watu wako Israeli wote pamoja, watakaojua kila mtu pigo lake mwenyewe, na msiba wake mwenyewe, . . . Basi usikie huko mbinguni, . . . ukamsamehe, ukampatilize kila mtu kwa kadiri ya njia zake zote.” (2 Mambo ya Nyakati 6:28-30) Ni wewe tu unayejua ‘pigo lako mwenyewe, na msiba wako mwenyewe.’ Kwa hiyo, ni muhimu sana kutambua mahitaji yako na mambo unayotamani. Ukiyatambua, “[Yehova] atakupa haja za moyo wako.”—Zaburi 37:4.

Imarisha Uhusiano Wako Pamoja na Yehova

Yehova anafurahia kuwa na uhusiano wa karibu na watu wa kawaida. Neno Lake linatuhakikishia hivi: “‘Mimi nitakuwa baba kwenu, na nyinyi mtakuwa wana na mabinti kwangu,’ asema Yehova Mweza-Yote.” (2 Wakorintho 6:18) Kwa hakika, Yehova na Mwana wake wanataka tufanikiwe na tuishi milele. Inatia moyo sana kujua kwamba Yehova atatusaidia kutimiza madaraka yetu katika familia, kazini, na katika kutaniko la Kikristo.

Hata hivyo, sote tunakabili hali ngumu. Afya mbaya, matatizo ya familia, mapato ya chini, au mambo mengineyo yanaweza kutuhuzunisha. Huenda tusijue jinsi ya kushughulikia jaribu fulani. Magumu yanayozidi kuongezeka yanasababishwa, moja kwa moja au kwa njia isiyo ya moja kwa moja, na yule mshtaki mwovu, Shetani Ibilisi, ambaye anapiga vita ya kiroho dhidi ya watu wa Mungu. Hata hivyo, kuna mtu fulani anayetuelewa na kutusaidia kudumisha uhusiano wa karibu pamoja na Yehova. Yeye ni Yesu Kristo aliye na cheo cha juu mbinguni. Tunasoma hivi: “Tuna kuhani wa cheo cha juu, si mmoja asiyeweza kushiriki hisia za udhaifu wetu mbalimbali, bali mmoja ambaye amejaribiwa katika mambo yote kama sisi wenyewe, lakini asiye na dhambi. Kwa hiyo, acheni tukaribie kwa uhuru wa usemi kwenye kiti cha ufalme cha fadhili isiyostahiliwa, ili tuweze kupokea rehema na kupata fadhili isiyostahiliwa kwa msaada katika wakati ufaao.”—Waebrania 4:15, 16.

Tunatiwa moyo kujua kwamba si lazima tuwe watu mashuhuri au matajiri ili tupate kibali cha Mungu. Hata ukikabili hali ngumu, uwe kama mtunga-zaburi aliyesali hivi: “Nami ni maskini na mhitaji, Bwana atanitunza. Ndiwe msaada wangu na mwokozi wangu.” (Zaburi 31:9-14; 40:17) Uwe na hakika kwamba Yehova anawapenda watu wa kawaida. Kwa hakika ‘tunaweza kutupa hangaiko letu lote juu yake kwa sababu yeye hutujali.’—1 Petro 5:7.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 10 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

[Picha katika ukurasa wa 29]

Wafuasi wengi wa Yesu walikuwa watu wasio na elimu na wa kawaida

[Picha katika ukurasa wa 30]

Wakristo hujitahidi kuwa na imani yenye nguvu

[Picha katika ukurasa wa 31]

Si lazima tuwe watu mashuhuri ili tupate kibali cha Mungu