Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kazi ya Kuhubiri Yenye Kufurahisha Sana

Kazi ya Kuhubiri Yenye Kufurahisha Sana

Kazi ya Kuhubiri Yenye Kufurahisha Sana

“Jua linawaka sana. Inaonekana hatutafika mwisho wa safari yetu tunapopitia kijia cha mlimani. Baada ya kupita vizuizi vingi, hatimaye tunafika kwenye kijiji cha mbali zaidi tulichokuwa tunaelekea. Uchovu wetu unakwisha na tunafurahi tunapobisha mlango wa kwanza na kukaribishwa vizuri. Jioni inapofika, tayari tumewaachia watu vitabu vyote tulivyokuwa navyo na kuanzisha mafunzo kadhaa ya Biblia. Watu wanatamani kujifunza. Sasa inatubidi kuondoka lakini tunaahidi tutarudi.”

MAMBO kama hayo yaliyoonwa ni ya kawaida miongoni mwa kikundi kimoja cha mapainia nchini Mexico. Wameazimia kushiriki kwa bidii kutimiza kazi ambayo Yesu Kristo aliwapa wanafunzi wake: “Mtakuwa mashahidi wangu . . . hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.” (Matendo 1:8) Kampeni za pekee zinazofanywa na mapainia hupangwa nchini Mexico ili kuhubiri maeneo yasiyohubiriwa na makutaniko na ambayo hayafikiwi na habari njema za Ufalme wa Mungu kwa ukawaida. Kwa kawaida, maeneo hayo ni ya mbali na hayafikiki kwa urahisi. Pia mapainia husaidia makutaniko ya mbali yaliyo na maeneo makubwa.

Ili kuamua ni sehemu gani ya nchi itakayohubiriwa na mapainia hao, ofisi ya tawi ya Mashahidi wa Yehova huchunguza mahitaji ya eneo. * Baada ya kuchunguza mahitaji hayo, vikundi vya mapainia wa pekee hutumwa kuhubiri maeneo hayo. Wanapewa magari yanayofaa barabara mbaya zisizo na lami. Magari hayo hutumiwa pia kama mahali pa kuweka vitabu na pa kulala inapohitajiwa.

Kuna Itikio Zuri

Tangu Oktoba mwaka wa 1996, wahubiri wengine wa habari njema wameombwa kushiriki katika kazi hiyo pamoja na mapainia wa pekee. Wahubiri wa Ufalme na vilevile mapainia wa kawaida wanaotaka kutumikia mahali palipo na uhitaji mkubwa hujiunga na mapainia wa pekee katika sehemu mbalimbali. Wengine wao hutumwa katika makutaniko yaliyo katika maeneo hayo ya pekee ili kuhubiri na kuwasaidia wanaopendezwa. Wahubiri na mapainia wengi wachanga wamekubali mwaliko huo, nao wamejionea mambo mengi yenye kutia moyo.

Kwa mfano, Abimael, kijana Mkristo aliyekuwa na kazi yenye mshahara mkubwa katika kampuni ya simu za mkononi, aliamua kushiriki katika kazi ya kuhubiri maeneo hayo ya mbali. Waajiri wake walipojua kwamba alitaka kuacha kazi, waliahidi kumpandisha cheo na kumwongezea mshahara. Wafanyakazi wenzake walisisitiza kwamba hiyo ilikuwa nafasi ya pekee na ingekuwa upumbavu kuikataa. Hata hivyo, Abimael alikuwa ameazimia kuunga mkono kazi hiyo ya pekee ya kuhubiri kwa miezi mitatu. Baada ya kufurahia utumishi huo, Abimael ameamua kuendelea kutumikia katika kutaniko la mbali ambapo wahubiri wa Ufalme wanahitajiwa sana. Sasa ana kazi ya mshahara mdogo na amejifunza kufanya maisha yake kuwa sahili.

Ilimbidi Julissa kusafiri kwa basi kwa muda wa saa 22 ili kufika kwenye eneo lake. Kwenye mkondo wa mwisho wa safari yake aliachwa na basi la mwisho. Hata hivyo, kulikuwa na gari la mizigo lililowasafirisha wafanyakazi. Julissa alijipa moyo na kuwaomba wambebe. Yaelekea alikuwa na woga kwa kuwa kati ya wanaume hao wengi, hakukuwa na mwanamke mwingine ila yeye. Alipoanza kumhubiria mwanamume mmoja kijana, alitambua kwamba mwanamume huyo alikuwa Shahidi wa Yehova! Julissa anasema, “mbali na hilo, dereva wa gari hilo alikuwa mzee wa kutaniko nililokuwa nimetumwa!”

Wazee Wanashiriki

Hata hivyo, kazi hii si ya vijana peke yao. Dada mzee, Adela, alikuwa akitamani sana kutumia muda mwingi zaidi katika kazi ya kuhubiri. Alipata nafasi ya kuongeza utumishi wake alipoalikwa kushiriki katika kazi hii ya pekee ya kuhubiri. Anasema hivi: “Nilifurahia sana utumishi wangu hivi kwamba niliwaomba wazee wa kutaniko waniruhusu niendelee kutumikia huko. Ninafurahi kwa sababu ingawa nimezeeka, bado ninaweza kumtumikia Yehova.”

Vivyo hivyo, Martha mwenye umri wa miaka 60, alichochewa na uthamini kwa Yehova na upendo kwa wanadamu kushiriki katika kazi hiyo. Alipoona kwamba mapainia hawangeweza kuwafikia watu wanaoishi mbali kwenye maeneo ya milima-milima, aliwanunulia gari la kutumia. Gari hilo liliwawezesha kuhubiri eneo kubwa zaidi na kuwaeleza watu wengi zaidi kweli ya Biblia.

Itikio Linalosisimua

Lengo la wale wanaoshiriki katika kazi hii ya pekee ya kuhubiri ni “kufanya wanafunzi.” Wamepata matokeo mazuri sana kuhusiana na kazi hiyo. Watu wanaoishi mbali wamepokea kweli ya Biblia inayookoa uhai. (Mathayo 28:19, 20) Mafunzo mengi ya Biblia yameanzishwa. Mafunzo hayo yanaongozwa na wahubiri wanaoishi katika eneo hilo au wale waliobaki huko. Katika sehemu fulani, wahubiri wamepangwa katika vikundi, na kwingineko hata makutaniko madogo yameanzishwa.

Magdaleno na wenzake walitumia usafiri wa umma ili kufika kwenye eneo la mbali walikotumwa. Wakiwa njiani, waliamua kumhubiria dereva. “Mtu huyo alituambia kwamba juma moja kabla ya hapo, Mashahidi fulani walitembelea familia yake alipokuwa safarini. Aliporudi watu wa familia yake walimweleza mambo waliyoambiwa. Tulimwambia kwamba hatuishi katika ujirani huo, bali tulitoka katika majimbo mbalimbali nchini ili kushiriki katika kazi hii ya pekee ya kuhubiri na kwamba sote tuligharimia safari yetu. Dereva huyo alipendezwa na kusema kwamba yeye pamoja na familia yake wangeanza kujifunza Biblia juma hilo. Hata alichangia kazi hiyo kwa kutotutoza nauli.”

Magdaleno pia alivutiwa sana na itikio la wenyeji wa milima ya Chiapas. “Mimi na mke wangu tulifurahia kuwaeleza vijana 26 wa Kanisa la Presbiteri ujumbe wa Ufalme. Wote walisikiliza kwa makini kwa dakika 30. Walitoa Biblia zao, nasi tukawatolea ushahidi kamili kuhusu makusudi ya Yehova. Wakazi wengi wa eneo hilo wana Biblia katika lugha yao ya Tzeltal.” Wengi walioanza kujifunza Biblia wanafanya maendeleo.

Upinzani Ulipungua

Kwa sababu ya upinzani kutoka kwa watu fulani, watu wa kijiji kimoja cha Chiapas hawakuwa wamesikia ujumbe wa Biblia kwa muda unaozidi miaka miwili. Mtumishi wa wakati wote anayeitwa Teresa, alitambua kwamba Mashahidi wengine waliogopa kuhubiri katika kijiji hicho. “Wote walishangaa kuona kwamba wanakijiji hao walitaka kusikia. Baada ya kumaliza kuhubiri, mvua kubwa ilianza kunyesha. Tulipokuwa tukitafuta mahali pa kujikinga na mvua, tulifika nyumbani kwa mtu mkarimu anayeitwa Sebastián, ambaye alitukaribisha ili tujikinge. Tulipokuwa ndani nilimwuliza kama ametembelewa tayari. Aliposema la, nilianza kumtolea ushahidi na kuanzisha funzo la Biblia kwa kutumia kitabu Ujuzi Uongozao Kwenye Uhai Udumuo Milele. * Tulipomaliza, Sebastián alitusihi huku akitokwa na machozi turudi na kuendelea kujifunza naye.”

Kikundi kingine cha mapainia waliotembelea jimbo la Chiapas wanasema hivi: “Kwa msaada wa Yehova tulipata matokeo mazuri. Katika juma la kwanza tulianzisha mafunzo 27, na katika juma la pili tuliwaalika watu watazame video The Bible—Its Power in Your Life. Watu 60 walihudhuria. Wote waliifurahia sana. Mwishowe, tulipendekeza kikundi kianzishwe kwa ajili ya kujifunza Biblia. Jambo la kushangaza ni kwamba vikundi viwili vilianzishwa katika kijiji hicho.

“Baada ya kumaliza kuhubiri kwenye maeneo tuliyogawiwa, tulirudi kutembelea na kuwatia moyo waliopendezwa, na kuona jinsi watu hao waliopangwa kuwa vikundi vya kujifunza Biblia walivyokuwa wakiendelea. Tuliwakaribisha kwenye mkutano wa watu wote na Funzo la Mnara wa Mlinzi. Hata hivyo, hakukuwa na mahali pa kutosha kufanyia mikutano. Mtu aliyeturuhusu kutumia nyumba yake kwa ajili ya funzo alituonyesha ua wa nyumba yake na kusema: ‘Mikutano inaweza kufanywa kwenye ua huu.’”

Mwisho wa juma hilo mapainia waliokuwa wakitembelea eneo hilo pamoja na watu waliopendezwa walisaidia kutayarisha ua huo kwa ajili ya mikutano. Watu 103 walihudhuria mkutano huo wa kwanza. Sasa mafunzo ya Biblia 40 yanaongozwa katika kijiji hicho.

‘Kazi Iliyofurahisha Sana’

Mbali na kupata matokeo mazuri katika kazi ya kuhubiri, walioshiriki katika kazi hiyo walinufaika sana. Painia mchanga anayeitwa María aliyeshiriki katika kazi hiyo, anasema hivi: “Nilifurahia sana kazi hiyo kwa sababu mbili. Furaha yangu katika kazi ya kuhubiri iliongezeka, nikawa na uhusiano wa karibu zaidi pamoja na Yehova. Wakati mmoja tulipokuwa tukipanda mlima tulichoka sana. Baada ya kumwomba Yehova msaada, tuliona ukweli wa andiko la Isaya 40:29-31 linalosema: ‘Wale wanaomngojea BWANA watapata nguvu mpya.’ Kwa hiyo tulifika na kuongoza mafunzo pamoja na watu waliotukaribisha vizuri.”

Painia mwingine machanga mwenye umri wa miaka 17 anayeitwa Claudia, anasema hivi: “Nimenufaika sana. Nimepata shangwe ya kuwa mhubiri stadi zaidi, na hiyo imenitia moyo kuweka miradi ya kiroho. Pia nimekomaa kiroho. Nilipokuwa nyumbani mama yangu alinifanyia kila kitu. Sasa, kwa sababu nimejifunza mambo mengi, ninachukua mambo kwa uzito zaidi. Kwa mfano, sikupenda vyakula vingi. Lakini sasa, kwa sababu imenibidi kuzoea hali tofauti-tofauti silalamiki tena kuhusu chakula. Utumishi huo umenisaidia kuwa na marafiki wazuri. Tunatumia vitu tulivyo navyo pamoja na tunasaidiana.”

Kuvuna kwa Shangwe

Kazi hiyo ya pekee imekuwa na matokeo gani? Mapema mwaka wa 2002, mapainia 28,300 walikuwa wameshiriki katika kazi hiyo ya pekee. Walikuwa wameongoza mafunzo ya Biblia 140,000, na kutumia saa zaidi ya milioni mbili katika kazi ya kuhubiri. Ili kuwasaidia watu kujifunza kweli ya Biblia, waliwaachia vitabu 121,000 hivi na magazeti yapatayo 730,000. Ni jambo la kawaida kwa mapainia fulani kuongoza mafunzo ya Biblia 20 au zaidi.

Watu walionufaika na matendo hayo ya upendo wanashukuru sana kwa jitihada ya pekee iliyofanywa ili wafikiwe na ujumbe wa Biblia. Wajapokuwa maskini, wengi husisitiza kwamba wahubiri wakubali michango yao. Mwanamke mmoja mwenye umri wa miaka 70 huwapa mapainia mchango fulani kila wanapomtembelea. Yeye hulia wanapokataa mchango wake. Watu wa familia moja maskini huwaambia wahubiri wa wakati wote wanaowatembelea kwamba kuku alitaga mayai kwa ajili yao hasa na kuwasihi wayachukue.

Jambo muhimu zaidi ni kwamba watu hao wenye moyo mweupe wanathamini kikweli mambo ya kiroho. Kwa mfano, mwanamke fulani kijana hutembea kwa muda wa saa tatu na nusu ili kuhudhuria mikutano ya Kikristo bila kukosa hata mmoja. Ijapokuwa ana tatizo la magoti, mwanamke mmoja mzee anayependezwa, alisafiri kwa muda wa saa mbili ili ajifunze Biblia wakati wa ziara ya mwangalizi wa mzunguko. Watu fulani wasiojua kusoma walitaka kujifunza kusoma na kuandika ili wanufaike zaidi na elimu ya Biblia. Wamebarikiwa sana kwa jitihada zao.

Katika kitabu cha Matendo, Luka anaeleza maono ambayo mtume Paulo aliona: “Mwanamume fulani Mmakedonia alikuwa amesimama akimsihi sana na kusema: ‘Vuka uingie Makedonia utusaidie.’” Paulo alikubali mwaliko huo. Leo, katika maeneo ya mbali nchini Mexico, wengi wameitikia wakionyesha roho kama hiyo, na kujitoa kutangaza habari njema “hadi sehemu ya mbali zaidi sana ya dunia.”—Matendo 1:8; 16:9, 10.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 4 Hivi karibuni, zaidi ya asilimia 8 ya eneo la Mexico halikuwa likihubiriwa kwa ukawaida na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova. Hiyo inamaanisha kwamba kuna watu zaidi ya 8,200,000 wanaoishi katika maeneo ya mbali yasiyohubiriwa kwa ukawaida.

^ fu. 17 Kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Picha katika ukurasa wa 9]

Mashahidi wengi nchini Mexico wameshiriki katika kampeni ya pekee ya kuhubiri