Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Epuka Eneo la Hatari!

Epuka Eneo la Hatari!

Epuka Eneo la Hatari!

NI WAJIBU wa wataalamu wa mambo ya volkano kuchunguza na kuchanganua ishara kisha kuonya watu juu ya milipuko ya volkano inayokaribia. (Mlima Fugen ulipolipuka, polisi walilazimika kuzuia watu wasiingie kwenye eneo la hatari.) Hali kadhalika, wanafunzi wa Biblia huchunguza ishara ya “umalizio wa mfumo wa mambo” na kutahadharisha wengine juu ya hatari inayokaribia.—Mathayo 24:3.

Katika sura hiyohiyo ya Biblia ambayo huonya juu ya msiba mkubwa wa ulimwenguni pote unaokaribia, tunaweza kusoma ufafanuzi huu kuhusu matukio ya mwanzo-mwanzo: “Taifa litainuka dhidi ya taifa na ufalme dhidi ya ufalme, na kutakuwa na upungufu wa chakula na matetemeko ya dunia mahali pamoja baada ya pengine. . . . Manabii wengi wasio wa kweli watainuka na kuongoza wengi vibaya; na kwa sababu ya kuongezeka kwa uasi-sheria upendo wa idadi iliyo kubwa zaidi utapoa. . . . Na habari njema hii ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa kwa ajili ya kuwa ushahidi kwa mataifa yote; na ndipo mwisho utakapokuja.”—Mathayo 24:7-14.

Si lazima tuwe wataalamu wa habari ili kufahamu jinsi unabii huo unavyotimizwa wakati huu. Tumeona ukitimia hasa tangu mwaka wa 1914. Karne hii imekuwa na vita viwili vya ulimwengu, vita vingi sana vya wenyewe kwa wenyewe, vita vidogo-vidogo, na mapambano ya kijamii na ya kidini. Mbali na ufukara unaosababishwa na misiba ya asili, mwanadamu pia amepungukiwa na chakula kwa sababu ya vita hivyo. Matetemeko ya dunia yamesababisha vifo vya watu wengi. Madhehebu zenye viongozi wenye kutilika shaka na wafuasi washupavu zimechipuka. “Kuongezeka kwa uasi-sheria” kumefanya watu wasionyeshe upendo, na ujirani mwema si jambo la kawaida tena.

Hapana shaka kwamba kazi ya kuhubiri ya ulimwenguni pote, ambayo ni sehemu nyingine ya ishara hiyo, inatimizwa. Ebu tazama jalada la gazeti hili, na utaona maneno “Unaotangaza Ufalme wa Yehova” yakiwa sehemu ya kichwa. Mnara wa Mlinzi linalochapishwa katika lugha 132 na kugawanywa katika nakala zaidi ya milioni 22, ni kifaa muhimu kwa wale wanaotangaza “habari njema hii ya ufalme” katika dunia yote inayokaliwa na watu. Habari njema hiyo yatia ndani ujumbe kwamba Muumba wa ulimwengu, Yehova Mungu, amesimamisha Ufalme wa mbinguni ambao utaharibu mfumo huu mwovu wa mambo na kuleta paradiso duniani. Kwa kweli, ishara kwamba karibuni Mungu atachukua hatua inaonekana sasa, ikionyesha kwamba uhai wa watu katika mfumo huu wa mambo umo hatarini.—Linganisha 2 Timotheo 3:1-5; 2 Petro 3:3, 4; Ufunuo 6:1-8.

Siku ya Yehova Yenye Kutia Hofu

Ni nini kitakachotukia wakati ufikapo wa Yehova wa kutekeleza hukumu? Sikiliza jinsi yeye mwenyewe afafanuavyo kinaganaga yale yatakayotokea: “Nami nitaonyesha mambo ya ajabu katika mbingu na katika dunia, damu, na moto, na minara ya moshi. Jua litageuzwa kuwa giza, na mwezi kuwa damu, kabla haijaja hiyo siku ya BWANA iliyo kuu na itishayo.”—Yoeli 2:30, 31.

Siku hiyo, yenye kutia hofu zaidi na yenye kuleta uharibifu mkubwa kuliko mlipuko wowote wa volkano au tetemeko la dunia, imekaribia. Nabii Sefania asema: “Hiyo siku ya BWANA iliyo kuu i karibu; i karibu, nayo inafanya haraka sana. . . . Nchi yote pia itateketezwa kwa moto wa wivu wake; maana atawakomesha watu wote wakaao katika nchi hii, naam, ukomo wa kutisha.” Ingawa “fedha yao wala dhahabu yao havitaweza kuwaokoa katika siku ile ya ghadhabu ya BWANA,” kuna njia ya kuokoka siku hiyo yenye kutia hofu.—Sefania 1:14-18.

Akionyesha jinsi ya kuokoka, Sefania asema: “Kabla haijawajilia hasira kali ya BWANA, kabla haijawajilia siku ya hasira ya BWANA. Mtafuteni BWANA, enyi nyote mlio wanyenyekevu wa dunia . . . itafuteni haki, utafuteni unyenyekevu; huenda mtafichwa katika siku ya hasira ya BWANA.” (Sefania 2:2, 3) Tunaweza kupata kimbilio kwa ‘kumtafuta Yehova, kuitafuta haki, na kuutafuta unyenyekevu.’ Ni nani wanaomtafuta Yehova leo?

Yaelekea wewe huhusianisha neno “Yehova” na Mashahidi wa Yehova kwa sababu ya kazi yao ya kuhubiri. Huenda ukawa ulipata gazeti hili kutoka kwa mmoja wao. Wao wanajulikana kuwa raia wenye maadili wanaoishi maisha manyofu. Wanajitahidi kuvaa “utu mpya,” unaotia ndani kusitawisha unyenyekevu. (Wakolosai 3:8-10) Wao hukiri kwamba wanafanya hivyo kwa sababu wanafundishwa na tengenezo la Yehova lenye kuonekana, ambalo linawakilishwa duniani pote na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova ya kwao. Naam, unaweza kupata kimbilio pamoja na “ushirika mzima wa ndugu” miongoni mwa Mashahidi wa Yehova ulimwenguni pote.—1 Petro 5:9.

Pata Kimbilio Sasa

Ili kupata kimbilio kwa kumtafuta Yehova, ni lazima tuwe rafiki zake. Jambo hilo lahusisha nini? Biblia yajibu: “Je, hamjui kwamba urafiki na ulimwengu ni uadui na Mungu? Kwa hiyo, yeyote yule atakaye kuwa rafiki ya ulimwengu anajifanya mwenyewe kuwa adui ya Mungu.” (Yakobo 4:4) Ili tuwe rafiki za Mungu, ni lazima tuepuke kabisa kujihusisha kihisia-moyo na ulimwengu mwovu wa sasa ambao una mtazamo wa kuasi Mungu.

Biblia yatuonya kwa upole hivi: “Msiwe mkipenda ama ulimwengu ama vitu vilivyo katika ulimwengu. Ikiwa yeyote aupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo katika yeye; kwa sababu kila kitu kilicho katika ulimwengu—tamaa ya mwili na tamaa ya macho na wonyesho wa mtu wa kujivunia njia yake ya kutegemeza maisha—hakitokani na Baba, bali hutokana na ulimwengu. Zaidi ya hilo, ulimwengu unapitilia mbali na ndivyo na tamaa yao, lakini yeye ambaye hufanya mapenzi ya Mungu hudumu milele.” (1 Yohana 2:15-17) Watu wengi leo huchochewa na tamaa za kimwili—tamaa ya ngono isiyodhibitiwa, kufuatia fedha kwa pupa, na kutumia mamlaka vibaya. Lakini ni lazima mtu ashinde tamaa hizo ili awe upande wa Yehova.—Wakolosai 3:5-8.

Huenda ukawa umesoma jarida hili mara kwa mara, na huenda ukakubaliana na jinsi linavyoonyesha utimizo wa unabii wa Biblia. Lakini huenda ukasita kuchukua hatua zaidi ya kushirikiana na Mashahidi wa Yehova. Hata hivyo, tukabilipo msiba, je, inatosha tu kusikia onyo? Kama ilivyokuwa na mlipuko wa Mlima Fugen, tunahitaji kuchukua hatua kuhusiana na onyo hilo. Kumbuka kwamba waandishi wa habari na wapiga-picha angalau 15 waliotaka kupata habari motomoto walikufa. Kwa kweli, mpiga-picha mmoja alikufa kidole chake kikiwa kwenye kidude cha kupigia picha. Mtaalamu mmoja wa mambo ya volkano—ambaye alikuwa amesema, “Ikiwa siku moja nitakufa, nataka nife karibu na volkano”—alikufa tu kama alivyotaka. Wote walikuwa wamejitoa kwa kazi yao na shughuli zao. Lakini walikufa—matokeo ya kupuuza onyo.

Wengi leo husikia ujumbe juu ya uamuzi wa Mungu wa kuharibu mfumo huu mwovu wa mambo na kwa kadiri fulani wanafahamu ukweli wa onyo hilo. ‘Huenda uharibifu huo ukaja hatimaye,’ huenda wakasababu, ‘lakini si leo.’ Kwa manufaa yao, wao huiahirisha siku ya Yehova ili wasikengeushwe waache yale wanayoona kuwa muhimu zaidi wakati huu.

Baruku alikuwa na tatizo kama hilo. Akiwa mwandishi wa nabii wa kale Yeremia, Baruku aliwaonya Waisraeli kwa ujasiri juu ya uharibifu wa Yerusalemu uliokuwa unakaribia. Lakini wakati mmoja, yeye alichoka na utume wake. Hivyo, Yehova akamsahihisha: “Je! unajitafutia mambo makuu? usiyatafute.” Hata iwe ni mali, umashuhuri, au usalama unaotokana na vitu vya kimwili, Baruku hakupaswa ‘kujitafutia mambo makuu.’ Alipaswa kupendezwa na jambo moja, kufanya mapenzi ya Mungu ili kusaidia watu wawe upande Wake. Matokeo yangekuwa kwamba angepokea ‘roho yake ikiwa nyara.’ (Yeremia 45:1-5) Hali kadhalika, badala ya ‘kujitafutia mambo makuu,’ tunapaswa kumtafuta Yehova, jambo linaloweza kuokoa uhai wetu.

Kwenye Mlima Fugen, zaidi ya polisi 12 na zimamoto wa kujitolea walikuwa kazini wakati mtiririko moto sana wa volkano ulipowaua. Walikuwa wakijaribu kuwasaidia na kuwalinda watu waliokuwa hatarini. Walikuwa kama wanaume na wanawake wenye nia njema wanaojihusisha sana na kuboresha mambo katika ulimwengu huu. Ingawa huenda wakawa na nia nzuri, “yaliyopotoka hayawezi kunyoshwa.” (Mhubiri 1:15) Mfumo wa mambo ambao umepotoka hauwezi kunyoshwa. Je, ni jambo linalopatana na akili kuwa “rafiki wa ulimwengu” kwa kujaribu kuokoa mfumo wa ulimwenguni pote ambao Mungu ameazimia kuuondoa?

Baada ya Kukimbia, Usirudi

Kuna tofauti kati ya kukimbia mfumo huu ulio hatarini, na kubaki katika utunzaji na ulinzi wa “ushirika mzima wa ndugu.” (1 Petro 2:17) Na tusisahau wakulima ambao, baada ya kuhamishwa, walirudi kutazama mashamba yao karibu na Mlima Fugen. Yaelekea walikuwa wakitamani sana kurudia maisha ya “kawaida” waliyokuwa wakiishi. Lakini unatambua kwamba uamuzi wao wa kurudi haukuwa wa hekima. Yamkini hilo halikuwa ndilo jaribio lao la kwanza kuingia katika eneo la hatari. Huenda waliingia katika eneo hilo la hatari kwa muda mfupi tu bila chochote kutukia. Huenda wakati ule mwingine walikaa kwa muda mrefu kidogo, na bado hakuna chochote kilichotukia. Yaelekea sasa walizoea kuvuka mpaka wa usalama na kupata ujasiri wa kukaa kwa muda mrefu katika eneo la hatari.

Yesu Kristo alitaja hali kama hiyo ambayo ingetukia wakati wa “umalizio wa mfumo wa mambo.” Yeye alisema: “Kama walivyokuwa katika siku hizo kabla ya furiko, wakila na kunywa, wanaume wakioa na wanawake wakiozwa, hadi siku ambayo Noa aliingia ndani ya safina; nao hawakujali mpaka furiko likaja na kuwafagilia mbali wote, ndivyo kuwapo kwa Mwana wa binadamu kutakavyokuwa.”—Mathayo 24:3, 38, 39.

Ona kwamba Yesu alitaja kula, kunywa na kuoana. Mambo hayo yenyewe si mabaya machoni pa Yehova. Basi, ni nini kilichokuwa kibaya? Watu wa wakati wa Noa “hawakujali,” wakiishi maisha yaliyohusisha tu shughuli zao za kawaida. Mtu hawezi kuishi maisha ya “kawaida” wakati wa hatari. Baada ya kukimbia ulimwengu huu ambao umehukumiwa uharibifu, au kujitenga nao, unapaswa kupambana na msukumo wowote wa kutaka kurudi ili kujinufaisha na chochote kile ambacho chaweza kupatikana humo. (1 Wakorintho 7:31) Huenda ukaweza kuacha eneo salama kiroho na kurudi bila madhara, bila hata yeyote kujua. Lakini yaelekea jambo hilo litakupa ujasiri na kukufanya urudi katika ulimwengu tena na kukaa huko kwa muda mrefu hata zaidi. Muda si muda ungeweza kusitawisha mtazamo huu: “Mwisho hautakuja leo.”

Pia, fikiria wale madereva watatu wa teksi ambao walikufa wakingojea waandishi wa habari na wapiga-picha wakati mtiririko wa volkano ulipotiririka kwa kasi chini ya mlima. Leo wengine wanaweza kuandamana na watu ambao wamejasiria kurudi katika ulimwengu. Hata sababu iwe nini, ni wazi kwamba haifai kujihatarisha kwa kushawishwa urudi katika eneo la hatari.

Wote waliokufa kutokana na mlipuko wa Mlima Fugen walivuka mpaka wa usalama na kuingia katika eneo la hatari. Ingawa walitarajia kwamba mlima huo ungelipuka siku moja, hakuna hata mmoja aliyefikiri ungelipuka siku hiyo. Kwa kuchunguza ishara ya umalizio wa mfumo wa mambo, wengi wanatarajia siku ya Yehova ije wakati fulani lakini yaelekea hawaitarajii ije karibuni. Wengine hata wanaona kwamba siku hiyo haiwezi kuwa “leo.” Mtazamo kama huo ni hatari kwelikweli.

“Siku ya Yehova itakuja kama mwizi,” mtume Petro akaonya. Tunahitaji kuwa macho, ‘tukingojea na kuweka karibu akilini kuwapo kwa siku ya Yehova,’ tukifanya ‘kabisa yote tuwezayo ili mwishowe tupatikane naye tukiwa bila doa na bila waa na katika amani.’ (2 Petro 3:10-14) Baada ya kuharibiwa kwa mfumo wa mambo wa sasa ulio mwovu, kutakuwa na dunia paradiso chini ya Ufalme wa Mungu. Na tusishawishwe kamwe kuthubutu kuingia katika eneo la hatari kwa kisingizio chochote kile, kwa kuwa siku ile tuvukapo mpaka kurudi katika ulimwengu kumbe ndiyo inayoweza kuwa siku ya Yehova.

Pata kimbilio pamoja na watu wa Yehova na ukae pamoja nao.

[Picha katika ukurasa wa 7]

Pata kimbilio pamoja na watu wa Yehova na ukae pamoja nao

[Picha katika ukurasa wa 4]

Iwasa/Sipa Press