Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Onyesha Imani—Amua kwa Hekima!

Onyesha Imani—Amua kwa Hekima!

“[Endelea] kuomba kwa imani, bila kutia shaka hata kidogo.”—YAK. 1:6.

NYIMBO: 81, 70

1. Ni nini kilichoathiri uwezo wa Kaini wa kufanya uamuzi wa hekima, na matokeo yalikuwa nini?

KAINI alihitaji kufanya uamuzi: Kushinda hisia zake zilizomwelekeza kwenye dhambi, au kuruhusu hisia hizo ziongoze matendo yake. Vyovyote vile, angepatwa na matokeo ambayo yangeathiri maisha yake yote. Kama ujuavyo, Kaini alifanya uamuzi mbaya. Uamuzi aliofanya ulimwongoza kumwua ndugu yake mwaminifu Abeli. Na uamuzi wake uliathiri uhusiano wake na Muumba wake.—Mwa. 4:3-16.

2. Uwezo wetu wa kufanya maamuzi kwa hekima ni muhimu kadiri gani?

2 Sisi pia tunahitaji kufanya maamuzi. Si kila uamuzi tunaofanya unaohusisha kifo. Hata hivyo, maamuzi mengi tunayofanya yanaweza kuathiri sana maisha yetu. Hivyo, uwezo wa kufanya maamuzi mazuri unaweza kutusaidia kuishi kwa utulivu bila matatizo mengi, badala ya kuwa na maisha yenye vurugu, migogoro, na yenye kukatisha tamaa.—Met. 14:8.

3. (a) Ili kufanya maamuzi kwa hekima, tunapaswa kuwa na imani katika nini? (b) Tutachunguza maswali gani?

3 Ni nini kitakachotusaidia kufanya maamuzi kwa hekima? Kwa hakika, tunahitaji kumwamini Mungu bila kutilia shaka utayari na uwezo wake wa kutusaidia kuwa na hekima. Pia, tunahitaji kuwa na imani katika Neno la Yehova na njia yake ya kufanya mambo, huku tukitegemea shauri lake lililoongozwa na roho. (Soma Yakobo 1:5-8.) Kadiri tunavyozidi kumkaribia na kulipenda Neno lake, ndivyo tunavyozidi kuamini kwamba maamuzi yake ndiyo bora. Kwa sababu hiyo, tunasitawisha mazoea ya kuchunguza Neno la Mungu kabla ya kufanya maamuzi. Lakini tunaweza kuboreshaje uwezo wetu wa kufanya maamuzi? Na je, kuwa tayari kufanya maamuzi kunamaanisha kushikilia maamuzi yetu hata hali iweje?

MAISHA YANAHUSISHA KUFANYA MAAMUZI

4. Adamu alihitaji kufanya uamuzi gani, na matokeo yalikuwa nini?

4 Tangu kuumbwa kwa wanadamu, wanaume na wanawake wamehitaji kufanya maamuzi muhimu. Adamu alihitaji kuchagua kumsikiliza Muumba wake au Hawa. Alikuwa tayari kufanya uamuzi, lakini unaonaje uamuzi aliofanya? Mke wake aliyepotoshwa alimshawishi kufanya uamuzi mbaya sana, uamuzi ambao ulifanya afukuzwe kutoka Paradiso na baadaye ukamgharimu uhai wake mwenyewe. Na huo ulikuwa mwanzo tu wa matokeo ya maamuzi yake. Bado tunateseka kwa sababu ya matokeo mabaya ya uamuzi wa Adamu.

5. Tunapaswa kuwa na maoni gani kuhusu kufanya maamuzi?

5 Wengine wanaweza kufikiri kwamba maisha yangekuwa mazuri zaidi ikiwa hatungehitaji kufanya maamuzi. Je, unahisi hivyo? Kumbuka, Yehova hakuwaumba wanadamu wakiwa kama mashine isiyoweza kufikiri au kufanya maamuzi. Kwa kweli, Biblia inatufundisha jinsi ya kufanya maamuzi ya hekima. Ingawa Yehova anataka tufanye maamuzi, hakukusudia tuumie kwa kutumia uwezo huo. Acheni tuchunguze baadhi ya mambo yanayothibitisha jambo hilo.

6, 7. Waisraeli wa kale walihitaji kufanya uamuzi gani, na kwa nini ilikuwa vigumu kwao kufanya uamuzi wa hekima? (Tazama picha mwanzoni mwa makala hii.)

6 Baada ya kuirithi Nchi ya Ahadi, Waisraeli wa kale walihitaji kufanya uamuzi fulani wa msingi na muhimu sana: Uamuzi wa kumwabudu Yehova au kutumikia mungu au miungu mingine. (Soma Yoshua 24:15.) Huenda uamuzi huo ungeonekana kuwa rahisi. Hata hivyo, uamuzi wao ungehusisha uhai au kifo. Katika siku za Waamuzi, Waisraeli walifanya maamuzi yasiyo ya hekima tena na tena. Walimwacha Yehova na kuabudu miungu ya uwongo. (Amu. 2:3, 11-23) Au fikiria tukio fulani lililotukia baadaye kwenye historia, watu wa Mungu walipolazimika kufanya uamuzi. Nabii Eliya aliwaeleza wazi uamuzi waliohitaji kufanya: Kumtumikia Yehova au kutumikia mungu wa uwongo, Baali. (1 Fal. 18:21) Eliya aliwakemea watu hao kwa kutokuwa na msimamo. Huenda ukafikiri kwamba ilikuwa rahisi kufanya uamuzi huo kwa kuwa sikuzote ni jambo la hekima na lenye faida kumtumikia Yehova. Kwa kweli, mtu mwenye uwezo mzuri wa kufikiri hawezi kuvutiwa au kuwa na uhusiano na Baali. Lakini bado Waisraeli hao walikuwa “[wakiyumba-yumba] juu ya maoni mawili tofauti.” Kwa hekima, Eliya aliwahimiza wachague namna ya ibada iliyo bora, yaani, ibada ya Yehova.

7 Kwa nini huenda ingekuwa vigumu sana kwa Waisraeli kufanya uamuzi wa hekima? Kwanza, walikuwa wamepoteza imani kumwelekea Yehova na kukataa kuisikiliza sauti yake. Hawakuwa wamejijengea msingi wa ujuzi sahihi au hekima kutoka kwa Mungu; wala hawakumtegemea Yehova. Ikiwa wangetenda kupatana na ujuzi sahihi, wangefanya maamuzi ya hekima. (Zab. 25:12) Isitoshe, walikuwa wamewaruhusu wengine wawaathiri au hata kuwafanyia maamuzi. Watu katika nchi hiyo ambao hawakuwa waabudu wa Yehova, waliathiri kufikiri kwa Waisraeli na kuwafanya wafuate umati huo wa wapagani. Yehova alikuwa amewaonya mapema kuhusu hilo.—Kut. 23:2.

JE, WENGINE WANAPASWA KUTUFANYIA MAAMUZI?

8. Tunajifunza somo gani muhimu kuhusu kufanya maamuzi kutokana na historia ya Waisraeli?

8 Mifano iliyotajwa hapo juu inaonyesha somo lililo wazi. Kila mmoja wetu anahitaji kufanya maamuzi. Na maamuzi ya hekima na yanayofaa yanategemea ujuzi wa Maandiko. Andiko la Wagalatia 6:5 linatukumbusha hivi: “Kila mmoja ataubeba mzigo wake mwenyewe.” Hatupaswi kumpa mtu mwingine jukumu la kutufanyia maamuzi. Badala yake, tunapaswa kujifunza kibinafsi kile kinachofaa machoni pa Mungu na kuchagua kulitenda.

9. Kwa nini huenda ikawa hatari kuwaruhusu wengine watufanyie maamuzi?

9 Ni katika njia gani tunaweza kuangukia hatari ya kuwaruhusu wengine watufanyie maamuzi? Kushinikizwa na marafiki kunaweza kutuongoza kufanya maamuzi mabaya. (Met. 1:10, 15) Hata hivyo, haidhuru wengine wanatushinikiza kadiri gani, ni jukumu letu kufuata dhamiri yetu iliyozoezwa na Biblia. Tukiruhusu wengine watufanyie maamuzi, kihalisi tutakuwa tumeamua “[kwenda] njiani pamoja nao” au kuwafuata. Bado huo ni uamuzi, lakini ulio na matokeo mabaya sana.

10. Paulo alihitaji kuwaonya Wagalatia kuhusu nini?

10 Mtume Paulo aliwaonya Wagalatia waziwazi kuhusu hatari ya kuwaruhusu wengine wawafanyie maamuzi ya kibinafsi. (Soma Wagalatia 4:17.) Baadhi ya watu kutanikoni walitaka kuwafanyia wengine maamuzi ya kibinafsi ili kuwatenga na mitume. Kwa nini? Watu hao wabinafsi walikuwa wakijitafutia makuu. Walikuwa wamevuka mipaka na hawakuheshimu jukumu la Wakristo wenzao la kujifanyia maamuzi.

11. Tunaweza kuwasaidiaje wengine wanapofanya maamuzi ya kibinafsi?

11 Paulo aliweka mfano mzuri kwa kuheshimu haki ya ndugu zake ya kuwa na uhuru wa kujifanyia maamuzi. (Soma 2 Wakorintho 1:24.) Leo, wanapotoa shauri kuhusu mambo ya kibinafsi, wazee wanapaswa kufuata mfano huo. Wanafurahia kushiriki habari zinazotegemea Biblia pamoja na wengine katika kundi. Hata hivyo, wazee huwa waangalifu kwa kuwaruhusu ndugu na dada mmojammoja kujifanyia maamuzi. Hilo linapatana na akili kwa kuwa ndugu hao ndio watakaopatwa na matokeo ya maamuzi yao. Tunajifunza somo hili muhimu: Tunaweza kuwa tayari kuwasaidia wengine na kuwaonyesha kanuni au shauri la Kimaandiko. Lakini bado wengine wana haki na jukumu la kujifanyia maamuzi. Wakifanya hivyo kwa hekima, watanufaika. Ni wazi kwamba tunapaswa kuepuka mwelekeo wowote wa kufikiri kwamba tuna mamlaka ya kuwafanyia ndugu na dada maamuzi.

Wazee wenye upendo huwasaidia wengine wajifunze kujifanyia maamuzi (Tazama fungu la 11)

USIRUHUSU HISIA ZIONGOZE MAAMUZI YAKO

12, 13. Kwa nini ni hatari kuamua tu kufuata moyo wetu ikiwa tumekasirika au kuvunjika moyo?

12 Msemo fulani unaojulikana sana unasema: Fuata moyo wako. Lakini inaweza kuwa hatari kufanya hivyo. Na kwa njia fulani, kufanya hivyo hakupatani na Maandiko. Biblia inatuonya tusiruhusu moyo wetu usio mkamilifu au hisia zituongoze tunapofanya maamuzi. (Met. 28:26) Pia, masimulizi ya Biblia yanaonyesha matokeo yenye kuhuzunisha ya kufuata moyo wetu. Tatizo la msingi ni kwamba ndani ya wanadamu wasio wakamilifu, kuna moyo “wenye hila kuliko kitu kingine chochote nao ni hatari.” (Yer. 3:17; 13:10; 17:9; 1 Fal. 11:9) Kwa hiyo, tutapatwa na nini tukiamua tu kufuata moyo wetu?

13 Moyo wa Mkristo ni muhimu, kwa kuwa tunaamriwa tumpende Yehova kwa moyo wetu wote na jirani yetu kama tunavyojipenda. (Mt. 22:37-39) Lakini Maandiko yaliyotajwa katika fungu lililotangulia yanaonyesha hatari ya kuruhusu hisia ziongoze fikira na matendo yetu. Kwa mfano, ni nini kinachoweza kutukia ikiwa tutafanya maamuzi tukiwa tumekasirika? Ikiwa tumewahi kufanya hivyo, huenda tunajua vema matokeo ya uamuzi kama huo. (Met. 14:17; 29:22) Vilevile, inaelekea hatutafanya maamuzi mazuri ikiwa tumevunjika moyo. (Hes. 32:6-12; Met. 24:10) Kumbuka kwamba Neno la Mungu linaonyesha hekima ya kuwa “mtumwa wa sheria ya Mungu.” (Rom. 7:25) Ni wazi kwamba tunaweza kupotoshwa kwa urahisi na hisia zetu ikiwa tutaziruhusu zituongoze tunapofanya maamuzi muhimu.

UNAPOHITAJI KUBADILI UAMUZI WAKO

14. Tunajuaje kwamba huenda ikafaa kubadili maamuzi tuliyofanya?

14 Tunahitaji kufanya maamuzi ya hekima. Hata hivyo, hilo halimaanishi kwamba hatupaswi kutangua maamuzi yetu baada ya kuyafanya. Nyakati nyingine, huenda tukahitaji kufikiria upya uamuzi tuliofanya na hata kuubadili. Fikiria jinsi Yehova alivyoshughulika na Waninawi katika siku za Yona. “Naye Mungu wa kweli akaona matendo yao, kwamba walikuwa wamegeuka kutoka katika njia yao mbaya; naye Mungu wa kweli akajuta juu ya msiba ambao alikuwa amesema ataleta juu yao; naye hakuuleta.” (Yona 3:10) Alipoona jinsi Waninawi walivyotubu na kubadili mtazamo wao, Yehova alibadili uamuzi wake. Kwa kufanya hivyo, alionyesha usawaziko, unyenyekevu, na huruma. Isitoshe, Mungu haamui jinsi atakavyotenda kwa sababu ya kuwaka hasira ghafula, kama ambavyo watu wengi hufanya.

15. Ni nini kinaweza kufanya tubadili uamuzi tuliofanya mwanzoni?

15 Nyakati nyingine, huenda ikafaa kufikiria upya uamuzi fulani tuliofanya. Hilo linaweza kutokea hali zinapobadilika. Pindi nyingine, Yehova alibadili maamuzi yake hali zilipobadilika. (1 Fal. 21:20, 21, 27-29; 2 Fal. 20:1-5) Au habari mpya inaweza kutupatia sababu ya kubadili uamuzi wetu. Mfalme Daudi aliambiwa habari za uwongo kumhusu mjukuu wa Sauli, Mefiboshethi. Daudi alipojua ukweli, alibadili uamuzi wake. (2 Sam. 16:3, 4; 19:24-29) Wakati mwingine, linaweza kuwa jambo la hekima tukifanya hivyo pia.

16. (a) Taja baadhi ya miongozo tunayoweza kutumia ili kufanya maamuzi ya hekima. (b) Tunapaswa kuonaje maamuzi tuliyofanya wakati uliopita, na kwa nini?

16 Neno la Mungu linatushauri tusiharakishe tunapohitaji kufanya uamuzi muhimu. (Met. 21:5) Tunapotumia muda kufikiria kwa makini mambo yote yanayohusiana na uamuzi tunaotaka kufanya, inaelekea tutapata matokeo mazuri zaidi. (1 The. 5:21) Kabla ya kufanya uamuzi, kichwa cha familia anapaswa kutumia wakati kufanya utafiti katika Maandiko na machapisho ya Kikristo, na vilevile kutafuta ushauri au maoni ya washiriki wengine wa familia yake. Kumbuka kwamba Mungu alimhimiza Abrahamu asikilize sauti ya mke wake. (Mwa. 21:9-12) Wazee pia wanapaswa kutumia wakati kufanya utafiti. Na ikiwa wao ni wanaume wenye usawaziko na kiasi, hawataogopa kupoteza heshima yao ikiwa wanapata habari mpya inayohusiana na uamuzi waliokuwa wamefanya na hivyo kulazimika kubadili uamuzi huo. Wanapaswa kuwa tayari kubadili kufikiri kwao na maamuzi yao inapohitajika, na ni jambo linalofaa kwetu sote kufuata mfano huo. Kufanya hivyo kutachochea amani na utaratibu katika kutaniko.—Mdo. 6:1-4.

SHIKAMANA NA UAMUZI WAKO

17. Tunawezaje kufanikiwa zaidi tunapofanya maamuzi?

17 Maamuzi fulani ni mazito kuliko mengine. Tunapotaka kufanya maamuzi mazito, tunahitaji kuyafikiria kwa uzito na kusali kuyahusu, na hilo linaweza kuchukua muda. Baadhi ya Wakristo hukabili uamuzi wa kuoa, na ikiwa wataoa, wataoa nani. Uamuzi mwingine muhimu na unaoleta baraka nyingi ni kuamua tutaanza lini utumishi wa wakati wote, na tutafanya nini ili kufaulu katika utumishi huo. Katika hali kama hizo, ni muhimu kuamini kabisa kwamba Yehova anaweza na huandaa mwongozo wenye hekima. (Met. 1:5) Hivyo, ni muhimu kutumia mwongozo wa Biblia, ambao ndio chanzo bora zaidi cha mashauri, na kutafuta mwongozo wa Yehova kupitia sala. Na kumbuka kwamba Yehova anaweza kutusaidia kuwa na sifa zinazohitajiwa ili tufanye maamuzi yanayopatana na mapenzi yake. Unapofanya maamuzi muhimu, zoea kujiuliza hivi: ‘Je, uamuzi huu utathibitisha kwamba nampenda Yehova? Je, utaleta furaha na amani katika familia yangu? Na je, utaonyesha kwamba mimi ni mwenye subira na fadhili?’

18. Kwa nini Yehova anatarajia tujifanyie maamuzi?

18 Yehova hatulazimishi kumpenda na kumtumikia. Huo ni uamuzi wetu. Kupatana na uhuru wa kuchagua ambao ametupatia, anaheshimu jukumu na haki yetu ya ‘kujichagulia’ ikiwa tutamtumikia. (Yos. 24:15; Mhu. 5:4) Lakini anatarajia tushikamane na maamuzi mengine ambayo tunafanya kwa kutegemea mwongozo wake. Tukiwa na imani katika njia ya Yehova ya kufanya mambo na kanuni ambazo ametuandalia kwa fadhili, tunaweza kufanya maamuzi ya hekima na kuonyesha kwamba sisi ni imara katika njia zetu zote.—Yak. 1:5-8; 4:8.