Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAKALA YA 51

“Yehova . . . Huwaokoa Waliovunjika Moyo”

“Yehova . . . Huwaokoa Waliovunjika Moyo”

“Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo; huwaokoa waliovunjika moyo.”​—ZAB. 34:18, maelezo ya chini.

WIMBO 30 Baba Yangu, Mungu Wangu, Rafiki Yangu

MUHTASARI *

1-2. Tutazungumzia nini katika makala hii?

HUENDA nyakati nyingine tukatafakari kuhusu ukweli wa kwamba maisha ni mafupi na jinsi siku zetu ‘zilivyojaa taabu.’ (Ayu. 14:1) Hivyo, inaeleweka kwamba pindi kwa pindi sisi huvunjika moyo. Watumishi wengi wa Yehova wa nyakati za zamani walihisi hivyo pia. Wengine hata walitaka kufa. (1 Fal. 19:2-4; Ayu. 3:1-3, 11; 7:15, 16) Lakini tena na tena, Yehova​—Mungu waliyemtumaini—​aliwafariji na kuwaimarisha. Masimulizi yao yaliandikwa ili kutufariji na kutufundisha.​—Rom. 15:4.

2 Katika makala hii tutazungumzia baadhi ya watumishi wa Yehova ambao walivumilia majaribu yenye kuvunja moyo. Nao ni Yosefu mwana wa Yakobo, mjane Naomi na Ruthu binti mkwe wake, Mlawi aliyeandika Zaburi ya 73, na mtume Petro. Yehova aliwaimarishaje? Na tunaweza kujifunza mambo gani kutokana na mifano yao? Majibu ya maswali hayo, yanatuhakikishia kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo,” na “huwaokoa waliovunjika moyo.”​—Zab. 34:18, maelezo ya chini.

YOSEFU ALIVUMILIA UKATILI NA UKOSEFU WA HAKI

3-4. Yosefu alipatwa na nini alipokuwa kijana?

3 Yosefu alikuwa na umri wa miaka 17 hivi alipoota ndoto mbili zilizotoka kwa Mungu. Ndoto hizo zilionyesha kwamba siku moja Yosefu angekuwa mtu muhimu, angeheshimiwa katika familia yao. (Mwa. 37:5-10) Lakini muda mfupi tu baada ya Yosefu kuota ndoto hizo, maisha yake yalibadilika kabisa. Badala ya kumpa heshima, ndugu zake walimuuza utumwani. Mwishowe alijikuta katika nyumba ya ofisa Mmisri aliyeitwa Potifa. (Mwa. 37:21-28) Ndani ya muda mfupi sana maisha ya Yosefu yalibadilika kutoka kuwa mwana anayependwa sana na baba yake hadi kuwa mtumwa wa hali ya chini wa ofisa mpagani wa makao ya mfalme huko Misri.​—Mwa. 39:1.

4 Kisha, matatizo ya Yosefu yakaongezeka hata zaidi. Mke wa Potifa alimshtaki Yosefu kwa uwongo kwamba alitaka kumbaka. Bila hata kufanya uchunguzi wa shtaka hilo, Potifa alimtupa Yosefu gerezani na alifungwa katika vyuma. (Mwa. 39:14-20; Zab. 105:17, 18) Wazia jinsi kijana Yosefu alivyohisi aliposhtakiwa kwa uwongo kwamba alitaka kumbaka mke wa Potifa. Na fikiria jinsi ambavyo huenda madai hayo yangeliletea suto jina la Yehova. Hapana shaka kwamba Yosefu alikuwa na sababu ya kuvunjika moyo!

5. Yosefu alifanya nini ili asivunjike moyo?

5 Alipokuwa mtumwa na baadaye mfungwa, Yosefu hakuwa na uhuru wa kwenda mahali popote alipotaka na mambo ambayo angeweza kufanya yalidhibitiwa. Ni nini kilichomsaidia kuwa na usawaziko? Badala ya kukazia fikira mambo ambayo hangeweza kutimiza, alifanya kwa bidii kazi aliyokuwa amepewa. Zaidi ya yote, aliendelea kumwona Yehova kuwa Mtu muhimu zaidi maishani mwake. Kwa sababu hiyo, Yehova alibariki kila kitu ambacho Yosefu alifanya.​—Mwa. 39:21-23.

6. Huenda Yosefu alifarijiwa jinsi gani na ndoto zake?

6 Huenda Yosefu alitiwa moyo pia kwa kutafakari ndoto za kinabii alizokuwa ameota mapema. Ndoto hizo zilionyesha kuwa angeiona familia yake tena na kwamba maisha yake yangekuja kuwa mazuri. Na ndivyo ilivyokuwa. Yosefu alipokuwa na umri wa miaka 37 hivi, ndoto zake za kinabii zilianza kutimizwa kwa njia ya pekee!​—Mwa. 37:7, 9, 10; 42:6, 9.

7. Kulingana na 1 Petro 5:10, ni nini kitakachotusaidia kuvumilia majaribu?

7 Somo kwetu. Simulizi la Yosefu linatukumbusha kwamba ulimwenguni kuna ukatili na kwamba watu watatutendea isivyo haki. Hata mwamini mwenzetu anaweza kutuumiza. Lakini ikiwa tutamwona Yehova kuwa Mwamba au Kimbilio letu, hatutavunjika moyo au kuacha kumtumikia. (Zab. 62:6, 7; soma 1 Petro 5:10.) Kumbuka pia kwamba huenda Yosefu alikuwa na umri wa miaka 17 hivi, Yehova alipoanza kushughulika naye kwa njia ya pekee. Ni wazi kwamba Yehova anawatumaini watumishi wake vijana. Leo, vijana wengi ni kama Yosefu. Wao pia wana imani katika Yehova. Baadhi yao wamefungwa gerezani isivyo haki kwa sababu wameendelea kuwa washikamanifu kwa Mungu.​—Zab. 110:3.

WANAWAKE WAWILI WALIOLEMEWA NA HUZUNI

8. Naomi na Ruthu walipatwa na nini?

8 Kwa sababu ya njaa kali, Naomi na familia yake waliondoka nyumbani kwao huko Yuda na kwenda kuishi wakiwa wakaaji wageni katika eneo la Moabu. Wakiwa huko, Elimeleki, mume wa Naomi alikufa na kumwacha na wana wao wawili. Baada ya muda, wana hao wawili walioa wanawake Wamoabu, Ruthu na Orpa. Miaka kumi hivi baadaye, wana wa Naomi walikufa bila kuwa na watoto. (Rut. 1:1-5) Wazia jinsi wanawake hao watatu walivyolemewa na huzuni! Bila shaka, Ruthu na Orpa wangeweza kuolewa tena. Hata hivyo, ni nani ambaye angemtunza Naomi ambaye alikuwa anazeeka? Naomi alikuwa ameshuka moyo sana hivi kwamba pindi fulani alisema hivi: “Msiniite Naomi. Niiteni Mara, kwa maana Mweza-Yote amefanya maisha yawe machungu sana kwangu.” Akiwa amevunjika moyo, Naomi aliamua kurudi Bethlehemu, na Ruthu alienda pamoja naye.​—Rut. 1:7, 18-20.

Mungu aliwathibitishia Naomi na Ruthu kwamba anaweza kuwasaidia waabudu wake washinde hisia za kuvunjika moyo na huzuni. Je anaweza kukusaidia vivyo hivyo wewe pia? (Tazama fungu la 8 hadi 13) *

9. Kulingana na Ruthu 1:16, 17, 22, Ruthu alimtia moyo Naomi jinsi gani?

9 Suluhisho la matatizo ya Naomi lilikuwa upendo mshikamanifu. Kwa mfano, Ruthu alimwonyesha upendo mshikamanifu Naomi kwa kushikamana naye. (Soma Ruthu 1:16, 17, 22.) Wakiwa Bethlehemu, alifanya kazi ya kuokota shayiri kwa bidii kwa ajili yake na Naomi. Matokeo ni kwamba baada ya muda mfupi, mwanamke huyo kijana alijipatia sifa nzuri.​—Rut. 3:11; 4:15.

10. Yehova aliwaonyeshaje upendo watu wenye uhitaji kama vile Naomi na Ruthu?

10 Yehova alikuwa amewapa Waisraeli sheria iliyoonyesha huruma iliyowasaidia watu wenye uhitaji kama vile Naomi na Ruthu. Aliwaambia watu wake kwamba wanapovuna mazao, wasivune kwenye ukingo wa mashamba yao ili maskini waweze kukusanya masalio. (Law. 19:9, 10) Hivyo, Naomi na Ruthu hawakuhitaji kuwa ombaomba ili kupata chakula. Wangeweza kupata chakula kwa njia ambayo haikuwavunjia heshima.

11-12. Boazi aliwapaje Naomi na Ruthu sababu ya kushangilia?

11 Mmiliki wa shamba ambalo Ruthu alikuwa akikusanya nafaka alikuwa mwanamume tajiri aliyeitwa Boazi. Aliguswa moyo sana na ushikamanifu na upendo ambao Ruthu alimwonyesha Naomi, mama mkwe wake, hivi kwamba aliamua kukomboa urithi wa familia yao na kumchukua Ruthu awe mke wake. (Rut. 4:9-13) Boazi na Ruthu walipata mtoto waliyemwita Obedi; naye alikuja kuwa babu ya Mfalme Daudi.​—Rut. 4:17.

12 Wazia shangwe aliyokuwa nayo Naomi alipombeba Obedi, mtoto mchanga, na kumshukuru Yehova kutoka moyoni! Lakini Naomi na Ruthu watajionea mambo mazuri hata zaidi wakati ujao. Wakati wa ufufuo, watajua kwamba Obedi alikuwa babu ya Masihi Aliyeahidiwa, Yesu Kristo!

13. Tunajifunza nini kutokana na simulizi la Naomi na Ruthu?

13 Somo kwetu. Tunapopitia majaribu, tunaweza kuvunjika moyo, au hata kushuka moyo. Huenda hatuoni suluhisho la matatizo yetu. Nyakati kama hizo, tunapaswa kumtumaini kabisa Baba yetu wa mbinguni na kukaa karibu na waabudu wenzetu. Ni kweli kwamba huenda Yehova asiondoe jaribu letu. Kwa mfano, hakumrudishia Naomi mume na watoto wake waliokufa. Lakini atatusaidia kukabiliana na matatizo yetu, labda kupitia matendo ya upendo mshikamanifu yanayoonyeshwa na familia yetu ya kiroho.​—Met. 17:17.

MLAWI AMBAYE KARIBU AJIKWAE

Mwandikaji wa Zaburi 73 alikuwa karibu kujikwaa kwa sababu ya yale yaliyoonekana kuwa ni mafanikio ya watu ambao hawamtumikii Yehova. Inaweza kutokea hivyo kwetu pia (Tazama fungu la 14 hadi 16)

14. Kwa nini Mlawi fulani alivunjika moyo sana?

14 Mwandikaji wa Zaburi ya 73 alikuwa Mlawi. Hivyo, alikuwa na pendeleo la kutumikia kwenye mahali pa ibada pa Yehova. Licha ya hilo, pindi fulani maishani mwake hata yeye alivunjika moyo. Kwa nini? Alianza kuwaonea wivu waovu na wenye kiburi, si kwa sababu ya uovu wao, bali kwa sababu ya ufanisi wao. (Zab. 73:2-9, 11-14) Ni kana kwamba walikuwa na kila kitu​—utajiri, maisha mazuri, na hawakuwa na mahangaiko. Yale yaliyoonekana kuwa mafanikio yalimvunja moyo sana mtunga zaburi, hivi kwamba alisema: “Kwa hakika nimeusafisha moyo wangu bure na kunawa mikono yangu katika ukosefu wa hatia.” Ni wazi kwamba alikuwa katika hatari kubwa sana ya kiroho.

15. Kulingana na Zaburi 73:16-19, 22-25, Mlawi aliyeandika Zaburi hiyo alishindaje hisia za kuvunjika moyo?

15 Soma Zaburi 73:16-19, 22-25. Mlawi aliingia “mahali patakatifu pa Mungu penye utukufu.” Akiwa huko, inaelekea akiwa kati ya waabudu wenzake, aliweza kuchanganua hali yake kwa utulivu, kwa kina, na kwa sala. Matokeo ni kwamba alianza kuona njia yake ya kufikiri imepotoka, na kwamba alikuwa ameanza kutembea kwenye njia hatari ambayo ingeharibu uhusiano wake pamoja na Yehova. Pia, alitambua kwamba waovu wako “kwenye ardhi yenye utelezi” na watafikia “mwisho wao unaotisha.” Ili afaulu kushinda wivu na hisia za kuvunjika moyo, Mlawi huyo aliyeandika Zaburi alihitaji kuona mambo kama Yehova anavyoyaona. Alipofanya hivyo, kwa mara nyingine tena alikuwa na amani, na akawa mwenye furaha. Alisema hivi: “Isipokuwa [Yehova] tu sitamani chochote duniani.”

16. Tunaweza kujifunza nini kutoka kwa Mlawi fulani?

16 Somo kwetu. Acheni tusiwaonee wivu kamwe watu waovu wanaoonekana kana kwamba wamefanikiwa. Furaha yao ni ya kijuu-juu na ni ya muda mfupi; na wakati wao ujao hautadumu milele. (Mhu. 8:12, 13) Ikiwa tutawaonea wivu, tunaweza kuvunjika moyo na tunaweza kupoteza hali yetu nzuri ya kiroho. Hivyo, ukijikuta unawaonea wivu watu waovu wanaoonekana kana kwamba wamefanikiwa, fanya kama Mlawi alivyofanya. Tii ushauri wa Mungu wenye upendo, na ushirikiane na wale ambao wanafanya mapenzi ya Yehova. Unapompenda Yehova kuliko kitu kingine chochote, utapata furaha ya kweli. Na utabaki kwenye njia inayoongoza kwenye “uzima ulio wa kweli.”​—1 Tim. 6:19.

UDHAIFU WA PETRO ULIMVUNJA MOYO

Tunaweza kupata msaada au kuwasaidia wengine kwa kutafakari kuhusu jinsi ambavyo Petro alishinda hisia za kuvunjika moyo na kuendelea kukazia fikira utumishi wake kwa Mungu (Tazama fungu la 17 hadi 19)

17. Petro alikuwa na sababu zipi za kuvunjika moyo?

17 Mtume Petro alikuwa mwanamume mwenye bidii; lakini pia pindi nyingine alitenda bila kufikiri, na kuna nyakati ambazo hakusita kueleza hisia zake mara moja. Matokeo ni kwamba, pindi fulani alisema au kufanya mambo ambayo baadaye alijutia. Kwa mfano, Yesu alipowaambia mitume wake kwamba angeteseka na kufa, Petro alimkemea na kumwambia hivi: “Hutapatwa kamwe na mambo hayo.” (Mt. 16:21-23) Lakini Yesu alimrekebisha Petro. Kikundi cha watu kilipokuja kumkamata Yesu, Petro alitenda bila kufikiri, akamkata sikio mtumwa wa kuhani mkuu. (Yoh. 18:10, 11) Kwa mara nyingine tena, Yesu alimrekebisha mtume huyo. Isitoshe, Petro alijigamba kwamba hata ikiwa mitume wengine watakwazika kuhusiana na Kristo, yeye hangefanya hivyo kamwe! (Mt. 26:33) Lakini kujiamini huko kupita kiasi kulisababisha awaogope wanadamu, na Petro akamkana Bwana wake mara tatu. Akiwa amevunjika moyo sana, Petro ‘alienda nje akalia kwa uchungu.’ (Mt. 26:69-75) Lazima alijiuliza ikiwa kuna siku Yesu atamsamehe.

18. Yesu alimsaidiaje Petro kushinda hisia za kuvunjika moyo?

18 Hata hivyo, Petro hakujiruhusu alemewe na kuvunjika moyo. Baada ya kujikwaa, alisimama tena, na baadaye aliendelea kumtumikia Yehova pamoja na mitume wengine. (Yoh. 21:1-3; Mdo. 1:15, 16) Ni nini kilichomsaidia asimame tena? Kwanza, awali Yesu alisali kwamba imani ya Petro isidhoofike, naye alimhimiza Petro arudi na kuwaimarisha ndugu zake. Yehova alijibu sala hiyo ya Yesu ya kutoka moyoni. Baadaye, Yesu alimtokea Petro kibinafsi na bila shaka alimtia moyo. (Luka 22:32; 24:33, 34; 1 Kor. 15:5) Baada ya mitume kujaribu kuvua samaki usiku kucha bila mafanikio, Yesu aliwatokea. Pindi hiyo, Yesu alimpa Petro fursa ya kuonyesha kama kweli anampenda sana. Yesu alikuwa amemsamehe rafiki yake mpendwa na alimkabidhi kazi nyingine.​—Yoh. 21:15-17.

19. Andiko la Zaburi 103:13, 14 linatufundisha nini kuhusu jinsi Yehova anavyotuona tunapotenda dhambi?

19 Somo kwetu. Njia ambayo Yesu alishughulika na Petro inaonyesha rehema ya Yesu, naye anamwiga Baba yake kikamilifu. Hivyo tunapokosea, hatupaswi kujihukumu kwamba Yehova hatatusamehe. Tunapaswa kukumbuka kwamba Shetani anataka tuhisi hivyo. Badala ya kuhisi hivyo, acheni tujitahidi kujiona​—na kuwaona wale wanaotukosea—​kama Baba yetu wa mbinguni mwenye huruma na upendo anavyotuona.​—Soma Zaburi 103:13, 14.

20. Tutachunguza nini katika makala inayofuata?

20 Mfano wa Yosefu, Naomi na Ruthu, Mlawi fulani, na Petro unatuhakikishia kwamba “Yehova yuko karibu na wale waliovunjika moyo.” (Zab. 34:18) Nyakati nyingine anaruhusu tupatwe na majaribu na tupatwe na hali zenye kuvunja moyo. Hata hivyo, tunapofaulu kuvumilia majaribu hayo kwa msaada wa Yehova, imani yetu inaimarishwa. (1 Pet. 1:6, 7) Katika makala inayofuata, tutachunguza zaidi jinsi Yehova anavyowategemeza washikamanifu wake ambao wamevunjika moyo, labda kwa sababu ya kutokamilika kwao au kwa sababu ya hali ngumu wanazopitia.

WIMBO 7 Yehova, Nguvu Yetu

^ fu. 5 Yosefu, Naomi na Ruthu, Mlawi fulani, na mtume Petro walipitia hali zenye kuvunja moyo. Katika makala hii, tutaona jinsi Yehova alivyowafariji na kuwaimarisha. Pia, tutachunguza mambo tunayoweza kujifunza kutokana na mifano yao na kutokana na jinsi Mungu alivyoshughulika nao kwa huruma.

^ fu. 56 MAELEZO YA PICHA: Naomi, Ruthu, na Orpa walihuzunika na kuvunjika moyo kwa sababu ya vifo vya wenzi wao. Baadaye, Ruthu na Naomi walishangilia pamoja na Boazi baada ya Obedi kuzaliwa.