Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

HABARI KUU

Je, Dini Inapoteza Waumini?

Je, Dini Inapoteza Waumini?

Gaffar alizaliwa nchini Uturuki naye alichukizwa na wazo lililofundishwa na dini yake kwamba Mungu ni mkatili. Mke wake Hediye, alianza kuwa na shaka kuhusu mafundisho ya dini yake tangu alipokuwa na umri wa miaka tisa. Anasema hivi: “Nilifundishwa kwamba tayari maisha yetu yamepangwa na Mungu. Kwa kuwa mimi ni yatima, nilijiuliza, ‘Kwani nilifanya nini wazazi wangu wakafa?’ Mara nyingi nililia usiku kucha. Kufikia wakati nilipokuwa na umri wa miaka 15, nilikuwa nimeacha kupendezwa na dini yangu.”

JE, WEWE umekatishwa tamaa na dini? Watu wengi sana hawapendezwi na dini. Katika nchi nyingi, idadi inaongezeka ya watu wanaosema kwamba wao ‘si watu wa dini’—na jambo hilo linaonyesha kwamba hali ya dini inazidi kuwa mbaya. Baadhi ya nchi hizo zimeorodheshwa hapa.

Kwa Nini Watu Wanaacha Dini?

Kuna sababu kadhaa zinazowafanya watu wakatishwe tamaa na dini. Sababu hizo zinatia ndani jeuri na ugaidi unaochochewa na kuungwa mkono na dini, kashfa za ngono zinazowahusu viongozi wa dini, na matatizo mengine yasiyo ya wazi ambayo yanawafanya watu wengi zaidi waache dini. Mambo hayo yanatia ndani:

  • Utajiri: “Kadiri unavyopata utajiri, ndivyo inavyokuwa rahisi zaidi kuacha kupendezwa na dini,” kinasema kitabu Global Index of Religion and Atheism. Maoni hayo yanapatana na akili, kwa kuwa katika nchi nyingi, watu wengi zaidi wamekuwa matajiri. Katika maeneo fulani, watu wanaishi “maisha ambayo yangemfanya mfalme mkuu zaidi aliyeishi miaka mia mbili iliyopita aone wivu,” anasema John V. C. Nye, profesa wa mambo ya uchumi.

    BIBLIA INASEMA NINI: Biblia ilitabiri kwamba katika “siku za mwisho,” watu wangependa pesa na raha kuliko wanavyompenda Mungu na jirani. (2 Timotheo 3:1-5) Mwandikaji mmoja wa Biblia aliyetambua hatari za kiroho zinazohusianishwa na utajiri alisema maneno haya: “Usinipe umaskini wala utajiri.” Kwa nini alikuwa na maoni hayo? Alitoa sababu ifuatayo: “Nisije nikashiba nikakukana.”—Methali 30:8, 9.

  • Utamaduni wa kidini na maadili: Watu wengi, hasa vijana, huona kuwa dini haiwezi kuwanufaisha na imepitwa na wakati. Wengine huona kuwa haiaminiki. Tim Maguire, ofisa wa habari katika shirika linaloitwa Humanist Society Scotland alisema: “Unapotafakari mambo ambayo dini zimefanya katika karne zilizopita,” unatambua “watu wameamua kujitenga nazo kwa kuwa hawana imani tena kwamba zinaweza kuwawekea viwango vya maadili wanavyopaswa kufuata.”

    BIBLIA INASEMA NINI: Yesu Kristo alionya hivi kuhusu walimu wa uwongo: “Kwa matunda yao mtawatambua. . . . Kila mti mzuri huzaa matunda mazuri, lakini kila mti uliooza huzaa matunda yasiyofaa.” (Mathayo 7:15-18) “Matunda yasiyofaa” yanatia ndani kujihusisha na mambo ya kisiasa na kuunga mkono mazoea yanayomchukiza Mungu, kama vile ngono kati ya watu wa jinsia moja. (Yohana 15:19; Waroma 1:25-27) Pia, yanatia ndani kuacha kufundisha mafundisho yenye kunufaisha yaliyo katika Maandiko na badala yake kufundisha desturi na utamaduni usio na faida yoyote. (Mathayo 15:3, 9) Yesu alisema: “Lisha kondoo wangu wadogo.” (Yohana 21:17) Hata hivyo, leo watu wengi sana wana njaa ya kiroho.

  • Dini na pesa: Kulingana na Kituo cha Utafiti cha Pew, watu wengi wanahisi kwamba dini hukazia sana mambo ya pesa. Kinachofanya jambo hilo liwe baya zaidi ni kwamba viongozi fulani wa kidini wanaishi maisha ya kifahari ambayo wafuasi wao hawawezi kuishi. Kwa mfano, katika jiji moja nchini Ujerumani ambako si rahisi kwa watu wengi wanaoenda kanisani kupata mahitaji ya msingi, askofu alishtakiwa kwa kuishi maisha ya anasa. Maisha hayo yamewachukiza Wakatoliki wengi wa eneo hilo. Pia, ripoti moja katika gazeti GEO linasema kwamba nchini Nigeria, “ambako watu milioni 100 hupata mshahara wa chini ya euro 1 kwa siku, maisha ya anasa ya makasisi fulani yameanza kuzua utata.”

    BIBLIA INASEMA NINI: Paulo, aliyeandika vitabu fulani vya Biblia, alisema hivi: “Sisi si wachuuzi wa neno la Mungu.” (2 Wakorintho 2:17) Hata ingawa Paulo alikuwa mhudumu maarufu katika kutaniko la Kikristo la karne ya kwanza, mara nyingi alifanya kazi ya mikono ili asiwalemee wengine kifedha. (Matendo 20:34) Mtazamo wake ulionyesha kwamba alitii amri hii ya Yesu: “Mlipokea bure, toeni bure.”—Mathayo 10:7, 8.

Kupatana na kanuni hizo, Mashahidi wa Yehova hawauzi machapisho yao na wanawafundisha watu Biblia bila malipo. Hawadai fungu la kumi wala kukusanya sadaka kwenye mikutano yao. Badala yake, pesa zinazohitajika hupatikana kupitia michango ya hiari.—Mathayo 6:2, 3.

Ilitabiriwa Watu Wataacha Kushirikiana na Dini!

Miaka michache iliyopita, haikuwa rahisi kuwazia hali inayokabili dini leo. Hata hivyo, Mungu aliona jambo hilo mapema na kutueleza katika Biblia. Akitumia lugha ya mfano, Mungu alifananisha dini zote za uwongo na kahaba anayeitwa “Babiloni Mkubwa.”—Ufunuo 17:1, 5.

Mfano huo unafaa kwa kuwa dini ya uwongo, ingawa inadai kuwa yenye uaminifu kwa Mungu, imeshirikiana na watawala wa ulimwengu ili kujipatia mamlaka na utajiri. Andiko la Ufunuo 18:9 linasema kwamba ‘wafalme wa dunia walifanya uasherati pamoja naye.’ Pia, neno hilo “Babiloni” linafaa kwa kuwa chanzo cha mafundisho na mazoea mengi ya dini ya uwongo, kama vile kutokufa kwa nafsi, utatu, na ushirikina, kilitokana na Babiloni la kale, jiji lililojaa dini ya uwongo na ushirikina. *Isaya 47:1, 8-11.

Babiloni lenye nguvu lilianguka wakati ambapo maji ya Mto Efrati yaliyolinda jiji hilo ‘yalikaushwa’ na hivyo kufungua njia kwa jeshi la Wamedi na Waajemi kulivamia. (Yeremia 50:1, 2, 38) Kwa kweli, jeshi hilo lilishinda Babiloni katika usiku mmoja!—Danieli 5:7, 28, 30.

Babiloni Mkubwa pia ‘amekaa juu ya maji mengi.’ Biblia inatuambia kuwa maji hayo yanamaanisha “watu na umati,” yaani mamilioni ya watu ambao huunga mkono dini ya uwongo. (Ufunuo 17:1, 15) Biblia ilitabiri kwamba maji hayo ya mfano yangekauka. Jambo hilo linaonyesha kwamba Babiloni la leo liko karibu kuangamizwa. (Ufunuo 16:12; 18:8) Lakini ni nani atakayemwangamiza Babiloni? Washiriki wake wa kisiasa wanaompenda watamgeuka na kumchukia. Watampora au kula nyama yake.—Ufunuo 17:16, 17. *

Kupungua kwa maji ya mto kule Babiloni kuliwakilisha jinsi watu watakavyotoka katika Babiloni Mkubwa

“Tokeni Kwake”!

Kwa sababu ya mambo yatakayompata Babiloni Mkubwa, Mungu anaonya hivi kwa upendo: “Tokeni kwake, watu wangu, ikiwa hamtaki kushiriki pamoja naye dhambi zake, na ikiwa hamtaki kupokea sehemu ya mapigo yake.” (Ufunuo 18:4) Ona kwamba neno “ikiwa,” limerudiwa mara mbili. Naam, onyo ambalo Mungu anatoa limeelekezwa kwa watu ambao wanasumbuliwa na mafundisho yenye kudhuru na wanaotafuta kibali cha Mungu—watu kama vile Gaffar na Hediye, waliotajwa mapema.

Kabla ya kujifunza Biblia, Gaffar aliamini kwamba watu wanamtii Mungu kwa sababu tu wanamwogopa. Anasema, “Nilifarijika kujua kwamba Yehova ni Mungu mwenye upendo, na kwamba anataka tumtii hasa kwa sababu tunampenda.” (1 Yohana 4:8; 5:3) Hediye alipata amani ya akili alipojifunza kwamba si Mungu aliyemfanya awe yatima na kwamba hali yake haikuwa imepangwa mapema. Alifarijiwa na Maandiko kama vile Yakobo 1:13 linalosema kwamba Mungu hawajaribu watu na mambo maovu. Yeye na Gaffar walikubali kweli ya Biblia na kutoka katika “Babiloni.”—Yohana 17:17.

Babiloni Mkubwa atakapoangamizwa, watu ambao wametii na kutoka kwake ili ‘wamwabudu Baba kwa roho na kweli’ hawatapatwa na madhara. (Yohana 4:23) Tumaini lao ni kuona dunia ‘ikijawa na kumjua Yehova kama vile maji yanavyoifunika bahari.’—Isaya 11:9.

Naam, dini ya uwongo pamoja na matunda yake maovu itafikia mwisho, kwa kuwa Mungu ‘hawezi kusema uwongo.’ (Tito 1:2) Tofauti na hilo, ibada ya kweli itadumu milele!

^ fu. 16 Ili upate habari zaidi kuhusu Babiloni Mkubwa na ili ufahamu Biblia inasema nini kuhusu hali ya wafu, ukweli kumhusu Mungu, na kuhusu ushirikina, ona kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Kitabu hicho kinapatikana kwenye tovuti ya www.jw.org/sw.

^ fu. 18 Ona makala yenye kichwa “Maoni ya Biblia—Mwisho wa Dunia,” katika toleo hili la Amkeni!