Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

MAONI YA BIBLIA

Mwisho wa Dunia

Mwisho wa Dunia

Andiko la 1 Yohana 2:17 linasema: “Dunia inapita, pamoja na tamaa zake.” (Union Version) Hiyo ni dunia gani? Itapita jinsi gani na lini?

Mwisho wa “dunia” gani?

BIBLIA INASEMA NINI?

Kwa kuwa dunia inayotajwa hapo ina ‘tamaa’ ambazo Mungu anashutumu, ni wazi kwamba si dunia halisi. Ni wanadamu wanaompuuza Mungu, na jambo hilo linawafanya kuwa adui zake. (Yakobo 4:4) Wanadamu hao “watahukumiwa adhabu ya uharibifu wa milele.” (2 Wathesalonike 1:7-9) Kwa upande mwingine, watu wanaotii agizo la Yesu Kristo la kuepuka kuwa “sehemu ya ulimwengu” wanatumaini la uzima wa milele.—Yohana 15:19.

Andiko la 1 Yohana 2:17 linamalizia hivi: “Yeye anayefanya mapenzi ya Mungu anadumu milele.” Ndiyo, mtu huyo atakuwa na tumaini la kuishi milele hapa duniani, kwa kuwa andiko la Zaburi 37:29 linasema hivi: “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”

“Msiwe mkiupenda ulimwengu au vitu vilivyo katika ulimwengu. Yeyote akiupenda ulimwengu, kumpenda Baba hakumo ndani yake.”1 Yohana 2:15.

Mwisho wa dunia utakuja jinsi gani?

BIBLIA INASEMA NINI?

Mwisho utakuja kupitia hatua mbili kuu. Kwanza, Mungu ataharibu dini ya uwongo, inayofananishwa na kahaba anayeitwa “Babiloni Mkubwa.” (Ufunuo 17:1-5; 18:8) Ingawa anadai kuwa mshikamanifu kwa Mungu, amekuwa akishirikiana na viongozi wa kisiasa wa ulimwengu huu. Hata hivyo, viongozi hao watamgeuka. “Watamchukia yule kahaba na kumfanya kuwa ukiwa na uchi, nao watakula sehemu zake zenye nyama [au, utajiri] na kumteketeza kabisa kwa moto.”—Ufunuo 17:16.

Pili, Mungu ataelekeza fikira zake kwa viongozi hao wa kisiasa—“wafalme wa dunia nzima inayokaliwa.” Wataharibiwa pamoja na watu wote waovu katika “vita vya ile siku kuu ya Mungu Mweza-Yote,” ambayo pia inaitwa “Har–Magedoni.”—Ufunuo 16:14, 16.

Mtafuteni Yehova, ninyi nyote mlio wapole wa dunia . . . Utafuteni uadilifu, utafuteni upole. Huenda mkafichwa katika siku ya hasira ya Yehova.” Sefania 2:3.

Mwisho wa dunia utakuja lini?

BIBLIA INASEMA NINI?

Mwisho utakuja wakati wanadamu watakapokuwa wameonywa kikamili kupitia kazi ya ulimwenguni pote ya kutangaza Ufalme wa Mungu. Ufalme huo ni serikali itakayotawala dunia nzima wakati ambapo serikali za wanadamu zitaondolewa. (Danieli 7:13, 14) Yesu Kristo alisema hivi: “Hii habari njema ya ufalme itahubiriwa katika dunia yote inayokaliwa ili kuwa ushahidi kwa mataifa yote, na ndipo ule mwisho utakapokuja.” (Mathayo 24:14) Kazi hiyo ya kuhubiri, inayoonyesha haki na rehema ya Mungu, ni sehemu ya “ishara” yenye mambo mengi ya siku za mwisho. Ishara hiyo inatia ndani pia vita kati ya mataifa, matetemeko ya nchi, njaa, na magonjwa.—Mathayo 24:3; Luka 21:10, 11.

Mbali na kutabiri matukio ya ulimwengu, Biblia inatueleza pia kuhusu mabadiliko ya kijamii katika “siku za mwisho.” Inasema hivi: “Kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo. Kwa maana watu watakuwa wenye kujipenda wenyewe, wenye kupenda pesa, . . . wasiotii wazazi, . . . wasiojizuia, wakali, wasiopenda wema, . . . wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.” *2 Timotheo 3:1-5.

Ulimwengu huu mwovu karibuni ‘utapitilia mbali.’—1 Yohana 2:17

Hali hizo zinatambulisha kipindi kilichoanza mwaka wa 1914 hivi, wakati wa Vita vya Kwanza vya Ulimwengu. Tangu mwaka huo, Mashahidi wa Yehova wametangaza Ufalme wa Mungu katika kila sehemu ya ulimwengu, nao wanaona kuwa ni pendeleo kubwa kushiriki katika kazi hii. Ndiyo sababu gazeti lao kuu linaitwa Mnara wa Mlinzi Unaotangaza Ufalme wa Yehova.

“Kwa hiyo, endeleeni kukesha, kwa sababu hamwijui ile siku wala saa.”Mathayo 25:13.

^ fu. 14 Ili upate habari zaidi ona sura ya 9 ya kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova. Pia kinapatikana kwenye www.jw.org/sw.