Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 MAHOJIANO | RACQUEL HALL

Mwanamke Myahudi Anaeleza Sababu Iliyomfanya Achunguze upya Imani Yake

Mwanamke Myahudi Anaeleza Sababu Iliyomfanya Achunguze upya Imani Yake

Racquel Hall alizaliwa na mama Myahudi wa Israel na baba Mwaustria ambaye alibadili imani yake na kuwa Myahudi. Wazazi wa mama yake walikuwa wanaharakati wa haki za Wayahudi ambao walihamia Israel mnamo 1948, mwaka ambao nchi hiyo ilitangazwa kuwa Jamhuri huru. Mwandishi wa Amkeni! alimwuliza Rac-quel kile kilichomfanya achunguze upya imani yake ya Kiyahudi.

Tueleze kuhusu malezi yako.

Nilizaliwa katika mwaka wa 1979 nchini Marekani. Nilipokuwa na umri wa miaka mitatu, wazazi wangu walitalikiana. Mama alinilea kulingana na tamaduni za Kiyahudi na alinipeleka kwenye yeshivas, au shule za Kiyahudi. Nilipokuwa na umri wa miaka saba, tulihamia Israel kwa mwaka mmoja, nami nilienda shule katika makazi ya kijamaa ya Israel yaliyoitwa kibuzi. Kisha mimi na Mama tulihamia Mexico.

Ingawa hakukuwa na sinagogi katika eneo hilo, niliendelea kufuata desturi za Kiyahudi. Nilikuwa nikiwasha mishumaa siku ya Sabato, nikisoma Torati yetu, na kusali kwa kutumia siddur, au kitabu chetu cha sala. Nilipokuwa shuleni, mara nyingi niliwaambia wanafunzi wenzangu kwamba dini yangu ndiyo dini ya kwanza kabisa. Sikuwa nimewahi kusoma ile sehemu inayoitwa Agano Jipya, inayokazia hasa huduma na mafundisho ya Yesu Kristo. Kwa kweli, Mama alinionya nisiisome, kwa kuwa aliogopa imani yangu ingepotoshwa na mafundisho hayo.

Ni nini kilichokufanya usome Agano Jipya?

Nilipofikisha umri wa miaka 17, nilirudi Marekani ili nimalize masomo yangu. Huko rafiki yangu aliniambia kwamba maisha yangu hayangekuwa na kusudi iwapo singemjua Yesu.

“Watu wanaomwamini Yesu wamepotea,” nikamjibu.

“Umewahi kusoma Agano Jipya?” akauliza.

“Sijawahi,” nikamjibu.

“Kwa hiyo,” akaniambia, “huoni kwamba ni ujinga, kutoa maoni kuhusu kitu ambacho hujui chochote kukihusu?”

Maneno yake yalinichoma sana, kwa kuwa sikuzote niliona kuwa  ni upumbavu kutoa maoni kuhusu jambo usilolijua. Baada ya kukosolewa hivyo, nilienda na Biblia yake nyumbani na nikaanza kusoma Agano Jipya.

Mambo uliyosoma yalikuathiri kwa njia gani?

Nilishangaa kufahamu kwamba waandikaji wa Agano Jipya walikuwa Wayahudi. Pia, kadiri nilivyosoma, ndivyo nilivyokuja kumwona Yesu kuwa Myahudi mwenye fadhili na mnyenyekevu aliyetaka kuwasaidia watu, si kuwatumia vibaya. Hata nilienda kwenye maktaba na kuazima vitabu kumhusu. Hata hivyo, hakuna kitabu chochote kati ya hivyo kilichonisadikisha kwamba yeye ndiye Masihi. Vitabu vingine vilisema kwamba yeye ndiye Mungu—jambo ambalo kwa maoni yangu halikupatana na akili. Kwani Yesu alisali kwa nani—kwake yeye mwenyewe? Isitoshe, Yesu alikufa. Hata hivyo, Biblia inasema hivi kumhusu Mungu: “Wewe hufi.” *

Ulipataje majibu ya maswali hayo?

Ukweli haujipingi, na nilikuwa nimeazimia kupata ukweli. Kwa hiyo nilisali kwa Mungu kwa unyoofu huku nikitokwa na machozi, nayo ilikuwa mara yangu ya kwanza kusali bila kutumia siddur. Nilipomaliza tu kusali nilisikia mlango wangu ukibishwa. Mashahidi wawili wa Yehova walisimama mlangoni kwangu. Walinipa kitabu kimoja wanachotumia kujifunza Biblia. Kitabu hicho, pamoja na mazungumzo niliyokuwa nayo na Mashahidi, yalinisadikisha kwamba mafundisho yao yanategemea Biblia. Kwa mfano, Mashahidi wanatambua kwamba Yesu si sehemu ya Utatu, bali yeye ni “Mwana wa Mungu” * na “mwanzo wa uumbaji wa Mungu.” *

Punde tu baada ya hapo nilirudi Mexico, ambako niliendelea kujifunza unabii kumhusu Masihi pamoja na Mashahidi. Nilishangaa kuona kwamba kuna unabii chungu nzima! Lakini bado niliendelea kuwa na shaka kwa kadiri fulani. Nilijiuliza ‘Je, ni Yesu pekee aliyetimiza unabii huo?’ na ‘Namna gani ikiwa alikuwa tu mwigizaji stadi?’

Ni nini hasa kilichokusadikisha?

Mashahidi walinionyesha unabii ambao hakuna mtu angeweza kuigiza. Kwa mfano, zaidi ya miaka 700 mapema, nabii Mika alikuwa ametabiri kwamba Masihi angezaliwa huko Bethlehemu, Yudea. * Ni nani anayeweza kuamua mahali atakapozaliwa? Isaya aliandika kwamba Masihi angeuawa kama mhalifu anayedharauliwa, lakini angezikwa pamoja na matajiri. * Utabiri wote huo ulitimizwa na Yesu.

Uthibitisho mwingine unahusiana na ukoo wa Yesu. Biblia ilisema kwamba Masihi angekuwa mzao wa Mfalme Daudi. * Kwa kuwa Wayahudi wa kale walikuwa na rekodi za umma na za kibinafsi za ukoo, iwapo Yesu hakuwa ametoka katika nasaba ya Daudi, maadui wake wangetangaza jambo hilo hadharani! Lakini hawangeweza kufanya hivyo, kwa kuwa hakuna ambaye angeweza kubisha kwamba Yesu alikuwa mzao wa Daudi. Hata umati ulimwita “Mwana wa Daudi.” *

Katika mwaka wa 70 W.K.—miaka 37 baada ya Yesu kufa—majeshi ya Roma yaliharibu Yerusalemu, na rekodi za familia zilipotea au zikaharibiwa. Kwa hiyo, ili nasaba yake iweze kutambuliwa, lazima Masihi angetokea kabla ya 70 W.K.

Kufahamu mambo hayo kulikuathirije?

Kwenye Kumbukumbu la Torati 18:18, 19, ilitabiriwa kwamba Mungu angemwinua nabii katika Israeli aliye kama Musa. Mungu alisema, yeyote ambaye “hatasikiliza maneno yangu ambayo atayasema katika jina langu, mimi mwenyewe nitamtaka ajibu.” Kujifunza Biblia yote kwa kina kulinisadikisha kwamba Yesu wa Nazareti ndiye aliyekuwa nabii huyo.