Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

 HABARI KUU

Jilinde Dhidi ya Uhalifu!

Jilinde Dhidi ya Uhalifu!

“Kwa kawaida rafiki zangu walinisindikiza hadi nyumbani usiku. Lakini jioni moja nilikuwa nimechoka sana kwa hiyo nikaamua kuchukua teksi.

“Dereva huyo hakunipeleka nyumbani. Badala yake, alinipeleka kwenye shamba lililokuwa limeachwa ukiwa, kisha akajaribu kunilala kinguvu. Nilipopiga mayowe kwa nguvu zangu zote, alirudi nyuma. Aliponikaribia tena, nilipiga mayowe na kukimbia.

“Zamani nilifikiri, ‘Kupiga mayowe kunaweza kunisaidiaje?’ Lakini sasa ninajua kwamba kupiga mayowe kuna faida kubwa!”—KARIN. *

KATIKA nchi nyingi, uhalifu ni jambo linaloweza kukupata wakati wowote. Kwa mfano, katika nchi moja hakimu fulani alisema hivi: “Ukweli wenye kusikitisha ni kwamba kila mtu atapatwa na uhalifu.” Huenda sehemu fulani zikawa hazina uhalifu sana. Hata hivyo, si jambo la hekima kupuuza mambo kwa kuwa hilo linaweza kufanya mtu ashambuliwe kwa urahisi.

Iwe unaishi katika maeneo yaliyo na uhalifu mwingi au mchache, unaweza kufanya nini ili maisha yako na ya wapendwa wako yawe salama zaidi? Njia moja ni kwa kufuata kanuni hii inayopatikana katika Biblia: “Mtu mwangalifu huona hatari akajificha, lakini wajinga hujitokeza mbele wakaumia.” (Methali 22:3, Biblia Habari Njema) Polisi wanapendekeza kwamba watu wanapaswa kuchukua hatua za kujilinda mapema ili kuepuka kupatwa na uhalifu.

Matokeo ya uhalifu si kuumizwa kimwili na kupoteza mali tu. Watu wengi hupatwa pia na madhara ya kiakili na kihisia yanayodumu kwa muda mrefu. Kwa hiyo, ni muhimu tufanye yote tunayoweza ili kuwa salama zaidi! Ukiwa na lengo hilo akilini, ona jinsi unavyoweza kuchukua hatua za kujilinda dhidi ya aina nne za uhalifu—unyang’anyi, kutendewa vibaya kingono, uhalifu unaofanywa kupitia Intaneti, na kuibiwa utambulisho.

 UNYANG’ANYI

Unahusisha nini? Unyang’anyi ni wizi wa kutumia nguvu au kutisha kutumia nguvu.

Unawaathirije watu? Baada ya visa vingi vya uhalifu wa kutumia nguvu huko Uingereza, mwendesha mashtaka mmoja alisema kwamba ingawa waathiriwa hawakupatwa na madhara yoyote ya kimwili, wote waliathiriwa vibaya sana kiakili. Anasema: “Wengi wao husema wana wasiwasi usiokoma na wanashindwa kulala . . .  na karibu wote walisema kwamba maisha yao ya kila siku yameathiriwa sana na mambo yaliyowapata.”

Unaweza kufanya nini?

  • Wezi hupenda kutumia fursa yoyote wanayopata; hakikisha unafahamu kinachoendelea karibu na wewe

    Uwe macho. Wezi hupenda kutumia fursa yoyote wanayopata. Wanapenda kuwavizia watu wasiokuwa macho. Kwa hiyo, uwe mwangalifu kuhusu watu wanaokutazama, hakikisha unafahamu kinachoendelea karibu na wewe, na usidhoofishe uwezo wako wa kufikiri au wa kufanya maamuzi kwa kunywa kileo kupita kiasi au kutumia vibaya dawa. Kitabu kimoja kuhusu afya kinasema kwamba “mtu anapokunywa kileo au kutumia dawa za kulevya,” inakuwa vigumu sana kwake “kufikiri na kuchanganua hali hatari inayoweza kutokea.”

  • Linda mali yako. Funga milango na madirisha ya gari na nyumba yako. Usimruhusu mtu usiyemjua aingie nyumbani kwako. Weka vitu vya thamani mahali ambapo haviwezi kuonekana; usiviache peupe. “Wenye kiasi wana hekima,” inasema Methali 11:2. Wezi—kutia ndani watoto wa mitaani—mara nyingi huwashambulia watu ambao huonyesha waziwazi vito vyao vyenye thamani na vifaa vya kielektroniki.

  • Omba mashauri. “Njia ya mpumbavu ni sawa machoni pake, lakini anayesikiliza shauri ni mwenye hekima.” (Methali 12:15) Ikiwa unasafiri, sikiliza mashauri ya wenyeji wenye kutumainika, kutia ndani wenye mamlaka. Wanaweza kukueleza ni maeneo gani unayopaswa kuepuka na kukuonyesha jinsi unavyoweza kujilinda na kulinda mali zako.

KUTENDEWA VIBAYA KINGONO

Kunahusisha nini? Kutendewa vibaya kingono hakuhusishi tu kulalwa kinguvu bali kunatia ndani matendo mengine ya kingono ambayo mtu anatishwa, analazimishwa, au anaogopeshwa ili ayafanye.

Kunawaathirije watu? “Jambo lenye kusikitisha zaidi ni [kwamba] huathiriki tu wakati unapotendewa vibaya kingono,” anaeleza mwanamke mmoja aliyelalwa kinguvu. “Jambo hilo hukusumbua kwa muda mrefu sana na kubadili mtazamo wako kuhusu maisha. Pia tendo hilo hubadili maisha ya wapendwa wako.” Bila shaka, mhasiriwa hapaswi kulaumiwa kwa kutendewa vibaya kingono. Mwenye kumtendea vibaya ndiye anayepaswa kulaumiwa.

Unaweza kufanya nini?

  • Usipuuze hisia zako. Idara ya Polisi ya North Carolina, Marekani inashauri hivi: “Ikiwa hujihisi salama ukiwa mahali fulani au ukiwa na mtu fulani—ondoka. Usimruhusu mtu yeyote akulazimishe kuendelea kuwa mahali hapo ikiwa hujihisi salama.”

  • Jiamini; uwe macho. Watu wanaowavizia wengine ili kufanya ngono nao hutafuta watu wasio macho wanaoweza kushambuliwa kwa urahisi. Kwa hiyo, tembea kwa njia inayoonyesha kwamba huna wasiwasi na ukae macho.

  • Tenda kwa haraka. Piga mayowe. (Kumbukumbu la Torati 22:25-27) Kimbia  au umshambulie anayekuvizia bila yeye kutazamia. Ikiwezekana, kimbilia mahali salama uwapigie simu polisi. *

UHALIFU UNAOFANYWA KUPITIA INTANETI

Unahusisha nini? Uhalifu unaofanywa kupitia Intaneti unatia ndani kuepuka kulipa kodi, kutoa habari za uwongo ili mtu apokee huduma za jamii, kutumia kadi ya mkopo ya mtu mwingine, na kutotuma bidhaa zilizoagizwa ambazo tayari zimelipiwa. Pia unatia ndani mbinu za ulaghai za kuwekeza pesa katika biashara fulani na minada inayofanywa kwenye Intaneti.

Unawaathirije watu? Uhalifu huo huwagharimu wahasiriwa—na jamii kwa ujumla—mabilioni ya pesa. Fikiria mfano mmoja. Sandra alipokea barua-pepe ambayo alidhani kwamba imetoka kwenye benki yake iliyokuwa ikiomba awape habari zake za kibinafsi. Dakika chache tu baada ya kutuma habari hizo, alishtuka kuona kwamba dola 4,000 (za Marekani) zilikuwa zimetolewa kutoka kwenye akaunti yake na kupelekwa kwenye akaunti ya benki nyingine. Haraka Sandra akatambua kwamba alikuwa ametapeliwa.

Unaweza kufanya nini?

  • Jihadhari! Usidanganyike na Tovuti zinazoonekana kuwa halali, na kumbuka kwamba mashirika halali ya kifedha hayawezi kukuomba utume habari za kibinafsi kupitia barua-pepe. Kabla ya kununua chochote au kuwekeza pesa kupitia Intaneti, hakikisha kwamba kampuni hiyo ni halali. “Mtu asiye na uzoefu huamini kila neno, lakini mtu mwerevu huzifikiria hatua zake,” inasema Methali 14:15. Uwe mwangalifu sana unaposhughulika na kampuni zilizo katika nchi nyingine. Inaweza kuwa vigumu sana kutatua matatizo yanapotokea.

  • Chunguza kampuni na sera zake. Jiulize: ‘Ofisi za kampuni hii ziko wapi? Je, nambari yao ya simu ni sahihi? Je, bidhaa ninazonunua zitakuwa na gharama nyingine za ziada ambazo hazijaonyeshwa? Bidhaa hizo zitaletwa lini? Ninaweza kuzirudisha au kurudishiwa pesa?’

  • Tahadhari ikiwa unaahidiwa faida kubwa kuliko ilivyo kawaida. Watu wenye pupa na wanaotaka vitu vya bwerere ndio hasa hulengwa na wezi wanaotumia Intaneti. Huenda mtego ukatia ndani kupata pesa nyingi kwa kazi kidogo, kupewa mkopo au kadi ya mkopo hata ikiwa hustahili kuipata, au uwekezaji ambao utakuletea faida kubwa sana. Tume ya Biashara ya Marekani (FTC) inasema: “Uwe makini sana unapochunguza ikiwa uwekezaji uliotangazwa ni halali. Ikiwa unaahidiwa faida kubwa sana, hasara itakuwa kubwa sana. Usiruhusu mtu yeyote akushinikize uwekeze kabla ya kuwa na uhakika kwamba biashara hiyo ni halali.”

KUIBIWA UTAMBULISHO

Kunahusisha nini? Kuibiwa utambulisho kunahusisha kupata habari za mtu kwa njia isiyo halali na kuzitumia kulaghai au kufanya uhalifu mwingine.

Kunawaathirije watu? Wezi wanaweza kutumia utambulisho wako kupata kadi za mkopo au kupata mikopo au kufungua akaunti mpya. Kisha wanakusanya madeni wakitumia jina lako! Hata ikiwa mwishowe utafaulu kufanya madeni hayo yafutiliwe mbali, sifa yako kuhusiana na mambo ya kifedha itakuwa imeharibiwa kwa miaka kadhaa. Mtu mmoja aliyeibiwa utambulisho wake anasema hivi: “Kuwa na sifa ya kutolipa madeni huathiri maisha yako—sifa hiyo ni mbaya sana hata kuliko kunyang’anywa pesa.”

Unaweza kufanya nini?

  • Linda habari zako za siri. Ikiwa wewe hufanya shughuli zako za benki au hununua vitu kupitia Intaneti, badilisha maneno yako ya siri mara kwa mara, hasa baada ya kutumia kompyuta ya umma. Kama ilivyotajwa  awali, tilia shaka barua-pepe zinazokuomba habari za kibinafsi.

    Wezi wa utambulisho hawatumii kompyuta peke yake. Wao hujaribu kila wawezalo kupata hati muhimu kama vile stetimenti za benki, vitabu vya hundi, kadi za mikopo, na nambari yako ya kitambulisho. Kwa hiyo, weka hati hizo mahali salama, na rarua kabisa habari zote muhimu kabla ya kuzitupa. Bila shaka, ikiwa unashuku umepoteza hati fulani au imeibiwa, taarifu wenye mamlaka mara moja.

  • Chunguza akaunti zako mara kwa mara. “Kuwa macho ndiyo silaha yenye nguvu zaidi dhidi ya . . . wizi wa utambulisho,” inasema FTC, ikiongezea, “Kugundua mapema kwamba utambulisho umeibiwa kunaweza kuzuia hasara kubwa.” Kwa hiyo chunguza stetimenti zako za benki kwa ukawaida, angalau kila mwezi, na uangalie ikiwa kuna utendaji wowote usio wa kawaida.

Bila shaka, huenda ukapatwa na lolote katika ulimwengu wa leo. Hata watu waangalifu sana wamepatwa na uhalifu. Kwa sababu hiyo, sikuzote sisi hufaidika ikiwa tutafuata hekima na uelewaji unaopatikana katika Biblia. “Usiiache, nayo itakutunza. Ipende, nayo itakulinda.” (Methali 4:6) Jambo zuri hata zaidi ni kwamba Biblia inaahidi kwamba uhalifu utakoma.

Karibuni Uhalifu Utakoma

Kwa nini tunaweza kuwa na uhakika kwamba Mungu ataondoa uhalifu? Fikiria mambo yafuatayo:

  • Mungu anataka kukomesha uhalifu. “Mimi, Yehova, napenda haki, nachukia unyang’anyi pamoja na ukosefu wa uadilifu.”—Isaya 61:8.

  • Ana uwezo wa kukomesha uhalifu. “Uwezo na uadilifu wake ni mkuu, amejaa wema wala hapotoshi haki kamwe.”—Ayubu 37:23, Biblia Habari Njema.

  • Ameahidi atawaharibu waovu na kuwahifadhi waadilifu. “Watenda-maovu watakatiliwa mbali.” “Waadilifu wenyewe wataimiliki dunia, nao watakaa milele juu yake.”—Zaburi 37:9, 29.

  • Amewaahidi washikamanifu wake kwamba kutakuwa na ulimwengu mpya wenye amani. “Wapole wataimiliki dunia, nao watapata furaha yao tele katika wingi wa amani.”—Zaburi 37:11.

Je, maneno hayo yanagusa moyo wako? Ikiwa ndivyo, tafadhali tenga wakati wa kuisoma Biblia ili ujifunze mengi kuhusu kusudi la Mungu kwa wanadamu. Hakuna kitabu kingine kilicho na hekima nyingi kuliko Biblia. Hakuna kitabu kingine kinachotoa tumaini la kuwa na ulimwengu usio na uhalifu wakati ujao. *

Mungu anaahidi ulimwengu mpya wenye amani ambao hautakuwa na uhalifu

^ fu. 5 Majina yamebadilishwa.

^ fu. 22 Watu wengi walioshambuliwa kingono wanamjua aliyewashambulia. Kwa habari zaidi, ona “Ninawezaje Kujilinda na Washambuliaji wa Kingono?” kwenye ukurasa wa 228 wa kitabu Maswali Ambayo Vijana Huuliza—Majibu Yafanyayo Kazi, Buku la 1. Kitabu hiki kinapatikana pia kwenye tovuti ya www.jw.org/sw.

^ fu. 44 Habari zaidi kuhusu mafundisho muhimu ya Biblia inaweza kupatikana katika kitabu Biblia Inafundisha Nini Hasa? Pata nakala yako bila malipo kutoka kwa Mashahidi wa Yehova, au kisome kwenye Tovuti ya www.jw.org/sw.