Hamia kwenye habari

Je, Biblia Ilitabiri Mitazamo na Matendo ya Watu Leo?

Je, Biblia Ilitabiri Mitazamo na Matendo ya Watu Leo?

Jibu la Biblia

 Ndiyo, Biblia ilitabiri kwamba katika siku zetu, watu kwa ujumla wangekuwa wabaya zaidi. Ilionyesha kwamba badiliko hilo lingewafanya watu wengi zaidi wapuuze viwango vya maadili vinavyowawezesha wanadamu kuishi kwa upatano. a (2 Timotheo 3:1-5) Biblia ilitabiri pia kwamba si watu wote ambao wangeathiriwa na mtazamo huo. Badala yake, kwa msaada wa Mungu wangejitahidi kushinda uvutano mbaya uliopo na wangejifunza kufikiri na kutenda kulingana na mapenzi yake.—Isaya 2:2, 3.

Katika makala hii

 Biblia ilitabiri nini kuhusu mitazamo na matendo ya watu leo?

 Biblia inafafanua mitazamo na matendo yasiyofaa ya aina mbalimbali yanayochochewa na ubinafsi ambayo yangekuja kuwa ya kawaida. Watu wangekuwa “wasiojizuia,” “wenye kujipenda wenyewe” na “wanaopenda raha badala ya kumpenda Mungu.”—2 Timotheo 3:2-4.

 Leo, unabii huo umetimizwa kwa kuwa watu wa siku hizi wanajifikiria kupita kiasi, wanajitanguliza, wanafikiria zaidi kujitosheleza, kujipendeza, na mambo kama hayo yanayowafanya wajihisi wana kusudi maishani. Tabia hizo ni za kawaida sana siku hizi hivi kwamba kuna vikundi vya watu wanaoitwa Kizazi cha Mimi Kwanza. Watu wengi wanajipenda sana wenyewe hivi kwamba ‘hawapendi wema,’ yaani, hawana uwezo wa kupenda sifa nzuri. Wamekuwa “wasio na shukrani,” hivi kwamba hawaoni umuhimu wa kuonyesha shukrani kwa ajili ya vitu walivyo navyo au mambo ambayo watu wengine wanawafanyia.—2 Timotheo 3:2, 3.

 Ubinafsi ndiyo chanzo cha mitazamo yote ambayo ni ishara ya siku zetu:

  •   Pupa. “Kupenda pesa” limekuwa jambo la kawaida, mara nyingi watu wanapima mafanikio yao maishani kupitia uwezo wao wa kifedha au mali zao.—2 Timotheo 3:2.

  •   Kiburi. Watu wengi ni “wenye kujidai, wenye majivuno,” na “waliojaa kiburi.” (2 Timotheo 3:2, 4) Wao hujisifu na kutia chumvi kuhusu uwezo, sifa, au utajiri wao.

  •   Uchongezi. “Wakufuru” na “wachongezi” wanapatikana kila mahali. (2 Timotheo 3:2, 3) Maneno hayo yanarejelea wale wanaowadhihaki watu wengine au kumdhihaki Mungu au wanaosema uwongo kuwahusu.

  •   Ukaidi. Watu wengi ‘si washikamanifu,’ ‘hawataki makubaliano yoyote,’ “wasaliti,” na “wenye vichwa vigumu.” (2 Timotheo 3:2-4) Wanaonyesha sifa hizo mbaya kwa kukataa kusikiliza maoni ya wengine, kusuluhisha mambo, au kutimiza ahadi walizoweka awali.

  •   Jeuri. Watu wengi leo ni “wakali,” wasiozuia hasira, na mara nyingi wanawatendea wengine kwa ukatili sana.—2 Timotheo 3:3.

  •   Uasi sheria. Yesu alitabiri kwamba kutakuwa na ‘ongezeko la uasi sheria’ katika siku zetu. (Mathayo 24:12) Alitabiri pia kuenea kwa “machafuko” au “misukosuko.”—Luka 21:9, maelezo ya chini.

  •   Kukosa upendo katika familia. Wale “wasiotii wazazi” na “wasio na upendo wa asili [katika familia]” wamefanya kuwe na ongezeko la watu wasiotunza familia zao, wanaowatenda vibaya na kwa ukatili watu wa familia.—2 Timotheo 3:2, 3.

  •   Unafiki wa kidini. Idadi ya watu ‘wanaoonekana kama watu wanaomwogopa Mungu’ inazidi kuongezeka. (2 Timotheo 3:5) Lakini badala ya kujitiisha na kufanya mapenzi ya Mungu, wanafuata viongozi wa kidini ambao wanawaambia mambo wanayotaka kusikia.—2 Timotheo 4:3, 4.

 Watu wenye ubinafsi wangewaathirije wengine?

 Kwa sababu watu wengi ni wabinafsi, kuna watu wengi sana wanaougua kiakili na kihisia kuliko wakati mwingine wowote. (Mhubiri 7:7) Kwa mfano, baadhi ya watu ambao ni wenye kupenda pesa wanawatumia wengine vibaya ili kujifaidi wenyewe. Watu ambao hawana upendo wa asili wanawatenda vibaya watu wa familia, jambo linalowaathiri kihisia na kuwafanya washuke moyo au kujiua. Na kila msaliti au mtu asiye mshikamanifu anawasababishia wengine uchungu mwingi wa kihisia. Uchungu huo si rkahisi kusahau.

 Kwa nini watu kwa ujumla wangekuwa wabaya?

 Biblia inafafanua sababu zinazotokeza mielekeo hii:

  •   Upendo wa kweli kumwelekea Mungu na jirani unapungua. (Mathayo 24:12) Na kadiri unavyopungua, ubinafsi unazidi kuongezeka.

  •   Shetani Ibilisi amefukuzwa mbinguni na kutupwa duniani. (Ufunuo 12:9, 12) Tangu wakati huo, uvutano wake mwovu, wenye ubinafsi umeenea hata zaidi.—1 Yohana 5:19.

 Tunapaswa kutendaje kadiri watu wanavyozidi kuwa wabaya?

 Neno la Mungu linasema hivi: “Jiepushe nao.” (2 Timotheo 3:5) Hilo halimaanishi tujitenge mbali na jamii. Badala yake, tunapaswa kuepuka kuwa na urafiki wa karibu na wale wanaoishi maisha yenye ubinafsi, bila kumtegemea Mungu.—Yakobo 4:4.

 Je, watu wote watakuwa wabaya?

 Hapana. Biblia ilitabiri kwamba kungekuwa na watu “wanaolia kwa uchungu na kwa maumivu makali kwa sababu ya mambo yote yanayochukiza yanayofanywa.” (Ezekieli 9:4) Watu hao wangekataa roho ya ubinafsi na kuruhusu viwango vya Mungu viongoze maisha yao. Maneno na matendo yao yangekuwa tofauti kabisa na ya watu wengine kwa ujumla. (Malaki 3:16, 18) Kwa mfano, wangejitahidi kudumisha amani na watu wote na wangekataa kujiunga na vita na jeuri.—Mika 4:3.

 Je, hatimaye jamii ya wanadamu itasambaratika?

Hapana. Jamii ya wanadamu haitakuwa mbaya kiasi cha kwamba kusiwe na amani na mpangilio wowote. Badala yake, hivi karibuni Mungu atawaondoa watu ambao wamekusudia kukiuka viwango vyake. (Zaburi 37:38) Atatokeza “dunia mpya,” yaani, jamii mpya ya wanadamu itakayoishi hapa duniani, na watu wapole wataishi kwa amani milele. (2 Petro 3:13; Zaburi 37:11, 29) Tumaini hilo si ndoto tu. Hata sasa, Biblia inawasaidia watu kubadili mwenendo wao na kuanza kuishi kupatana na mapenzi ya Mungu ya uadilifu.—Waefeso 4:23, 24.

a Unabii wa Biblia na hali mbaya zilizopo ulimwenguni zinaonyesha kwamba tunaishi katika “siku za mwisho,” ambazo zingekuwa nyakati za “hatari” au za “taabu.” (2 Timotheo 3:1; Biblia Habari Njema) Ili kupata habari zaidi, ona makala yenye kichwa: “Ni Nini Ishara ya “Siku za Mwisho”?