Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Tuteseke?

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Tuteseke?

Vijana Huuliza . . .

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Tuteseke?

“Mungu yuko juu mbinguni mahali ambapo kila kitu ni kizuri, na sisi huku chini tunateseka.”—Mary. *

VIJANA wa leo wamezaliwa katika ulimwengu mkatili. Matetemeko ya ardhi na misiba ya kiasili ambayo huua maelfu ya watu huonwa kuwa mambo ya kawaida. Vita na mashambulizi ya kigaidi huripotiwa sana katika vyombo vya habari. Magonjwa, uhalifu, na misiba huua wapendwa wetu. Mary, aliyenukuliwa juu, alikumbwa na msiba. Alisema maneno hayo kwa uchungu baada ya kifo cha baba yake.

Tunapokumbwa na msiba, ni kawaida kufadhaika, kuhisi pengo maishani, au hata kukasirika. Huenda ukajiuliza hivi, ‘Kwa nini jambo hilo limetukia?’ ‘Kwa nini limenipata?’ au ‘Kwa nini limetukia sasa?’ Maswali hayo yanahitaji majibu yenye kuridhisha. Lakini ili tupate majibu sahihi, tunapaswa kuyatafuta mahali panapofaa. Kama vile kijana anayeitwa Turrell alivyosema, nyakati nyingine watu “huumia sana hivi kwamba hawawezi kufikiri vizuri.” Hivyo, huenda ukahitaji kupata njia ya kujituliza ili uweze kufikiri vizuri.

Kukabili Hali Ngumu

Huenda ikawa vigumu kukubali kwamba kifo na kuteseka ni mambo ya kawaida maishani. Ayubu alisema hivi kwa kufaa: “Mwanadamu, aliyezaliwa na mwanamke, ana maisha mafupi na yenye kujaa msukosuko.”—Ayubu 14:1.

Biblia inaahidi ulimwengu mpya ambapo “uadilifu utakaa.” (2 Petro 3:13; Ufunuo 21:3, 4) Hata hivyo, kabla mambo hayo mazuri yatimie, lazima wanadamu wavumilie uovu mwingi. Biblia inasema hivi: “Ujue jambo hili, ya kwamba katika siku za mwisho kutakuwa na nyakati za hatari zilizo ngumu kushughulika nazo.”—2 Timotheo 3:1.

Hali hizo ngumu zitaendelea mpaka lini? Wanafunzi wa Yesu waliuliza swali kama hilo. Lakini, Yesu hakuwapa siku wala saa hususa ambapo mfumo huu wa mambo wenye taabu nyingi utakoma. Badala yake, Yesu alisema: “Yule ambaye atavumilia mpaka mwisho ndiye atakayeokolewa.” (Mathayo 24:3, 13) Maneno ya Yesu yanatutia moyo tuwe na maoni yenye usawaziko. Ni lazima tuwe tayari kuvumilia hali ngumu kabla ya mwisho kuja.

Je, Tumlaumu Mungu?

Je, ni jambo la akili kumkasirikia Mungu kwa sababu ameruhusu tuteseke? Sivyo, ukikumbuka kwamba Mungu ameahidi kumaliza mateso yote. Si jambo la akili pia kuwa na maoni ya kwamba Mungu ndiye anayesababisha magumu yote. Misiba mingi ni tokeo la mambo yasiyotazamiwa. Kwa mfano, wazia upepo ukiangusha mti na kumjeruhi mtu. Huenda watu wakasema kwamba hilo ni tendo la Mungu. Lakini Mungu hakuuangusha mti huo. Biblia inasema kwamba mambo hayo yamesababishwa na “wakati na tukio lisilotazamiwa.”—Mhubiri 9:11.

Huenda pia tukaathiriwa na maamuzi mabaya. Kwa mfano, vijana wanaweza kuendesha gari wakiwa wamelewa, kisha msiba wa barabarani utokee. Ni nani anayepaswa kulaumiwa? Ni Mungu? La, vijana hao wamepata matokeo ya maamuzi yao mabaya.—Wagalatia 6:7.

Huenda ukauliza, ‘Je, Mungu hana uwezo wa kukomesha mateso sasa?’ Watu fulani waaminifu wakati wa Biblia walijiuliza hivyo. Nabii Habakuki alimuuliza Mungu hivi: “Kwa nini unawatazama wale wanaotenda kwa hila, na kukaa kimya wakati mtu mwovu anapommeza mtu aliye mwadilifu kuliko yeye?” Hata hivyo Habakuki hakukata kauli haraka-haraka. Alisema hivi: “Nitaendelea kuangalia, ili kuona atakaloniambia.” Baadaye Mungu akamhakikishia kwamba katika “wakati uliowekwa,” angemaliza mateso. (Habakuki 1:13; 2:1-3) Hivyo, tunapaswa kuwa na subira tukimngojea Mungu amalize uovu kwa wakati wake uliowekwa.

Epuka kukata kauli haraka kwamba Mungu anataka tuteseke au anatujaribu. Ni kweli kwamba mateso yanaweza kutusaidia tusitawishe sifa nzuri na Biblia inasema kwamba majaribu ambayo Mungu anaruhusu yatupate yanaweza kuboresha imani yetu. (Waebrania 5:8; 1 Petro 1:7) Watu wengi wanaopata majaribu au hali za kuhuzunisha husitawisha subira na huruma. Lakini hatupaswi kukata kauli kwamba Mungu ndiye anayewafanya wateseke. Mawazo hayo hayaonyeshi kwamba tunamwona Mungu kuwa mwenye upendo na hekima. Biblia inasema hivi waziwazi: “Mtu akiwa chini ya jaribu, yeye asiseme: ‘Mungu ananijaribu.’ Kwa maana Mungu hawezi kujaribiwa na mambo maovu wala yeye mwenyewe hamjaribu yeyote.” Badala yake, “kila zawadi njema na kila tuzo kamilifu” hutoka kwa Mungu!—Yakobo 1:13, 17.

Kwa Nini Mungu Anaruhusu Uovu?

Basi, ni nani anayesababisha uovu? Kumbuka kwamba Mungu ana wapinzani, hasa ‘yule anayeitwa Ibilisi na Shetani, anayeipotosha dunia nzima inayokaliwa.’ (Ufunuo 12:9) Mungu aliwaweka wazazi wetu wa kwanza Adamu na Hawa katika ulimwengu usio na matatizo. Lakini Shetani alimwambia Hawa kwamba angeishi vizuri bila kuongozwa na Mungu. (Mwanzo 3:1-5) Kwa kusikitisha, Hawa aliamini uwongo wa Shetani na kumwasi Mungu. Adamu alijiunga naye katika uasi huo. Matokeo yakawa nini? Biblia inasema: “Kifo kikaenea kwa watu wote.”—Waroma 5:12.

Badala ya kumaliza uasi huo kwa kumharibu Shetani na wafuasi wake, Mungu aliona ni vema aruhusu wakati upite. Hilo lingetimiza nini? Jambo moja ni kwamba ingethibitika kuwa Shetani ni mwongo! Pia ingethibitika kwamba kuishi bila mwongozo wa Mungu kungetokeza tu matatizo. Je, hivyo sivyo mambo yalivyo? “Ulimwengu mzima unakaa katika nguvu za yule mwovu.” (1Yohana 5:19) Isitoshe, “mwanadamu amemtawala mwanadamu kwa kumuumiza.” (Mhubiri 8:9) Dini zinafundisha mambo yanayopingana. Maadili yamezorota kuliko wakati mwingine wowote. Serikali za wanadamu zimejaribu kila aina ya utawala. Wametia sahihi mikataba na kutunga sheria, lakini bado watu wa kawaida hawajatimiziwa mahitaji yao. Vita vimeleta mateso zaidi na zaidi.

Ni wazi kwamba Mungu anahitaji kuingilia kati na kukomesha uovu! Lakini atafanya hilo kwa wakati wake. Mpaka wakati huo, tuna pendeleo la kuunga mkono utawala wa Mungu kwa kutii sheria na kanuni zake zinazopatikana katika Biblia. Mambo mabaya yanapotukia, tunaweza kufarijiwa na tumaini la kuishi katika ulimwengu usio na matatizo.

Si Wewe Tu Unayeathirika

Tunapoteseka, huenda tukajiuliza, ‘Kwa nini ninateseka?’ Hata hivyo, mtume Paulo anatukumbusha kwamba sio sisi tu tunaoteseka. Paulo anasema kwamba “uumbaji wote unaendelea kuugua pamoja na kuwa katika maumivu pamoja mpaka sasa.” (Waroma 8:22) Kujua jambo hilo kunaweza kukusaidia ukabiliane na mateso. Kwa mfano Nicole alifadhaishwa na mashambulizi ya kigaidi ya Septemba 11, 2001, huko New York City na Washington, D.C. Anasema hivi: “Niliogopa sana.” Lakini aliposoma masimulizi ya jinsi Wakristo wenzake walivyokabiliana na msiba huo, mtazamo wake ulibadilika. * “Nilitambua kwamba sikuwa peke yangu kamwe. Pole kwa pole maumivu na huzuni yangu ilianza kutoweka.”

Wakati mwingine inafaa uzungumze na mtu kama vile mzazi, mtu aliyekomaa, au mzee Mkristo. Ukimwambia mtu unayemwamini hisia zako unaweza kupata “neno jema” lenye kufariji. (Methali 12:25) Kijana Mkristo Mbrazili anasema hivi: “Baba yangu alikufa miaka tisa iliyopita na ninajua Yehova atamfufua siku moja. Nilijihisi vizuri nilipoandika jinsi nilivyohisi. Pia nilizungumza waziwazi na rafiki zangu Wakristo.” Je, una ‘marafiki wa kweli’ ambao unaweza kuzungumza nao? (Methali 17:17) Basi omba msaada wao wenye upendo! Usiogope kulia au kuonyesha hisia zako. Hata Yesu ‘alitokwa na machozi’ alipofiwa na rafiki yake!—Yohana 11:35.

Biblia inatuhakikishia kwamba siku moja ‘tutawekwa huru kutoka katika utumwa wa uharibifu’ na kufurahia “uhuru wenye utukufu wa watoto wa Mungu.” (Waroma 8:21) Kabla ya wakati huo, watu wengi wazuri watateseka. Farijika kwa kujua kinachosababisha mateso na kwamba hayataendelea kwa muda mrefu.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Baadhi ya majina yamebadilishwa.

^ fu. 20 Ona mfululizo wenye kichwa “Ujasiri Wakati wa Msiba,” katika toleo la Amkeni! la Januari 8, 2002.

[Picha katika ukurasa wa 14]

Huenda ukajihisi vizuri ukionyesha huzuni yako