Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Kitu Bora Kuliko Marekebisho

Kitu Bora Kuliko Marekebisho

Kitu Bora Kuliko Marekebisho

MTI ukizaa matunda yasiyofaa, hauwezi kuboreshwa kwa kukata matawi machache. Lazima mti wenyewe ukatwe na mizizi yake ing’olewe. Kisha mti mwingine upandwe, ambao unazaa matunda mazuri.—Mathayo 7:16-20.

Vivyo hivyo, hata watetezi wa marekebisho wenye malengo mazuri hushughulikia tu dalili za matatizo yanayokumba jamii, yaani, ufisadi, ukosefu wa haki, umaskini, na unyang’anyi. Lakini, kisababishi ni tofauti. Mfumo wote unapaswa kubadilishwa. Hilo ndilo Biblia inaahidi.

Ufalme wa Mungu ni serikali ya mbinguni ambayo itafanya mengi zaidi ya kurekebisha na kupanga upya jamii. Serikali hiyo itaanzisha njia mpya ya kuendesha shughuli za wanadamu na kuwaunganisha wanadamu wote chini ya utawala wake. Serikali hiyo itashughulikia mambo kama vile elimu, kazi, makao, chakula, afya, na mazingira.

Zaburi 72:12-14 inatoa unabii juu ya yale ambayo Mfalme wa Kimasihi atawafanyia wanadamu: “Atamkomboa maskini anayelilia msaada, pia mwenye kuteseka na yeyote ambaye hana msaidizi. Atamsikitikia mtu wa hali ya chini na maskini, naye ataziokoa nafsi za maskini. Ataikomboa nafsi yao kutoka katika ukandamizaji na katika jeuri.”

Lakini ikiwa ufisadi, ukosefu wa haki, na umaskini utakomeshwa kabisa, serikali na watu wanapaswa kubadilika. Hivyo, Ufalme huo utampa kila mtu mwongozo ili awe na maisha yenye furaha, yenye kusudi, na yenye kuridhisha. Biblia inaahidi kwamba Ufalme wa Mungu utawasaidia raia zake walio duniani kujibadilisha. Vipi?

Ufalme huo utawafundisha raia zake matakwa ya Yehova Mungu, hivyo ukiwasaidia kusitawisha imani na upendo. (Isaya 11:9) Kumpenda Mungu huchochea moyo wa mtu kutenda. Kwa mfano, katika karne ya kwanza, Yesu alikutana na Zakayo, mkusanya-kodi mkuu, ambaye alikuwa akijitajirisha kwa kuongeza kodi kiharamu. Yesu hakuanza kumwaibisha afisa huyo mfisadi ili abadilike. Badala yake, Yesu alimsaidia Zakayo kutambua makosa yake na kutubu. Zakayo alichochewa kwa kumpenda Mungu na kwa ujuzi sahihi wa kanuni zake. Alifanya mabadiliko makubwa.—Luka 19:1-10.

Je, hilo si suluhisho bora kwa matatizo ya jamii? Serikali kamilifu yenye uadilifu ambayo itashughulikia hali za wanadamu huku kila mtu akisaidiwa kubadili matendo yake! Je, wakati huo tutahitaji marekebisho katika jamii? Hayatahitajiwa tena, kwa kuwa Mungu atakuwa amefanya vitu vyote kuwa vipya. Mambo ya zamani yatakuwa yamepitilia mbali.—Ufunuo 21:4, 5.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Ufalme wa Mungu utaleta mabadiliko ya kudumu wala si marekebisho

[Picha katika ukurasa wa 11]

Yesu alipokuwa duniani aliwasaidia watu kufanya mabadiliko maishani