Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Namna Uwezavyo Kusaidia

Namna Uwezavyo Kusaidia

Namna Uwezavyo Kusaidia

“Watoto walioshuka moyo wanahitaji msaada. Lakini watoto hawawezi kujitafutia msaada. Ni lazima kwanza mtu mzima atambue tatizo hilo na kulichukua kwa uzito. Hilo ndilo jambo gumu.”—Dakt. Mark S. Gold.

WAWEZA kufanya nini ukishuku kwamba tineja wako ameshuka moyo? Kwanza, usikate kauli mara moja kuhusu jambo hilo. Kwani, dalili unazoona zaweza kuwa ni za tatizo lingine. * Na zaidi, vijana wote huhuzunika pindi kwa pindi. Lakini iwapo hali hiyo yaendelea na yaonekana kuwa ni tatizo kubwa zaidi ya kule kuhuzunika kwa kawaida, itakuwa vema kumwona daktari. Kwa habari hii, yafaa kukumbuka maneno ya Yesu: “Watu wenye afya hawahitaji tabibu, bali wenye kuugua wahitaji.”—Mathayo 9:12.

Mtajie daktari wako waziwazi habari zozote zitakazosaidia, kutia ndani mabadiliko yoyote ya hivi karibuni katika maisha ya tineja huyo ambayo huenda yanamfanya alegee. Hakikisha kwamba daktari amesikiliza dalili zenyewe kwa muda mrefu vya kutosha kabla ya kubainisha ugonjwa. Dakt. David G. Fassler aonya hivi: “Haiwezekani kukusanya habari zote zinazohitajiwa ili kutambua ugonjwa wa mtoto katika kipindi kimoja cha dakika ishirini tu.”

Muulize daktari maswali yoyote uliyo nayo waziwazi. Kwa mfano, iwapo daktari akuambia kwamba tineja wako ameshuka moyo sana, huenda ukataka kuuliza ni kwa nini anafikiri hivyo wala si vinginevyo. Iwapo unashuku uchunguzi wa daktari, mwambie ungependa kupata maoni ya mtaalamu mwingine. Kwa wazi, daktari yeyote mnyoofu na mwaminifu hatakupinga usifanye hivyo.

Kukubali na Kukabili Hali Yenyewe

Kwa hakika, iwapo tineja wako ameshuka moyo sana, usiaibike eti kwa sababu ana ugonjwa huo. Ukweli ni kwamba vijana wazuri sana waweza kushuka moyo. Kwa kweli, Biblia huonyesha kwamba watu fulani waliojitahidi sana kumtumikia Mungu waliumia kihisia, haidhuru umri wao. Fikiria mfano wa Yobu mwaminifu, aliyehisi kwamba Mungu alikuwa amemwacha na akachukia kuishi. (Ayubu 10:1; 29:2, 4, 5) Hana alikuwa mtumishi wa Mungu aliyekuwa na “uchungu rohoni mwake” hivi kwamba hakuweza kula. (1 Samweli 1:4-10) Kisha kuna yule mtumishi wa Mungu, Yakobo, aliyeomboleza kwa siku nyingi baada ya kifo cha mwanaye na “akakataa kutulizwa.” Kwani, hata Yakobo alisema jinsi alivyotamani kujiunga na mwanaye kaburini! (Mwanzo 37:33-35) Kwa hiyo, mfadhaiko hausababishwi sikuzote na udhaifu wa kiroho.

Hata hivyo, tineja anaposhuka moyo wazazi waweza kuteseka sana. “Lazima niwe mwangalifu sana nisimuumize hisia,” asema mama ya tineja aliyeshuka moyo. “Nina wasiwasi, ninaogopa, ninakuwa mkatili, ninakasirika na kuchoka.” Mwingine akiri hivi: “Nilipoenda madukani na kumwona mama akinunua vitu pamoja na bintiye tineja nilivunjika moyo kwa kuwa nilihisi kwamba singeweza kufanya hivyo pamoja na [binti yangu] tena kamwe.”

Kuhisi hivyo ni kawaida. Hata hivyo, nyakati nyingine hisia hizo zaweza kuvunja moyo sana. Hilo litukiapo, mbona usizungumze na rafiki unayemwamini? Mithali 17:17 husema: “Rafiki hupenda sikuzote; na ndugu amezaliwa kwa siku ya taabu.” Vilevile, usisahau kusali. Biblia hutuhakikishia kwamba tukimtwika Mungu mzigo wetu, atatutegemeza.—Zaburi 55:22.

Kulaumu-laumu

Wazazi wengi wa matineja walioshuka moyo huvunjika moyo sana na kuhisi kwamba walichangia hali hiyo kwa njia fulani. Mzazi mmoja akiri hivi: “Mtoto wako anaposhuka moyo, unajilaumu na hakuna awezaye kubadili maoni yako. Kila mara unajiuliza, ‘Tulikosea wapi? Tatizo lilianzia wapi? Mimi nilichangiaje tatizo hilo?’” Wazazi wanawezaje kufikiri ifaavyo wanapokabili hali hiyo?

Hapana shaka kwamba uhasama nyumbani waweza kumwathiri mtoto vibaya sana. Kwa kufaa, Biblia huwashauri akina baba hivi: “Msiwe mkichochea watoto wenu wakasirike, ili wasishuke moyo.” (Wakolosai 3:21) Hivyo basi, wazazi wapaswa kuchunguza jinsi wanavyoshughulika na watoto wao na kufanya marekebisho yahitajiwayo. Hata hivyo, kushuka moyo hakusababishwi kila mara na malezi mabaya. Kwa kweli, ugonjwa huo waweza kuwakumba hata wale walio katika nyumba zenye upendo mwingi. Kwa hiyo, wazazi wanaojitahidi wawezavyo kuwasaidia watoto wao, hawapaswi kujilaumu.

Vivyo hivyo, ni jambo la maana kutomlaumu tineja aliyeshuka moyo. Kwani, yamkini yeye hawezi kuudhibiti ugonjwa huo. “Singemlaumu kamwe kwa kuugua tetekuwanga na homa ya vichomi,” asema mama mmoja. “Lakini aliposhuka moyo nilimlaumu,” yeye akiri. “Nilimlaumu mtoto wangu kwa kuwa mgonjwa—hilo lanifanya nijihisi vibaya sana.” Wazazi wanapoona mshuko wa moyo kuwa ugonjwa badala ya udhaifu, hiyo itawasaidia wao na wengine kukazia fikira jinsi wawezavyo kumtegemeza mgonjwa.

Kumlea tineja aliyeshuka moyo kwaweza kutokeza mikazo mingi katika uhusiano wa wazazi. Mke mmoja asema hivi: “Tulilaumiana, hasa tulipofikiria kuhusu maisha tuliyokuwa tumetarajia kuishi na maisha tuliyoishi kwa sababu ya hali ya mwana wetu.” Tim, aliye na binti aliyeshuka moyo, akiri hivi: “Ni rahisi kumlaumu mwenzi wako. Endapo wazazi wana matatizo ya ndoa kabla mtoto hajaanza kuonyesha dalili za kushuka moyo, vitabia vya kiajabu-ajabu vya mtoto vyaweza kusababisha ndoa kuvunjika.” Usiruhusu mshuko wa moyo wa mtoto uvunje ndoa yenu! Kwa hakika, hakuna faida yoyote ya kulaumu-laumu—iwe ni kujilaumu, kumlaumu mtoto wako, au mwenzi wako. Jambo la maana ni kumtegemeza mgonjwa.

Kuandaa Utegemezo

Biblia yawashauri Wakristo hivi: “Semeni kwa kuliwaza nafsi zilizoshuka moyo.” (1 Wathesalonike 5:14) Iwapo kijana aliyeshuka moyo anaona kwamba hafai, unaweza kusaidia. Vipi? Bila shaka, si kwa kukata shauri mara moja hivi, “Hupaswi kuhisi hivyo” au, “Hupaswi kuwa na mtazamo huo.” Badala yake, jitahidi kuwa mwenye huruma kwa kuonyesha “hisia-mwenzi.” (1 Petro 3:8) Paulo aliwashauri Wakristo ‘watoe machozi pamoja na watu watoao machozi.’ (Waroma 12:15) Kumbuka kwamba mtu aliyeshuka moyo kabisa huumia kikweli. Maumivu yake si ya kujitungia, wala hajifanyi tu ili wengine wampe uangalifu. Baada ya kusikiliza, jaribu kumfanya mgonjwa ajieleze waziwazi. Muulize ni kwa nini anahisi hivyo. Kisha, msaidie tineja kwa upole na kwa subira aone ni kwa nini hapaswi kujiona kuwa hafai. Kumhakikishia juu ya upendo na rehema ya Mungu kutasaidia kupunguza mahangaiko ya mgonjwa.—1 Petro 5:6, 7.

Kuna mambo mengine unayoweza kufanya. Kwa mfano, huenda ikafaa uhakikishe kwamba tineja wako aliyeshuka moyo anapumzika, anakula, na kufanya mazoezi ya kutosha. (Mhubiri 4:6) Ikiwa daktari ampendekezea dawa fulani, ni jambo la hekima kumwonyesha tineja umuhimu wa kutumia dawa hizo. Usikate tamaa kamwe unapomtegemeza, na usiache kumpenda.

Pasipo shaka, tineja anaposhuka moyo, yeye na washiriki wengine wa familia hufadhaika. Mwishowe, sifa za subira, uvumilivu, na upendo zitakuwa msingi wa kuwasaidia matineja walioshuka moyo.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 3 Yasemekana kwamba magonjwa fulani—kutia ndani ongezeko lisilo la kawaida la chembe nyeupe za damu zenye kiini kimoja, ugonjwa wa sukari, upungufu wa damu, ugonjwa wa tezi ya koromeo, na kiwango cha chini cha sukari katika damu kuliko kawaida—yaweza kutokeza dalili zinazofanana na za kushuka moyo.

[Blabu katika ukurasa wa 11]

Mtu aliyeshuka moyo kabisa huumia sana. Maumivu si ya kujitungia

[Sanduku katika ukurasa wa 13]

IWAPO WEWE NI TINEJA ALIYESHUKA MOYO

Kuna watu wanaoweza kukusaidia, na una matumaini. Huenda umeshuka moyo kwa sababu ya (1) mvurugiko wa utendaji wa kemikali mwilini au (2) hali za maisha ambazo huwezi kuzidhibiti. Vyovyote vile, si wewe uliyejiletea hali hiyo. Hata hivyo, wapaswa kufanya nini kuhusu hali hiyo?

Biblia husema kwamba “yuko rafiki aambatanaye na mtu kuliko ndugu.” (Mithali 18:24) Mbona usitafute rafiki kama huyo na umweleze jinsi unavyohisi? Mzazi wako mmoja au mtu mwingine aliyekomaa aweza kuwa rafiki yako mkubwa unapopambana na mshuko wa moyo.

Wazazi wako wakishuku kwamba umeshuka moyo sana, huenda wakakupeleka kwa daktari aliye na ujuzi wa kutibu ugonjwa huo. Hilo ni jambo la hekima, kwani mara nyingi mshuko wa moyo waweza kupunguzwa sana kwa matibabu, mahala inapowezekana. Kwa mfano, iwapo kuna mvurugiko katika utendaji wa kemikali mwilini, dawa ya kupunguza mshuko wa moyo yaweza kupendekezwa. Iwapo una tatizo hilo, usione haya kutumia dawa. Dawa hiyo husaidia kiwango cha kemikali mwilini mwako kirudie tu hali ya kawaida, na hiyo yaweza kuwa njia ya kukusaidia kupata shangwe na nguvu maishani mwako.

Watu wengi walioshuka moyo wamefarijika kwa kusoma Biblia na kumkaribia Mungu kupitia sala. Biblia yatuhakikishia hivi: “Bwana yu karibu nao waliovunjika moyo, na waliopondeka roho huwaokoa.” *Zaburi 34:18.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 28 Kwa habari zaidi, ona makala “Vijana Huuliza . . . Je, Nimwambie Mtu Fulani Kwamba Nimeshuka Moyo?” katika gazeti la Amkeni! la Oktoba 22, 2000.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 14]

MSAADA NA TUMAINI KWA WALIOSHUKA MOYO

Kwa kuwa kushuka moyo ni suala tata, mfululizo huu mfupi wa makala haungeweza kuzungumzia mambo yote kuhusu ugonjwa huo. Hata hivyo, wachapishaji wa gazeti la Amkeni! wana uhakika kwamba hoja zilizotajwa zaweza kuwasaidia matineja na wazazi wao kuvumilia ugonjwa huo unaofadhaisha.

Huenda umetambua kwamba mawaidha mengi yaliyotolewa katika makala iliyotangulia yalitegemea Biblia. Kwa kweli, hicho ni kitabu cha kale. Hata hivyo, shauri lake latumika leo sawa na lilivyotumika ilipoandikwa. Kwa nini? Kwa sababu, japo hali zimebadilika, wanadamu hawajabadilika. Twakabili mambo yale yale ya msingi ambayo vizazi vilivyopita vilikabili. Tofauti ni kwamba sasa matatizo hayo ni mengi na yameenea sana.

Hata hivyo, kuna sababu nyingine inayofanya Biblia iweze kutumika sana: Imepuliziwa na Mungu. (2 Timotheo 3:16) Akiwa Muumba wetu, yeye ajua tunachohitaji ili kufurahia maisha kabisa.

Bila shaka, Biblia si kitabu cha kitiba. Hivyo, haituondolei uhitaji wa kutafuta matibabu yanayofaa kwa magonjwa, kama vile mshuko wa moyo. Hata hivyo, Biblia ina kanuni zinazoweza kutusaidia kuwafariji wanaougua. Zaidi ya hayo, ina ahadi ya Mungu kwamba hivi karibuni atatuponya magonjwa yetu yote. (Zaburi 103:3) Naam, Yehova akusudia “kuifufua mioyo yao waliotubu [“wanaopondwa,” NW].”—Isaya 57:15.

Je, wataka kujifunza zaidi kuhusu tumaini hilo tukufu? Tafadhali wasiliana na Mashahidi wa Yehova walio karibu nawe au uwaandikie kwa kutumia anwani ifaayo iliyoorodheshwa katika ukurasa wa 5 wa gazeti hili.

[Picha katika ukurasa wa 10]

Jitahidi kuonyesha hisia-mwenzi

[Picha katika ukurasa wa 11]

Iwapo tineja aendelea kushuka moyo, ni jambo la hekima kumwona daktari

[Picha katika ukurasa wa 12]

Ukiwa mzazi, usifanye haraka kujilaumu, kumlaumu mwenzi wako, au tineja wako