Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Mungu Alikubali Biashara ya Watumwa?

Je, Mungu Alikubali Biashara ya Watumwa?

Maoni ya Biblia

Je, Mungu Alikubali Biashara ya Watumwa?

WATU weusi wanaotiririka jasho na kuburuza miguu wanapanda ngazi ya mbao huku wakibeba mizigo mikubwa kupindukia ya marobota ya pamba. Wanyapara wasio na huruma wanawapiga kwa viboko. Watoto wanaopiga mayowe wananyakuliwa kinguvu kutoka mikononi mwa mama zao wanaolia machozi kisha wanauzwa kwa wale wanaolipa bei ya juu zaidi mnadani. Yamkini matendo hayo makatili na yenye kuhuzunisha yanakukumbusha kuhusu utumwa.

Jambo la ajabu ni kwamba wafanyabiashara wa watumwa na wamiliki wengi wa watumwa walisemekana kuwa watu walioshikilia dini sana. Mwanahistoria James Walvin aliandika hivi: “Kulikuwa na mamia ya watu kama hao, Wazungu na Wamarekani, waliomtukuza Bwana kwa baraka zake, na kutoa shukrani kwa mafanikio ya biashara huko Afrika, walipofunga safari kwa merikebu kuelekea Ulimwengu Mpya kwa kufuatana na pepo za msimu.”

Hata watu kadhaa wamesisitiza kwamba Mungu alikubali biashara ya watumwa. Kwa mfano, Alexander McCaine alisema katika hotuba kwenye Mkutano Mkuu wa Kanisa la Methodisti la Kiprotestanti mwaka wa 1842 kwamba utumwa “uliagizwa na Mungu Mwenyewe.” Je, McCaine alisema kweli? Je, Mungu alikubali wasichana watekwe na kubakwa, jamaa itenganishwe bila huruma, na watu wapigwe kikatili; mambo ambayo yalikuwa ya kawaida katika biashara ya watumwa ya siku za McCaine? Na namna gani wale mamilioni wanaoishi na kufanya kazi kama watumwa katika hali ngumu sana leo? Je, Mungu anakubali matendo hayo makatili?

Utumwa na Waisraeli

Biblia inasema kwamba ‘mtu mmoja anayo mamlaka juu ya mwenziwe kwa hasara yake.’ (Mhubiri 8:9) Maneno hayo ni ya kweli hasa inapohusu utumwa wenye kukandamiza wa aina mbalimbali ambao umeanzishwa na wanadamu. Yehova Mungu anawajali wale ambao wameteseka kwa sababu ya utumwa.

Kwa mfano, fikiria hali iliyowapata Waisraeli. Biblia inatuambia kwamba Wamisri “wakafanya maisha yao [Waisraeli] kuwa uchungu kwa kazi ngumu; kazi ya chokaa na ya matofali, na kila namna ya kazi ya mashamba; kwa kazi zao zote walizowatumikisha kwa ukali.” Waisraeli “wakaugua kwa sababu ya ule utumwa, wakalia; kilio chao kikafika juu kwa Mungu.” Je, Yehova aliwajali? Bila shaka. “Mungu akasikia kuugua kwao, Mungu akakumbuka agano lake alilolifanya na Ibrahimu na Isaka na Yakobo.” Isitoshe, Yehova aliwaambia watu wake hivi: “Nitawatoa ninyi mtoke chini ya mizigo ya Wamisri, nami nitawaokoa na utumwa wao.”—Kutoka 1:14; 2:23, 24; 6:6-8.

Kwa wazi, Yehova hakukubali ‘mtu mmoja awe na mamlaka juu ya mwenziwe’ katika utumwa wenye kukandamiza. Lakini, je, Mungu hakuwaruhusu watu wake kuwa na watumwa baadaye? Ndiyo. Hata hivyo, utumwa ulioruhusiwa huko Israeli ulikuwa tofauti sana na utumwa wenye kukandamiza ambao umekuwapo tangu zamani.

Sheria ya Mungu ilisema kwamba adhabu ya kumteka na kumuuza mtu ilikuwa kifo. Isitoshe, Yehova alitoa mwongozo ili kuwalinda watumwa. Kwa mfano, mtumwa aliyelemazwa na bwana wake angeachiliwa huru. Ikiwa mtumwa angekufa kwa sababu alipigwa na bwana wake, huyo bwana aliweza kuadhibiwa hukumu ya kifo. Wanawake watekwa walifanywa kuwa watumwa, au waliolewa na mabwana wao. Lakini haikuruhusiwa watumiwe vibaya ili kutosheleza tamaa ya ngono. Bila shaka, Sheria iliwaongoza Waisraeli wanyoofu wawatendee watumwa kwa heshima na fadhili, kana kwamba walikuwa wafanyakazi walioajiriwa.—Kutoka 20:10; 21:12, 16, 26, 27; Mambo ya Walawi 22:10, 11; Kumbukumbu la Torati 21:10-14.

Baadhi ya Wayahudi walikubali kwa hiari kuwa watumwa kwa Wayahudi wenzao ili walipe deni. Desturi hiyo ililinda watu wasione njaa na kuwasaidia watoke katika hali ya umaskini. Isitoshe, watumwa waliotaka uhuru walipaswa kuachiliwa katika pindi fulani kulingana na kalenda ya Wayahudi. * (Kutoka 21:2; Mambo ya Walawi 25:10; Kumbukumbu la Torati 15:12) Msomi Myahudi, Moses Mielziner, alisema hivi kuhusu sheria hizo zilizohusu watumwa: “Mtumwa alitendewa sikuzote kama mwanadamu, alionwa kuwa mtu mwenye haki fulani za asili ambazo hata bwana wake hangeweza kuziondoa bila kuadhibiwa.” Jambo hilo ni tofauti jinsi gani na mifumo mbalimbali ya utumwa yenye kukandamiza ambayo imekuwapo tangu zamani!

Utumwa na Wakristo

Wakristo wa karne ya kwanza waliishi chini ya mfumo wa uchumi wa Milki ya Roma ambao uliruhusu utumwa. Kwa hiyo, Wakristo fulani walikuwa watumwa na wengine walimiliki watumwa. (1 Wakorintho 7:21, 22) Lakini, je, hilo lilimaanisha kwamba wanafunzi wa Yesu walikandamiza watumwa wao? Hasha! Hata sheria ya Roma iwe iliruhusu nini, tunaweza kuwa na uhakika kwamba Wakristo hawakuwakandamiza wale waliokuwa chini ya mamlaka yao. Hata mtume Paulo alimhimiza Filemoni amtendee mtumwa wake Onesimo, aliyekuwa amekuwa Mkristo, kama “ndugu.” *Filemoni 10-17.

Biblia haitaji kamwe kwamba Mungu alikusudia wanadamu wafanye wanadamu wenzao kuwa watumwa. Isitoshe, hakuna unabii wowote ule katika Biblia unaodokeza kwamba wanadamu fulani watakuwa watumwa wa wanadamu wenzao katika ulimwengu mpya wa Mungu. Badala yake, katika Paradiso itakayokuja, wenye haki “wataketi kila mtu chini ya mzabibu wake, na chini ya mtini wake; wala hapana mtu atakayewatia hofu.”—Mika 4:4.

Biblia haikubali kwa vyovyote kutenda wengine vibaya kwa njia yoyote ile. Badala yake, inahimiza watu waheshimiane na kusiwe na ubaguzi miongoni mwa wanadamu. (Matendo 10:34, 35) Biblia inawasihi wanadamu kuwatendea wengine jinsi wanavyotaka kutendewa. (Luka 6:31) Isitoshe, Biblia inawahimiza Wakristo wawe wanyenyekevu na kuwaona wengine kuwa bora, bila kujali hali yao katika jamii. (Wafilipi 2:3) Kanuni hizo hazipatani kabisa na utumwa wenye kukandamiza ambao umekuwapo katika nchi nyingi katika karne za karibuni.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 11 Mpango wa Sheria ulioruhusu baadhi ya watumwa kubaki kwa bwana wao unaonyesha wazi kwamba watumwa hawakukandamizwa huko Israeli.

^ fu. 13 Baadhi ya Wakristo leo vilevile ni waajiri; wengine wameajiriwa kazi. Kama vile mwajiri Mkristo hawakandamizi wale wanaomfanyia kazi, wanafunzi wa Yesu katika karne ya kwanza waliwatendea watumishi wao kwa kupatana na kanuni za Kikristo.—Mathayo 7:12.