Hamia kwenye habari

Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Elimu?

Mashahidi wa Yehova Wana Maoni Gani Kuhusu Elimu?

 Maoni yetu kuhusu elimu yanategemea kanuni zilizo katika Biblia. Kila Shahidi hutumia dhamiri yake iliyozoezwa na Biblia kuamua jinsi atakavyotumia kanuni kutoka kwa Mungu. Zifuatazo ni baadhi yake. *

 Elimu ni muhimu

 Elimu inamsaidia mtu kusitawisha “hekima inayotumika na uwezo wa kufikiri,” sifa ambazo zinasifiwa sana na Biblia. (Methali 2:​10, 11; 3:​21, 22) Isitoshe, Yesu aliwaambia wafuasi wake wawe walimu wa mambo aliyowaamuru. (Mathayo 28:19, 20) Hivyo, tunawatia moyo na kuwasaidia wale walio kutanikoni wawe na elimu ya kutosha, inayotia ndani ustadi wa kusoma, kuandika, na kuwasiliana, * na vilevile kuelewa dini na tamaduni nyingine.​—1 Wakorintho 9:​20-​22; 1 Timotheo 4:​13.

 Serikali pia zimeona thamani ya elimu na mara nyingi zimeweka sheria kwamba vijana wanapaswa kupata masomo ya msingi na ya sekondari. Tunatii sheria hizo kupatana na amri hii: “Kila mtu na ajitiishe kwa mamlaka zilizo kubwa,” au serikali. (Waroma 13:1) Pia, tunawatia moyo watoto wetu wajitahidi sana shuleni na wafanye vema, wasiridhike tu kupata mambo ya msingi. * Kama vile Neno la Mungu linavyosema: “Kila mfanyacho, fanyeni kwa moyo wote, kwa sababu ya Bwana na si kwa ajili ya mtu.”​—Wakolosai 3:​23, Biblia Habari Njema.

 Elimu inatusaidia kuandalia familia zetu. Kulingana na Biblia, “ikiwa yeyote hawaandalii mahitaji watu wake mwenyewe, hasa watu wa nyumba yake, ameikana imani naye ni mbaya kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Elimu ya ulimwengu inatusaidia kutimiza wajibu wa Kimaandiko wa kuziandalia familia zetu. Kama kitabu The World Book Encyclopedia kinavyosema, kusudi moja kuu la elimu ni “kuwawezesha watu wafanikiwe katika jamii . . . kwa kufanya kazi kuchangia uchumi.” Mtu aliyesoma na mwenye ustadi fulani anaweza kuiandalia familia yake vizuri kuliko mtu asiye na ustadi wala elimu ya msingi.​—Methali 22:29.

 Wazazi pia wanawaandalia watoto wao kwa kuwapa kile watakachohitaji wakiwa watu wazima, na elimu ni muhimu kuhusiana na hilo. (2 Wakorintho 12:14) Tunawatia moyo wazazi wawaandalie watoto wao elimu hata ikiwa haitolewi bure, haipatikani kwa urahisi, au ni kinyume cha utamaduni wa jamii. * Pia tunawapa wazazi madokezo ya kuwasaidia wahusike katika masomo ya watoto wao. *

 Mtu anapaswa kuwa na maoni yenye usawaziko kuhusu elimu

 Tunachagua elimu kwa uangalifu. Biblia inasema: “Mjinga huamini kila neno, lakini mwerevu hutafakari kila hatua.” (Methali 14:15) Tunatumia kanuni hii kwa kuchunguza kwa uangalifu aina mbalimbali za elimu ya ziada inayopatikana, gharama yake, na faida ya elimu hiyo. Kwa mfano, chuo cha kiufundi mara nyingi kinatoa elimu yenye thamani kwa muda mfupi.

 Elimu ya kiroho ina thamani kubwa kuliko elimu ya ulimwengu. Tofauti na elimu ya ulimwengu, elimu ya Biblia inaandaa ujuzi wa Mungu unaookoa uhai. (Yohana 17:3) Pia inafundisha viwango vya maadili​—“lililo la uadilifu na la haki na lililo sawa, njia yote ya lililo jema.” (Methali 2:9) Mtume Paulo alipata elimu inayoweza kulinganishwa leo na elimu ya chuo kikuu, lakini alikiri kwamba kulikuwa na “thamani bora zaidi ya kumjua Kristo Yesu.” (Wafilipi 3:8; Matendo 22:3) Vivyo hivyo leo, Mashahidi wengi wa Yehova wamepata elimu ya juu ya ulimwengu, lakini wanaamini kwamba elimu yao ya kiroho ina thamani kubwa zaidi. *

Elimu ya kiroho inamfundisha mtu kuwa na viwango vya juu vya maadili

 Elimu ya juu inaweza kusababisha hatari za kiadili na za kiroho

 Methali ya Biblia inasema hivi: “Mtu mwerevu huona hatari na kujificha, lakini wajinga husonga mbele na kupata madhara.” (Methali 22:3) Mashahidi wa Yehova wanahisi kwamba mazingira katika baadhi ya vyuo vikuu na taasisi kama hizo za elimu ya juu yanaweza kuhatarisha hali ya kiroho na ya kiadili ya mtu. Kwa sababu hiyo, Mashahidi wengi wamechagua kutojiingiza au kuwaingiza watoto wao katika mazingira kama hayo. Wanahisi kwamba katika taasisi za elimu ya juu, mara nyingi mawazo yasiyo ya kweli kama haya yanaendelezwa:

  •   Maoni yasiyo sahihi: Pesa zinaleta furaha na usalama

     Mara nyingi elimu ya juu inatajwa kuwa njia hakika ya kupata kazi yenye mshahara mnono, hivyo wanafunzi wengi wanaenda chuo kikuu hasa ili kupata pesa. Wengine wanatumaini kwamba pesa zitawaletea furaha na usalama, lakini Biblia inafunua ubatili wa mawazo hayo. (Mhubiri 5:​10) Jambo la muhimu hata zaidi ni kwamba Biblia pia inafundisha kuwa “kupenda pesa ndicho chanzo cha mambo mabaya ya kila aina” na mara nyingi linaweza kufanya upoteze imani. (1 Timotheo 6:​10) Mashahidi wa Yehova wanafanya yote wawezayo kuepuka kunaswa na “nguvu za udanganyifu za utajiri.”​—Mathayo 13:22.

  •   Maoni yasiyo sahihi: Elimu ya juu itafanya uheshimiwe katika jamii

     Kwa mfano, Nika Gilauri, waziri mkuu wa zamani wa Georgia, aliandika hivi kuhusu mawazo ya kawaida nchini kwao: “Ili uheshimiwe nchini Georgia ni lazima uwe na cheti cha chuo kikuu. . . . [Wakati uliopita,] vijana ambao hawakuwa na vyeti hivyo walionwa kuwa wanaziabisha familia zao.” * Tofauti na hilo, Biblia inaonya dhidi ya kujitafutia makuu katika ulimwengu huu. Yesu aliwaambia hivi viongozi wa kidini waliotafuta umashuhuri katika siku zake: “Mnawezaje kuniamini, huku mkipeana utukufu ninyi wenyewe?” (Yohana 5:​44) Mazingira ya chuo kikuu yanaweza kumfanya mtu awe na roho ya kiburi, ambayo Mungu anachukia.​—Methali 6:​16, 17; 1 Petro 5:5.

  •   Maoni yasiyo sahihi: Kila mtu anapaswa kujiwekea viwango vya mema na mabaya

     Mashahidi wa Yehova wanakubali viwango vilivyowekwa na Mungu vya mema na mabaya. (Isaya 5:​20) Hata hivyo, kulingana na makala kwenye jarida Journal of Alcohol and Drug Education, wanafunzi wengi wanashinikizwa na wenzao katika chuo kikuu na hivyo “wanafanya maamuzi yaliyo kinyume na wanachojua kuwa sawa au makosa.” * Wazo hilo linapatana na kanuni hii ya Biblia: “Kushirikiana na watu wabaya huharibu tabia nzuri.” (1 Wakorintho 15:33) Katika mazingira ya chuo kikuu, mazoea ambayo Mungu hushutumu, kama ulevi, matumizi ya dawa za kulevya, na kufanya ngono nje ya ndoa, ni mambo ya kawaida na hata watu wanatiwa moyo kuyafanya.​—1 Wakorintho 6:​9, 10; 2 Wakorintho 7:1.

  •   Maoni yasiyo sahihi: Elimu ya juu ndiyo njia bora ya kuboresha ulimwengu

     Ni kweli kwamba wengi hufuatia elimu ya juu, si ili kupata utajiri, umashuhuri, au anasa, bali ni ili kuboresha maisha yao na ya ulimwengu. Hayo ni malengo mazuri, lakini Mashahidi wa Yehova wamechagua njia tofauti. Kama Yesu, tunauona Ufalme wa Mungu kuwa tumaini pekee la kuboresha ulimwengu. (Mathayo 6:​9, 10) Hata hivyo, hatuungoji tu Ufalme utatue matatizo ya ulimwengu bila kuchukua hatua yoyote. Badala yake, kama Yesu, tunahubiri “hii habari njema ya Ufalme” kotekote duniani, na kuwasaidia maelfu ya watu kila mwaka kuboresha maisha yao. *​—Mathayo 24:14.

^ Vijana Mashahidi wanaoishi nyumbani wanatii mwelekezo wa wazazi wao kuhusu elimu maadamu haupingani na sheria za Mungu.​—Wakolosai 3:​20.

^ Kwa sababu hiyo, tumechapisha nakala zaidi ya milioni 11 za vifaa vya kuwasaidia watu kusoma na kuandika kama broshua Jitahidi Kusoma na Kuandika. Na ulimwenguni pote tuna madarasa ya kuwafundisha watu kusoma na kuandika bila malipo katika lugha 120. Kati ya mwaka wa 2003 na 2017, tumewafundisha watu 70,000 hivi kusoma na kuandika.

^ Ona makala yenye kichwa “Je, Niache Shule?

^ Kwa mfano, tunawatia moyo wazazi wawapeleke wana na binti zao shuleni. Ona makala yenye kichwa “Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Shuleni?” katika Mnara wa Mlinzi la Machi 15, 2003.

^ Tazama makala yenye kichwa “Jinsi ya Kumsaidia Mtoto Wako Afanye Vizuri Shuleni.”

^ Tazama sehemu ya jw.org yenye kichwa “Maoni Kuhusu Chanzo cha Uhai.”

^ Kitabu Practical Economics: Economic Transformation and Government Reform in Georgia 2004​—2012, ukurasa wa 170.

^ Buku la 61, Na. 1, April 2017, ukurasa wa 72.

^ Tazama sehemu ya jw.org “Biblia Inabadili Maisha” ili usome masimulizi halisi ya maisha kuhusu nguvu za Neno la Mungu na ujumbe wa Ufalme.