Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Shuleni?

Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Shuleni?

Je, Nimpeleke Mtoto Wangu Shuleni?

HEBU wazia kwamba huwezi kusoma ukurasa huu. Namna gani kama huwezi kuzungumza lugha rasmi ya nchi yako? Tuseme kwamba hujui nchi yako iko wapi katika ramani ya ulimwengu. Watoto wengi sana watakua bila kujua mambo hayo. Namna gani mtoto wako?

Je, umpeleke mtoto wako shuleni? Katika nchi nyingi, elimu ya msingi na ya sekondari ni ya lazima na mara nyingi huwa bila malipo. Mkataba Kuhusu Haki za Mtoto unasema kwamba kila mtoto ana haki ya kupata elimu. Azimio la Watu Wote la Haki za Binadamu linasema hivyo pia. Hata hivyo katika nchi fulani huenda elimu ikawa inalipiwa na hivyo kuwa mzigo mkubwa kifedha kwa wazazi. Hebu tuchunguze jambo hilo kulingana na maoni ya wazazi Wakristo wanaotaka watoto wao wajue kusoma na kuandika, iwe ni katika shule za kawaida au kupitia njia nyingine.

Waliojua Kusoma na Kuandika Nyakati za Biblia

Watumishi wengi wa Mungu wanaotajwa katika Biblia walijua kusoma na kuandika. Mitume wa Yesu, Petro na Yohana walikuwa wavuvi Wayahudi lakini waliandika vitabu vya Biblia katika Kigiriki, wala si katika lugha yao ya Kigalilaya. * Yaonekana wazazi wao walihakikisha kwamba watoto wao walipata elimu ya msingi. Waandikaji wengine wa Biblia ambao pia walijua kusoma na kuandika walitia ndani mchungaji Daudi, mkulima Amosi, na Yuda ndugu wa kambo wa Yesu ambaye huenda alikuwa seremala.

Ayubu angeweza kusoma na kuandika, na kitabu cha Biblia chenye jina lake kinaonyesha kwamba alijua sayansi kwa kadiri fulani. Huenda pia alikuwa na ujuzi katika uandishi, kwa kuwa maneno yake yaliyonukuliwa katika kitabu cha Ayubu yameandikwa kwa mtindo wa kishairi. Tunajua kwamba Wakristo wa mapema walijua kusoma na kuandika kwa kuwa mambo ya Kimaandiko ambayo yaelekea waliandika yamepatikana kwenye vigae vya udongo.

Elimu Ni Muhimu kwa Wakristo

Ili wampendeze Mungu Wakristo wote wanahitaji kuongeza ujuzi wao wa Biblia. (Wafilipi 1:9-11; 1 Wathesalonike 4:1) Unaweza kufanya maendeleo ya kiroho kwa kujifunza Maandiko kwa bidii na vichapo vinavyozungumzia Biblia. Kwa kuwa Mungu amewapa waabudu wake Neno lake lililoandikwa, anatazamia wajitahidi kadiri wawezavyo kujua kusoma na kuandika. Itakuwa rahisi kufuata shauri la Biblia ikiwa tutaisoma na kuielewa. Bila shaka, huenda tukalazimika kusoma sehemu fulani za Biblia mara kadhaa ili kuelewa na kuweza kutafakari.—Zaburi 119:104; 143:5; Mithali 4:7.

Kila mwaka, watu wa Yehova hupokea vichapo vingi vyenye manufaa ambavyo vinatayarishwa chini ya mwongozo wa “mtumwa mwaminifu na mwenye busara.” (Mathayo 24:45-47) Vichapo hivyo huzungumzia maisha ya familia, desturi, dini, sayansi, na kadhalika. Na jambo lililo muhimu zaidi ni kwamba vina mashauri ya Kimaandiko kuhusu mambo ya kiroho. Ikiwa watoto wako hawajui kusoma, basi watakosa habari muhimu sana.

Ni muhimu kujifunza historia ya wanadamu kwa kuwa hutusaidia kuelewa ni kwa nini tunahitaji Ufalme wa Mungu. Ujuzi wa msingi kuhusu jiografia unafaa pia. Biblia hutaja nchi nyingi kama vile Israeli, Misri, na Ugiriki. Je, mtoto wako anaweza kuonyesha nchi hizo ziko wapi kwenye ramani ya ulimwengu? Je, anaweza kuonyesha nchi yake kwenye ramani? Ikiwa mtu hawezi kusoma ramani huenda asiweze kutimiza huduma yake kikamili katika eneo alilogawiwa.—2 Timotheo 4:5.

Mapendeleo Kutanikoni

Wazee Wakristo na watumishi wa huduma wana madaraka mengi yanayohusisha kusoma. Kwa mfano, kuna hotuba mbalimbali za kutaniko wanazopaswa kutayarisha. Wanahitajika pia kuweka rekodi za vichapo na michango. Bila elimu ya msingi, inaweza kuwa vigumu sana kushughulikia madaraka hayo kwa njia inayofaa.

Wafanyakazi wa kujitolea hufanya kazi katika Betheli mbalimbali ulimwenguni. Ili wafanyakazi hao waweze kuwasiliana vizuri na kufanya kazi zao, kama vile kutafsiri vichapo na kurekebisha mashine, ni lazima wajue kusoma na kuandika lugha rasmi ya nchi wanamoishi. Ikiwa watoto wako watakuja kupata mapendeleo hayo, inatazamiwa wawe na elimu ya msingi. Kuna sababu gani nyingine zinazofaa za kumpeleka mtoto wako shuleni?

Umaskini na Ushirikina

Huenda watu walio maskini wakawa hoi katika hali fulani. Hata hivyo, elimu ya kiwango cha kawaida inaweza kutusaidia na kuwasaidia watoto wetu wasiteseke isivyo lazima. Ni watu wachache sana wasiojua kusoma na kuandika wanaoweza kupata mahitaji yao ya lazima maishani. Wakati mwingine, watoto na hata wazazi hufa kwa kukosa matibabu kwa sababu mapato yao ni madogo. Mara nyingi watu wasio na elimu nyingi au wasio na elimu yoyote ndio hukosa chakula kinachofaa na makao mazuri. Elimu au angalau uwezo wa kusoma na kuandika unaweza kumsaidia mtu kwa kiasi fulani kukabiliana na matatizo hayo.

Kujua kusoma na kuandika humsaidia mtu kutofuata sana mambo ya ushirikina. Bila shaka ushirikina umeenea sana miongoni mwa watu wenye elimu na wasio na elimu. Lakini ni rahisi kwa watu wasio na elimu kudanganywa na kutumiwa vibaya kuliko watu wengine, kwa kuwa hawawezi kusoma habari zinazofunua udanganyifu huo. Hivyo, wana maelekeo ya kuwa washirikina na kuamini kwamba mganga anayewasiliana na roho anaweza kuwaponya kimuujiza.—Kumbukumbu la Torati 18:10-12; Ufunuo 21:8.

Lengo la Elimu Si Kupata Kazi Tu

Watu wengi huona kwamba kusudi kuu la elimu ni kuchuma pesa. Hata hivyo, wengine walio na elimu hawana kazi, au mapato yao hayatoshi kwa mahitaji yao ya lazima. Kwa hiyo, huenda wazazi wengine wakafikiri kwamba hakuna manufaa ya kumpeleka mtoto shuleni. Mbali na kumsaidia mtu kuchuma pesa; elimu huwatayarisha watoto katika maisha yao kwa ujumla. (Mhubiri 7:12) Ikiwa mtu anaweza kuongea, kusoma, na kuandika lugha rasmi ya nchi anamoishi, itakuwa rahisi kushughulika na madaktari, wafanyakazi wa serikali, au wafanyakazi wa benki bila kuogopa.

Katika maeneo mengine, huenda watoto wasio na elimu wakapelekwa kwa mtu fulani ili wafundishwe kazi mbalimbali kama vile kutengeneza matofali, kuvua samaki, kushona, na kadhalika. Inafaa kwa watoto kujifunza kazi fulani, lakini watoto hao wasipoenda shuleni yaelekea hawatajifunza kusoma na kuandika vizuri. Wakipata elimu ya msingi kwanza kisha wajifunze kazi fulani, yaelekea watoto hao wataepuka kutumiwa vibaya nayo maisha yao yatakuwa yenye kuridhisha zaidi.

Yesu wa Nazareti alikuwa seremala na yaonekana Yosefu, baba yake mlezi, alimfundisha kazi fulani. (Mathayo 13:55; Marko 6:3) Yesu pia alijua kusoma na kuandika, hata alipokuwa na umri wa miaka 12, aliweza kuzungumzia mambo mazito na wanaume wenye elimu waliokuwa hekaluni. (Luka 2:46, 47) Kazi ambayo Yesu alijifunza haikumzuia kupata elimu ya aina nyingine.

Je, Wasichana Waelimishwe Pia?

Wakati mwingine wazazi huwapeleka shuleni watoto wao wa kiume lakini hawawapeleki binti zao. Labda wazazi fulani hufikiri kwamba kumwelimisha msichana ni kupoteza pesa kwa kuwa wanaamini kwamba hatimaye msichana ataolewa na kunufaisha familia ya mume wake badala ya familia yao. Lakini kutojua kusoma na kuandika kutamzuia msichana asitimize mambo fulani. Kichapo kimoja cha shirika la Umoja wa Mataifa la Hazina ya Watoto (UNICEF) kinasema: “Uchunguzi mwingi ambao umefanywa umeonyesha kwamba kuwaelimisha wasichana ni mojawapo ya njia bora zaidi ya kumaliza janga la umaskini.” (Poverty and Children: Lessons of the 90s for Least Developed Countries) Wasichana walioelimishwa wanaweza kufanya maamuzi yenye hekima zaidi, na hivyo kunufaisha wote katika familia.

Uchunguzi kuhusu vifo vya watoto wachanga huko Benin, Afrika Magharibi, ulionyesha kwamba watoto 167 kati ya watoto 1,000 wa akina mama wasiojua kusoma na kuandika hufa wakiwa chini ya umri wa miaka mitano, wakilinganishwa na watoto 38 kati ya watoto 1,000 wa akina mama walio na elimu ya sekondari. Shirika hilo linamalizia hivi: “Hivyo, idadi ya watoto wachanga wanaokufa huko Benin, kama ilivyo katika sehemu nyingine za ulimwengu, inategemea kiwango cha elimu.” Hivyo basi, unaweza kupata manufaa mbalimbali kwa kuwaelimisha binti zako.

Je, Madarasa ya Watu Wazima Yawe Badala ya Elimu ya Kawaida

Kunapokuwa na uhitaji, Mashahidi wa Yehova huanzisha madarasa ya kuwafundisha washiriki wa kutaniko wasiojua kusoma na kuandika. * Madarasa hayo husaidia watu wajifunze kusoma na kuandika katika lugha yao. Je, madarasa hayo yachukue mahali pa elimu ya kawaida? Je, wapaswa kutazamia kutaniko lielimishe watoto wako hata ingawa wanaweza kwenda kwenye shule za kawaida?

Ingawa madarasa hayo ni mpango wa fadhili unaofanywa na makutaniko ya Mashahidi wa Yehova, yanakusudiwa watu wazima ambao hawakuwahi kwenda shuleni wakiwa watoto. Inawezekana kwamba wazazi wao hawakujua umuhimu wa kujifunza kusoma na kuandika, au hawangeweza kupata shule katika maeneo walimoishi. Watu hao wanaweza kusaidiwa kwa kujiunga na madarasa yanayofanywa makutanikoni. Lakini madarasa hayo hayawezi kuchukua mahali pa elimu ya kawaida, wala elimu ya msingi. Katika madarasa hayo watu hawafunzwi sayansi, hesabu, na historia. Hata hivyo, masomo hayo yanaweza kufundishwa katika shule za kawaida.

Barani Afrika, madarasa hayo hufundishwa kwa lugha za kienyeji na ni mara chache hufundishwa kwa lugha rasmi ya nchi. Hata hivyo, shule za kawaida hufundisha kwa lugha rasmi. Shule hizo hunufaisha watoto zaidi kwa sababu vitabu na vichapo mbalimbali huchapishwa katika lugha rasmi ya nchi. Ingawa madarasa ya kutaniko yanaweza kumsaidia mtoto wa shule, madarasa hayo hayawezi kuchukua mahali pa elimu ya kawaida. Hivyo basi, hali zikiruhusu, watoto wanapaswa kupelekwa shule za kawaida.

Daraka la Wazazi

Wanaume wanaoongoza kutaniko katika mambo ya kiroho wanapaswa kuwa Wakristo ambao ni kielelezo kizuri. Wanapaswa kusimamia watu wa nyumbani mwao na watoto wao kwa “njia bora.” (1 Timotheo 3:4, 12) Kusimamia kwa “njia bora” kunatia ndani kufanya kila tuwezalo tusiwatie watoto wetu katika hali itakayowazuia kutimiza mambo fulani baadaye.

Mungu amewapa wazazi Wakristo daraka kubwa. Wanapaswa kuwalea watoto wao kulingana na Neno lake na kuwasaidia ‘wapende maarifa.’ (Mithali 12:1; 22:6; Waefeso 6:4) Mtume Paulo aliandika: “Hakika ikiwa yeyote hawaandalii kitu wale walio wake mwenyewe, na hasa kwa ajili ya wale walio washiriki wa nyumbani mwake, ameikana imani naye ni mbaya zaidi kuliko mtu asiye na imani.” (1 Timotheo 5:8) Tunapaswa pia kuwaelimisha watoto wetu kwa njia inayofaa.

Wakati mwingine, shule fulani hukosa kuwafundisha watoto ifaavyo kwa sababu ya msongamano, ukosefu wa pesa, au labda walimu hawana furaha kwa kuwa wanalipwa mishahara duni. Kwa hiyo, wazazi wanapaswa kupendezwa na yale ambayo watoto wao wanajifunza shuleni. Ni jambo la hekima kujuana na walimu, hasa mwanzoni mwa kila muhula, hata kuwaomba mashauri kuhusu namna ambavyo watoto wanaweza kuwa wanafunzi bora. Hivyo, huenda walimu wakahisi kwamba wanathaminiwa na kuchochewa kujitahidi zaidi kufundisha watoto ifaavyo.

Elimu ni sehemu muhimu katika ukuzi wa mtoto. Mithali 10:14 inasema: “Watu wenye akili huweka akiba ya maarifa.” Hiyo ni kweli hasa kuhusiana na ujuzi wa Biblia. Watu wa Yehova, vijana kwa wazee, wapaswa kuwa na maarifa mengi iwezekanavyo ili kuwasaidia wengine kiroho na ‘kujionyesha wenyewe kuwa wenye kukubaliwa na Mungu, wasio na lolote la kuaibikia, wakilitumia sawasawa neno la ile kweli.’ (2 Timotheo 2:15; 1 Timotheo 4:15) Kwa hiyo, je, unapaswa kuwapeleka watoto wako shuleni? Bila shaka, utaona kwamba unapaswa kufanya hivyo ingawa hiyo itategemea hali nchini mwako. Lakini wazazi Wakristo wanahitaji kujibu swali hili muhimu sana, ‘Je, ninapaswa kuwaelimisha watoto wangu?’ Hata uwe unaishi wapi, utakubali kwamba unapaswa kuwaelimisha watoto wako.

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 5 Labda walizungumza lugha ya Kigalilaya iliyotokana na Kiaramu au iliyotokana na Kiebrania. Ona Insight on the Scriptures Buku la 1, ukurasa wa 144-146, kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

[Sanduku/Picha katika ukurasa wa 12, 13]

ISIPOWEZEKANA KWENDA SHULENI

Hali fulani hufanya isiwezekane kwenda shuleni. Kwa mfano, gazeti Refugees lilisema kwamba katika kambi za wakimbizi mtoto 1 tu kati ya watoto 5 ndiye anayeweza kwenda shuleni. Wakati mwingine shule hufungwa kwa muda mrefu kwa sababu ya migomo. Huenda shule zikawa mbali sana au zisiwepo katika eneo fulani. Kunyanyaswa kwa Wakristo pia kunaweza kufanya watoto wafukuzwe shuleni.

Unaweza kuwasaidiaje watoto wako katika hali hizo? Unaweza kufanya nini iwapo una watoto kadhaa na unaishi katika eneo ambalo gharama ya kuwaelimisha ni ya juu mno usiweze kuwapeleka wote shuleni? Je, unaweza kumpeleka mtoto mmoja au wawili shuleni bila kuhatarisha hali yao ya kiroho? Iwapo inawezekana, watoto hao wanaweza kuwafundisha wale wengine mambo wanayojifunza shuleni.

Katika nchi fulani watoto husomea nyumbani. * Watoto wanaposomea nyumbani, kwa kawaida mzazi mmoja hutumia muda wa saa kadhaa kila siku kumfundisha mtoto wake. Siku za wazee wa ukoo, wazazi walifanikiwa sana kuwafundisha watoto wao. Yaonekana Yosefu, mwana wa Yakobo, alizoezwa vizuri na wazazi wake, hivyo angeweza kusimamia wengine akiwa na umri mdogo.

Huenda ikawa vigumu kupata programu rasmi ya mafunzo kwenye kambi za wakimbizi, lakini wazazi wanaweza kutumia vichapo vya Mashahidi wa Yehova kufundishia. Kwa mfano, Kitabu Changu cha Hadithi za Biblia kinaweza kutumiwa kufundisha watoto wachanga. Gazeti la Amkeni! huwa na makala zinazozungumzia mambo mbalimbali. Kitabu Life—How Did It Get Here? By Evolution or by Creation? kinaweza kutumiwa kufundisha habari za kisayansi. Kitabu Yearbook of Jehovah’s Witnesses kina ramani ndogo ya ulimwengu na huzungumzia maisha na kazi ya kuhubiri katika nchi mbalimbali.

Watoto wanaweza kunufaika sana ikiwa mambo wanayofundishwa yametayarishwa vizuri kulingana na kiwango cha uelewevu wao. Wakiendelea kusoma na kujifunza, itakuwa rahisi kwao kuzoea mazingira ya shule za kawaida iwapo zitapatikana baadaye. Unaweza kuwasaidia watoto wako wapate elimu nzuri kwa kuchukua hatua zinazofaa na kuwa mwenye bidii. Na hilo linaweza kunufaisha kwelikweli!

[Maelezo ya Chini]

^ fu. 40 Ona makala “Kusomea Nyumbani—Je, Kunakufaa Wewe?” katika gazeti la Amkeni! la Aprili 8, 1993, ukurasa wa 9-12.

[Picha]

Unaweza kufanya nini iwapo unaishi mahali ambapo watoto wako hawawezi kwenda kwenye shule za kawaida?