Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA PILI

Biblia​—Kitabu Kutoka Kwa Mungu

Biblia​—Kitabu Kutoka Kwa Mungu

1, 2. Kwa nini Biblia ni zawadi nzuri kutoka kwa Mungu?

WEWE huhisije unapopewa zawadi na rafiki yako mpendwa? Unatazamia kwa hamu kuifungua na unafurahi sana kwa sababu rafiki yako anakupenda. Unamshukuru kwa kukupa zawadi hiyo.

2 Biblia ni zawadi kutoka kwa Mungu, kwa sababu inatueleza habari ambazo hatuwezi kuzipata mahali pengine popote. Kwa mfano, inatueleza kwamba Mungu aliumba mbingu, dunia, na mwanaume na mwanamke wa kwanza. Ina kanuni zinazoweza kutusaidia kukabiliana na matatizo. Katika Biblia, tunajifunza jinsi Mungu atakavyotimiza kusudi lake la kuifanya dunia kuwa mahali bora pa kuishi. Biblia ni zawadi bora sana.

3. Unapoendelea kujifunza Biblia utaelewa jambo gani?

3 Unapoendelea kujifunza Biblia, utaelewa kwamba Mungu anataka uwe rafiki yake. Kadiri unavyojifunza mengi zaidi kumhusu, ndivyo uhusiano wako pamoja naye utakavyoimarika.

4. Ni nini kinachokuvutia kuhusu kutafsiriwa kwa Biblia?

4 Mabilioni ya nakala za Biblia zimetafsiriwa na kuchapishwa katika lugha 2,600 hivi. Zaidi ya asilimia 90 ya watu ulimwenguni wanaweza kujisomea Biblia katika lugha zao. Kwa kuongezea, zaidi ya watu milioni moja hupata Biblia kila juma! Kwa kweli, hakuna kitabu kingine kama Biblia.

5. Kwa nini tunaweza kusema kwamba Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu’?

5 Biblia ‘imeongozwa na roho ya Mungu.’ (Soma 2 Timotheo 3:16.) Hata hivyo, huenda wengine wakafikiri hivi: ‘Kwa kuwa Biblia iliandikwa na wanadamu inawezaje kuwa kitabu kutoka kwa Mungu?’ Biblia inajibu: “Wanadamu walisema yaliyotoka kwa Mungu kama walivyoongozwa na roho takatifu.” (2 Petro 1:21) Ni kama vile tu babu anapomwomba mjukuu wake amsaidie kuandika barua. Barua hiyo ni ya nani? Hiyo ni barua ya babu wala si ya mjukuu. Vivyo hivyo, Mtungaji wa Biblia ni Mungu, wala si wanadamu aliowatumia kuiandika. Mungu aliwaongoza kuandika mawazo yake. Kwa kweli, Biblia ni “neno la Mungu.”—1 Wathesalonike 2:13; soma Maelezo ya Ziada 2.

Biblia Takatifu—Tafsiri ya Ulimwengu Mpya inapatikana katika lugha mbalimbali

BIBLIA NI SAHIHI

6, 7. Kwa nini tunasema kwamba Biblia inapatana?

6 Biblia iliandikwa kwa zaidi ya miaka 1,600. Waandikaji wake waliishi nyakati tofauti-tofauti. Wengine walikuwa na elimu ya juu ilhali wengine walikuwa na elimu ya kawaida. Kwa mfano, mwandikaji mmoja alikuwa daktari. Wengine walikuwa wakulima, wavuvi, wachungaji, manabii, waamuzi, na wafalme. Ingawa iliandikwa na watu tofauti, Biblia yote inapatana. Ujumbe wake haupingani. *

7 Kitabu cha kwanza cha Biblia kinaeleza jinsi matatizo yalivyoanza, na kitabu cha mwisho kinaeleza jinsi ambavyo Mungu atayaondoa matatizo na kuifanya dunia kuwa paradiso. Biblia inaeleza historia ya mwanadamu tangu zamani na inaonyesha kwamba sikuzote kusudi la Mungu hutimia.

8. Toa mifano inayoonyesha kwamba Biblia ni sahihi inapozungumzia mambo ya sayansi.

8 Biblia si kitabu cha sayansi, hata hivyo, inazungumzia mambo ya sayansi kwa usahihi. Kitabu kutoka kwa Mungu kinapaswa kuwa hivyo. Kwa mfano, kitabu cha Mambo ya Walawi kina maagizo ambayo Mungu aliwapa Waisraeli ili kuzuia kuenea kwa magonjwa. Mambo hayo yaliandikwa miaka mingi kabla ya wanasayansi kugundua jinsi virusi na bakteria wanavyoeneza magonjwa. Pia, Biblia inaeleza kwa usahihi kwamba dunia imening’inizwa pasipo na kitu. (Ayubu 26:7) Hata wakati ambapo watu wengi waliamini kwamba dunia ni tambarare, Biblia ilisema kwamba dunia ni duara.—Isaya 40:22.

9. Tunajifunza nini kutokana na unyoofu wa waandikaji wa Biblia?

9 Biblia ni sahihi inapozungumzia historia. Hata hivyo, vitabu vingi vya historia si sahihi kabisa kwa sababu waandikaji wake hawakuwa wanyoofu. Kwa mfano, nyakati nyingine hawakuandika mataifa yao yaliposhindwa vitani. Tofauti na hao, waandikaji wa Biblia walikuwa wanyoofu na waliandika hata taifa lao la Israeli liliposhindwa vitani. Waliandika pia kuhusu makosa yao. Kwa mfano, katika kitabu cha Hesabu, Musa aliandika kosa zito alilofanya na hivyo akaadhibiwa na Mungu. (Hesabu 20:2-12) Unyoofu wa waandikaji wa Biblia unathibitisha kwamba ni kitabu kutoka kwa Mungu. Kwa hiyo, tunaweza kuiamini Biblia.

KITABU CHENYE USHAURI MZURI

10. Kwa nini ushauri wa Biblia ni wenye faida kwetu?

10 Biblia “[imeongozwa] na roho ya Mungu [nayo] ni yenye faida kwa kufundisha, kwa kukaripia, kwa kunyoosha mambo.” (2 Timotheo 3:16) Naam, ushauri wake una faida kwetu pia. Yehova ndiye aliyetuumba, kwa hiyo anaelewa jinsi tunavyohisi na kufikiri. Anatujua vizuri zaidi kuliko tunavyojijua, na anataka tuwe na furaha. Anajua mambo yanayotufaa na yasiyotufaa.

11, 12. (a) Yesu alitoa ushauri gani mzuri katika Mathayo sura ya 5 hadi ya 7? (b)Ni mambo gani mengine tunayoweza kujifunza katika Biblia?

11 Katika Mathayo sura ya 5 hadi ya 7, Yesu alitoa ushauri mzuri wa jinsi ya kuwa na furaha, jinsi ya kusuluhisha matatizo, jinsi ya kusali, na mtazamo unaofaa kuhusu pesa. Ingawa alitoa ushauri huo miaka 2,000 iliyopita, bado ni wenye nguvu na unatufaidi leo pia.

12 Pia, katika Biblia Yehova anatufundisha kanuni ambazo zinaweza kutusaidia kuwa na familia yenye furaha, kuwa wafanyakazi bora, na kuishi kwa amani pamoja na wengine. Sikuzote kanuni za Biblia ni zenye faida, kwa watu wa namna na hali zote.—Soma Isaya 48:17; soma Maelezo ya Ziada 3.

KWA NINI UAMINI UNABII WA BIBLIA?

Mwandikaji wa Biblia Isaya alitabiri kuhusu kuharibiwa kwa jiji la Babiloni

13. Nabii Isaya alitabiri nini kuhusu jiji la Babiloni?

13 Unabii mwingi wa Biblia umetimizwa. Kwa mfano, Isaya alitabiri kwamba jiji la Babiloni lingeharibiwa. (Isaya 13:19) Alieleza waziwazi jinsi ambavyo jiji hilo lingeharibiwa. Jiji hilo lilikuwa na kuta, malango, na lilizungukwa na mto. Hata hivyo, Isaya alitabiri kwamba mto huo ungekaushwa na malango yangeachwa wazi. Majeshi yangeingia jijini bila kupigana. Isaya hata alitabiri kuhusu mfalme ambaye angeharibu jiji la Babiloni, yaani, Koreshi.—Soma Isaya 44:27–45:2; soma Maelezo ya Ziada 4.

14, 15. Unabii wa Isaya ulitimizwaje?

14 Miaka mia mbili baada ya unabii huo kutolewa, jeshi fulani lilifika likiwa tayari kushambulia jiji la Babiloni. Ni nani aliyekuwa kiongozi wa jeshi hilo? Kama ilivyotabiriwa, ni Koreshi, mfalme wa Uajemi. Wakati ulikuwa umefika wa kutimizwa kwa sehemu ya mwisho ya unabii huo.

15 Wababiloni walishambuliwa siku ambayo walikuwa na sherehe. Walidhani walikuwa salama kwa sababu jiji lilizungukwa na mto mkubwa na lilikuwa na kuta kubwa. Nje ya jiji, Koreshi na jeshi lake waligeuza mkondo wa mto ili kupunguza kina chake. Maji yalipungua na jeshi la Uajemi likavuka. Hata hivyo, jeshi la Koreshi lingeingiaje katika jiji la Babiloni lenye kuta kubwa? Kama ilivyotabiriwa, malango ya jiji yalikuwa wazi, hivyo, jeshi liliingia bila kupigana.

16. (a) Isaya alitabiri nini kuhusu jiji la Babiloni? (b) Tunajuaje kwamba unabii wa Isaya ulitimia?

16 Isaya alitabiri kwamba jiji la Babiloni halingekaliwa tena. Aliandika: “Halitakaliwa kamwe, wala halitakuwa makao ya watu kwa vizazi vyote.” (Isaya 13:20) Je, unabii huo ulitimia? Kilomita 80 hivi kusini mwa Baghdad, nchini Iraq, ni magofu tu yaliyobaki katika eneo ambalo lilikuwa Babiloni. Hakuna wakaaji wowote katika eneo hilo hadi leo. Yehova aliliharibu jiji la Babiloni “kwa ufagio wa maangamizi [au, uharibifu].”Isaya 14:22, 23. *

Magofu ya Babiloni

17. Kwa nini tunaweza kuamini ahadi zote za Mungu?

17 Kwa kuwa unabii mwingi wa Biblia umetimia, tunaamini yale ambayo Biblia inasema kuhusu wakati ujao. Tunaweza kuwa na uhakika kwamba Yehova atatimiza ahadi ya kuifanya dunia kuwa paradiso. (Soma Hesabu 23:19.) Naam, tuna tumaini la “uzima wa milele ambao Mungu, asiyeweza kusema uwongo, aliahidi zamani za kale.”Tito 1:2. *

BIBLIA INAWEZA KUBADILI MAISHA YAKO

18. Paulo alisema nini kuhusu “neno la Mungu”?

18 Tumejifunza kwamba Biblia ni tofauti na vitabu vingine. Biblia ina upatano, na ni sahihi kisayansi na kihistoria. Pia, inatupatia ushauri mzuri na ina unabii mwingi ambao umetimia. Hata hivyo, Biblia ina faida kubwa zaidi. Mtume Paulo aliandika hivi: “Neno la Mungu liko hai nalo ni lenye nguvu.” Andiko hilo linamaanisha nini?—Soma Waebrania 4:12.

19, 20. (a) Biblia inawezaje kukusaidia kujichunguza? (b) Unawezaje kuonyesha kwamba unathamini zawadi ya Biblia?

19 Biblia inaweza kubadili maisha yako. Inaweza kukusaidia kujichunguza. Inaweza kukusaidia kujua hisia na mawazo yako. Kwa mfano, huenda tukafikiri kwamba tunampenda Mungu. Hata hivyo, ili kuthibitisha kwamba tunampenda, tunahitaji kutumia yale tunayojifunza katika Biblia.

20 Kwa kweli, Biblia ni kitabu kutoka kwa Mungu. Anataka uisome, ujifunze, na uipende. Thamini zawadi hiyo na uendelee kujifunza. Hatimaye utaelewa kusudi la Mungu kwa wanadamu. Katika sura inayofuata tutajifunza kuhusu kusudi hilo.

^ fu. 6 Watu fulani husema kwamba ujumbe wa Biblia unatofautiana, hata hivyo madai hayo si ya kweli. Ona sura ya 7 ya kitabu BibliaNeno la Mungu au la Binadamu? kilichochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 16 Ikiwa ungependa kujifunza mengi zaidi kuhusu unabii wa Biblia, unaweza kusoma broshua Kitabu kwa Ajili ya Watu Wote, ukurasa wa 27 hadi 29, iliyochapishwa na Mashahidi wa Yehova.

^ fu. 17 Kuharibiwa kwa Babiloni ni mfano mmoja tu wa unabii wa Biblia ambao ulitimizwa. Unaweza kupata habari zaidi za unabii unaomhusu Yesu Kristo katika Maelezo ya Ziada 5.