Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 8

Wengine Wana Mamlaka Kuliko Sisi

Wengine Wana Mamlaka Kuliko Sisi

NINA hakika utakubali kwamba wengine wana mamlaka kuliko wewe na mimi. Unafikiri ni nani aliye na mamlaka zaidi?— Ni Yehova Mungu. Namna gani Mwana wake, aliye Mwalimu Mkuu? Je, yeye ana mamlaka kutushinda?— Bila shaka.

Yesu alikuwa ameishi na Mungu mbinguni. Yeye alikuwa Mwana mwenye mwili wa roho, au malaika. Je, Mungu aliumba malaika wengine au wana wenye miili ya roho?— Ndiyo, aliumba mamilioni ya malaika. Malaika hao pia wana nguvu nyingi na uwezo mwingi kutushinda.—Zaburi 104:4; Danieli 7:10.

Unakumbuka jina la malaika aliyezungumza na Maria?— Alikuwa Gabrieli. Alimwambia Maria kwamba mtoto wake angekuwa Mwana wa Mungu. Mungu aliuweka uhai wa Mwana wake mwenye mwili wa roho ndani ya tumbo la Maria ili Yesu azaliwe kama mtoto duniani.—Luka 1:26, 27.

Inawezekana Maria na Yosefu walimwambia Yesu nini?

Unaamini muujiza huo? Unaamini kwamba Yesu alikuwa ameishi na Mungu mbinguni?— Yesu alisema hivyo. Yesu alijuaje mambo hayo? Labda alipokuwa mvulana mdogo Maria alimwambia maneno ambayo Gabrieli alisema. Inawezekana pia Yosefu alimwambia Yesu kwamba Mungu ndiye Baba yake halisi.

Yesu alipobatizwa, Mungu hata alizungumza kutoka mbinguni, akisema: “Huyu ni Mwanangu.” (Mathayo 3:17) Na usiku kabla ya kifo chake, Yesu alisali hivi: “Baba, nitukuze kando yako kwa utukufu niliokuwa nao kando yako kabla ya ulimwengu kuwako.” (Yohana 17:5) Yesu aliomba arudishwe mbinguni akaishi tena na Mungu. Angewezaje kuishi huko?— Ingewezekana tu kama Yehova Mungu angemfanya kuwa na mwili wa roho tena, au malaika.

Hebu nikuulize swali muhimu. Je, malaika wote ni wazuri? Unaonaje?— Ni kweli kwamba kuna wakati ambapo malaika wote walikuwa wazuri, kwa sababu Yehova ndiye aliyewaumba na kila kitu ambacho Yehova ameumba ni kizuri. Hata hivyo ilikuwaje mmoja wa malaika hao akageuka na kuwa mbaya?

Ili tupate jibu, hebu turudi nyuma wakati Mungu alipowaumba mwanamume na mwanamke wa kwanza, Adamu na Hawa. Watu wengine husema eti habari kuhusu Adamu na Hawa ni hadithi tu ambayo si kweli. Lakini Mwalimu Mkuu alijua kwamba ilikuwa kweli.

Baada ya Mungu kuwaumba Adamu na Hawa, aliwaweka katika bustani maridadi mahali palipoitwa Edeni. Bustani hiyo ilikuwa paradiso. Wangepata watoto wengi, familia kubwa, na wangeishi milele katika Paradiso. Lakini kuna somo la maana ambalo walihitaji kujifunza. Ni somo ambalo tayari tumezungumzia. Hebu tuone kama tunakumbuka.

Adamu na Hawa wangewezaje kuishi milele katika Paradiso?

Yehova aliwaambia Adamu na Hawa kwamba wangekula matunda yote waliyotaka kutoka kwenye miti ya bustani. Lakini hawakupaswa kula matunda ya mti mmoja tu. Mungu aliwaambia jambo ambalo lingetokea kama wangekula matunda ya mti huo. Alisema: “Mtakufa hakika.” (Mwanzo 2:17) Kwa hiyo, Adamu na Hawa walihitaji kujifunza somo gani?—

Somo la utii. Maisha yetu yanategemea utii wetu kwa Yehova Mungu! Haikutosha kwa Adamu na Hawa kusema tu kwamba wangemtii Mungu. Walipaswa kuonyesha utii wao kwa matendo. Kama wangemtii Mungu ingeonyesha kwamba wanampenda na wanataka awe Mtawala wao. Halafu wangeishi milele katika Paradiso. Lakini kula matunda ya mti huo kungeonyesha nini?—

Kungeonyesha kwamba kwa kweli wao hawana shukrani kwa vitu ambavyo Mungu alikuwa amewapa. Kama ungalikuwapo, je, ungalimtii Yehova?— Mwanzoni, Adamu na Hawa walitii. Lakini mtu fulani aliyekuwa na uwezo kuwashinda akamdanganya Hawa. Akamfanya Hawa akose kumtii Yehova. Mtu huyo ni nani?—

Ni nani aliyemfanya nyoka azungumze na Hawa?

Biblia inasema kwamba nyoka alizungumza na Hawa. Lakini unajua kwamba nyoka hawezi kuzungumza. Basi iliwezekanaje?— Malaika mmoja alifanya ionekane ni kama nyoka ndiye anayezungumza. Lakini kwa hakika ni malaika aliyekuwa akizungumza. Malaika huyo alikuwa ameanza kufikiria mambo mabaya. Alitaka Adamu na Hawa wamwabudu na kumsikiliza. Alitaka kuwa kama Mungu.

Kwa hiyo huyo malaika mbaya akaweka mawazo mabaya katika akili ya Hawa. Akitumia nyoka, alimwambia: ‘Mungu hakuwaambia ukweli. Hamtakufa mkila matunda ya mti huo. Mtakuwa kama Mungu.’ Je, ungeamini maneno hayo?—

Hawa akaanza kutamani kitu ambacho Mungu hakuwa amempa. Akala matunda ya mti uliokatazwa. Kisha akampa Adamu. Adamu hakuamini maneno ya nyoka. Lakini tamaa yake ya kutaka kuwa na Hawa ikawa yenye nguvu sana kuliko upendo wake kwa Mungu. Basi naye akala matunda ya mti huo.—Mwanzo 3:1-6; 1 Timotheo 2:14.

Matokeo yakawa nini?— Adamu na Hawa wakapoteza ukamilifu wao, wakazeeka na kufa. Na kwa sababu sasa hawakuwa wakamilifu, watoto wao wote pia hawakuwa wakamilifu na hatimaye walizeeka na kufa. Mungu hakusema uwongo! Kwa kweli uhai unategemea kumtii Mungu. (Waroma 5:12) Biblia inatuambia kwamba malaika aliyemdanganya Hawa anaitwa Shetani Ibilisi, na malaika wengine waliogeuka wakawa wabaya wanaitwa roho waovu.—Yakobo 2:19; Ufunuo 12:9.

Ni nini kilichowapata Adamu na Hawa baada ya kukosa kumtii Mungu?

Unaelewa sasa ni kwa nini malaika mzuri aliyeumbwa na Mungu aligeuka akawa mbaya?— Ni kwa sababu alianza kufikiria mambo mabaya. Alitaka aabudiwe. Alijua kwamba Mungu alikuwa amewaambia Adamu na Hawa wawe na watoto, na alitaka wote wamwabudu Mungu. Ibilisi hataki hata mtu mmoja amtii Yehova. Kwa hiyo anajaribu kuweka mawazo mabaya katika akili zetu.—Yakobo 1:13-15.

Ibilisi anasema kwamba hakuna mtu ambaye kwa kweli anampenda Yehova. Anasema kwamba mimi na wewe hatumpendi Mungu na kwamba hatupendi kufuata maagizo ya Mungu. Anasema kwamba tunamtii Yehova wakati tu mambo yanapokuwa mazuri kwetu. Je, Ibilisi anasema kweli? Je, sisi tuko hivyo?

Mwalimu Mkuu alisema kwamba Ibilisi ni mwongo! Yesu alionyesha kwamba anampenda Yehova sana kwa kumtii. Na Yesu hakumtii Mungu wakati tu mambo yalikuwa rahisi. Alimtii kila wakati, hata wakati ambapo watu wengine walifanya iwe vigumu kutii. Alikuwa mwaminifu kwa Yehova hadi kifo. Na ndiyo sababu Mungu alimfufua ili aishi milele.

Sasa unafikiri ni nani aliye adui yetu mkubwa zaidi?— Bila shaka, ni Shetani Ibilisi. Unaweza kumwona?— La! huwezi kumwona. Lakini tunajua kwamba yuko na ana uwezo kutushinda. Hata hivyo ni nani aliye na uwezo zaidi kuliko Ibilisi?— Ni Yehova Mungu. Kwa hiyo tunajua kwamba Mungu anaweza kutulinda.