Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 28

Jinsi ya Kujua Yule Tunayepaswa Kumtii

Jinsi ya Kujua Yule Tunayepaswa Kumtii

WAKATI mwingine ni vigumu kujua yule tunayepaswa kumtii. Labda mama au baba anakuambia ufanye jambo fulani. Lakini mwalimu shuleni au polisi anaweza kukuambia ufanye jambo jingine tofauti. Ikiwa hali iko hivyo, utamtii nani?—

Mapema katika Sura ya 7 ya kitabu hiki, tulisoma Waefeso 6:1-3 katika Biblia. Mistari hiyo inasema kwamba watoto wanapaswa kuwatii wazazi wao. Andiko hilo linasema: “Watiini wazazi wenu katika muungano na Bwana.” Je, unajua maana ya kuwa “katika muungano na Bwana?”— Wazazi walio katika muungano na Bwana huwafundisha watoto wao kutii sheria za Mungu.

Lakini kuna watu wazima ambao hawamwamini Yehova. Vipi ikiwa mmoja atakuambia kwamba ni sawa kuiba mtihani shuleni au kuchukua kitu kutoka dukani bila kulipa? Je, ni sawa kwa mtoto kuiba?—

Kumbuka kwamba wakati mmoja Mfalme Nebukadneza aliamuru kila mtu ainamie sanamu ya dhahabu aliyokuwa ametengeneza. Lakini Shadraki, Meshaki, na Abednego hawakufanya hivyo. Unajua ni kwa nini?— Kwa sababu Biblia inasema kwamba watu wanapaswa kumwabudu Yehova peke yake.—Kutoka 20:3; Mathayo 4:10.

Petro anamwambia nini Kayafa?

Baada ya kifo cha Yesu, mitume wake walipelekwa mbele ya Sanhedrini, mahakama kuu ya dini ya Wayahudi. Kuhani mkuu Kayafa akawaambia: “Hakika tuliwaagiza msiendelee kufundisha juu ya msingi wa jina hili [Yesu], na bado, tazameni! mmejaza Yerusalemu fundisho lenu.” Kwa nini mitume hawakutii Sanhedrini?— Petro alimjibu Kayafa hivi kwa niaba ya wengine wote: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:27-29.

Wakati huo, viongozi wa kidini wa Wayahudi walikuwa na mamlaka kubwa sana. Hata hivyo, nchi yao ilikuwa ikitawalwa na serikali ya Roma. Mtawala wa serikali hiyo aliitwa Kaisari. Hata ingawa Wayahudi hawakutaka kutawaliwa na Kaisari, serikali ya Roma iliwafanyia watu mambo mengi mazuri. Na serikali siku hizi huwafanyia raia wao mambo mengi mazuri. Unajua baadhi ya mambo hayo?—

Serikali inajenga barabara, inawalipa polisi ili watulinde na zimamoto ili watusaidie. Pia inaweza kuandaa masomo kwa watoto na kuwatunza wazee. Serikali inahitaji pesa ili kufanya mambo hayo. Je, unajua serikali inatoa pesa hizo wapi?— Kutoka kwa watu. Pesa ambazo watu wanalipa serikali zinaitwa kodi.

Mwalimu Mkuu alipoishi duniani, Wayahudi wengi hawakutaka kulipa kodi kwa serikali ya Roma. Basi siku moja makuhani wakawapa watu pesa ili wamwulize Yesu swali la ujanja. Swali lilikuwa: ‘Je, ni lazima tumlipe Kaisari kodi au hapana?’ Hili lilikuwa swali la ujanja. Kama Yesu angejibu, ‘Ndiyo, ni lazima mlipe kodi,’ Wayahudi wengi hawangefurahi. Lakini Yesu hangesema, ‘La, hamhitaji kulipa kodi.’ Ingekuwa kosa kusema hivyo.

Basi, Yesu alifanya nini? Alisema: ‘Nionyesheni sarafu.’ Ilipoletwa, Yesu akawauliza: ‘Ina picha na jina la nani?’ Watu hao wakasema: ‘La Kaisari.’ Basi Yesu akawaambia: “Kwa vyovyote, basi, mlipeni Kaisari vitu vya Kaisari, lakini mlipeni Mungu vitu vya Mungu.”—Luka 20:19-26.

Yesu alijibuje swali la ujanja la watu hawa?

Hakuna mtu ambaye angeweza kukosoa jibu hilo. Ikiwa Kaisari anawafanyia watu mambo mazuri, basi ni sawa tu kutumia pesa ambazo Kaisari anatengeneza ili kumlipa kwa ajili ya mambo hayo. Kwa njia hiyo, Yesu alionyesha kwamba ni sawa kulipa serikali kodi kwa ajili ya mambo ambayo inatufanyia.

Kwa sasa labda wewe ni mtoto na hivyo huwezi kulipa kodi. Lakini kuna kitu ambacho unapaswa kuipa serikali. Unajua ni nini?— Ni kutii sheria za serikali. Biblia inasema: ‘Tiini mamlaka zilizo kubwa.’ Mamlaka hizi ni wale walio na uwezo katika serikali. Kwa hiyo, Mungu ndiye anayesema kwamba tunapaswa kutii sheria za serikali.—Waroma 13:1, 2.

Labda kuna sheria inayosema usitupe karatasi au takataka mtaani. Je, uitii sheria hiyo?— Ndiyo, Mungu anataka uitii. Je, uwatii polisi pia?— Serikali inawalipa polisi ili walinde watu. Kuwatii ni sawa na kutii serikali.

Basi ikiwa unataka kuvuka barabara na polisi anasema “Ngoja!” ufanye nini?— Ikiwa wengine wanakimbia na kuvuka, je, utavuka pia?— Unapaswa kungoja, hata kama ni wewe peke yako unayengoja. Mungu anakuambia utii.

Labda kuna hatari katika ujirani, naye polisi anasema: “Msiende barabarani. Msitoke nje.” Lakini labda utasikia watu wakipiga kelele na ukataka kujua ni nini kinachoendelea. Je, ni vizuri utoke nje kuona?— Je, hiyo itakuwa kutii “mamlaka zilizo kubwa”?—

Katika sehemu nyingi, serikali pia hujenga shule, na kuwalipa walimu. Je, unafikiri kwamba Mungu anataka umtii mwalimu?— Hebu fikiria. Serikali humlipa mwalimu ili afundishe, kama vile polisi anavyolipwa ili kuwalinda watu. Kwa hiyo kumtii polisi au mwalimu ni sawa na kutii serikali.

Kwa nini tumtii polisi?

Lakini namna gani mwalimu akisema ni lazima ufanye tendo la ibada kwa sanamu fulani? Utafanya nini?—Wale Waebrania watatu hawakuinama ili kuabudu sanamu hata wakati Mfalme Nebukadneza alipowaamuru wafanye hivyo. Unakumbuka ni kwa nini?— Kwa sababu walitaka kumtii Mungu.

Mwandishi wa historia, Will Durant, aliandika kuhusu Wakristo wa mapema na akasema kwamba ‘uaminifu wao mkuu haukuwa kwa Kaisari.’ La, ulikuwa kwa Yehova! Kwa hiyo kumbuka kwamba tunapaswa kumweka Mungu kwanza maishani mwetu.

Tunatii serikali kwa sababu hivyo ndivyo Mungu anataka tufanye. Lakini tukiambiwa tufanye jambo ambalo Mungu anasema tusifanye, tuseme nini?— Tunapaswa kusema kama vile mitume walivyomwambia kuhani mkuu: “Lazima tumtii Mungu kuwa mtawala kuliko wanadamu.”—Matendo 5:29.

Biblia inatufundisha tuheshimu mamlaka. Soma yaliyoandikwa kwenye Mathayo 5:41; Tito 3:1; na 1 Petro 2:12-14.