Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 6

Mwalimu Mkuu Aliwahudumia Wengine

Mwalimu Mkuu Aliwahudumia Wengine

JE, UNAFURAHI mtu anapokufanyia jambo zuri?— Ndiyo, watu wengine pia wanapenda kufanyiwa mambo mazuri. Sisi sote hufurahi tunapofanyiwa mambo mazuri. Mwalimu Mkuu alijua hivyo, na kila wakati aliwafanyia watu mambo mazuri. Alisema hivi: ‘Nilikuja kuhudumu si kuhudumiwa.’ —Mathayo 20:28.

Wanafunzi wa Yesu walibishania nini?

Kwa hiyo, tunapaswa kufanya nini ikiwa tunataka kuwa kama Mwalimu Mkuu?— Ni lazima tuwahudumie wengine kwa kuwafanyia mambo mazuri. Ni kweli kwamba watu wengi hawafanyi hivyo. Wengi wanapenda kuhudumiwa. Wakati mmoja hata wafuasi wa Yesu walitaka wahudumiwe. Kila mmoja wao alitaka kuwa mkuu au mtu wa maana kuliko wenzake.

Siku moja Yesu alipokuwa anasafiri na wanafunzi wake, waliingia mji wa Kapernaumu, karibu na Bahari ya Galilaya. Wote wakaingia katika nyumba moja. Kisha Yesu akawauliza: “Mlikuwa mkibishania nini barabarani?” Wakanyamaza kwa sababu wakiwa barabarani walikuwa wakibishana kuhusu ni nani aliye mkubwa zaidi kati yao. —Marko 9:33, 34.

Yesu alijua kwamba si vizuri mwanafunzi wake yeyote ajifikirie kuwa mkubwa kuliko wengine. Kwa hiyo kama tulivyojifunza katika sura ya kwanza, Yesu alimsimamisha mtoto mdogo katikati yao na kuwaambia kwamba wanapaswa kuwa wanyenyekevu kama mtoto huyo. Lakini bado hawakuelewa. Muda mfupi tu kabla ya Yesu kufa, aliwafunza somo ambalo hawangesahau kamwe. Yesu alifanya nini?—

Wote walipokuwa wakila pamoja, Yesu alisimama akachukua kitambaa, akajifunga kiunoni. Kisha akatia maji ndani ya beseni. Ni lazima wafuasi wake walishangaa anataka kufanya nini. Wakiwa wanatazama, Yesu aliinama na kuosha miguu yao wote. Kisha akaipangusa miguu yao akitumia kile kitambaa. Hebu fikiria jambo hilo! Kama ungekuwapo pale, ungeonaje?—

Yesu aliwafunza wanafunzi wake somo gani?

Wanafunzi wake waliona haifai Mwalimu Mkuu awahudumie kwa kuwaosha miguu. Waliona aibu. Hata Petro alijaribu kumkataza Yesu asimtendee tendo hilo la unyenyekevu. Lakini Yesu akasema kwamba ni muhimu awahudumie.

Kwa kawaida hatuoshi miguu ya wengine leo. Lakini hali ilikuwa hivyo Yesu alipokuwa duniani. Unafikiri ni kwa nini?— Katika nchi walikoishi Yesu na wafuasi wake, watu walivaa viatu ambavyo havikufunika miguu. Kwa hiyo walipotembea barabarani, miguu yao ilijaa vumbi. Lilikuwa tendo jema kuosha miguu ya mgeni aliyekuja nyumbani.

Lakini hakuna mwanafunzi wa Yesu hata mmoja aliyejitolea kuosha miguu ya wengine. Basi Yesu akawaosha. Kwa kuwaosha miguu, Yesu aliwafunza wanafunzi wake somo muhimu. Walihitaji kujifunza somo hilo. Pia sisi leo tunahitaji kujifunza somo hilo.

Je, unajua somo hilo?— Baada ya Yesu kurudi mezani tena, alieleza: ‘Je, mnajua jambo ambalo nimewafanyia? Ninyi huniita, “Mwalimu,” na, “Bwana,” nanyi mnasema sawasawa, kwa maana ndivyo nilivyo. Kwa hiyo, ikiwa mimi, nijapokuwa Bwana na Mwalimu, niliiosha miguu yenu, ninyi pia mnapaswa kuoshana miguu.’ —Yohana 13:2-14.

Unaweza kufanya nini ili kuwasaidia wengine?

Mwalimu Mkuu alionyesha kwamba anataka wanafunzi wake wahudumiane. Hakutaka kila mtu ajifikirie tu. Hakutaka wajifikirie kuwa bora sana hivi kwamba watu wengine wanapaswa kuwahudumia wakati wote. Alitaka wawe na moyo wa kuwahudumia wengine.

Hilo lilikuwa somo zuri, sivyo?— Je, wewe utawahudumia wengine kama Mwalimu Mkuu?— Sisi sote tunaweza kuwatumikia wengine. Watafurahi tukifanya hivyo. Na zaidi sana, tutamfurahisha Yesu na Baba yake.

Si vigumu kuwahudumia watu wengine. Ukiwa mwangalifu, utaona mambo mengi ambayo unaweza kuwafanyia wengine. Hebu fikiria: Je, kuna jambo unaloweza kufanya ili kumsaidia mama yako? Unajua kwamba yeye huwafanyia mambo mengi mkiwa familia. Je, unaweza kumsaidia?— Mbona usimwulize?

Labda unaweza kutayarisha meza kabla ya mlo. Au labda unaweza kuondoa vyombo mezani baada ya familia kumaliza kula. Watoto wengine wanatupa takataka kila siku. Chochote unachoweza kufanya, utakuwa unawahudumia wengine, kama Yesu alivyofanya.

Je, una ndugu au dada wadogo ambao unaweza kuwahudumia? Kumbuka kwamba Yesu, aliye Mwalimu Mkuu, aliwahudumia hata wanafunzi wake. Utakuwa unafanya kama Yesu ukiwatumikia ndugu na dada zako wadogo. Unaweza kuwafanyia nini?— Labda unaweza kuwasaidia kujifunza kuweka vitu vyao vya kuchezea mahali panapofaa wanapomaliza kucheza. Au unaweza kuwavalisha nguo. Au unaweza kuwasaidia kutandika vitanda vyao. Je, unaweza kufikiria mambo mengine unayoweza kuwafanyia?— Watakupenda ukiwafanyia mambo hayo, kama vile wafuasi wa Yesu walivyompenda.

Ukiwa shuleni pia unaweza kuwatumikia wengine. Labda unaweza kuwahudumia wanafunzi wenzako au mwalimu wenu. Mtu akiangusha vitabu vyake, inafaa umsaidie kuviokota. Unaweza kujitolea kufuta ubao au kumsaidia mwalimu wenu kufanya jambo jingine. Hata kumfungulia mtu mlango ni tendo zuri.

Wakati mwingine, utaona kwamba watu hawasemi asante wanapohudumiwa. Unafikiri tunapaswa kuacha kutenda mazuri ikiwa watu hawana shukrani?— La! Watu wengi hawakumwambia Yesu asante kwa kazi zake nzuri. Lakini hilo halikumzuia kufanya mambo mazuri.

Kwa hiyo tusiache kamwe kuwahudumia wengine. Na tumkumbuke Mwalimu Mkuu, Yesu, na kila wakati tujaribu kufuata mfano wake.

Ili ujue zaidi kuhusu kuwasaidia watu wengine, soma Mithali 3:27, 28; Waroma 15:1, 2; na Wagalatia 6:2.