Hamia kwenye habari

Hamia kwenye yaliyomo

SURA YA 10

Yesu Ana Mamlaka Kuliko Roho Waovu

Yesu Ana Mamlaka Kuliko Roho Waovu

JE, UNAKUMBUKA kilichomfanya malaika mmoja wa Mungu awe Shetani Ibilisi?— Tamaa yake ya kutaka kuabudiwa ilimfanya amwasi Mungu. Je, malaika wengine walimfuata Shetani?— Ndiyo. Biblia inawaita ‘malaika wa Shetani,’ au roho waovu.—Ufunuo 12:9.

Je, hao malaika wabaya wanamwamini Mungu?— Biblia inasema hivi: ‘Roho waovu wanaamini Mungu yuko.’ (Yakobo 2:19) Lakini wanaogopa wakati huu. Na wanaogopa kwa sababu wanajua kwamba Mungu atawaadhibu kwa sababu ya mabaya ambayo wamefanya. Kwani wamefanya nini?—

Biblia inasema kwamba malaika hao waliacha makao yao yanayowafaa mbinguni wakaja kuishi duniani kama wanadamu. Walikuja kwa sababu walitaka kufanya ngono pamoja na wanawake warembo duniani. (Mwanzo 6:1, 2; Yuda 6) Ngono ni nini?—

Ngono ni tendo linalokuwa kati ya mwanamume na mwanamke, wanapokaribiana sana kwa njia ya pekee. Baadaye, mtoto anaweza kukua ndani ya tumbo la mama. Lakini ni makosa kwa malaika kufanya ngono. Mungu anaruhusu tu ngono kati ya mwanamume na mwanamke ambao wameoana. Kwa njia hiyo ikiwa mtoto atazaliwa, mume na mke wanaweza kumtunza.

Malaika hawa walifanya mambo gani mabaya?

Malaika walipovaa miili ya wanadamu na kufanya ngono na wanawake duniani, watoto wao wakawa majitu. Walikuwa wabaya sana na waliwaumiza watu. Kwa sababu hiyo Mungu alileta gharika kubwa sana ili kuharibu majitu hao pamoja na wanadamu wote waovu. Lakini alimwambia Noa ajenge safina, au mashua kubwa sana, ili watu wachache waliofanya mema wapate kuokoka. Mwalimu Mkuu alisema kwamba ni muhimu kukumbuka yaliyotokea wakati wa Gharika.—Mwanzo 6:3, 4, 13, 14; Luka 17:26, 27.

Unajua ni nini kilichowapata malaika wabaya wakati wa Gharika?— Waliacha miili yao ya wanadamu wakarudi mbinguni. Lakini hawangeendelea kuwa malaika wa Mungu, kwa hiyo wakawa malaika wa Shetani, au roho waovu. Namna gani watoto wao, wale majitu?— Walikufa katika Gharika, pamoja na watu wengine wote ambao hawakumtii Mungu.

Kwa nini kuna matatizo mengi duniani sasa kuliko wakati mwingine wowote?

Tangu wakati wa Gharika, Mungu hakuwaruhusu roho waovu wawe kama wanadamu tena. Lakini hata kama hatuwaoni, roho waovu bado wanajaribu kuwashawishi watu wafanye mabaya. Wanasababisha matatizo mengi sasa kuliko wakati mwingine wowote. Hii ni kwa sababu walitupwa hapa duniani kutoka mbinguni.

Unajua ni kwa nini hatuwezi kuwaona roho waovu?— Ni kwa sababu wana miili ya roho. Lakini tuna uhakika kwamba wako. Biblia inasema kwamba Shetani ‘anapotosha dunia nzima,’ akisaidiwa na roho waovu. —Ufunuo 12:9, 12.

Je, sisi pia tunaweza kudanganywa na Ibilisi na roho wake waovu?— Ndiyo, inawezekana tusipokuwa waangalifu. Hata hivyo tusiogope. Mwalimu Mkuu alisema: ‘Ibilisi hana uwezo juu yangu.’ Tukiwa karibu sana na Mungu, yeye atatulinda kutokana na Ibilisi na roho wake waovu. —Yohana 14:30.

Ni muhimu kujua ni mambo gani mabaya ambayo roho waovu watajaribu kutushawishi tufanye. Yafikirie. Roho waovu walifanya mambo gani mabaya walipokuja duniani?— Kabla ya Gharika, walifanya ngono na wanawake, jambo ambalo malaika hawakupaswa kufanya. Leo roho waovu wanafurahi wakati watu wanakosa kutii sheria ya Mungu kuhusu ngono. Hebu nikuulize, Ni nani pekee wanaopaswa kufanya ngono?— Ndiyo, ni wale tu waliooana.

Leo wavulana na wasichana wadogo wanafanya ngono, lakini ni kosa kufanya hivyo. Biblia inataja ‘kiungo cha uzazi,’ au uume. (Mambo ya Walawi 15:1-3) Sehemu ya uzazi ya mwanamke inaitwa uke. Yehova aliumba sehemu hizi za mwili kwa kusudi la pekee la kufurahiwa na watu waliooana tu. Roho waovu wanafurahi wakati watu wanapofanya mambo ambayo Yehova anakataza. Kwa mfano, roho waovu hufurahi wakati mvulana na msichana wanapocheza na uume au uke wao. Hatutaki kuwafurahisha roho waovu, sivyo?—

Kuna kitu kingine ambacho roho waovu wanapenda lakini Yehova anachukia. Unajua hicho ni nini?— Ni jeuri. (Zaburi 11:5) Watu wanapokuwa wakatili na kuumiza wengine, hiyo ni jeuri. Kumbuka kwamba hivyo ndivyo wana wa roho waovu, yaani, wale majitu walivyofanya.

Roho waovu pia wanapenda kuogopesha watu. Wakati mwingine wanajifanya kuwa watu waliokufa. Hata wanaweza kuiga sauti za watu waliokufa. Kwa kufanya hivyo, roho waovu wanafanya watu waamini kwamba wafu wako hai na kwamba wanaweza kuongea na wale walio hai. Ndiyo, roho waovu wanafanya watu wengi waamini mizuka.

Kwa hiyo tunapaswa kuwa macho tusidanganywe na Shetani na roho waovu. Biblia inatuonya hivi: ‘Shetani na watumishi wake hujaribu kujifanya waonekane kuwa malaika wazuri.’ (2 Wakorintho 11:14, 15) Lakini kwa kweli, roho waovu ni wabaya. Hebu tuone vile wanavyoweza kujaribu kutufanya tuwe kama wao.

Watu wanajifunzaje kuhusu jeuri na ngono isiyo halali na kuhusu viumbe wenye miili ya roho na mashetani?— Je, si kwa kutazama vipindi fulani katika televisheni, sinema, mashirika mabaya shuleni, rafiki wabaya, na kusoma vitabu vya katuni? Je, kufanya mambo hayo hutuleta karibu na Mungu au karibu na Ibilisi na roho wake waovu? Unaonaje?—

Ni nini kinachoweza kutokea tukitazama jeuri?

Unafikiri ni nani anayetaka tusikilize na kutazama mambo mabaya?— Bila shaka ni Shetani na roho wake waovu. Kwa hiyo, mimi na wewe tunahitaji kufanya nini?— Tunahitaji kusoma, kusikiliza, na kutazama mambo mazuri ambayo yatatusaidia kumtumikia Yehova. Je, unaweza kuwazia baadhi ya mambo hayo mazuri ambayo tunaweza kufanya?—

Inafaa tufanye mambo gani mazuri?

Tukifanya mambo mazuri, hakuna haja ya kuogopa roho waovu. Yesu ana nguvu kuwashinda na wanamwogopa. Siku moja roho waovu walisema hivi walipomwona Yesu: “Je, umekuja kutuangamiza?” (Marko 1:24) Tutafurahi sana wakati ambapo Yesu atamharibu Shetani na roho wake waovu, sivyo?— Kwa sasa, tunaweza kuwa na hakika kwamba Yesu atatulinda dhidi ya roho waovu tukiwa karibu naye na Baba yake wa mbinguni.

Hebu tusome kuhusu yale tunayohitaji kufanya kwenye 1 Petro 5:8, 9 na Yakobo 4:7, 8.